SOMO LA 11

Jinsi Unavyoweza Kunufaika Zaidi Unaposoma Biblia

Jinsi Unavyoweza Kunufaika Zaidi Unaposoma Biblia

Je, umewahi kuhisi kwamba ni vigumu kuanza kazi fulani kubwa? Kabla ya kuanza kazi hiyo, huenda uliigawa katika visehemu vidogo ili iwe rahisi kuikamilisha. Ndivyo ilivyo pia kuhusu kusoma Biblia. Huenda unajiuliza, ‘Nitaanzia wapi?’ Katika somo hili, tutachunguza mambo rahisi unayoweza kufanya ili ufurahie kusoma na kujifunza Biblia.

1. Kwa nini tunapaswa kusoma Biblia kwa ukawaida?

Mtu anayesoma Biblia au “sheria ya Yehova” kwa ukawaida, atakuwa na furaha na atafanikiwa. (Soma Zaburi 1:1-3.) Unaweza kuanza kwa kusoma Biblia kwa dakika chache kila siku. Kadiri unavyozidi kulifahamu Neno la Mungu, ndivyo utakavyofurahia zaidi kusoma Biblia.

2. Ni nini kitakachokusaidia unufaike unaposoma Biblia?

Ili unufaike zaidi unaposoma Biblia, unahitaji kutua na kufikiria mambo unayosoma. Unapaswa kuisoma na ‘kutafakari.’ (Yoshua 1:8, maelezo ya chini) Unaposoma, jiulize maswali kama vile: ‘Habari hii inanifundisha nini kumhusu Yehova Mungu? Nitaitumiaje katika maisha yangu? Ninawezaje kutumia mistari hii kuwasaidia wengine?’

3. Unawezaje kutenga wakati wa kusoma Biblia?

Je, ni vigumu kwako kupata muda wa kusoma Biblia? Wengi wetu huhisi hivyo. Jitahidi kutumia ‘vizuri kabisa wakati wako.’ (Waefeso 5:16) Unaweza kufanya hivyo kwa kutenga wakati hususa wa kusoma Biblia kila siku. Baadhi ya watu hutenga muda wa kusoma Biblia asubuhi mapema. Wengine hupenda kusoma mchana, labda wakati wa chakula cha mchana. Na wengine husoma Biblia jioni kabla ya kulala. Ni wakati gani ambao utakufaa wewe?

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi unavyoweza kufurahia kusoma Biblia. Pia, ona jinsi unavyoweza kujitayarisha vizuri ili unufaike zaidi unapojifunza Biblia.

Kama vile tunavyojifunza kupenda vyakula vya aina mbalimbali, vivyo hivyo tunaweza kujifunza kufurahia kusoma Biblia

4. Jifunze kufurahia kusoma Biblia

Huenda isiwe rahisi kuanza kusoma Biblia. Hata hivyo, tunaweza ‘kukuza hamu’ ya kufanya hivyo, kama vile mtu anavyojifunza kuzoea ladha ya chakula kipya. Soma 1 Petro 2:2, kisha mzungumzie swali hili:

  • Je, unafikiri ukisoma Biblia kila siku, utafurahia na utatamani kuendelea kuisoma?

Onyesha VIDEO ili kuona jinsi watu fulani walivyoanza kupenda kusoma Biblia. Kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, vijana walishinda changamoto zipi?

  • Ni nini kilichowasaidia kuendelea kukazia lengo lao la kusoma Biblia?

  • Walifanya nini ili wafurahie zaidi kusoma Biblia?

Madokezo ya jinsi ya kuanza:

  • Chagua tafsiri inayotegemeka na inayoeleweka kwa urahisi. Tumia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa inapatikana katika lugha yenu.

  • Anza kusoma sehemu zinazokuvutia zaidi. Ili kupata mapendekezo, ona chati “Ratiba ya Kusoma Biblia.”

  • Andika orodha ya sura ulizosoma. Tumia “Chati ya Rekodi Yako ya Kusoma Biblia” iliyo katika chapisho hili.

  • Tumia programu ya JW Library®. Unaweza kutumia programu hiyo kusoma na kusikiliza Biblia ukiwa mahali popote, kwa kutumia simu au kifaa kingine cha kielektroni.

  • Tumia nyongeza zilizo katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Kuna ramani, chati, na kamusi ambazo zinaweza kukusaidia ufurahie zaidi kusoma Biblia.

5. Jitayarishe kabla ya kujifunza Biblia

Soma Zaburi 119:34, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini ni vizuri kusali kabla ya kusoma Biblia au unapojitayarisha kujifunza Biblia?

Unaweza kunufaikaje zaidi na kila kipindi cha kujifunza? Unapotayarisha somo fulani katika kitabu hiki, jaribu kutumia njia ifuatayo:

  1. Soma mafungu ya kwanza ya somo hilo.

  2. Soma maandiko yaliyotajwa, na uchunguze jinsi yanavyohusiana na habari hiyo.

  3. Weka alama kwenye maneno au mafungu ya maneno yanayojibu kila swali; kufanya hivyo kutakusaidia mnapozungumzia somo hilo pamoja na mwalimu wako.

Je, wajua?

Mashahidi wa Yehova wametumia tafsiri mbalimbali za Biblia. Hata hivyo, tunapendelea hasa Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwa sababu ni sahihi, ni rahisi kuielewa, na inatumia jina la Mungu.​—Ona makala iliyo kwenye mtandao, “Je, Mashahidi wa Yehova Wana Biblia Yao Wenyewe?”

WATU FULANI HUSEMA: “Kujifunza Biblia ni kazi ngumu sana. Mara nyingi huwa nimechoka na sina wakati wa kujifunza.”

  • Wewe una maoni gani?

MUHTASARI

Ili unufaike zaidi na Biblia, panga ratiba ya kuisoma, sali ili uelewe mambo unayosoma, na ujitayarishe kabla ya kila kipindi cha kujifunza Biblia.

Ungejibuje?

  • Ni nini kitakachokusaidia unufaike zaidi unaposoma Biblia?

  • Unaweza kutenga wakati gani wa kusoma na kujifunza Biblia?

  • Kwa nini ni muhimu kujitayarisha kabla ya kila kipindi cha kujifunza Biblia?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza mapendekezo yanayoweza kukusaidia unufaike zaidi unapoisoma Biblia.

“Jinsi ya Kunufaika Zaidi Unapoisoma Biblia” (Mnara wa Mlinzi Na. 1 2017)

Pata mapendekezo kutoka kwa watu waliosoma Biblia kwa miaka mingi.

Funzo la Kibinafsi Lenye Matokeo (2:06)