Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Arusi Zenye Shangwe Zinazomletea Yehova Heshima

Arusi Zenye Shangwe Zinazomletea Yehova Heshima

Arusi Zenye Shangwe Zinazomletea Yehova Heshima

Welsh na Elthea walifunga ndoa kule Soweto, Afrika Kusini, mwaka wa 1985. Pindi kwa pindi wao hutazama kitabu chao cha picha za arusi wakiwa na binti yao Zinzi, na kukumbuka siku hiyo yenye shangwe. Zinzi hupenda kuwatambulisha wageni waliokuja arusini na hasa hufurahia picha za mamake akiwa amevalia kwa umaridadi sana.

ARUSI ilianza kwa hotuba ya ndoa iliyotolewa katika jumba moja la jumuiya huko Soweto. Vijana Wakristo wakaimba kwaya wakimsifu Mungu. Kisha wageni wakafurahia mlo huku nyimbo za Ufalme zikiimba kwa sauti ya chini. Hakukuwa na pombe, muziki wenye sauti kubwa, wala kucheza dansi. Badala yake, wageni walifurahia mazungumzo na kuwapongeza maarusi hao. Mambo yote yalichukua muda wa saa tatu hivi. “Ilikuwa arusi ambayo siku zote nitaikumbuka kwa furaha,” asema Raymond, ambaye ni mzee Mkristo.

Walipofanya arusi, Welsh na Elthea walikuwa wafanyakazi wa kujitolea kwenye ofisi ya tawi ya Afrika Kusini ya Watch Tower Bible and Tract Society. Wao wangeweza tu kugharimia arusi ndogo. Wakristo wengine wameamua kuacha huduma ya wakati wote na kufanya kazi za kimwili ili kugharimia arusi kubwa mno. Lakini, Welsh na Elthea hawajuti kwamba walifanya arusi ndogo kwa sababu hiyo iliwawezesha kuendelea kumtumikia Mungu wakiwa watumishi wa wakati wote hadi Zinzi alipozaliwa.

Lakini, namna gani maarusi wakiamua kuwe na muziki na dansi kwenye arusi yao? Namna gani wakiamua kuandaa mvinyo na pombe nyinginezo? Namna gani kama wana uwezo wa kugharimia arusi kubwa yenye mambo mengi? Wanaweza kuhakikishaje kwamba arusi yao itakuwa pindi yenye furaha ambayo inawastahili waabudu wa Mungu? Maswali kama hayo yanahitaji kufikiriwa kwa uzito, kwa sababu Biblia inaamuru hivi: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo jingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

Kuepuka Sherehe Yenye Kelele za Ulevi na Ulafi

Ni vigumu kuwazia arusi ambayo haina shangwe. Lakini, kwa upande mwingine kuna hatari kubwa sana ya mambo kupita kiasi na kuwa sherehe mbaya sana ya kelele za ulevi na ulafi. Katika arusi nyingi za watu ambao si Mashahidi wa Yehova, mambo fulani yasiyomletea Yehova heshima hutendeka. Kwa mfano, ni kawaida kunywa pombe na kulewa. Inasikitisha kwamba jambo hilo hata limetendeka katika arusi fulani za Kikristo.

Biblia inaonya kwamba “kileo huleta ugomvi.” (Mithali 20:1) Neno la Kiebrania ambalo limetafsiriwa ‘kuleta ugomvi’ lamaanisha “kufanya kelele.” Ikiwa pombe inaweza kumfanya mtu mmoja awe mwenye kelele, ebu wazia vile inavyoweza kuwafanya watu wengi wanaokusanyika pamoja na kunywa pombe kupindukia! Ni wazi kwamba pindi kama hizo zinaweza kugeuka kuwa ‘vipindi vya kulewa, sherehe zenye kelele za ulevi na ulafi, na mambo kama hayo,’ ambayo yameorodheshwa katika Biblia kuwa “kazi za mwili.” Matendo kama hayo huwafanya watu ambao hawatubu wasistahili kurithi uhai udumuo milele chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Wagalatia 5:19-21.

Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “sherehe yenye kelele za ulevi na ulafi,” lilitumiwa kuelezea maandamano ya vijana waliolewa kidogo ambao walikuwa wakiimba, wakicheza dansi, na kupiga muziki. Pombe nyingi inaponywewa kwenye arusi, na muziki unaimba kwa sauti kubwa na watu wanacheza dansi bila kujidhibiti, kuna hatari kubwa kwamba arusi hiyo itageuka kuwa sherehe yenye kelele za ulevi na ulafi. Katika hali kama hiyo, walio dhaifu wanaweza kushawishiwa kwa urahisi na kutenda kazi nyinginezo za mwili kama “uasherati, ukosefu wa usafi, mwenendo mlegevu, [au kushindwa na] hasira za ghafula.” Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuzuia kazi hizo za mwili zisiharibu shangwe ya arusi ya Kikristo? Ili kujibu swali hilo, ebu tuchunguze mambo ambayo Biblia inasema kuhusu arusi fulani.

