Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maelezo ya Ziada

Maelezo ya Ziada
  1.  Jinsi ya Kumtambua Babiloni Mkubwa

  2.  Masihi Angetokea Lini?

  3.  Matibabu Yanayohusisha Damu

  4.  Mume na Mke Kutengana

  5.  Sikukuu na Sherehe

  6.  Magonjwa ya Kuambukiza

  7.  Masuala ya Kibiashara na Kisheria

 1. Jinsi ya Kumtambua Babiloni Mkubwa

Tunajuaje kwamba “Babiloni Mkubwa” anawakilisha dini zote za uwongo? (Ufunuo 17:5) Fikiria mambo yafuatayo:

  • Anapatikana ulimwenguni pote. Babiloni Mkubwa anafafanuliwa kuwa mwanamke aliyeketi juu ya “umati na mataifa.” Ana “ufalme juu ya wafalme wa dunia.”​—Ufunuo 17:15, 18.

  • Yeye si mfumo wa kisiasa au wa kibiashara. “Wafalme wa dunia” na “wafanyabiashara” hawaangamizwi pamoja naye.​—Ufunuo 18:9, 15.

  • Anapotosha ukweli kumhusu Mungu. Anaitwa kahaba kwa sababu anafanya mapatano na serikali za ulimwengu ili ajinufaishe kifedha na kwa njia nyingine. (Ufunuo 17:1, 2) Anawapotosha watu wa mataifa yote. Na amesababisha vifo vya watu wengi.​—Ufunuo 18:23, 24.

Rudi kwenye somo la 13 jambo kuu la 6

 2. Masihi Angetokea Lini?

Biblia ilitabiri kwamba majuma 69 yangepita kabla ya Masihi kutokea.—Soma Danieli 9:25.

  • Majuma 69 yalianza lini? Yalianza mwaka wa 455 K.W.K. Wakati huo, Gavana Nehemia aliwasili Yerusalemu ili “kurudisha na kujenga upya” jiji hilo.​—Danieli 9:25; Nehemia 2:1, 5-8.

  • Yale majuma 69 yalikuwa na urefu gani? Katika baadhi ya unabii wa Biblia, siku moja huwakilisha mwaka mmoja. (Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6) Basi, juma moja linawakilisha miaka saba. Katika unabii huu, majuma 69 ni miaka 483 (yaani, 69 mara 7).

  • Yale majuma 69 yaliisha lini? Tukihesabu miaka 483 kuanzia mwaka wa 455 K.W.K. tunafika kwenye mwaka wa 29 W.K. a Huo ndio mwaka hususa ambao Yesu alibatizwa na kuwa Masihi!​—Luka 3:1, 2, 21, 22.

Rudi kwenye somo la 15 jambo kuu la 5

 3. Matibabu Yanayohusisha Damu

Matibabu fulani yanahusisha kutumia damu ya mgonjwa. Wakristo hawakubali baadhi ya matibabu hayo. Kwa mfano, kutoa mchango wa damu au mtu kuhifadhi damu yake kabla ya kufanyiwa upasuaji.​—Kumbukumbu la Torati 15:23.

Hata hivyo, huenda matibabu mengine yakakubalika. Matibabu hayo yanatia ndani kutoa damu ili ifanyiwe vipimo, kuchuja na kusafisha damu (hemodialysis), uzimuaji wa damu (hemodilution), kutumia mashine ya uokoaji wa chembe za damu (cell-salvage) na mashine ya kusaidia moyo au mapafu kufanya kazi (heart-lung bypass machine). Kila Mkristo anapaswa kuamua mwenyewe jinsi damu yake itakavyotumiwa wakati wa matibabu, jinsi itakavyofanyiwa vipimo, au ikiwa itatolewa na kurudishwa mwilini bila kuhifadhiwa. Huenda kila daktari akatumia mbinu hizo kwa njia tofauti. Hivyo, Mkristo anapaswa kujua vizuri jinsi ambavyo damu yake itatumiwa kabla ya kukubali kufanyiwa upasuaji, vipimo, au matibabu yoyote. Fikiria maswali yafuatayo:

  • Namna gani ikiwa damu yangu itaelekezwa nje ya mwili wangu na kukatiza mzunguko wa damu kwa muda fulani? Je, dhamiri yangu itaniruhusu kuona damu hiyo kuwa bado sehemu ya mwili wangu na kwamba haipaswi ‘kumwagwa ardhini’?​—Kumbukumbu la Torati 12:23, 24.

