SOMO LA 12

Ni Nini Kitakachokusaidia Uendelee Kujifunza Biblia?

Ni Nini Kitakachokusaidia Uendelee Kujifunza Biblia?

Kujifunza Biblia ni kama safari. Hata hivyo, kuna changamoto. Wakati mwingine, huenda ukawa na shaka kama utaendelea kujifunza Biblia. Kwa nini ni muhimu kuendelea kujitahidi? Ni nini kitakachokusaidia uendelee licha ya changamoto?

1. Kwa nini kujifunza Biblia ni jambo muhimu?

“Neno la Mungu liko hai nalo ni lenye nguvu.” (Waebrania 4:​12) Biblia ni yenye thamani kwa sababu inafunua mawazo na hisia za Mungu kukuelekea. Inakusaidia kupata ujuzi, tumaini, na hekima ya kweli. Jambo muhimu zaidi ni kwamba Biblia inakusaidia uwe rafiki ya Yehova. Unapojifunza Biblia unaruhusu nguvu zake zifanye maisha yako yawe bora.

2. Kwa nini ni muhimu kutambua thamani ya kweli za Biblia?

Kweli zilizo katika Biblia ni kama hazina zenye thamani. Ndiyo sababu Biblia inatutia moyo ‘tununue kweli na tusiiuze kamwe.’ (Methali 23:23) Tunapotambua thamani ya kweli za Biblia, tutajitahidi kuendelea kujifunza hata tukikabili changamoto.​—Soma Methali 2:4, 5.

3. Yehova anaweza kukusaidiaje kuendelea kujifunza?

Kwa kuwa yeye ni Muumba mweza-yote na Rafiki yako, Yehova anataka kukusaidia ujifunze kumhusu. Atakupa “hamu na nguvu za kutenda.” (Soma Wafilipi 2:13.) Basi, ikiwa nyakati nyingine unakosa hamu ya kujifunza au kufuata mambo unayojifunza, anaweza kukusaidia. Anaweza pia kukupa nguvu za kushinda changamoto na upinzani. Sali kwa Yehova kwa ukawaida ukimwomba akusaidie uendelee kujifunza Biblia.​—1 Wathesalonike 5:17.

CHIMBA ZAIDI

Ona jinsi unavyoweza kuendelea kujifunza Biblia licha ya kuwa na shughuli nyingi au unapokabili upinzani kutoka kwa wengine. Kisha fikiria jinsi Yehova anavyoweza kukusaidia uendelee kujifunza.

4. Hakikisha kwamba kujifunza Biblia ni jambo muhimu kwako

Nyakati fulani huenda ukahisi una shughuli nyingi sana hivi kwamba huna wakati wa kujifunza Biblia. Ni nini kinachoweza kukusaidia? Soma Wafilipi 1:10, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Unafikiri ni mambo gani yaliyo “muhimu zaidi” maishani?

  • Unaweza kufanya nini ili kujifunza Biblia kuwe jambo muhimu kwako?

  1. Ukiweka mchanga kwenye ndoo kisha ujaribu kuongeza mawe, mawe hayatakuwa na nafasi ya kutosha

  2. Ukiweka mawe kwanza kwenye ndoo utakuwa na nafasi ya kuongeza mchanga. Vivyo hivyo, ukitanguliza “mambo muhimu zaidi” maishani, utafaulu kuyatimiza na pia utakuwa na muda wa kufanya mambo mengine

Kujifunza Biblia hutimiza uhitaji wetu wa kiroho, yaani, uhitaji wetu wa kumjua na kumwabudu Mungu. Soma Mathayo 5:3, kisha mzungumzie swali hili:

  • Tutanufaikaje ikiwa tutaona kujifunza Biblia kuwa jambo muhimu maishani mwetu?

5. Endelea kujifunza licha ya upinzani

Wakati mwingine, huenda watu wakajaribu kukuvunja moyo uache kujifunza Biblia. Ona mfano wa Francesco. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, familia na marafiki wa Francesco walitendaje alipowaambia mambo aliyokuwa akijifunza?

  • Alinufaikaje kwa kuendelea kujifunza Biblia?

Soma 2 Timotheo 2:24, 25, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Marafiki na watu wa familia yako wanahisije kuhusu mambo unayojifunza?

  • Kulingana na mistari hii, unapaswa kufanya nini ikiwa mtu fulani hafurahii kukuona ukijifunza Biblia? Kwa nini?

6. Mtegemee Yehova akusaidie

Tunapoendelea kumkaribia Yehova, ndivyo tamaa yetu ya kumfurahisha inavyozidi kuongezeka. Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu kufanya mabadiliko maishani ili kuishi kulingana na viwango vyake. Usikate tamaa ikiwa utahisi hivyo. Yehova atakusaidia. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, Jim alifanya mabadiliko gani ili amfurahishe Yehova?

  • Ni nini kilichokuvutia kuhusu mfano wake?

Soma Waebrania 11:6, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yehova atawafanyia nini wale “wanaomtafuta kwa bidii,” yaani, wale wanaojitahidi kumjua na kufanya mambo yanayomfurahisha?

  • Hilo linakufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyohisi anapoona jitihada zako za kujifunza Biblia?

HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini unajifunza Biblia?”

  • Utajibuje swali hilo?

MUHTASARI

Ingawa mara nyingi si rahisi kujifunza Biblia, kufanya hivyo kunaweza kukusaidia ufurahie maisha milele. Endelea kumtegemea Yehova, naye atakubariki.

Ungejibuje?

  • Kwa nini kweli za Biblia ni zenye thamani kwako?

  • Unaweza kuhakikishaje kwamba unatanguliza “mambo muhimu zaidi”?

  • Kwa nini unapaswa kumwomba Yehova akusaidie uendelee kujifunza Biblia?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza mambo manne ambayo yamewasaidia watu wengi kutumia wakati wao vizuri.

“Jinsi ya Kutumia Wakati Wako Vizuri” (Amkeni!, Februari 2014)

Ona jinsi Yehova alivyomsaidia mwanamke fulani ambaye mume wake hakuelewa kwa nini anajitahidi kumpendeza Mungu.

Yehova Anatuimarisha Ili Tubebe Mzigo Wetu (5:05)

Ona jinsi mwanamume fulani alivyonufaika kwa sababu mke wake aliendelea kujifunza Biblia.

Nilichunguza Ukweli kwa Makini (6:30)

Wakati mwingine watu husema Mashahidi wa Yehova wanavunja familia. Je, huo ni ukweli?

“Je, Mashahidi wa Yehova Huvunja Familia au Huziimarisha?” (Makala iliyo kwenye mtandao)