Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 05

Biblia Ni Ujumbe Kutoka kwa Mungu

Biblia Ni Ujumbe Kutoka kwa Mungu

Yehova ametupatia Biblia. Biblia ni zawadi nzuri sana ambayo ina vitabu mbalimbali 66. Huenda ukajiuliza: ‘Biblia ilitoka wapi? Ni nani aliyeitunga?’ Ili kujibu maswali hayo, tutazungumzia jinsi ujumbe wa Mungu katika Biblia ulivyotufikia.

1. Ikiwa Biblia iliandikwa na wanadamu, kwa nini tunasema ni Neno la Mungu?

Biblia iliandikwa na watu 40 kwa kipindi cha miaka 1,600 hivi, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi 98 W.K. Waandikaji hao walitoka katika malezi mbalimbali. Ingawa hivyo, ujumbe walioandika unapatana. Linawezekanaje? Hilo linawezekana kwa sababu Mungu ndiye Mtungaji wa Biblia. (Soma 1 Wathesalonike 2:13.) Waandikaji hao hawakuandika mawazo yao wenyewe. Badala yake, “walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” a (2 Petro 1:21) Mungu alitumia roho yake takatifu kuwaongoza au kuwachochea watu hao waandike mawazo yake.​—2 Timotheo 3:16.

2. Je, kila mtu duniani anaweza kuipata Biblia?

“Kila taifa na kabila na lugha na watu” wanaweza kunufaika na habari njema iliyo katika Biblia. (Soma Ufunuo 14:6.) Mungu amehakikisha kwamba Biblia inapatikana katika lugha nyingi zaidi kuliko kitabu kingine chochote. Karibu kila mtu anaweza kuipata Biblia. Inapatikana kila mahali na katika lugha nyingi sana.

3. Yehova amehakikishaje kwamba Biblia imehifadhiwa ingawa watu wamejaribu kuiharibu?

Biblia iliandikwa kwenye vitu vinavyoweza kuharibika, kama vile ngozi na mafunjo. Lakini watu walioipenda Biblia waliinakili kwa mkono tena na tena kwa makini sana. Ingawa watu wenye mamlaka walijaribu kuiharibu, watu fulani walihatarisha uhai wao ili kuilinda. Yehova amehakikisha kwamba hakuna mtu au kitu chochote ambacho kimemzuia kuwasiliana nasi kupitia Biblia. Biblia inasema: “Neno la Mungu wetu linadumu milele.”​—Isaya 40:8.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze mengi kuhusu jinsi Mungu alivyowaongoza watu kuiandika Biblia, jinsi alivyoihifadhi, na jinsi alivyohakikisha kwamba watu wote wanaweza kuipata.

4. Biblia inatuambia ni nani aliyeitunga

Onyesha VIDEO. Kisha soma 2 Timotheo 3:16, na mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Ikiwa Biblia iliandikwa na wanadamu, kwa nini inaitwa Neno la Mungu?

  • Je, unafikiri inapatana na akili kuamini kwamba Mungu aliwatumia wanadamu kuwasilisha mawazo yake?

Karani anaweza kuandika barua yenye ujumbe kutoka kwa bosi wake. Vivyo hivyo, wanadamu waliandika Biblia, lakini ujumbe wake ulitoka kwa Mungu

5. Biblia iliokoka upinzani mkali

Kwa kuwa Biblia ilitoka kwa Mungu, basi tunatazamia kwamba angeilinda ili isiharibiwe. Katika historia yote, watu wenye mamlaka wamejaribu kuiangamiza Biblia. Viongozi wa kidini wamejaribu kuificha. Lakini licha ya upinzani na vitisho vya kuuawa, watu wengi walihatarisha uhai wao ili kuilinda. Ili ujifunze kuhusu mmoja wao, onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Baada ya kujua jitihada nyingi zilizofanywa ili kuilinda Biblia, je, unachochewa kuisoma? Kwa nini?

Soma Zaburi 119:97, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini watu wengi walihatarisha uhai wao ili kutafsiri na kuisambaza Biblia?

6. Kitabu kwa ajili ya watu wote

Biblia ndicho kitabu ambacho kimetafsiriwa na kusambazwa zaidi duniani. Soma Matendo 10:34, 35, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kwa nini Mungu anataka Neno lake litafsiriwe na kusambazwa kwa wingi?

  • Wewe binafsi unapendezwa na jambo gani kuhusu Biblia?

Karibu

Asilimia 100

ya watu ulimwenguni

wanaweza kuipata Biblia katika lugha wanayoielewa

Inapatikana katika lugha zaidi ya

3,000

ikiwa nzima

au sehemu fulani ya Biblia

5,000,000,000

Inakadiriwa nakala bilioni tano zimechapishwa,

idadi kubwa kuliko kitabu kingine chochote

WATU FULANI HUSEMA: “Biblia ni kitabu cha zamani kilichoandikwa na wanadamu.”

  • Wewe una maoni gani?

  • Ni nini kinachothibitisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu?

MUHTASARI

Biblia ni Neno la Mungu, na amehakikisha kwamba watu wote wanaweza kuipata.

Ungejibuje?

  • Mungu aliwaongozaje wanadamu kuandika Biblia?

  • Ni jambo gani linalokupendeza kuhusu kuhifadhiwa, kutafsiriwa, na kusambazwa kwa Biblia?

  • Baada ya kujua jitihada ambazo Mungu amefanya ili kuwasiliana nawe kupitia Biblia, unahisije?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Soma kuhusu historia ya Biblia​—kuanzia hati za awali hadi tafsiri za kisasa.

“Jinsi Biblia Ilivyotufikia” (Amkeni!, Novemba 2007)

Jifunze kuhusu hatari tatu ambazo Biblia ilikabili katika jitihada za kuiangamiza.

“Jinsi Biblia Ilivyookoka” (Mnara wa Mlinzi Na. 4 2016)

Ona jinsi watu walivyohatarisha uhai wao ili kuitafsiri Biblia.

Waliithamini Biblia (14:26)

Biblia imenakiliwa na kutafsiriwa mara nyingi. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba ujumbe wake haujabadilishwa?

“Je, Biblia Imebadilishwa au Kupotoshwa?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

a Kama itakavyofafanuliwa katika Somo la 7, roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu.