Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 19A

Mito ya Baraka Kutoka kwa Yehova

Mito ya Baraka Kutoka kwa Yehova

Fikiria baadhi ya mistari ya Biblia inayotaja “mto” na “maji” kurejelea baraka zinazotiririka kutoka kwa Yehova. Tunaposoma mistari hiyo, tunatiwa moyo kuona njia ambayo Yehova anatumia kutubariki. Jinsi gani?

YOELI 3:18 Unabii huu unaonyesha kijito kinachotiririka kutoka hekaluni. Kinatiririka ili kunywesha “Bonde [lililokauka] la Miti ya Mishita.” Basi Yoeli na Ezekieli wanaona mto unaoleta uhai mahali pasipo na uhai. Katika visa vyote viwili, mto huo unatoka katika nyumba ya Yehova, au hekalu.

ZEKARIA 14:8 Nabii Zekaria anaona “maji yaliyo hai” yakitiririka kutoka katika jiji la Yerusalemu. Nusu ya maji hayo yanaelekea kwenye bahari ya mashariki, yaani, Bahari ya Chumvi, na nusu nyingine, kwenye bahari ya magharibi, yaani, Bahari ya Mediterania. Yerusalemu lilikuwa “jiji la Mfalme mkuu,” Yehova Mungu. (Mt. 5:35) Zekaria anapotaja jiji hilo anatukumbusha jinsi Yehova atakavyotawala dunia nzima wakati ujao. Kwa muda mrefu tumeelewa kwamba maji ya unabii huu yanaonyesha kwamba Yehova atabariki vikundi viwili vya wanadamu waaminifu katika Paradiso, wale watakaookoka dhiki kuu na wale watakaofufuliwa baadaye.

UFUNUO 22:1, 2 Mtume Yohana anaona mto wa mfano unaofanana na mto alioona Ezekieli. Hata hivyo, hautiririki kutoka hekaluni bali unatoka kwenye kiti cha ufalme cha Yehova. Basi, inaonekana maono haya, kama maono ya Zekaria, yanakazia baraka za utawala wa Mungu wakati wa Miaka Elfu Moja.

Bila shaka, kuna tofauti ndogo tu kati ya baraka zinazoletwa na utawala wa Yehova na baraka zinazowakilishwa na mto ambao Ezekieli aliona. Baraka hizo zote zinatoka kwa Yehova na zinawafikia watu wote waaminifu.

ZABURI 46:4 Ona jinsi mstari huu unavyozungumzia mambo yote mawili—ibada na utawala. Hapa tunaona mto unaoleta shangwe kwenye “jiji la Mungu,” yaani, Ufalme na utawala, na pia kwenye “hema la ibada la Aliye Juu Zaidi lililo takatifu na tukufu,” yaani ibada safi.

Tunapochunguza mistari hiyo, tunahakikishiwa kwamba Yehova atawabariki wanadamu waaminifu kwa njia mbili. Tutapata baraka milele, kwanza, kutokana na utawala wake na, pili, kutokana na mpango wake wa ibada safi. Basi acheni sasa tuazimie kuendelea kutafuta kutoka kwa Yehova na Mwana wake “maji yaliyo hai,” yaani, maandalizi yao ya upendo kwa ajili ya uzima wa milele!—Yer. 2:13; Yoh. 4:10.