Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 49

Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha—Sehemu ya 1

Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha—Sehemu ya 1

Mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa hivi karibuni, hutumaini kwamba furaha waliyokuwa nayo siku ya harusi itadumu milele. Na hilo linawezekana. Wakristo ambao wamekuwa katika ndoa kwa muda mrefu, na ambao wamejitahidi kabisa kufuata ushauri wa Biblia wanajua kwamba hilo linawezekana.

1. Biblia inatoa ushauri gani kwa waume?

Yehova amempa mume jukumu la kuwa kichwa cha familia. (Soma Waefeso 5:23.) Yehova anatarajia mume afanye maamuzi yatakayoinufaisha familia. Biblia inawashauri hivi waume: “Endeleeni kuwapenda wake zenu.” (Waefeso 5:25) Hilo linamaanisha nini? Mume mwenye upendo humtendea mke wake kwa fadhili wanapokuwa nyumbani na pia hadharani. Anahakikisha kwamba mke wake yuko salama na anafanya yote anayoweza ili kumtimizia mahitaji yake ya kimwili na ya kihisia. (1 Timotheo 5:8) Jambo muhimu zaidi, anamsaidia mke wake kusitawisha urafiki wa karibu na Yehova. (Mathayo 4:4) Kwa mfano, anaweza kusali na kusoma Biblia pamoja na mke wake. Mume anapomtendea mke wake kwa upendo na kumjali, anadumisha urafiki mzuri na Yehova.​—Soma 1 Petro 3:7.

2. Biblia inawapa wake ushauri gani?

Neno la Mungu linasema “mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Anawezaje kufanya hivyo? Anaweza kufikiria sifa nzuri za mume wake na jitihada anazofanya ili kumtunza yeye na watoto wao. Anaonyesha heshima kwa kuunga mkono maamuzi ya mume wake na kuzungumza naye kwa fadhili. Pia, anasema mambo mazuri kumhusu mume wake anapozungumza na watu wengine, hata kama mume wake si mwabudu wa Yehova.

3. Mume na mke wanawezaje kuimarisha ndoa yao?

Biblia inasema hivi kuhusu watu waliofunga ndoa: “Hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Mathayo 19:5) Hilo linamaanisha kwamba wanapaswa kujitahidi sana kuepuka jambo lolote linaloweza kudhoofisha upendo kati yao. Wanafanya hivyo kwa kutumia muda mwingi pamoja, na pia kuzungumza waziwazi na kwa upendo kuhusu mawazo na hisia zao. Hawaruhusu mtu au kitu kingine chochote kuwa muhimu kuliko mwenzi wao wa ndoa, isipokuwa Yehova. Wanakuwa waangalifu sana ili wasisitawishe uhusiano usiofaa na mtu mwingine yeyote.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze kanuni za Biblia ambazo zinaweza kuimarisha ndoa yenu.

4. Mume​—mpende na kumjali mke wako

Biblia inasema kwamba “waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28, 29) Hilo linamaanisha nini? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Ni kwa njia gani mume anaweza kuonyesha kwamba anampenda na kumjali mke wake?

Soma Wakolosai 3:12, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mume anawezaje kuonyesha sifa hizi katika ndoa yake?

5. Mke​—mpende na kumheshimu mume wako

Biblia inamtia moyo mke amheshimu mume wake, iwe mume ni mtumishi wa Yehova au la. Soma 1 Petro 3:1, 2, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Ikiwa mume wako si mwamini, bila shaka unatamani sana awe mwabudu wa Yehova. Unafikiri ni njia gani nzuri ya kumsaidia, je, ni kumhubiria kila wakati au ni kuwa mke mwenye fadhili, heshima, na tabia nzuri? Kwa nini?

Mume na mke wanaweza kufanya maamuzi mazuri pamoja. Hata hivyo, wakati mwingine huenda mke asikubaliane na maoni ya mume wake. Katika hali hiyo, mke anaweza kueleza maoni yake kwa utulivu na heshima, lakini anapaswa kutambua kwamba Yehova amempa mume jukumu la kufanya maamuzi yatakayoinufaisha familia. Mke anapaswa kufanya yote anayoweza ili kuunga mkono uamuzi wa mume wake. Akifanya hivyo, atachangia mazingira yenye furaha nyumbani. Soma 1 Petro 3:3-5, kisha mzungumzie swali hili:

  • Yehova anahisije mke anapomheshimu mume wake?

6. Mnaweza kushinda matatizo katika ndoa

Hakuna ndoa iliyo kamilifu. Kwa hiyo, mume na mke wanapaswa kushirikiana ili kushinda matatizo. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, ni mambo gani yanayoonyesha kwamba uhusiano kati ya mume na mke ulianza kudhoofika?

  • Walifanya nini ili kuimarisha ndoa yao?

Soma 1 Wakorintho 10:24 na Wakolosai 3:13. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:

  • Kufuata ushauri huo kunawezaje kuimarisha ndoa?

Biblia inasema kwamba tunapaswa kuheshimiana. Kumheshimu mtu kunatia ndani kumtendea kwa njia ya fadhili na staha. Soma Waroma 12:10, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, mume au mke anapaswa kutarajia kwamba mwenzi wake ndiye anayepaswa kuwa wa kwanza kuonyesha heshima? Kwa nini?

WATU FULANI HUSEMA: “Mimi na mwenzi wangu hatuna uhusiano wa karibu kama zamani.”

  • Unawezaje kuwaeleza kwamba Biblia inaweza kuwasaidia?

MUHTASARI

Mume na mke wanaweza kuwa na furaha ikiwa wanapendana, wanaheshimiana, na kutumia kanuni za Biblia.

Ungejibuje?

  • Mume anawezaje kuchangia furaha katika ndoa?

  • Mke anawezaje kuchangia furaha katika ndoa?

  • Ikiwa umefunga ndoa, ni kanuni gani ya Biblia inayoweza kuimarisha ndoa yenu?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Jifunze mapendekezo yanayoweza kuwasaidia muwe na familia yenye furaha.

Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha (broshua)

Tazama video ya muziki inayoonyesha baraka za kufuata ushauri wa Mungu katika ndoa.

Nimezama Katika Mapenzi (4:26)

Wenzi hawa wa ndoa waliwezaje kushinda matatizo makubwakutia ndani kutalikiana?

Tulijenga Upya Ndoa Yetu Kwa Msaada wa Mungu (5:14)