Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 51

Unawezaje Kumfurahisha Yehova Kupitia Mazungumzo Yako?

Unawezaje Kumfurahisha Yehova Kupitia Mazungumzo Yako?

Yehova alipotuumba alitupatia zawadi nzuri sana, yaani, uwezo wa kuzungumza. Je, anajali jinsi tunavyotumia zawadi hiyo? Bila shaka, anajali! (Soma Yakobo 1:26.) Basi, tunawezaje kutumia uwezo wetu wa kuzungumza kwa njia inayomfurahisha Yehova?

1. Tunawezaje kutumia vizuri zawadi ya kuzungumza?

Biblia inatuambia hivi: “Endeleeni kutiana moyo na kujengana.” (1 Wathesalonike 5:11) Je, kuna watu ambao unafikiri wanahitaji kutiwa moyo? Unaweza kufanya nini ili kuwatia moyo? Wahakikishie kwamba unawajali. Labda unaweza kuwaambia mambo mazuri unayopenda kuwahusu. Je, kuna andiko ambalo linaweza kumtia moyo mtu fulani unayemjua? Kuna maandiko mengi ambayo unaweza kutumia. Kumbuka kwamba unaweza pia kuwatia moyo sana kupitia jinsi unavyozungumza nao. Basi, sikuzote jitahidi kuzungumza kwa fadhili na upole.​​—Methali 15:1.

2. Tunapaswa kuepuka mazungumzo ya aina gani?

Biblia inasema: “Neno lililooza lisitoke kinywani mwenu.” (Soma Waefeso 4:29.) Hilo linamaanisha kwamba hatupaswi kutumia lugha chafu, au kusema maneno yasiyo ya fadhili, yenye kuudhi, yanayokusudiwa kuumiza hisia za mtu mwingine. Pia, tunapaswa kuepuka kupiga porojo na kuwachongea wengine.​—Soma Methali 16:28.

3. Ni nini ambacho kitatusaidia kuzungumza kwa njia itakayowajenga wengine?

Mara nyingi mambo tunayosema yanafunua kile kilicho moyoni mwetu au jambo ambalo tunafikiria. (Luka 6:​45) Basi, tunapaswa kujizoeza kufikiria mambo yenye kujenga, yaani, mambo yaliyo ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, yanayopendeka, na yanayostahili sifa. (Wafilipi 4:8) Ili tukazie fikira mambo hayo, tunapaswa kuchagua burudani na marafiki wetu kwa hekima. (Methali 13:20) Pia, tunahitaji kufikiria kwa makini mambo tutakayosema kabla ya kuzungumza. Fikiria jinsi maneno yako yatakavyowaathiri wengine. Biblia inasema hivi: “Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.”​—Methali 12:18.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze kuzungumza kwa njia itakayomfurahisha Yehova na itakayowatia moyo wengine.

4. Uwe mwangalifu kuhusu mambo unayosema

Wakati fulani, sisi husema mambo bila kufikiri na kujuta baadaye. (Yakobo 3:2) Soma Wagalatia 5:22, 23, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kati ya sifa hizo, unaweza kumwomba Yehova akupe sifa gani ambazo zitakusaidia kudhibiti mambo unayosema? Sifa hizo zinawezaje kukusaidia?

Soma 1 Wakorintho 15:33, kisha mzungumzie swali hili:

  • Njia yako ya kuzungumza inaweza kuathiriwaje na burudani na marafiki unaochagua?

Soma Mhubiri 3:1, 7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ni wakati gani ambao huenda ikawa jambo la hekima kukaa kimya au kusubiri wakati unaofaa ili kuzungumza?

5. Sema mambo mazuri kuwahusu wengine

Tunawezaje kuepuka kusema mambo yanayowaumiza wengine au kusema mambo yasiyo ya fadhili? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

  • Katika video hiyo, kwa nini ndugu huyo alitaka kubadili jinsi alivyozungumza kuhusu wengine?

  • Alifanya nini ili abadili njia yake ya kuzungumza?

Soma Mhubiri 7:16, kisha mzungumzie swali hili:

  • Tunapaswa kukumbuka nini tunaposhawishiwa kusema mambo yasiyofaa kuhusu mtu mwingine?

Soma Mhubiri 7:21, 22, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mistari hii inawezaje kukusaidia usikasirike mtu anaposema mambo yasiyofaa kukuhusu?

6. Uwe na fadhili unapozungumza na watu wa familia yako

Yehova anataka tuzungumze na watu wa familia yetu kwa njia ya fadhili na upendo. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Ni nini ambacho kitakusaidia uzungumze kwa fadhili na watu wa familia yako?

Soma Waefeso 4:31, 32, kisha mzungumzie swali hili:

  • Tunaweza kuzungumza jinsi gani na watu wa familia yetu ili kuwajenga?

Yehova alionyesha jinsi alivyohisi kumhusu Yesu, Mwana wake. Soma Mathayo 17:5, kisha mzungumzie swali hili:

  • Unawezaje kumwiga Yehova unapozungumza na watu wa familia yako?

Tafuta fursa za kuwapongeza wengine

WATU FULANI HUSEMA: “Mimi husema ninachofikiria. Sijali wengine watahisije.”

  • Je, unakubaliana na maoni hayo? Kwa nini?

MUHTASARI

Maneno yana nguvu. Tunapaswa kufikiria kwa makini mambo tunayosema, wakati wa kuyasema, na jinsi tunavyoyasema.

Ungejibuje?

  • Unaweza kutumia njia gani kuzungumza mambo yanayowajenga wengine?

  • Tunapaswa kuepuka mazungumzo ya aina gani?

  • Ni nini ambacho kitatusaidia ili sikuzote tuzungumze kwa njia ya fadhili na inayojenga?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ni nini ambacho kitatusaidia kuzungumza kwa njia inayowajenga wengine?

Sitawisha Ulimi wa Wenye Hekima (8:04)

Jifunze mambo yatakayokusaidia kuepuka lugha chafu.

“Je, Kweli Kutumia Lugha Chafu Ni Vibaya?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Jifunze jinsi unavyoweza kuepuka kunaswa na mtego wa kupiga porojo.

Ninawezaje Kuepuka Kupiga Porojo? (2:36)

Ona jinsi Yehova alivyomsaidia mwanamume fulani aache kutumia lugha chafu.

“Nilianza Kufikiria kwa Uzito Mwelekeo wa Maisha Yangu” (Mnara wa Mlinzi, Agosti 1, 2013)