SOMO LA 44

Je, Sherehe Zote Zinamfurahisha Mungu?

Je, Sherehe Zote Zinamfurahisha Mungu?

Yehova anataka tufurahie maisha na tuwe na pindi za kusherehekea. Lakini, je, sherehe na sikukuu zote zinamfurahisha? Tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda Yehova inapohusu sherehe na sikukuu?

1. Kwa nini sikukuu nyingi hazimfurahishi Yehova?

Huenda ukashangaa kujua kwamba sikukuu nyingi hazitegemei mafundisho ya kimaandiko au zina asili ya kipagani. Sikukuu hizo zinahusiana na dini za uwongo. Huenda zinahusiana na zoea la kuwasiliana na roho waovu, au zinaunga mkono fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa. Baadhi ya sherehe hizo zinahusiana na ushirikina au itikadi ya bahati. (Isaya 65:11) Yehova anawaamuru hivi waabudu wake: ‘Jitengeni na mwache kugusa kitu kichafu.’​—2 Wakorintho 6:17. a

2. Yehova anahisije kuhusu sherehe zinazowatukuza wanadamu?

Yehova anatuonya ili tusinaswe na mtego wa ‘kuwatumaini wanadamu.’ (Soma Yeremia 17:5.) Baadhi ya sikukuu huwatukuza watawala au wanajeshi. Sherehe nyingine hutukuza nembo za taifa au uhuru wa nchi. (1 Yohana 5:21) Na sherehe nyingine hutukuza harakati za kisiasa au za kijamii. Yehova atahisije ikiwa tutamtukuza mtu au shirika fulani, hasa ikiwa mtu au shirika hilo linaendeleza mawazo yaliyo kinyume na kusudi lake?

3. Ni tabia gani zinazoweza kufanya sherehe zisikubalike?

Biblia inakataza “kunywa kupita kiasi, karamu zenye vurugu, [na] mashindano ya kunywa.” (1 Petro 4:3) Katika sherehe fulani, watu hutenda jinsi wanavyotaka na kujihusisha na upotovu wa maadili. Ili tuendelee kuwa rafiki za Yehova, tunahitaji kujitenga kabisa na ukosefu huo wa maadili.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi unavyoweza kumfurahisha Yehova kwa kufanya maamuzi ya hekima kuhusu sikukuu na sherehe.

4. Epuka sherehe zinazomvunjia Yehova heshima

Soma Waefeso 5:10, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Tunapaswa kuhakikisha nini tunapoamua ikiwa tutasherehekea sikukuu fulani?

  • Ni sikukuu gani ambazo ni maarufu katika eneo unaloishi?

  • Je, unafikiri sikukuu hizo zinamfurahisha Yehova?

Kwa mfano, umewahi kujiuliza Mungu ana maoni gani kuhusu sherehe za siku ya kuzaliwa? Biblia haitaji hata mwabudu mmoja wa Yehova ambaye alisherehekea siku ya kuzaliwa, lakini inataja sherehe mbili za siku ya kuzaliwa ambazo zilisherehekewa na watu ambao hawakumwabudu Yehova. Soma Mwanzo 40:20-22 na Mathayo 14:6-10. Kisha mzungumzie maswali haya:

  • Sherehe hizo mbili za siku ya kuzaliwa zina mambo gani yanayofanana?

  • Kulingana na masimulizi hayo ya Biblia, unafikiri Yehova ana maoni gani kuhusu sherehe za siku ya kuzaliwa?

Lakini bado huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli Yehova anajali ikiwa nitasherehekea siku ya kuzaliwa au sherehe nyingine isiyopatana na Maandiko?’ Soma Kutoka 32:1-8. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Kwa nini tunapaswa kuhakikisha kwamba tunafanya mambo yanayokubalika kwa Yehova?

  • Tunawezaje kufanya hivyo?

Jinsi tunavyoweza kujua ikiwa sherehe fulani haimfurahishi Mungu

  • Je, inategemea mafundisho yasiyopatana na Maandiko? Ili kujua, chunguza chanzo chake.

  • Je, inawatukuza wanadamu, mashirika, au nembo za taifa? Tunamtukuza Yehova peke yake, na tunaamini kwamba yeye ndiye anayeweza kusuluhisha matatizo ulimwenguni.

  • Je, desturi na mazoea yake yanapingana na viwango vya Biblia? Tunapaswa kuendelea kuwa safi kiadili.

5. Wasaidie wengine waheshimu imani yako

Huenda ikawa vigumu kukataa wengine wanapokushinikiza ushiriki katika sherehe ambazo hazimfurahishi Yehova. Waeleze maamuzi yako kwa subira na kwa busara. Ili kuona mfano wa jinsi unavyoweza kufanya hivyo, onyesha VIDEO.

Soma Mathayo 7:12, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kulingana na mstari huu, je, unapaswa kuwaambia watu wa familia yako wasio waamini kwamba hawapaswi kusherehekea sikukuu fulani?

  • Unaweza kufanya nini ili kuwahakikishia watu wa familia yako kwamba ingawa hutasherehekea pamoja nao, bado unawapenda na kuwajali?

6. Yehova anataka tuwe na furaha

Yehova anataka tuwe na pindi zenye kufurahisha pamoja na marafiki na watu wa familia zetu. Soma Mhubiri 8:15, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mstari huu unaonyeshaje kwamba Yehova anataka tuwe na furaha?

Yehova anataka watu wake wawe na wakati mzuri wa kufurahia maisha pamoja. Onyesha VIDEO ili uone jinsi jambo hilo linavyoonekana wazi wakati wa makusanyiko yetu ya kimataifa.

Soma Wagalatia 6:10, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, tunahitaji kusherehekea sikukuu zilizo maarufu ili kuonyesha kwamba ‘tunawatendea wengine mema?’

  • Ni jambo gani ambalo lingekuletea furaha zaidi, je, ni kulazimika kutoa zawadi kwa sababu ni wakati wa sikukuu, au kutoa zawadi wakati wowote?

  • Mara kwa mara, Mashahidi wa Yehova hupanga pindi za pekee kwa ajili ya watoto wao na hata kuwapa zawadi wakati wowote. Ikiwa una watoto, ni mambo gani ya pekee unayoweza kuwafanyia?

WATU FULANI HUSEMA: “Vyanzo vya sikukuu si muhimu. Jambo muhimu ni kuwa na muda wa kufurahia pamoja na familia na marafiki.”

  • Wewe una maoni gani?

MUHTASARI

Yehova anataka tuwe na pindi za furaha pamoja na familia na marafiki. Lakini pia anataka tuepuke sikukuu ambazo hazimfurahishi.

Ungejibuje?

  • Tunapaswa kujiuliza maswali gani ili kujua ikiwa sherehe fulani haimfurahishi Yehova?

  • Tunawezaje kuwasaidia marafiki na watu wa familia zetu waelewe maamuzi yetu kuhusu sikukuu?

  • Tunajuaje kwamba Yehova anataka tuwe na pindi za kufurahia maisha?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza sababu nne zinazofanya tuamini kwamba sherehe za siku ya kuzaliwa hazimfurahishi Mungu.

“Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Siku za Kuzaliwa?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Ona jinsi kijana fulani alivyotenda kwa busara alipodhihakiwa shuleni kwa sababu hasherehekei Krismasi.

Tenda kwa Busara Unapodhihakiwa (2:04)

Mamilioni ya Wakristo wameamua kwamba hawatasherehekea Krismasi. Wanahisije kuhusu uamuzi wao?

“Wamepata Jambo Bora Kuliko Krismasi” (Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 2012)

a Chunguza Maelezo ya Ziada 5 ili uone jinsi unavyoweza kutenda watu wanaposherehekea sikukuu.