  • Namna gani ikiwa wakati wa matibabu kiasi fulani cha damu yangu kitatolewa ili kuboreshwa kisha kirudishwe mwilini mwangu? Je, hilo litasumbua dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia, au nitakubali matibabu hayo?

Rudi kwenye somo la 39 jambo kuu la 3

 4. Mume na Mke Kutengana

Neno la Mungu linahimiza mume na mke wasitengane na linasema waziwazi kwamba kutengana hakumpi yeyote kati yao haki ya kuoa au kuolewa tena. (1 Wakorintho 7:10, 11) Hata hivyo, baadhi ya Wakristo wameamua kutengana kwa sababu ya hali fulani.

  • Kukataa kimakusudi kutegemeza familia: Mume anapokataa kuandalia familia yake kimwili, hivi kwamba familia yake inakosa mahitaji ya lazima maishani.​—1 Timotheo 5:8.

  • Kutendewa vibaya kimwili: Mwenzi wa ndoa anapotendewa vibaya kimwili au kujeruhiwa kufikia hatua ya kwamba uhai wake unakuwa hatarini.​—Wagalatia 5:19-21.

  • Kuhatarisha kabisa uhusiano wa mtu pamoja na Yehova: Mwenzi wa ndoa anapompinga kabisa mume au mke wake hivi kwamba anashindwa kumtumikia Yehova.​—Matendo 5:29.

Rudi kwenye somo la 42 jambo kuu la 3

 5. Sikukuu na Sherehe

Wakristo hawashiriki katika sikukuu ambazo hazimfurahishi Yehova. Lakini kila Mkristo anapaswa kuongozwa na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kuamua jinsi atakavyotenda watu wengine wanaposherehekea sikukuu hizo. Fikiria mifano michache.

  • Mtu anapokutakia sikukuu njema. Unaweza kumjibu, “Asante.” Ikiwa mtu huyo anataka kujifunza mengi, unaweza kumweleza kwa nini husherehekei sikukuu hiyo.

  • Mwenzi wako wa ndoa, ambaye si Shahidi wa Yehova, anakukaribisha kwenye mlo pamoja na watu wa ukoo wakati wa sikukuu. Ikiwa dhamiri yako inakuruhusu kwenda, unaweza kumweleza mapema mwenzi wako kwamba ikiwa mlo huo utahusisha desturi za kipagani, basi hutashiriki katika desturi hizo.

  • Mwajiri wako anakupa zawadi ya pesa wakati wa sikukuu. Je, unapaswa kukataa pesa hizo? Unaweza kukubali. Je, mwajiri wako anaona pesa hizo kuwa zawadi ya sikukuu, au ni njia ya kukuonyesha shukrani kwa sababu ya kazi nzuri uliyofanya?

  • Mtu fulani anakupatia zawadi wakati wa sikukuu. Huenda mtu huyo akasema: “Ninajua husherehekei sikukuu hii, lakini ningependa kukupatia zawadi hii.” Labda mtu huyo anaonyesha tu fadhili. Hata hivyo, je, kuna sababu inayoonyesha kwamba anajaribu imani yako au anataka ushiriki katika sikukuu hiyo? Baada ya kufikiria mambo hayo, wewe mwenyewe utaamua ikiwa utapokea au kukataa zawadi hiyo. Tunapofanya maamuzi yoyote, tungependa kubaki na dhamiri safi na kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova.​—Matendo 23:1.

