Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 48

Chagua Marafiki Wako kwa Hekima

Chagua Marafiki Wako kwa Hekima

Tunafurahi kushirikiana na marafiki wazuri katika pindi za furaha. Pia, marafiki wazuri hutuimarisha tunapokabili matatizo. Lakini Biblia inatuonya kwamba si kila mtu anafaa kuwa rafiki yetu wa karibu. Basi unawezaje kuchagua marafiki wazuri? Fikiria maswali yafuatayo.

1. Marafiki unaochagua wanaathirije tabia yako?

Sisi huiga tabia za watu tunaoshirikiana nao. Tunaweza kuiga tabia nzuri au mbaya, iwe tunashirikiana nao moja kwa moja au kwenye mitandao ya kijamii. Biblia inasema hivi: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu [wale ambao hawampendi Yehova] ataumia.” (Methali 13:20) Marafiki wanaompenda na kumwabudu Yehova wanaweza kukusaidia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye, na kukusaidia kufanya maamuzi mazuri. Lakini tukishirikiana kwa ukaribu na watu ambao hawampendi Yehova, uhusiano wetu pamoja na Yehova utadhoofika. Ndiyo sababu Biblia inatutia moyo tuchague marafiki kwa hekima! Ikiwa marafiki wetu wanampenda Mungu, tutanufaika tunaposhirikiana nao, nao watanufaika pia. Kwa kufanya hivyo, ‘tutaendelea kutiana moyo na kujengana.’​—1 Wathesalonike 5:11.

2. Yehova anahisije kuhusu marafiki unaochagua?

Yehova huchagua marafiki wake kwa makini. “Ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.” (Methali 3:32) Yehova atahisije ikiwa tutachagua marafiki ambao hawampendi? Atahuzunika sana! (Soma Yakobo 4:4.) Lakini ili tumfurahishe Yehova na tuwe rafiki zake, tunapaswa kuepuka kushirikiana na watu wenye mazoea mabaya. Tunapaswa kumkaribia Yehova na kushirikiana na wale wanaompenda.​—Zaburi 15:1-4.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza kwa nini ni muhimu kuchagua marafiki wanaofaa na uone jinsi ya kujenga urafiki utakaokunufaisha.

3. Epuka kushirikiana na watu wabaya

Watu wasiompenda Mungu na viwango vyake si marafiki wazuri. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Tunawezaje kuanza kushirikiana na watu wabaya bila kujua?

Soma 1 Wakorintho 15:33, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Ni watu gani ambao hupaswi kushirikiana nao? Kwa nini?

Soma Zaburi 119:63, kisha mzungumzie swali hili:

  • Unapaswa kuchagua marafiki wa aina gani?

Tunda moja lililooza linaweza kuharibu matunda mengine yote. Rafiki mmoja mbaya anawezaje kukuathiri?

4. Tunaweza kuchagua marafiki wenye umri na hali mbalimbali

Biblia inazungumza kuhusu Daudi na Yonathani, wanaume walioishi katika taifa la kale la Israeli. Umri wao na hali zao zilitofautiana sana, lakini walikuwa marafiki wa karibu. Soma 1 Samweli 18:1, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini hatupaswi kuchagua tu marafiki wenye umri au hali kama zetu?

Soma Waroma 1:11, 12, kisha mzungumzie swali hili:

  • Marafiki wanaompenda Yehova wanaweza kutiana moyo jinsi gani?

Katika video inayofuata, ona jinsi ndugu mmoja kijana alivyopata marafiki mahali asipotarajia. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, kwa nini wazazi wa Akil walikuwa na wasiwasi kuhusu marafiki alioshirikiana nao shuleni?

  • Kwa nini mwanzoni alivutiwa na marafiki hao?

  • Ni nini ambacho kilimsaidia kushinda hisia za upweke?

5. Jinsi ya kusitawisha urafiki mzuri

Jifunze jinsi unavyoweza kupata marafiki wazuri, na jinsi unavyoweza kuwa rafiki mzuri. Onyesha VIDEO.

Soma Methali 18:24 na 27:17, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Marafiki wa kweli wanawezaje kusaidiana?

  • Je, una marafiki wazuri kama hao? Ikiwa huna, unawezaje kusitawisha urafiki kama huo?

Soma Wafilipi 2:4, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ili uwe na marafiki wazuri, unapaswa kuwa rafiki mzuri. Unawezaje kuwa rafiki mzuri?

Ili uwe na marafiki wazuri, unapaswa kuwa rafiki mzuri

WATU FULANI HUSEMA: “Bora kuwa na rafiki yeyote kuliko kukosa rafiki.”

  • Wewe una maoni gani?

MUHTASARI

Tunapochagua marafiki kwa hekima, tunamfurahisha Yehova na kujinufaisha pia.

Ungejibuje?

  • Kwa nini Yehova angependa tuchague marafiki wazuri?

  • Tunapaswa kuepuka marafiki wa aina gani?

  • Unawezaje kusitawisha urafiki imara na watu wanaofaa?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ona jinsi marafiki wazuri wanavyoweza kutusaidia wakati wa matatizo.

“Imarisha Urafiki Wako Pamoja na Wengine Kabla ya Mwisho Kufika” (Mnara wa Mlinzi, Novemba 2019)

Unapaswa kujua nini kuhusu kuwa na marafiki kwenye mitandao ya kijamii?

Tumia Mitandao ya Kijamii kwa Hekima (4:12)

Katika simulizi “Nilitamani Sana Kuwa na Baba,” ona sababu zilizofanya mwanamume fulani atafute marafiki wapya.

“Biblia Inabadili Maisha” (Mnara wa Mlinzi, Aprili 1, 2012)