Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 59

Unaweza Kuvumilia Mateso

Unaweza Kuvumilia Mateso

Wakristo wote wanatarajia kwamba watakabili upinzani au hata mateso. Je, hilo linapaswa kutuogopesha?

1. Kwa nini tunatarajia kuteswa?

Biblia inasema hivi waziwazi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Yesu aliteswa kwa sababu hakuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Sisi pia si sehemu ya ulimwengu, kwa hiyo hatushangai tunapoteswa na serikali za wanadamu au mashirika ya kidini.​—Yohana 15:18, 19.

2. Tunawezaje kujitayarisha kwa ajili ya mateso?

Sasa ndio wakati wa kujifunza kumtegemea Yehova kabisa. Tenga muda kila siku ili kusali kwake na kusoma Neno lake. Hudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida. Kufanya mambo hayo kutakupatia nguvu unazohitaji ili ukabili mateso kwa ujasiri, hata kama yanatoka kwa watu wa familia yako. Mtume Paulo, ambaye aliteswa mara nyingi, aliandika hivi: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”​—Waebrania 13:6.

Tunaweza pia kuimarisha ujasiri wetu kwa kuhubiri kwa ukawaida. Tunapohubiri tunajifunza kumtegemea Yehova na kuepuka mtego wa kuwaogopa wanadamu. (Methali 29:25) Ukisitawisha ujasiri wa kuhubiri sasa, utakuwa tayari kuendelea kuhubiri hata ikiwa serikali itajaribu kutuzuia kuhubiri.​—1 Wathesalonike 2:2.

3. Tunanufaikaje tunapovumilia mateso?

Bila shaka, hatufurahi tunapoteswa, lakini tunapovumilia mateso, imani yetu inaimarika. Tunamkaribia Yehova kwa sababu tunajionea jinsi anavyotusaidia tunapohisi kwamba hatuna nguvu za kuendelea kuvumilia. (Soma Yakobo 1:2-4.) Yehova anaumia anapoona tukiteseka, lakini anafurahi kuona tukivumilia. Biblia inasema hivi: “Ikiwa mnavumilia mateso kwa sababu ya kufanya mema, jambo hilo linakubalika kwa Mungu.” (1 Petro 2:20) Tukiendelea kuvumilia kwa uaminifu, Yehova atatupatia thawabu ya kuishi milele katika ulimwengu ambao tutamwabudu bila upinzani wowote.​—Mathayo 24:13.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze jinsi tunavyoweza kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova hata tunapokabili mateso, na baraka ambazo tutapata kwa kufanya hivyo.

4. Unaweza kuvumilia upinzani kutoka kwa watu wa familia

Yesu alijua kwamba baadhi ya watu katika familia zetu watajaribu kutuzuia kumwabudu Yehova. Soma Mathayo 10:34-36, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mtu anapoamua kumtumikia Yehova, watu wa familia yake wanaweza kumtendeaje?

Ili uone mfano wa jambo hilo, onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Utafanya nini ikiwa mtu wa familia au rafiki atajaribu kukuzuia kumtumikia Yehova?

Soma Zaburi 27:10 na Marko 10:29, 30. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:

  • Ahadi hii inawezaje kukusaidia unapokabili upinzani kutoka kwa watu wa familia au marafiki?

5. Endelea kumwabudu Yehova licha ya kuteswa

Tunahitaji ujasiri ili kumtumikia Yehova watu wengine wanapojaribu kutuzuia kumtumikia. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Mfano uliowekwa na akina ndugu na dada katika video hiyo unakuimarishaje?

Soma Matendo 5:27-29 na Waebrania 10:24, 25. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:

  • Kwa nini ni muhimu sana kuendelea kumwabudu Yehova hata ikiwa serikali inatuzuia kuhubiri au kuhudhuria mikutano?

6. Yehova atakusaidia uvumilie

Mashahidi wa Yehova wenye umri na malezi mbalimbali wameendelea kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu hata wanapoteswa. Ili uone jambo lililowasaidia, onyesha VIDEO. Kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Katika video hiyo, ni nini kilichowasaidia Mashahidi hao kuvumilia?

Soma Waroma 8:35, 37-39 na Wafilipi 4:13. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:

  • Andiko hili linakuhakikishiaje kwamba unaweza kuvumilia jaribu lolote?

Soma Mathayo 5:10-12, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini unaweza kuwa na furaha hata unapoteswa?

Mamilioni ya watumishi wa Yehova wameendelea kumtumikia kwa uaminifu licha ya upinzani. Wewe pia unaweza!

WATU FULANI HUSEMA: “Mimi siwezi kuvumilia mateso.”

  • Ni maandiko gani yanayoweza kuwasaidia watu hao kupata ujasiri?

MUHTASARI

Yehova anathamini jitihada zetu za kumtumikia licha ya mateso. Kwa msaada wake, tunaweza kufanikiwa kuvumilia!

Ungejibuje?

  • Kwa nini Wakristo wanapaswa kutarajia kwamba watateswa?

  • Unaweza kufanya nini sasa ili uwe tayari utakapokabili mateso?

  • Ni nini kinachoweza kukusaidia uwe na uhakika kwamba unaweza kuendelea kumtumikia Yehova hata unapokabili jaribu lolote?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ona ndugu kijana akieleza jinsi Yehova alivyomsaidia kuvumilia alipofungwa gerezani kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote.

Kuvumilia Licha ya Mnyanyaso (2:34)

Ona jambo lililowasaidia wenzi fulani wa ndoa waendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi licha ya upinzani.

Kumtumikia Yehova Wakati wa Mabadiliko (7:15)

Jifunze jinsi unavyoweza kukabili mateso kwa ujasiri.

“Jitayarishe Sasa kwa Ajili ya Mateso” (Mnara wa Mlinzi, Julai 2019)

Tunapaswa kuonaje upinzani kutoka kwa watu wa familia, na tunawezaje kufanikiwa kukabiliana na hali hiyo?

“Kweli Huleta, ‘Si Amani, Bali Upanga’” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 2017)