Barua Kutoka Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka Baraza Linaloongoza

Ndugu na Dada Wapendwa:

Upendo wetu kwa Mungu na kwa wanadamu wenzetu hutuchochea ‘kwenda . . . kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na kuwabatiza.’ (Mt. 28:​19, 20; Marko 12:​28-31) Upendo huo usio na ubinafsi una nguvu sana. Unaweza kugusa mioyo ya wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Mdo. 13:48.

Wakati uliopita tulikazia fikira kutoa machapisho na kukariri mambo ya kusema tunapohubiri. Sasa tunahitaji kuboresha ustadi wetu wa kuzungumza na watu. Tunaweza kuwaonyesha watu upendo kwa kuzungumzia habari zinazowavutia. Hilo linamaanisha kuwa tayari kubadilika kulingana na hali na kufikiria kwa makini mambo yanayomhangaisha na kumvutia kila mtu tunayezungumza naye. Broshua hii itatusaidiaje kufanya hivyo?

Broshua hii ina masomo 12 yanayotufundisha sifa mbalimbali tunazohitaji kusitawisha ili kuonyesha upendo na kufanya wanafunzi. Kila somo linazungumzia simulizi la Biblia linalokazia sifa ambayo Yesu au Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha walipohubiri habari njema. Lengo si kukariri mambo ya kusema tunapohubiri bali kutafuta njia za kuwaonyesha upendo wale tunaowahubiria. Ingawa kila sifa inahitajika tunaposhiriki aina mbalimbali za huduma yetu, tutachunguza kwa nini ni muhimu sana kusitawisha sifa fulani tunapoanzisha mazungumzo, tunapofanya ziara za kurudia, au kuongoza mafunzo ya Biblia.

Unapochunguza kila somo, fikiria kwa makini jinsi unavyoweza kuonyesha sifa hiyo unapozungumza na watu katika eneo lenu. Jitahidi kuimarisha upendo wako kwa Yehova na kwa wanadamu. Zaidi ya kuwa na mbinu hususa, upendo utakusaidia kufikia lengo lako la kufanya wanafunzi.

Tunathamini pendeleo kubwa la kufanya kazi pamoja nanyi bega kwa bega. (Sef. 3:9) Yehova na awabariki sana mnapoendelea kuwapenda watu na kufanya wanafunzi!

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova