Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Vielelezo Vizuri Vyakunufaisha?

Je, Vielelezo Vizuri Vyakunufaisha?

Je, Vielelezo Vizuri Vyakunufaisha?

“NYINYI mlipata kuwa kielelezo kwa waamini wote katika Makedonia na katika Akaya.” Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo waaminifu katika Thesalonike maneno hayo. Kielelezo walichoonyesha kwa waamini wenzao kilistahili kusifiwa kwelikweli. Hata hivyo, Wathesalonike wenyewe walikuwa wakifuata kielelezo cha Paulo na wenzake. Paulo alisema: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu, kama vile nyinyi mjuavyo ni watu wa namna gani sisi tulipata kuwa kwenu kwa ajili yenu; nanyi mkawa waigaji wetu.”—1 Wathesalonike 1:5-7.

Naam, Paulo hakuhubiri tu. Maisha yake mwenyewe yalikuwa kielelezo cha imani, uvumilivu, na kujitolea. Kwa sababu hiyo, Paulo na wenzake wakawa kitia-moyo chenye nguvu katika maisha ya Wathesalonike, kilichowasukuma kukubali kweli “chini ya dhiki nyingi.” Hata hivyo, sio Paulo na wafanyakazi wenzake tu waliokuwa kitia-moyo kwa waamini hao. Vielelezo vya wengine waliovumilia dhiki viliwatia moyo pia. Paulo aliwaandikia Wathesalonike hivi: “Nyinyi mlipata kuwa waigaji, akina ndugu, wa makutaniko ya Mungu yaliyo katika Yudea katika muungano na Kristo Yesu, kwa sababu nyinyi pia mlianza kuteseka mikononi mwa wananchi wenzenu wenyewe mambo yaleyale kama yale ambayo wao pia wanateseka mikononi mwa Wayahudi.”—1 Wathesalonike 2:14.

Kielelezo Kikuu—Yesu Kristo

Ingawa Paulo mwenyewe alikuwa kielelezo kilichostahili kufuatwa, hakukosa kamwe kuelekeza kwa Yesu Kristo, aliye kielelezo kikuu wapaswacho Wakristo kukifuata. (1 Wathesalonike 1:6) Kristo ni Kielelezo chetu kikuu sikuzote. Mtume Petro aliandika: “Kwenye mwendo huu mliitwa, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.”—1 Petro 2:21.

Hata hivyo, Yesu aliishi duniani karibu miaka 2,000 iliyopita. Sasa yeye ni kiumbe wa kiroho “akaaye katika nuru isiyokaribika” na “hakuna hata mmoja kati ya watu ambaye amemwona au aweza kumwona.” (1 Timotheo 6:16) Basi twaweza kumwigaje? Njia moja ni kwa kujifunza yale masimulizi manne katika Biblia juu ya maisha ya Yesu. Gospeli hizo zaeleza utu wake, maisha yake, na ‘mtazamo wake wa kiakili.’ (Wafilipi 2:5-8) Unaweza kupata ujuzi zaidi kwa kujifunza kwa makini kitabu kiitwacho Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, kinachozungumzia matukio ya maisha ya Yesu kwa kindani sana na kwa kufuatana na wakati yalipotukia. *

Kielelezo cha kujitolea cha Yesu kilikuwa na matokeo makubwa katika maisha ya mtume Paulo. Aliwaambia Wakristo Wakorintho hivi: “Kwa upande wangu hakika mimi nitatumia kwa mteremo zaidi sana na kutumiwa kabisa kwa ajili ya nafsi zenu.” (2 Wakorintho 12:15) Alikuwa na mtazamo kama Kristo kwelikweli! Tunapotafakari kielelezo chake kikamilifu, hata sisi twapaswa kusukumwa kumwiga Kristo maishani mwetu.

Kwa mfano, Yesu alitufundisha kutegemea ahadi ya Mungu ya kuandaa riziki. Lakini hakufundisha tu. Alionyesha imani ya aina hiyo na kumtegemea Yehova katika maisha yake ya kila siku. Alisema: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 6:25; 8:20) Je, mambo ya kimwili ndiyo yaongozayo mawazo yako na utendaji wako? Ama, je, maisha yako yathibitisha kwamba unatafuta Ufalme kwanza? Nawe unauonaje utumishi wa Yehova? Unauona kama vile Yesu tunayemwiga anavyouona? Biblia yasema kwamba Yesu hakuhubiri tu kuhusu bidii, bali alionyesha bidii yenye kuwaka moto katika visa vingi. (Yohana 2:14-17) Zaidi ya hayo, Yesu alikuwa kielelezo bora kama nini kwa kuonyesha upendo! Hata alitoa uhai wake mwenyewe kwa ajili ya wanafunzi wake! (Yohana 15:13) Je, wewe unafuata kielelezo cha Yesu kwa kupenda ndugu zako Wakristo? Ama unaruhusu kutokamilika kwa wengine kukuzuie usiwapende?

Tuendeleapo kujitahidi kufuata kielelezo cha Kristo, tutakosea mara nyingi. Hata hivyo, bila shaka Yehova anapendezwa na jitihada zetu za ‘kumvaa Bwana Yesu Kristo.’—Waroma 13:14.

Vielelezo kwa Kundi”

Je, kuna wowote katika kutaniko leo wawezao kuwa vielelezo kwetu? Kwa hakika wako! Hasa ndugu wenye madaraka waliowekwa rasmi wapaswa kuwa vielelezo vizuri. Paulo alimwambia Tito, aliyetumikia makutaniko huko Krete na ambaye aliweka rasmi waangalizi, kwamba kila mzee aliyewekwa rasmi lazima awe ‘mtu asiye na shtaka.’ (Tito 1:5, 6) Vivyo hivyo, mtume Petro aliwashauri “wanaume wazee” wawe “vielelezo kwa kundi.” (1 Petro 5:1-3) Namna gani watumishi wa huduma? Wao pia lazima wawe wanaume “wahudumuo kwa njia bora.”—1 Timotheo 3:13.

Bila shaka, hatutarajii kwamba kila mzee au mtumishi wa huduma atakuwa stadi kabisa katika sehemu zote za huduma ya Kikristo. Paulo aliwaambia hivi Wakristo katika Roma: “Tuna zawadi zinazotofautiana kulingana na fadhili isiyostahiliwa tuliyopewa.” (Waroma 12:6) Akina ndugu wana vipawa tofauti-tofauti. Hatupaswi kutarajia kwamba wazee watasema na kutenda kwa ukamilifu. “Sisi sote hujikwaa mara nyingi,” Biblia yasema katika Yakobo 3:2. “Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” Hata hivyo, ijapokuwa kutokamilika kwao, wazee waweza kuwa ‘vielelezo kwa waaminifu katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili,’ kama alivyokuwa Timotheo. (1 Timotheo 4:12) Ikiwa wazee ni vielelezo vizuri, washiriki wa kundi watakuwa tayari kufuata shauri la Waebrania 13:7: “Kumbukeni wale ambao wanaongoza miongoni mwenu, . . . nanyi mfikiriapo jinsi mwisho wa mwenendo wao upatavyo kuwa, igeni imani yao.”

Vielelezo Vingine vya Kisasa

Katika miongo iliyopita, wengi wamejionyesha kuwa vielelezo vizuri. Je, wamishonari ambao wamejitolea na kuacha ‘nyumba au akina ndugu au akina dada au baba au mama au watoto au mashamba’ ili kutimiza utume wa Kikristo katika nchi za kigeni, waweza kuwa vielelezo kwetu? (Mathayo 19:29) Fikiria pia, waangalizi wasafirio na wake zao, wanaume na wanawake ambao wamejitolea kutumikia katika ofisi za Watch Tower Society, nao mapainia wanaotumikia makutanikoni. Je, vielelezo kama hivyo vyaweza kuwachochea wengine? Mhubiri mmoja Mkristo kule Asia anakumbuka mishonari mmoja aliyehitimu darasa la nane la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Alisema kwamba ndugu huyo mwaminifu alikuwa “tayari kuvumilia mbu wengi na unyevuanga mbaya sana. . . . Kilichopendeza hata zaidi kilikuwa uwezo wake wa kuhubiri katika lugha za Kichina na Kimalaysia, ingawa alikuwa Mwingereza.” Kielelezo chake kizuri kilikuwa na matokeo gani? Ndugu huyo akasema: “Utulivu wake na uhakika wake ulinitia moyo nitake kuwa mishonari wakati ambapo ningekuwa mtu mzima.” Si ajabu kwamba ndugu huyo akawa mishonari.

Katika fahirisi ya Watch Tower Publications Index kuna orodha ya masimulizi ya maisha ambayo yamechapishwa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Masimulizi hayo hueleza juu ya watu ambao wameacha kufuatia kazi na miradi ya ulimwengu, wameweza kushinda udhaifu mbalimbali, wamefanya mabadiliko makubwa katika nyutu zao, wamedumisha mtazamo unaofaa ijapokuwa taabu; na jinsi ambavyo wamekuwa na bidii, uvumilifu, ushikamanifu, unyenyekevu, na roho ya kujitolea. Msomaji mmoja aliandika hivi kuhusu masimulizi hayo: “Nisomapo mambo ambayo yamewapata wengine, mambo hayo hunisaidia kuwa Mkristo mnyenyekevu zaidi na mwenye shukrani zaidi, nayo yamenisaidia nisijifikirie mno wala kuwa na ubinafsi.”

Kwa kuongezea, usisahau vielelezo vizuri katika kutaniko lako mwenyewe: vichwa vya familia wanaoendelea kuandalia familia zao mahitaji ya kimwili na ya kiroho; akina dada—kutia ndani akina mama wasio na mwenzi wa ndoa—wanaopambana na mikazo ya kulea watoto huku wakihubiri kwa ukawaida; wazee na walio dhaifu wanaoendelea kuwa waaminifu ijapokuwa wanazidi kudhoofika na kuwa wagonjwa. Je, unatiwa moyo na vielelezo hivyo?

Ni kweli, ulimwengu umejaa vielelezo vibaya. (2 Timotheo 3:13) Hata hivyo, ebu fikiria jinsi Paulo alivyowahimiza Wakristo walioishi Yudea. Baada ya kusimulia mwenendo uliostahili kusifiwa wa wanaume na wanawake wengi wa kale wenye imani, Paulo aliwasihi: “Kwa hiyo, basi, kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi likituzingira, acheni sisi pia . . . tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu, tumkaziapo macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.” (Waebrania 12:1, 2) Leo pia, Wakristo wamezingirwa na “wingu kubwa” la vielelezo bora—vya kale na vya siku hizi. Je, unanufaishwa navyo kwelikweli? Utanufaika ukiazimia kuwa “mwigaji, si wa lililo baya, bali wa lililo jema.”—3 Yohana 11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Bila shaka, hatutarajii kwamba kila mzee au mtumishi wa huduma atakuwa stadi kabisa katika sehemu zote za huduma ya Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wazee wapaswa kuwa “vielelezo kwa kundi”