Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 16A

Je, Yerusalemu Linawakilisha Dini Zinazodai Kuwa za Kikristo?

Je, Yerusalemu Linawakilisha Dini Zinazodai Kuwa za Kikristo?

Zamani machapisho yetu yalisema kwamba Yerusalemu linawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo. Bila shaka, hali zilizokuwa katika Yerusalemu lililokosa uaminifu—kutia ndani ibada ya sanamu na uovu ulioenea—zinatukumbusha mambo yanayotendeka katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hata hivyo, miaka ya hivi karibuni machapisho yetu, kutia ndani chapisho unalosoma sasa, hayasemi unabii unafananisha jambo fulani hususa isipokuwa mahali ambapo Biblia inaonyesha hivyo waziwazi. Je, kuna msingi thabiti wa Kimaandiko wa kusema kwamba Yerusalemu linawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo? Hakuna.

Fikiria mambo yafuatayo: Wakati fulani Yerusalemu lilikuwa kituo cha ibada safi; baadaye, wakaaji wake waliasi imani. Kinyume chake, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazijawahi kamwe kuwa na ibada safi. Tangu dini zinazodai kuwa za Kikristo zilipoanzishwa katika karne ya nne W.K, sikuzote zimefundisha uwongo.

Isitoshe, baada ya Wababiloni kuharibu Yerusalemu, Yehova alilikubali jiji hilo na likawa tena kituo cha ibada safi. Kwa upande mwingine, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazijawahi kupata kibali cha Yehova, na baada ya kuharibiwa wakati wa dhiki kuu, hazitainuka tena.

Baada ya kufikiria mambo hayo tunaweza kufikia mkataa gani? Tunapochunguza unabii wa Biblia uliotimizwa kuhusiana na Yerusalemu lililokosa uaminifu, huenda tukasema, ‘Jambo hili au lile linafanana na mambo tunayoona leo katika dini zinazodai kuwa za Kikristo.’ Lakini inaonekana hakuna msingi wa Kimaandiko wa kusema kwamba Yerusalemu linawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo.