Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Namshukuru Yehova—Kupitia Utumishi wa Wakati Wote!

Namshukuru Yehova—Kupitia Utumishi wa Wakati Wote!

Simulizi la Maisha

Namshukuru Yehova—Kupitia Utumishi wa Wakati Wote!

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA STANLEY E. REYNOLDS

Nilizaliwa London, Uingereza, mwaka wa 1910. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, wazazi wangu walihamia kijiji kidogo cha Wiltshire kinachoitwa Westbury Leigh. Nikiwa mvulana mdogo, mara nyingi nilijiuliza, ‘Mungu ni nani?’ Hakuna mtu aliyeweza kuniambia. Nami sikujua ni kwa nini jumuiya ndogo kama yetu ilihitaji vikanisa viwili na vilevile kanisa la kumwabudu Mungu.

KATIKA 1935, miaka minne kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kuanza, mimi na ndugu yangu mchanga, Dick, tuliendesha baiskeli hadi Weymouth huko pwani ya kusini ya Uingereza ili tupige kambi wakati wa likizo. Tulipokuwa tumeketi katika hema letu tukisikiliza mvua kubwa ikinyesha na kujiuliza jambo la kufanya, mzee mmoja alitutembelea na kunipa vichapo vitatu vya kusaidia kujifunza Biblia—The Harp of God, Light I, na Light II. Nilivichukua, nikifurahi kupata kitu cha kuondoa uchoshi. Mara moja nikavutiwa sana na yale niliyosoma, lakini sikujua wakati huo kwamba mambo hayo yangebadilisha maisha yangu kabisa—na ya ndugu yangu pia.

Niliporudi nyumbani, mama yangu aliniambia kwamba Kate Parsons, aliyekuwa akiishi katika kijiji chetu, aligawanya vichapo hivyohivyo vya Biblia. Alijulikana sana kwa sababu, ajapokuwa mzee sana, aliendesha pikipiki ndogo na kutembelea watu katika jumuiya yetu iliyotawanyika-tawanyika. Nilikwenda kumwona, naye alifurahia kunipa kitabu Creation na Riches na vilevile vichapo vingine vya Watch Tower Society. Pia aliniambia kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Baada ya kusoma vitabu hivyo pamoja na Biblia yangu, nikajua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na nilitaka kumwabudu. Kwa hiyo nilituma barua ya kujiuzulu kwenye kanisa letu na kuanza kuhudhuria mafunzo ya Biblia nyumbani kwa John na Alice Moody. Waliishi huko Westbury, mji uliokuwa karibu na kwetu. Tulikuwa watu saba tu kwenye mikutano hiyo. Kabla na baada ya mikutano, Kate Parsons alipiga kinanda tulipoimba nyimbo za Ufalme pamoja kwa shauku!

Siku za Mapema

Nilitambua kuwa tunaishi katika nyakati muhimu, nami nilitamani sana kushiriki katika kazi ya kuhubiri iliyotabiriwa kwenye Mathayo 24:14. Kwa hiyo niliacha kuvuta sigareti, nikanunua mkoba, na kujiweka wakfu kwa Mungu Mkuu, Yehova.

Agosti mwaka wa 1936, Joseph F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society, alikuwa ametembelea Glasgow, Scotland, kuongea juu ya “Har–Magedoni.” Hata ingawa mji wa Glasgow ulikuwa umbali wa kilometa 600 hivi, niliazimia kuhudhuria mkusanyiko huko na kubatizwa. Sikuwa na fedha za kutosha, kwa hiyo nikabeba baiskeli yangu kwenye garimoshi hadi Carlisle, mji uliopo kwenye mpaka wa Scotland, na kuendesha baiskeli kuanzia hapo kwenda kilometa 160 kuelekea upande wa kaskazini. Pia niliendesha baiskeli karibu safari yote ya kurudi nyumbani, nikarudi nikiwa nimechoka sana lakini nimeimarishwa kiroho.

Kuanzia wakati huo na kuendelea, niliendesha baiskeli kwenda mahali popote ili kuwahubiria watu wa vijiji vya karibu-karibu. Siku hizo kila Shahidi alikuwa na kadi ya kutoa ushahidi yenye ujumbe wa Kimaandiko ili mwenye nyumba aisome. Pia tulitumia vinanda vyenye kubebeka vilivyorekodiwa hotuba za Biblia za msimamizi wa Sosaiti. Na, bila shaka, sikuzote tulibeba mfuko wa magazeti,  * ambao ulitutambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova.

Kufanya Upainia Wakati wa Vita

Ndugu yangu alibatizwa mwaka wa 1940. Vita ya ulimwengu ya pili ilikuwa imeanza mwaka wa 1939, na sote wawili tukaona uhitaji mkubwa wa wahubiri wa wakati wote. Kwa sababu hiyo, tukajaza maombi ya kuwa mapainia. Tulishukuru tulipopewa mgawo pamoja kwenda kwenye makao ya mapainia ya Bristol, ili kujiunga na Edith Poole, Bert Farmer, Tom na Dorothy Bridges, Bernard Houghton, na mapainia wengine ambao tulikuwa tumevutiwa na imani yao kwa muda mrefu.

Gari moja lililokuwa na maandishi mazito “MASHAHIDI WA YEHOVA” likafika upesi kutuchukua. Dereva alikuwa Stanley Jones ambaye baadaye alikuwa mishonari China na aliyefungwa huko kifungo cha upweke kwa miaka saba kwa sababu ya kuhubiri.

Vita ilipokuwa ikiendelea, hatukuweza kupata usingizi wa kutosha. Mabomu yalianguka karibu na makao yetu ya mapainia, nasi tulilazimika kuwa macho kwa sababu ya makombora yenye kulipuka. Jioni moja tulitoka jijini Bristol baada ya kusanyiko zuri lililohudhuriwa na Mashahidi 200 tukafika nyumbani kwetu kwa usalama licha ya kuanguka kwa vipande vingi vya makombora ya kulipulia ndege.

Asubuhi iliyofuata mimi na Dick tulirudi jijini kuchukua vitu fulani ambavyo tulikuwa tumeviacha huko. Tulishtuka. Jiji la Bristol lilikuwa magofu. Jiji lote lilikuwa limelipuliwa na kuchomeka. Park Street, mahali ambapo Jumba letu la Ufalme lilikuwa, ilikuwa magofu yenye kufuka moshi. Hata hivyo, hakuna Shahidi aliyeuawa wala kuumizwa. Kwa uzuri, tulikuwa tayari tumehamisha vichapo vya Biblia kutoka kwenye Jumba la Ufalme na kuviweka kwenye makao ya washiriki wa kutaniko. Tulimshukuru Yehova kwa yote hayo.

Uhuru Usiotazamiwa

Kutaniko la Bristol, ambalo nilitumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi, liliongezeka likawa na wahudumu 64 kufikia wakati nilipopokea hati za kusajiliwa katika utumishi wa kijeshi. Mashahidi wengine wengi walitiwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwemo, nami nilitazamia uhuru wangu wa kuhubiri ukatizwe vilevile. Kesi yangu ilisikizwa mbele ya Baraza la Mahakimu la Bristol ambapo Ndugu Anthony Buck, ofisa wa zamani wa gereza, aliniwakilisha. Alikuwa mwanamume jasiri na asiyehofu, mtetezi wa kweli za Biblia, na kwa sababu ya uwakilishaji wake mzuri, bila kutazamia nilipewa ruhusa ya kutohusishwa kabisa katika utumishi wa kijeshi chini ya sharti ya kwamba nitaendelea na huduma yangu ya wakati wote!

Nilisisimka kuwa na uhuru wangu, nami niliazimia kuutumia kuhubiri kwa kadiri iwezekanavyo. Nilipopokea simu niripoti kwenye ofisi ya tawi ya London ili nikaongee na Albert D. Schroeder, aliyekuwa msimamizi wa tawi, kama ilivyo kawaida nilijiuliza ni nini kilichokuwa kikiningojea. Hebu wazia jinsi nilivyoshangaa nilipoalikwa kwenda Yorkshire kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye, nikitembelea kutaniko tofauti kila juma ili kusaidia na kutia moyo akina ndugu. Nilijihisi sifai mgawo huo, lakini nilikuwa na ruhusa nami nilikuwa huru kwenda. Kwa hiyo nikakubali mwelekezo wa Yehova na kwenda kwa hiari.

Albert Schroeder alinijulisha kwa akina ndugu kwenye kusanyiko moja huko Huddersfield, na Aprili 1941, nikaanza mgawo wangu mpya. Ilikuwa shangwe kama nini kuwajua ndugu hao wapendwa! Upendo wao na fadhili zao zilinifanya nithamini hata zaidi kwamba Yehova ana watu waliojitoa kwake kabisa na ambao wanapendana.—Yohana 13:35.

Mapendeleo Zaidi ya Utumishi

Mkusanyiko usiosahaulika wa kimataifa wa siku tano ulifanywa mwaka wa 1941 katika jumba la De Montfort Hall la jiji la Leicester. Ijapokuwa watu walikuwa wanapimiwa chakula kwa sababu ya uhaba na kuwekewa vizuizi vya kusafiri, hudhudirio lilifikia kilele cha watu 12,000 Jumapili; ilhali wakati huo kulikuwa na Mashahidi wanaozidi tu 11,000 nchini. Hotuba za msimamizi wa Sosaiti zilizorekodiwa zilisikizwa, na kitabu Children kikatolewa. Mkusanyiko huo kwa kweli ulikuwa hatua muhimu katika historia ya kitheokrasi ya watu wa Yehova katika Uingereza, ukifanywa katikati ya Vita ya Ulimwengu ya Pili.

Upesi baada ya mkusanyiko huo, nilipokea mwaliko wa kutumikia pamoja na familia ya Betheli ya London. Nikiwa huko, nilifanya kazi katika idara ya usafirishaji na upakiaji na baadaye katika ofisi, nikishughulikia mambo yanayohusu makutaniko.

Familia ya Betheli ililazimika kuvumilia mashambulio ya ndege za vita London usiku na mchana, na pia misako ya daima iliyofanywa na wenye mamlaka kwa akina ndugu wenye madaraka waliokuwa wakifanya kazi hapo. Pryce Hughes, Ewart Chitty, na Frank Platt walifungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwemo, na hatimaye Albert Schroeder akafukuzwa nchini na kwenda Marekani. Ijapokuwa misongo hiyo, makutaniko na masilahi ya Ufalme yaliendelea kutunzwa vizuri.

Naenda Gileadi!

Vita ilipokwisha mwaka wa 1945, nilijaza ombi la kuhudhuria mazoezi ya mishonari kwenye Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower nami nikakubaliwa kuingia darasa la nane mwaka wa 1946. Sosaiti ilipanga kwamba baadhi yetu, kutia ndani Tony Attwood, Stanley Jones, Harold King, Don Rendell, na Stanley Woodburn, wasafiri kwa bahari kutoka bandari ya uvuvi ya Fowey, Cornwall. Shahidi mmoja wa huko alitukatia tikiti kwenye meli ndogo ya mizigo iliyobeba udongo mweupe. Vyumba vyetu vilikuwa vidogo sana, na sitaha ilikuwa imejaa maji. Tulifurahi kama nini hatimaye tulipokaribia bandari tuliyokuwa tukienda, Philadelphia!

Shule ya Gileadi ilikuwa katika eneo maridadi la South Lansing kuelekea sehemu ya kaskazini ya New York, na mazoezi niliyopokea huko niliyathamini sana. Wanafunzi wa darasa letu walitoka mataifa 18—ikiwa mara ya kwanza kwa Sosaiti kuandikisha wahudumu wengi sana kutoka nchi za kigeni—na sisi sote tukawa marafiki sana. Nilifurahia sana ushirika wa Kalle Salavaara kutoka Finland ambaye tuliishi naye katika chumba kimoja.

Wakati ulipita haraka, na mwishoni mwa miezi mitano, msimamizi wa Sosaiti, Nathan H. Knorr, alifika kutoka makao makuu ya Brooklyn kutupatia diploma zetu na kutuambia juu ya migawo yetu. Siku hizo, wanafunzi hawakujua watakakoenda mpaka ilipotangazwa kwenye sherehe ya kufuzu. Nilipewa mgawo wa kurudi Betheli ya London niendelee na kazi yangu huko.

Narudi London

Miaka ya baada ya vita ilikuwa migumu nchini Uingereza. Chakula na mambo mengine ya lazima, kutia ndani karatasi, viliendelea kupimwa. Lakini tulifanikiwa, na masilahi ya Ufalme wa Yehova yalisitawi. Zaidi ya kufanya kazi Betheli, nilitumika kwenye mikusanyiko ya wilaya na makusanyiko ya mzunguko na kutembelea makutaniko, kutia ndani mengine huko Ireland. Pia lilikuwa pendeleo kukutana na Erich Frost na ndugu na dada wengine kutoka Ulaya na kujifunza kutoka kwao juu ya uaminifu-maadili wa Mashahidi wenzetu ambao walikuwa wamevumilia ukatili katika kambi za mateso za Nazi. Kwa kweli utumishi wa Betheli ulikuwa pendeleo lenye baraka.

Kwa miaka kumi nilikuwa nimemjua Joan Webb, painia wa pekee aliyetumika katika Watford, mji uliopo kaskazini mwa London. Tulifunga ndoa mwaka wa 1952. Sisi sote tulitaka kuendelea na utumishi wa wakati wote, kwa hiyo tulifurahi wakati, baada ya kuondoka Betheli, niliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mzunguko wetu wa kwanza ulikuwa pwani ya kusini ya Uingereza, huko Sussex na Hampshire. Kazi ya mzunguko haikuwa rahisi siku hizo. Tulisafiri sanasana kwa basi, baiskeli, na kwa miguu. Makutaniko mengi yalikuwa na maeneo makubwa ya mashambani, ambayo mara nyingi ilikuwa vigumu kuyafikia, lakini idadi ya Mashahidi iliendelea kuongezeka.

Katika New York City Mwaka wa 1958

Mwaka wa 1957, nilipokea mwaliko mwingine kutoka Betheli: “Je, ungependa kuja ofisini usaidie katika mipango ya kusanyiko la kimataifa linalokaribia litakalofanyiwa huko Yankee Stadium na Polo Grounds katika New York City mwaka wa 1958?” Upesi mimi na Joan tukawa twashughulikia maombi kutoka kwa akina ndugu ya kusafiri kwa ndege na meli ambazo Sosaiti ilikuwa imekodi. Hilo likawa kusanyiko lililojulikana sana la Kimataifa la Mapenzi ya Mungu, lililohudhuriwa na umati wa watu 253,922. Kwenye mkusanyiko huu, watu 7,136 walionyesha wakfu wao kwa Yehova kupitia ubatizo wa maji—idadi maradufu ya wale waliobatizwa katika pindi ya kihistoria ya Pentekoste 33 W.K., kama inavyoripotiwa katika Biblia.—Matendo 2:41.

Mimi na Joan hatutasahau kamwe fadhili ya Ndugu Knorr alipotualika binafsi tuhudhurie kusanyiko hilo ili tusaidie kushughulikia wajumbe waliokuwa wakifika New York City kutoka nchi 123. Hilo lilikuwa jambo la furaha na lenye kuridhisha kwetu sote.

Baraka za Utumishi wa Wakati Wote

Tuliporudi, tuliendelea na kazi ya kusafiri hadi matatizo ya afya yalipotokea. Joan alilazwa hospitalini, nami nikawa na mshtuko mdogo wa akili. Tukaanza utumishi wa painia wa pekee lakini baadaye tukawa na pendeleo la muda la kutumika katika kazi ya mzunguko tena. Hatimaye, tulirudi Bristol ambapo tumebaki katika utumishi wa wakati wote. Ndugu yangu Dick, pamoja na familia yake, wanaishi karibu nasi, na mara kwa mara sisi hukutana na kukumbuka ya kale.

Macho yangu yaliharibika kabisa kwa sababu ya kubanduka kwa ngozi ya retina mwaka wa 1971. Tangu wakati huo nimekuwa na tatizo kubwa sana la kusoma, kwa hiyo naona kaseti za vichapo vya Biblia kuwa uandalizi mzuri ajabu kutoka kwa Yehova. Mimi na Joan tungali twaongoza mafunzo ya Biblia, na kwa miaka ambayo imepita, tumekuwa na pendeleo la kusaidia watu 40 wapate ujuzi wa kweli, kutia ndani familia moja ya watu saba.

Tulipoweka maisha yetu wakfu kwa Yehova zaidi ya miaka 60 iliyopita, tamaa yetu ilikuwa kuingia katika utumishi wa wakati wote na kudumu katika utumishi huo. Twashukuru kama nini kuwa na nguvu za kumtumikia Yehova Mkuu—njia pekee ambayo twaweza kumshukuru kwa wema wake kwetu na kwa miaka yetu ya furaha tukiwa pamoja!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Mfuko wa nguo ambao ungeweza kubebwa mabegani na uliotengenezwa kwa kusudi la kubebea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Consolation (ambalo baadaye likawa Amkeni!).

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na ndugu yangu Dick (mbali kushoto; Dick amesimama) na mapainia wengine mbele ya makao ya mapainia ya Bristol

[Picha katika ukurasa wa 25]

Makao ya mapainia ya Bristol mwaka wa 1940

[Picha katika ukurasa wa 26]

Stanley na Joan Reynolds katika siku yao ya arusi, Januari 12, 1952, na leo