SOMO LA 22

Unawezaje Kuwahubiria Wengine Habari Njema?

Unawezaje Kuwahubiria Wengine Habari Njema?

Unapojifunza kweli za Biblia, huenda ukafikiri hivi, ‘Kila mtu anapaswa kujua habari hizi!’ Ni kweli, kila mtu anapaswa kusikia ujumbe huu! Lakini huenda ukaogopa kuwaambia wengine kuhusu mambo unayojifunza. Tutazungumzia jinsi unavyoweza kushinda woga huo na jinsi unavyoweza kufurahia kuanza kuwaambia wengine habari njema za Biblia.

1. Unawezaje kuwaambia watu unaowafahamu mambo unayojifunza?

Wanafunzi wa Yesu walisema hivi: “Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Matendo 4:20) Walipenda sana mambo waliyojifunza hivi kwamba walitamani kuwaambia watu wengi iwezekanavyo mambo hayo. Je, wewe unahisi hivyo pia? Ikiwa ndivyo, tafuta fursa za kuwaambia kwa heshima watu wa familia na marafiki mambo unayojifunza.​—Soma Wakolosai 4:6.

Jinsi unavyoweza kuanza

  • Unapozungumza na watu wa familia yako, anzisha mazungumzo ya Biblia kwa kusema: “Juma hili nilijifunza jambo lenye kupendeza.”

  • Zungumzia andiko lenye kutia moyo pamoja na rafiki ambaye ni mgonjwa au aliye na mahangaiko.

  • Mfanyakazi mwenzako akikuuliza unaendeleaje, mwambie jambo ulilojifunza katika funzo lako la Biblia au kwenye mkutano wa kutaniko.

  • Waonyeshe rafiki zako tovuti ya jw.org/sw.

  • Waalike wengine katika funzo lako la Biblia, au uwaonyeshe jinsi wanavyoweza kuomba funzo la Biblia kwenye tovuti ya jw.org/sw.

2. Kwa nini ni muhimu kujiwekea lengo la kuhubiri pamoja na kutaniko?

Wanafunzi wa Yesu hawakuwahubiria habari njema watu waliowafahamu tu. Yesu aliwatuma “wawili wawili . . . katika kila jiji” ili wahubiri. (Luka 10:1) Utaratibu huo wa kuhubiri uliwapatia watu wengi zaidi nafasi ya kusikia habari njema. Pia, wanafunzi walipata shangwe nyingi kwa kuhubiri pamoja. (Luka 10:17) Je, wewe pia unaweza kujiwekea lengo la kuhubiri pamoja na kutaniko?

CHIMBA ZAIDI

Chunguza jinsi unavyoweza kushinda woga na kupata shangwe inayotokana na kuhubiri habari njema.

3. Yehova atakuwa pamoja nawe

Huenda baadhi ya wanafunzi wa Biblia wanaotaka kuanza kuhubiri, wakahangaishwa na jinsi watu watakavyowaona, au jinsi watu watakavyoitikia ujumbe.

  • Je, wewe unaogopa kuwaambia wengine mambo unayojifunza? Kwa nini?

Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Vijana hao Mashahidi walishindaje woga wao?

Soma Isaya 41:10, kisha mzungumzie swali hili:

  • Sala inaweza kukusaidiaje ikiwa unaogopa kuhubiri?

Je, wajua?

Kabla ya kuanza kuhubiri habari njema, Mashahidi wengi wa Yehova walifikiri hawawezi kamwe kufanya kazi hiyo. Kwa mfano, Sergey alihisi kwamba hafai na ilikuwa vigumu kwake kuzungumza na watu. Lakini baada ya kujifunza Biblia alisema hivi: “Ingawa nilikuwa na woga, nilianza kuwaeleza wengine kuhusu mambo niliyokuwa nikijifunza. Kwa kushangaza, nilipozungumza na wengine kuhusu Biblia nilipata ujasiri zaidi. Pia, imani yangu iliimarika hata zaidi.”

4. Uwe mwenye heshima

Unapowaambia wengine kuhusu habari njema, fikiria jambo utakalosema na jinsi utakavyolisema. Soma 2 Timotheo 2:24 na 1 Petro 3:15, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Unaweza kutumiaje ushauri ulio katika maandiko haya unapozungumza na wengine kuhusu Biblia?

  • Huenda baadhi ya watu wa familia yako na marafiki wasikubaliane na mambo unayowaambia. Unaweza kufanya nini? Utaepuka kufanya nini?

  • Kwa nini ni vizuri kutumia maswali kwa busara badala ya kuwalazimisha waamini mambo unayosema?

5. Kuhubiri habari njema huleta shangwe

Yehova alimpa Yesu kazi ya kuhubiri habari njema. Yesu aliionaje kazi hiyo? Soma Yohana 4:34, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Tunapokula chakula kizuri tunaendeleza uhai wetu na tunapata furaha. Kwa nini Yesu alilinganisha kula chakula na kufanya mapenzi ya Mungu, kutia ndani kuhubiri habari njema?

  • Unafikiri utafurahia mambo gani kwa kuhubiri habari njema?

Mapendekezo

  • Wakati wa mkutano wa katikati ya juma, sikiliza jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo.

  • Zungumza na mwalimu wako kuhusu kujiandikisha ili uwe mwanafunzi kwenye mkutano wa katikati ya juma. Migawo utakayopewa kwenye mkutano huo itakusaidia uwe tayari kuwaambia wengine mambo unayojifunza.

  • Tumia sehemu za “Watu Fulani Husema” au “Huenda Mtu Akauliza” katika masomo haya ili kufanya mazoezi ya kujibu maswali ambayo watu huuliza au unapopingwa.

HUENDA MTU AKAULIZA: “Una habari gani mpya?”

  • Unawezaje kutumia fursa hiyo kumwambia mambo ambayo umejifunza kwenye funzo lako la Biblia?

MUHTASARI

Kuwahubiria wengine habari njema huleta shangwe na huenda ikawa rahisi kuanza kuhubiri kuliko unavyofikiri.

Ungejibuje?

  • Kwa nini unapaswa kuwahubiria wengine habari njema?

  • Unawezaje kufanya hivyo kwa heshima?

  • Unawezaje kushinda woga wowote ulio nao kuhusu kuhubiri?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ona njia nne rahisi unazoweza kutumia kuhubiri habari njema ukitumia kadi ya mawasiliano ya jw.org.

Pendekezo la Kutoa Kadi ya Mawasiliano ya jw.org (1:43)

Jifunze kuhusu sifa nne zinazoweza kukusaidia kuhubiri habari njema.

“Je, Uko Tayari Kuwa Mvuvi wa Watu?” (Mnara wa Mlinzi, Septemba 2020)

Ona mfano wa Biblia unaoweza kutusaidia kuwa na ujasiri wa kuhubiri habari njema hata ikiwa tuna umri mdogo.

Yehova Atakusaidia Uwe Jasiri (11:59)

Ona jinsi unavyoweza kuzungumzia Biblia pamoja na watu wa familia yako ambao bado hawajajifunza kumhusu Yehova.

“Kuifikia Mioyo ya Watu wa Ukoo Wasio Waamini” (Mnara wa Mlinzi, Machi 15, 2014)