Arusi Ambayo Yesu Alihudhuria

Yesu na wanafunzi wake walialikwa kwenye arusi fulani kule Kana ya Galilaya. Walikubali mwaliko huo, na Yesu hata akaongezea shangwe ya pindi hiyo. Divai ilipokwisha, Yesu alitokeza kimuujiza divai nyingine bora sana. Inaonekana kwamba divai iliyobaki baada ya arusi ilitumiwa na bwana-arusi mwenye shukrani na familia yake kwa muda fulani.—Yohana 2:3-11.

Arusi ambayo Yesu alihudhuria inaweza kutufunza mambo kadhaa. Kwanza, Yesu na wanafunzi wake hawakuhudhuria karamu hiyo bila kualikwa. Biblia inasema waziwazi kwamba walialikwa. (Yohana 2:1, 2) Vilevile, katika vielezi viwili vya karamu za arusi, Yesu alirudia-rudia kutaja kwamba wageni waliokuwapo walialikwa.—Mathayo 22:2-4, 8, 9; Luka 14:8-10.

Kuna nchi ambazo ni desturi kwa kila mtu katika jumuiya kuhudhuria karamu ya arusi awe amealikwa au hajaalikwa. Lakini hiyo inaweza kutokeza magumu ya kifedha. Maarusi ambao si matajiri wanaweza kujiingiza katika deni ili kuhakikisha kwamba kuna chakula na kinywaji cha kuutosha umati mkubwa. Basi, maarusi Wakristo wakiamua kuwa na karamu ndogo yenye idadi fulani hususa ya watu walioalikwa, Wakristo wenzao ambao hawakualikwa wanapaswa kuelewa jambo hilo na kulistahi. Mtu mmoja aliyefunga ndoa kule Cape Town, Afrika Kusini, akumbuka kwamba alialika wageni 200 kwenye arusi yake. Lakini watu 600 wakaja na chakula kikaisha upesi. Miongoni mwa wale waliohudhuria bila kualikwa kulikuwa na wageni walioletwa wakiwa wamejaa basi, nao walikuwa wakizuru Cape Town mwisho-juma huo wa arusi. Kondakta wa basi alikuwa jamaa wa mbali wa bibi-arusi na alifikiri kwamba ana haki ya kuwaleta watu hao wote kwenye arusi hata bila kuwasiliana na bibi-arusi wala bwana-arusi!

Isipotajwa waziwazi kwamba kila mtu anakaribishwa kwenye karamu, mfuasi wa kweli wa Yesu angeepuka kuhudhuria karamu ya arusi bila kualikwa na kula vyakula na kunywa vinywaji ambavyo wageni walioalikwa wameandaliwa. Wale wanaoshawishiwa kuhudhuria bila kualikwa wanapaswa kujiuliza, ‘Je, kuhudhuria karamu hii ya arusi hakuonyeshi kwamba siwapendi maarusi hao? Je, sitavuruga mambo na kufanya wasifurahie pindi hiyo?’ Badala ya kuudhika kwamba hakualikwa, Mkristo anayeelewa mambo anaweza kwa upendo kupeleka ujumbe wa kuwapongeza maarusi hao akiwatakia baraka za Yehova. Hata anaweza kufikiria kuwapelekea maarusi hao zawadi ya kuongezea furaha kwa siku yao ya arusi.—Mhubiri 7:9; Waefeso 4:28.

Ni Nani Aliye na Daraka?

Ni desturi katika sehemu fulani za Afrika kwa watu wa jamaa wenye umri mkubwa kuchukua daraka la kufanya mipango ya arusi. Maarusi wanaweza kufurahia jambo hilo kwa kuwa linawaondolea mzigo wa kifedha. Huenda wakafikiri kwamba jambo hilo lawaondolea pia wajibu kwa jambo lolote ambalo huenda likatukia. Lakini, kabla ya kukubali msaada wowote wa watu wa jamaa wenye nia nzuri, ni vizuri maarusi wahakikishe kwamba matakwa yao yatafuatwa.

Ijapokuwa Yesu ni Mwana wa Mungu ‘aliyeteremka kutoka mbinguni,’ hakuna jambo linalodokeza kwamba alichukua daraka na kuongoza mambo mengi kwenye arusi iliyokuwa Kana. (Yohana 6:41) Badala yake, masimulizi ya Biblia yatuambia kwamba mtu mwingine aliwekwa kuwa “mwelekezi wa karamu.” (Yohana 2:8) Mtu huyo naye alifuata uongozi wa bwana-arusi, ambaye sasa ni kichwa cha familia.—Yohana 2:9, 10.

Watu wa jamaa ambao ni Wakristo wapaswa kumheshimu bwana-arusi huyo ambaye sasa ni kichwa cha familia aliyewekwa na Mungu. (Wakolosai 3:18-20) Yeye ndiye anayewajibika kwa mambo yanayotukia katika arusi yake. Bila shaka, bwana-arusi anapaswa kuwa mwenye usawaziko na ikiwezekana ayafikirie maoni ya wazazi wake, wakwe zake, na bibi-arusi. Lakini, watu wa jamaa wakisisitiza kwamba watapanga mambo kinyume cha matakwa ya maarusi, basi maarusi wanaweza kukataa msaada wao kwa fadhili na kujigharimia arusi yao ndogo. Wakifanya hivyo hakuna jambo litakalotokea ambalo litawafanya maarusi wasikitike wakumbukapo arusi yao. Kwa mfano, kwenye arusi ya Mkristo fulani huku Afrika, mtu mmoja wa jamaa ambaye si mwamini na ambaye alikuwa msimamizi wa sherehe alifanya tendo la kuwaheshimu wafu!

Nyakati nyingine maarusi huondoka kwenda kwenye fungate kabla ya karamu ya arusi kwisha. Katika hali kama hizo, bwana-arusi apaswa kufanya mpango ili wasimamizi wanaostahili wahakikishe kwamba kanuni za Biblia zinadumishwa na kwamba sherehe hiyo inaisha kwa wakati mzuri.

Kupanga kwa Uangalifu na kwa Usawaziko

Inaonekana kwamba kulikuwa na chakula kingi kizuri kwenye arusi ambayo Yesu alihudhuria, kwa sababu Biblia inaitaja kuwa karamu ya arusi. Kama ambavyo imetajwa, divai ilikuwa tele. Inaelekea kwamba kulikuwa na muziki ufaao na watu walicheza dansi kwa adabu kwa sababu ilikuwa kawaida kuwa na dansi katika vikusanyiko vya Wayahudi. Yesu alionyesha jambo hilo katika mfano wake maarufu wa mwana mpotevu. Baba tajiri katika hadithi hiyo alifurahi sana kuona mwana wake aliyetubu amerudi hivi kwamba alisema: “Acheni tule na kujifurahisha wenyewe.” Kulingana na Yesu, sherehe hiyo ilitia ndani “utumbuizo wa kimuziki na uchezaji-dansi.”—Luka 15:23, 25.

Hata hivyo, ni jambo la kutokeza kwamba Biblia haitaji muziki wala kucheza dansi kwenye arusi ya Kana. Hata dansi haitajwi katika masimulizi yoyote ya arusi katika Biblia. Basi inaonekana kwamba miongoni mwa watumishi waaminifu wa Mungu wa nyakati za Biblia, dansi ingetukia lakini haikuwa sehemu kuu ya arusi zao. Je, tunaweza kujifunza jambo kutokana na mambo hayo?

Katika arusi fulani za Wakristo huku Afrika, vyombo vyenye nguvu sana vya muziki hutumiwa. Muziki waweza kuwa wenye sauti kubwa sana hivi kwamba wageni hawawezi kuzungumza kwa starehe. Nyakati nyingine inakuwa wazi kwamba chakula kimepungua lakini dansi ambayo inaweza kupita kiasi kwa urahisi haipungui. Badala ya kuwa sherehe ya arusi, pindi kama hizo zaweza kuwa tu udhuru wa kucheza dansi. Isitoshe, mara nyingi muziki wenye sauti kubwa huwavutia watu wenye fujo ambao huja bila kualikwa.

Kwa kuwa masimulizi ya Biblia ya arusi hayasisitizi muziki na dansi, je, jambo hilo halipasi kuwaongoza wale wanaopanga kufanya arusi ambayo itamletea Yehova heshima? Na wakati wa kufanya matayarisho ya arusi kadhaa za hivi majuzi katika sehemu ya kusini mwa Afrika, vijana Wakristo waliochaguliwa kuwa katika msafara wa arusi walitumia muda wa saa nyingi sana wakifanya mazoezi magumu ya dansi watakazocheza. Kwa miezi kadhaa wakati mwingi sana ulitumiwa kufanya mazoezi hayo. Lakini Wakristo wanahitaji ‘kununua kabisa wakati’ kwa ajili ya “mambo yaliyo ya maana zaidi,” kama vile kazi ya kueneza evanjeli, funzo la binafsi, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo.—Waefeso 5:16; Wafilipi 1:10.

