Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 07

Yehova Ana Sifa Gani?

Yehova Ana Sifa Gani?

Unapata picha gani unapofikiria kumhusu Yehova Mungu? Je, unamwogopa na kuhisi kwamba huwezi kuwa rafiki yake kwa sababu yuko mbali sana kama vile nyota zilivyo mbali? Au je, unafikiri ni nguvu fulani isiyo na uhai kama vile mungurumo wa radi? Yehova ana sifa gani? Kupitia Neno lake, Biblia, Yehova ameeleza baadhi ya sifa zake na kuonyesha kwamba anakujali.

1. Kwa nini hatuwezi kumwona Mungu?

“Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Yehova hana mwili kama wa mwanadamu. Yeye ni Roho na anaishi mbinguni, mahali ambapo hatuwezi kuona.

2. Yehova ana sifa gani?

Ingawa hatuwezi kumwona Yehova, Yeye yupo na tunapojifunza kumhusu tunampenda kwa sababu ya sifa zake zenye kuvutia. Biblia inasema: “Yehova anapenda haki, naye hatawaacha washikamanifu wake.” (Zaburi 37:28) Pia, yeye ni “mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema,” hasa kuelekea watu wanaoteseka. (Yakobo 5:​11) “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho.” (Zaburi 34:18) Je, unajua kwamba tunaweza kumfurahisha au kumhuzunisha Yehova? Mtu anayeamua kufanya mambo mabaya humuumiza na kumhuzunisha. (Zaburi 78:​40, 41) Lakini mtu anayefanya mambo mazuri anamfurahisha.​​—Soma Methali 27:11.

3. Yehova ameonyeshaje kwamba anatupenda?

Sifa kuu zaidi ya Yehova ni upendo. Na kwa kweli, “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Yehova amefunua upendo wake kupitia Biblia na vilevile kupitia vitu alivyoumba. (Soma Matendo 14:17.) Kwa mfano, fikiria jinsi alivyotuumba. Ametupatia uwezo wa kuona rangi maridadi, kusikiliza muziki mzuri, na kufurahia chakula kitamu. Anataka tufurahie maisha.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi ambavyo Yehova hutimiza mambo mengi mazuri. Kisha uone jinsi ambavyo amefunua na kuonyesha sifa zake zenye kuvutia.

4. Roho takatifu ni nguvu ya Mungu ya utendaji

Kama vile ambavyo sisi hutumia mikono kufanya kazi, Yehova hutumia roho yake takatifu kutimiza mambo. Biblia inaeleza kwamba roho takatifu si mtu, bali ni nguvu ambayo Mungu hutumia kufanya kazi zake. Soma Luka 11:13 na Matendo 2:17, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Mungu ‘ataimimina’ roho yake takatifu juu ya wale wanaomwomba. Basi, unafikiri roho takatifu ni mtu au ni nguvu ya Mungu ya utendaji? Kwa nini unajibu hivyo?

Yehova hutumia roho yake takatifu kutimiza mambo mengi mazuri. Soma Zaburi 33:6 na 2 Petro 1:20, 21, kisha mzungumzie swali hili:

  • Yehova ametumia roho yake takatifu katika njia gani?

5. Yehova ana sifa zenye kuvutia

Musa mtumishi mwaminifu wa Mungu alitamani kumjua Muumba wake vizuri zaidi. Hivyo Musa alimwambia hivi Yehova: “Nifundishe njia zako ili nikujue.” (Kutoka 33:13) Basi, Yehova alimwambia Musa baadhi ya sifa zake. Soma Kutoka 34:4-6, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Ni sifa gani ambazo Yehova alimfunulia Musa?

  • Ni sifa gani za Yehova ambazo zinakuvutia zaidi?

6. Yehova anawajali watu

Waebrania, waliokuwa watu wa Mungu, walikuwa watumwa nchini Misri. Yehova alihisije walipokuwa wakiteseka? Cheza REKODI YA KUSIKILIZA na mfuatane na usomaji huo, au soma Kutoka 3:1-10. Kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Simulizi hili linakufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyohisi wanadamu wanapoteseka?​—Ona mstari wa 7 na 8.

  • Je, unafikiri Yehova anataka kuwasaidia wanadamu na je, ana uwezo wa kufanya hivyo? Kwa nini unafikiri hivyo?

7. Uumbaji unafunua sifa za Yehova

Yehova amefunua sifa zake kupitia vitu alivyoumba. Onyesha VIDEO. Kisha soma Waroma 1:20, na mzungumzie swali linalofuata:

  • Unapochunguza uumbaji unaona sifa gani za Yehova?

WATU FULANI HUSEMA: “Mungu ni nguvu inayopatikana kila mahali, hatuwezi kumjua vizuri.”

  • Wewe una maoni gani?

  • Kwa nini unafikiri hivyo?

MUHTASARI

Yehova ni Roho, hivyo hatuwezi kumwona. Ana sifa nyingi zenye kuvutia kutia ndani upendo.

Ungejibuje?

  • Kwa nini hatuwezi kumwona Yehova?

  • Roho takatifu ni nini?

  • Yehova ana sifa gani mbalimbali?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Jifunze mengi kuhusu sifa nne kuu za Yehova.

“Mungu Ana Sifa Gani?” (Mnara wa Mlinzi Na. 1 2019)

Chunguza uthibitisho unaoonyesha kwamba Yehova hapatikani kila mahali.

“Je, Mungu Yuko Kila Mahali?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Ona kwa nini Biblia inalinganisha roho takatifu na mkono wa Mungu.

“Roho Takatifu Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Ilikuwa vigumu kwa mwanamume fulani kipofu kuamini kwamba Mungu anamjali. Ona jambo lililofanya abadili maoni yake.

“Sasa Ninahisi Kwamba Ninaweza Kuwasaidia Wengine” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 2015)