Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 16

Yesu Alifanya Nini Alipokuwa Duniani?

Yesu Alifanya Nini Alipokuwa Duniani?

Watu wengi wanapofikiri kumhusu Yesu, wanamwona kuwa mtoto mchanga, nabii mwenye hekima, au mtu anayekaribia kufa. Lakini tunaweza kujifunza mengi kumhusu kwa kuchunguza maisha yake alipokuwa duniani. Katika somo hili, tutachunguza baadhi ya mambo muhimu sana ambayo Yesu alifanya na jinsi yanavyoweza kukusaidia.

1. Ni kazi gani iliyokuwa muhimu zaidi katika maisha ya Yesu?

Kazi muhimu katika maisha ya Yesu ilikuwa “[kutangaza] habari njema ya Ufalme wa Mungu.” (Soma Luka 4:43.) Yesu alihubiri habari njema kwamba Mungu atasimamisha ufalme, au serikali ambayo itaondoa matatizo yote ya wanadamu. a Yesu alitangaza kwa bidii ujumbe huo wenye kutia moyo kwa miaka mitatu na nusu.​—Mathayo 9:35.

2. Kwa nini Yesu alifanya miujiza?

Biblia inaeleza “matendo [mengi] yenye nguvu na mambo ya ajabu na ishara ambazo Mungu alifanya kupitia [Yesu].” (Matendo 2:22) Mungu alimpa Yesu nguvu za kutuliza dhoruba kubwa, kulisha maelfu ya watu, kuponya wagonjwa, na hata kufufua waliokufa. (Mathayo 8:23-27; 14:15-21; Marko 6:56; Luka 7:11-17) Miujiza ya Yesu ilithibitisha wazi kwamba Mungu alikuwa amemtuma. Pia ilionyesha kwamba Yehova ana nguvu za kutatua matatizo yetu yote.

3. Tunajifunza nini kutokana na maisha ya Yesu?

Yesu alimtii Yehova nyakati zote. (Soma Yohana 8:29.) Licha ya upinzani, Yesu alifanya kwa uaminifu mambo ambayo Baba yake alitaka afanye katika kipindi chote alichokuwa duniani. Yesu alithibitisha kwamba inawezekana kwa wanadamu kumtumikia Mungu hata wanapokabili hali ngumu. Hivyo, Yesu alituachia “kielelezo ili [tufuate] hatua zake kwa ukaribu.”​—1 Petro 2:21.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza jinsi Yesu alivyohubiri habari njema na kufanya miujiza.

4. Yesu alihubiri habari njema

Yesu alitembea mamia ya kilomita kwenye barabara zenye vumbi, akiwahubiria habari njema watu wengi iwezekanavyo. Soma Luka 8:1, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, Yesu aliwahubiria tu watu waliokusanyika ili kumsikiliza?

  • Yesu alifanya jitihada gani ili kuwatafuta watu?

Mungu alitabiri kwamba Masihi angetangaza habari njema. Soma Isaya 61:1, 2, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yesu alitimizaje unabii huu?

  • Je, unafikiri leo watu wanahitaji kusikia habari njema?

5. Yesu alifundisha masomo muhimu

Mbali na kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, Yesu alifundisha mambo mengine muhimu. Fikiria mifano michache katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani. Soma Mathayo 6:14, 34 na 7:12, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Yesu alitoa ushauri gani katika mistari hiyo?

  • Je, unafikiri ushauri huo unaweza kuwasaidia watu leo?

6. Yesu alifanya miujiza

Yehova alimpa Yesu uwezo wa kufanya miujiza mingi. Ili uone mfano mmoja, soma Marko 5:25-34 au onyesha VIDEO. Kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, yule mwanamke mgonjwa alikuwa na uhakika gani?

  • Ni jambo gani linalokupendeza kuhusu muujiza huo?

Soma Yohana 5:36, kisha mzungumzie swali hili:

  • Miujiza ya Yesu ‘ilitoa ushahidi’ kuhusu nini au ilithibitisha nini kumhusu?

Je, wajua?

Mambo mengi tunayojua kumhusu Yesu yanapatikana katika vitabu vinne vya Biblia vinavyoitwa vitabu vya Injili, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Kila kitabu cha Injili kina habari fulani kumhusu Yesu ambazo hazimo katika vile vitabu vingine. Habari hizo zinapounganishwa zinatokeza masimulizi yenye kupendeza kuhusu maisha ya Yesu.

  • MATHAYO

    alikuwa wa kwanza kuandika kitabu cha Injili. Alikazia mafundisho ya Yesu, hasa mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme wa Mungu.

  • MARKO

    aliandika kitabu kifupi zaidi cha Injili. Kina habari nyingi zenye kusisimua.

  • LUKA

    anazungumzia umuhimu wa sala na jinsi Yesu alivyowatendea wanawake.

  • YOHANA

    alifunua mengi kuhusu utu wa Yesu kwa kusimulia mazungumzo mengi kati ya Yesu na marafiki wa karibu na pia watu wengine.

WATU FULANI HUSEMA: “Yesu alikuwa mtu mzuri tu, lakini hakuwa Masihi.”

  • Wewe una maoni gani?

MUHTASARI

Yesu alihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu, alifanya miujiza, na kumtii Yehova nyakati zote.

Ungejibuje?

  • Ni kazi gani iliyokuwa muhimu zaidi katika maisha ya Yesu alipokuwa duniani?

  • Miujiza ya Yesu inathibitisha nini?

  • Yesu alifundisha masomo gani muhimu?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ni jambo gani ambalo Yesu alizungumzia zaidi wakati wa huduma yake duniani?

“Ufalme wa Mungu​—Una Umuhimu Gani kwa Yesu?” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 2014)

Chunguza mambo yanayothibitisha kwamba kweli miujiza ya Yesu ilitukia.

“Miujiza ya Yesu Unaweza Kujifunza Nini?” (Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 2004)

Soma jinsi mfano wa Yesu wa kujidhabihu ulivyomchochea mwanamume fulani.

“Niliishi Maisha ya Ubinafsi” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 2014)

Ona matukio muhimu ya huduma ya Yesu kwa mfuatano wa jinsi yalivyotokea.

“Matukio Muhimu Katika Maisha ya Yesu Duniani” (Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, Nyongeza A7)

a Somo la 31-33 litazungumzia kuhusu Ufalme wa Mungu kwa undani.