SOMO LA 35

Jinsi ya Kufanya Maamuzi Mazuri

Jinsi ya Kufanya Maamuzi Mazuri

Kila mtu hufanya maamuzi. Maamuzi tunayofanya yanaweza kuwa na matokeo mazuri au mabaya na yanaweza kuathiri urafiki wetu na Yehova. Kwa mfano, huenda tukahitaji kuamua mahali tutakapoishi, kazi tutakayofanya, au ikiwa tutafunga ndoa. Tunapofanya maamuzi mazuri, tunakuwa na maisha yenye furaha na tunamfurahisha Yehova.

1. Biblia inaweza kukusaidiaje kufanya maamuzi mazuri?

Kabla ya kufanya uamuzi, sali kwa Yehova umwombe akusaidie kisha uchunguze maoni yake katika Biblia kuhusu jambo hilo. (Soma Methali 2:3-6.) Wakati fulani, Yehova hutuambia jambo hususa la kufanya. Ikiwa kuna amri hususa, jambo la busara ni kutii mwongozo huo.

Namna gani ikiwa hakuna amri hususa katika Biblia kuhusu jambo unalopaswa kufanya? Bado Yehova atakuongoza “katika njia unayopaswa kutembea.” (Isaya 48:17) Jinsi gani? Unaweza kupata kanuni ambazo zitakuongoza. Kanuni za Biblia ni kweli za msingi zinazofunua mawazo na hisia za Mungu. Kwa kawaida tunaelewa maoni ya Mungu kuhusu jambo fulani tunaposoma simulizi la Biblia. Tunapoelewa jinsi Yehova anavyohisi, tunaweza kufanya maamuzi yanayomfurahisha.

2. Unapaswa kufikiria mambo gani kabla ya kufanya uamuzi?

Biblia inasema: “Mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Hilo linamaanisha kwamba kabla ya kufanya uamuzi tunapaswa kufikiria kwa makini mambo yote yanayohusika. Unapochunguza kila jambo, jiulize hivi: ‘Ni kanuni gani za Biblia zinazohusika? Ni uamuzi gani ambao utaniletea amani ya akili? Uamuzi wangu utakuwa na matokeo gani kwa watu wengine? Jambo muhimu zaidi, je, uamuzi huu utamfurahisha Yehova?’​—Kumbukumbu la Torati 32:29.

Yehova ana haki ya kutuamulia mambo mema na mabaya. Tunapoelewa vizuri sheria na kanuni zake na kuazimia kuzifuata, tunazoeza dhamiri yetu. Dhamiri ni uwezo ulio ndani yetu wa kutambua mambo yanayofaa na yasiyofaa. (Waroma 2:14, 15) Tukizoeza dhamiri yetu, itatusaidia kufanya maamuzi mazuri.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi dhamiri na kanuni za Biblia zinavyoweza kutusaidia kufanya maamuzi.

3. Fuata mwongozo wa Biblia

Kanuni za Biblia zinaweza kutusaidiaje kufanya maamuzi? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Yehova ametupatia zawadi gani ya pekee?

  • Kwa nini Yehova alitupatia uhuru wa kujiamulia?

  • Ametupatia nini ili kutusaidia kufanya maamuzi bora?

Ili uone mfano wa kanuni ya Biblia, soma Waefeso 5:15, 16. Kisha mzungumzie jinsi unavyoweza ‘kutumia vizuri kabisa wakati wako’ ili . . .

  • kusoma Biblia kwa ukawaida.

  • kuwa mume, mke, mzazi, mwana, au binti bora.

  • kuhudhuria mikutano ya kutaniko.

4. Zoeza dhamiri yako kufanya maamuzi mazuri

Kunapokuwa na amri hususa ya Maandiko kuhusu jambo, ni rahisi kufanya uamuzi unaofaa. Lakini vipi ikiwa hakuna amri hususa? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Dada katika video hiyo alichukua hatua gani ili kuzoeza dhamiri yake na kufanya uamuzi uliomfurahisha Yehova?

Kwa nini hatupaswi kuwaomba watu wengine watufanyie maamuzi? Soma Waebrania 5:14, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Ingawa huenda ikawa rahisi kuwaomba wengine watufanyie maamuzi, tunapaswa kuwa na uwezo wa kutofautisha nini?

  • Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuzoeza dhamiri yetu na kufanya maamuzi mazuri?

Dhamiri ni kama ramani inayotuongoza kufanya maamuzi maishani

5. Heshimu dhamiri za watu wengine

Maamuzi yetu hutofautiana na maamuzi ya watu wengine. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaheshimu dhamiri za watu wengine? Fikiria hali mbili zinazofuata:

Hali ya 1: Dada anayependa kujipamba anahamia kutaniko ambalo dada wengi wanakwazika wanapoona watu wakijipamba.

Soma Waroma 15:1 na 1 Wakorintho 10:23, 24, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kulingana na maandiko haya, dada huyo anaweza kuamua kufanya nini? Utafanya nini unaposhughulika na mtu ambaye dhamiri yake inamkataza kufanya jambo ambalo dhamiri yako inakubali?

Hali ya 2: Ndugu ambaye anajua kwamba Biblia haikatazi kunywa kileo kwa kiasi, lakini anaamua kutokunywa kileo. Anakaribishwa kwenye tafrija ambapo anaona akina ndugu wakinywa kileo.

Soma Mhubiri 7:16 na Waroma 14:1, 10, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kulingana na maandiko haya, ndugu huyo anaweza kuamua kufanya nini? Utafanya nini ukimwona mtu anafanya jambo ambalo dhamiri yako inakuzuia kufanya?

 Hatua zinazotusaidia kufanya maamuzi mazuri.

1. Mwombe Yehova akusaidie kuamua jambo la kufanya.​—Yakobo 1:5.

2. Fanya utafiti katika Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia ili upate kanuni zinazohusika. Unaweza pia kuzungumza na Wakristo wenye uzoefu.

3. Fikiria matokeo ya uamuzi utakaofanya, yaani, jinsi utakavyoathiri dhamiri yako na dhamiri za watu wengine.

WATU FULANI HUSEMA: “Una haki ya kufanya chochote unachopenda, bila kujali maoni ya watu wengine.”

  • Kwa nini tunapaswa kufikiria maoni ya Mungu, na maoni ya watu wengine?

MUHTASARI

Tunafanya maamuzi mazuri tunapochunguza maoni ya Yehova kuhusu jambo fulani na kufikiria ikiwa maamuzi yetu yatawasaidia watu wengine au kuwasababishia madhara.

Ungejibuje?

  • Unawezaje kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova?

  • Unawezaje kuizoeza dhamiri yako?

  • Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unaheshimu dhamiri za watu wengine?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Unawezaje kufanya maamuzi yatakayoimarisha urafiki wako na Mungu?

“Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima” (Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 2011)

Jifunze jinsi Yehova anavyotupatia ushauri.

Yehova Anawaongoza Watu Wake (9:50)

Ona mambo yaliyomsaidia mwanamume fulani kufanya uamuzi mgumu.

Yehova Anahakikisha Tunapata Mambo Mazuri (5:46)

Jifunze kufanya mambo yanayomfurahisha Yehova hata kama hakuna sheria hususa.

“Je, Sikuzote Unahitaji Amri ya Biblia?” (Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 2003)