Rudi kwenye somo la 44 jambo kuu la 1

 6. Magonjwa ya Kuambukiza

Kwa kuwa tunawapenda watu, hatungependa kuwaambukiza magonjwa. Tunaepuka kufanya hivyo ikiwa tuna ugonjwa unaoambukiza au tuna sababu za kuamini kwamba huenda tumeambukizwa. Tunafanya hivyo ili kutii amri hii ya Biblia: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”​—Waroma 13:8-10.

Mtu aliye na ugonjwa wa kuambukiza anawezaje kutii amri hiyo? Mtu huyo hapaswi kujaribu kuwakumbatia au kuwabusu watu wengine. Hapaswi kukasirika ikiwa wengine watakataa kumkaribisha nyumbani kwao kwa sababu wanataka kulinda familia zao. Na kabla ya kubatizwa, anapaswa kumjulisha mratibu wa baraza la wazee kuhusu ugonjwa wake ili abatizwe kwa njia ambayo itawalinda wengine watakaobatizwa. Kabla ya kuanza uchumba, mtu ambaye huenda ana ugonjwa wa kuambukiza anapaswa kukubali kwa hiari kufanyiwa vipimo vya damu. Ukifanya hivyo, utaonyesha kwamba unawajali wengine kwa ‘kuangalia, si faida zako mwenyewe, bali pia faida za wengine.’​—Wafilipi 2:4.

Rudi kwenye somo la 56 jambo kuu la 2

 7. Masuala ya Kibiashara na Kisheria

Tunaweza kuepuka matatizo mengi kwa kuandika makubaliano yote ya kifedha, hata ikiwa yanahusisha Mkristo mwenzetu. (Yeremia 32:9-12) Hata hivyo, huenda matatizo madogo yakatokea kati ya Wakristo kuhusu pesa au mambo mengine. Wanapaswa kutatua matatizo hayo haraka na kwa amani, kati yao wenyewe.

Hata hivyo, tunapaswa kushughulikiaje matatizo makubwa kama vile ulaghai au uchongezi? (Soma Mathayo 18:15-17.) Yesu alitufundisha hatua tatu ambazo tunapaswa kufuata:

  1. Jaribuni kutatua jambo hilo kati yenu wenyewe.​—Ona mstari wa 15.

  2. Hilo lisipowezekana, nenda na Mkristo mmoja au wawili walio wakomavu kiroho.​—Ona mstari wa 16.

  3. Ikiwa bado mnashindwa kutatua jambo hilo, basi unaweza kuwajulisha wazee wa kutaniko.​—Ona mstari wa 17.

Katika visa vingi, hatupaswi kuwapeleka ndugu zetu mahakamani kwa sababu hilo linaweza kuchafua jina la Yehova na kutaniko. (1 Wakorintho 6:1-8) Hata hivyo, kuna visa ambavyo vinapaswa kusuluhishwa kisheria: kwa mfano, kesi za talaka, kupewa ruhusa mahakamani ya kuwatunza na kuwalea watoto, kuamua malipo ya talaka, kupata malipo ya bima, kesi ya kufilisika, au kuidhinisha wasia. Mkristo anayeenda mahakamani ili kusuluhisha masuala kama hayo kwa njia ya amani havunji ushauri wa Biblia.

Ikiwa kisa hicho kinahusisha uhalifu mkubwa kama vile ubakaji, kumtendea mtoto vibaya, kupigwa, wizi wa kiasi kikubwa cha mali, au mauaji, Mkristo anapotoa taarifa kwa wenye mamlaka havunji ushauri wa Biblia.

Rudi kwenye somo la 56 jambo kuu la 3

a Kuanzia mwaka wa 455 K.W.K. hadi mwaka wa 1 K.W.K. ni miaka 454. Kuanzia mwaka wa 1 K.W.K. hadi mwaka wa 1 W.K. ni mwaka mmoja (hakukuwa na mwaka wa sufuri). Na kuanzia mwaka wa 1 W.K. hadi mwaka wa 29 W.K. ni miaka 28. Jumla ni miaka 483.