Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 18

Jinsi ya Kuwatambua Wakristo wa Kweli

Jinsi ya Kuwatambua Wakristo wa Kweli

Mabilioni ya watu wanadai kuwa Wakristo. Lakini viwango wanavyofuata maishani na mambo wanayoamini yanatofautiana. Basi, tunawezaje kuwatambua Wakristo wa kweli?

1. Inamaanisha nini kuwa Mkristo?

Wakristo ni wanafunzi au wafuasi wa Yesu Kristo. (Soma Matendo 11:26.) Wanaonyeshaje kwamba wao ni wanafunzi wa Yesu? Yesu alisema: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.” (Yohana 8:31) Hilo linamaanisha kwamba Wakristo wa kweli wanapaswa kutii mafundisho ya Yesu. Kama mafundisho ya Yesu yalivyotegemea Maandiko, mambo ambayo Wakristo wa kweli wanaamini yanapaswa pia kutegemea Biblia.​—Soma Luka 24:27.

2. Wakristo wa kweli wanaonyeshaje upendo?

Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Mpendane kama vile nilivyowapenda.” (Yohana 15:12) Yesu alionyeshaje kwamba anawapenda wanafunzi wake? Alitumia muda pamoja nao, aliwatia moyo na kuwasaidia. Hata alitoa uhai wake kwa ajili yao. (1 Yohana 3:16) Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli hawazungumzi tu kuhusu upendo. Wanaonyesha kupitia maneno na matendo yao kwamba wanapendana.

3. Wakristo wa kweli wanafanya kazi gani kwa bidii?

Yesu aliwapatia wanafunzi wake kazi. ‘Aliwatuma wahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu.’ (Luka 9:2) Wakristo wa mapema hawakuhubiri tu katika sehemu zao za ibada, bali pia walihubiri katika maeneo ya hadharani na kwenye nyumba za watu. (Soma Matendo 5:42; 17:17.) Vivyo hivyo, leo Wakristo wa kweli wanahubiri kweli za Biblia mahali popote ambapo watu wanapatikana. Wanawapenda jirani zao na hivyo wanafurahi kutumia wakati na nguvu zao kutangaza ujumbe wa tumaini na faraja unaopatikana katika Biblia.​—Marko 12:31.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza jinsi Wakristo wa kweli walivyo tofauti na watu ambao hawafuati mfano na mafundisho ya Yesu.

4. Wanatafuta kweli za Biblia

Wakristo wa mapema walithamini Neno la Mungu

Baadhi ya watu wanaodai kuwa Wakristo hawajitahidi kutafuta kweli muhimu za Biblia. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Baadhi ya makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo yamefanyaje iwe vigumu kwa watu kujifunza mambo ambayo Yesu alifundisha?

Yesu alifundisha kweli za Neno la Mungu. Soma Yohana 18:37, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kulingana na maneno ya Yesu, tunawezaje kuwatambua Wakristo “walio upande wa kweli”?

5. Wanahubiri kweli za Biblia

Wakristo wa mapema waliwahubiria wengine

Kabla Yesu hajarudi mbinguni, aliwapatia wanafunzi wake kazi ambayo inaendelea kufanywa mpaka leo. Soma Mathayo 28:19, 20 na Matendo 1:8, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kazi ya kuhubiri ingefanywa kufikia wakati gani, na mpaka wapi?

6. Wanatenda kulingana na mambo wanayohubiri

Ni nini kilichomsadikishia Tom kwamba amewapata Wakristo wa kweli? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, ni nini kilichofanya Tom aache kujihusisha na dini?

  • Kwa nini anaamini kwamba amepata kweli?

Matendo yana nguvu kuliko maneno. Soma Mathayo 7:21, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ni jambo gani lililo muhimu zaidi kwa Yesu​—je, ni mambo tunayodai kuwa tunaamini au ni mambo tunayotenda?

7. Wanapendana

Wakristo wa mapema walipendana

Je, kuna Wakristo ambao wamehatarisha uhai wao kwa ajili ya Wakristo wenzao? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, kwa nini Lloyd alihatarisha uhai wake ili kumlinda Ndugu Johanson?

  • Je, unafikiri alitenda kama Mkristo wa kweli?

Soma Yohana 13:34, 35, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Wanafunzi wa Yesu, yaani, Wakristo wa kweli, wanawatendeaje watu wa jamii au taifa lingine?

  • Wanafanyaje hivyo wakati wa vita?

WATU FULANI HUSEMA: “Wakristo wamefanya mambo mengi mabaya. Je, inawezekana kwamba kuna dini ya kweli miongoni mwao?”

  • Unaweza kumsomea mtu andiko gani linaloonyesha jinsi ya kuwatambua Wakristo wa kweli?

MUHTASARI

Wakristo wa kweli wanafuata mafundisho ya Biblia, wanaonyesha upendo usio na ubinafsi, na kuhubiri kweli za Neno la Mungu.

Ungejibuje?

  • Mambo ambayo Wakristo wa kweli wanaamini yanategemea nini?

  • Ni sifa gani inayowatambulisha Wakristo wa kweli?

  • Wakristo wa kweli wanafanya kazi gani?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Jifunze mengi kuhusu kikundi cha watu wanaojitahidi kufuata mfano na mafundisho ya Yesu Kristo.

Mashahidi wa Yehova Ni Nani? (1:13)

Ona jinsi mwanamke aliyekuwa mtawa Mkatoliki alivyopata “familia ya kweli ya kiroho.”

“Walitumia Biblia Kujibu Maswali Yangu Yote!” (Mnara wa Mlinzi, Aprili 1, 2014)

Jifunze jinsi Wakristo wa kweli wanavyowaonyesha upendo waabudu wenzao wanaohitaji msaada.

Kuwasaidia Ndugu Zetu Msiba Unapotokea​—Kisehemu (3:57)

Chunguza jinsi Wakristo wa mapema na Wakristo wa kweli leo wanavyofanya mambo ambayo Yesu alisema yangewatambulisha wafuasi wake.

“Ni Sifa Gani Zinazowatambulisha Wakristo wa Kweli?” (Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 2012)