Kutokana na kiasi cha divai ambayo Yesu aliandaa, inaonekana kwamba arusi iliyofanywa Kana ilikuwa kubwa na yenye mambo mengi. Lakini, kwa hakika pindi hiyo haikuwa yenye kelele na wageni hawakunywa pombe kupindukia kama ilivyokuwa ikitukia katika arusi fulani za Wayahudi. (Yohana 2:10) Kwa nini tuna hakika ya jambo hilo? Kwa sababu Bwana Yesu Kristo alihudhuria. Kati ya watu wote, Yesu ndiye angalikuwa mwangalifu zaidi kutii amri ya Mungu kuhusu mashirika mabaya: “Usiwe miongoni mwa wale wanywao divai kupita kiasi.”—Mithali 23:20, NW.

Basi, maarusi wakiamua kuwa na divai na pombe za aina nyinginezo katika arusi yao, wanapaswa kufanya mpango ili wasimamizi wanaostahili waisimamie vizuri. Na wakiamua kuwa na muziki, wanapaswa kuchagua muziki ufaao na msimamizi anayestahili ahakikishe muziki si wenye sauti kupita kiasi. Wageni hawapaswi kuanza kutawala na kuleta muziki wenye kutilika shaka au kuongeza sauti ya muziki kwa kiasi ambacho hakifai. Ikiwa watu watacheza dansi, wanaweza kucheza kwa utaratibu na kwa adabu. Watu wa ukoo ambao si waamini au Wakristo ambao hawajakomaa wakicheza dansi kwa njia chafu ya kukosa adabu au kwa njia ya kuamsha tamaa ya ngono, bwana-arusi anaweza kubadili muziki huo au kwa busara kukomesha dansi hiyo. La sivyo, arusi hiyo inaweza kuharibika na kuwa yenye fujo na ikwaze watu.—Waroma 14:21.

Kwa sababu kuna hatari katika dansi fulani za siku hizi, muziki wenye sauti kubwa, na pombe nyingi, mabwana-arusi wengine Wakristo wameamua kutopangia mambo hayo katika arusi yao. Mabwana-arusi wengine wameshutumiwa kwa kufanya hivyo, lakini wao wanapasa kupongezwa kwa kutaka kuepuka chochote ambacho huenda kikaletea suto jina takatifu la Mungu. Kwa upande mwingine, mabwana-arusi wengine hupanga kuwe na muziki ufaao, wakati wa kucheza dansi, na kuandaa pombe kwa kiasi. Kwa vyovyote vile, bwana-arusi anawajibika kwa mambo anayoyaruhusu katika arusi yake.

Katika Afrika, watu wengine ambao hawajakomaa hudharau arusi za Wakristo zinazofanywa kwa njia yenye heshima na wanasema eti kwamba kuhudhuria arusi hizo ni kama kuhudhuria mazishi. Lakini hayo si maoni yenye usawaziko. Kazi za mwili wenye dhambi zinaweza kusisimua kwa muda mfupi, lakini humwacha Mkristo akiwa na dhamiri chafu na huletea jina la Mungu suto. (Waroma 2:24) Kwa upande mwingine, roho takatifu ya Mungu hutokeza shangwe ya kweli. (Wagalatia 5:22) Wakristo wengi ambao wamefunga ndoa hufurahi kukumbuka siku za arusi zao, wakijua kwamba hiyo ilikuwa pindi yenye furaha wala haikuwa ‘sababu ya kukwaza.’—2 Wakorintho 6:3.

Welsh na Elthea bado wanakumbuka maneno ya jamaa zao wasioamini ambao walihudhuria arusi yao wakieleza jinsi walivyofurahia arusi hiyo. Mmoja wao alisema: “Tumechoka na arusi za siku hizi zenye kelele. Nilifurahia sana kuhudhuria arusi yenye heshima iliyo tofauti na nyinginezo.”

Jambo muhimu zaidi ni kwamba arusi zenye shangwe na zenye adabu humheshimu Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

MAMBO YA KUCHUNGUZA KWENYE KARAMU YA ARUSI

• Ukialika mtu wa jamaa ambaye si mwamini atoe hotuba fupi, je, umehakikisha kwamba hataingiza mapokeo yasiyo ya Kikristo?

• Ikiwa muziki utakuwapo, je, umechagua nyimbo zifaazo?

• Je, muziki utakuwa na sauti yenye kiasi?

• Ikiwa watu watacheza dansi, je, watacheza kwa adabu?

• Je, pombe itaandaliwa kwa kiasi?

• Je, wasimamizi wanaostahili watasimamia unywaji wa pombe?

• Je, umeweka wakati ufaao wa kumaliza karamu ya arusi?

• Je, wasimamizi wanaostahili watakuwapo ili kuhakikisha kwamba kuna utaratibu hadi mwisho?