Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wapaswa Kuchunguza Dini Nyingine?

Je, Wapaswa Kuchunguza Dini Nyingine?

Je, Wapaswa Kuchunguza Dini Nyingine?

“NILIKUWA nimehudhuria mikutano ya Kikristo kwa muda wa mwaka mmoja hivi, na nilifurahi kuwaeleza wengine kuhusu Ufalme wa Mungu,” asema Miguel, ambaye sasa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika Amerika Kusini. “Kisha nikaanza kusikiliza vipindi vya kidini kwenye redio na kutazama wahubiri wa kidini kwenye televisheni. Nilifikiri kwamba vipindi hivyo vingenisaidia kuwaelewa vizuri zaidi watu wa dini nyingine. Nilitambua kwamba mafundisho yao hayakupatana na Biblia, lakini nilikuwa mdadisi.”

Katika nchi hiyohiyo, Jorge alikuwa na bidii ya kufundisha wengine kuhusu ibada ya kweli. Hata hivyo, wakati fulani yeye pia akaanza kusikiliza programu za kidini kwenye redio na televisheni. Alizoea kusema “unahitaji kujua jinsi wengine wanavyofikiri.” Alipoulizwa juu ya hatari anazoweza kukabili kwa kusikiliza mafundisho hayo yasiyo ya kweli, alikuwa akijibu hivi: “Hakuna kitu kinachoweza kudhoofisha imani ya mtu anayejua kweli ya Biblia.” Mambo hayo yaliyoonwa yanatokeza swali la maana, Je, ni jambo la hekima kusikiliza yale ambayo wengine wanaamini?

Kutambua Ukristo wa Kweli

Baada ya mitume kufa, ibada ya kweli ilichafuliwa na namna mbalimbali za Ukristo bandia uliotokea hatua kwa hatua. Akiona kimbele jambo hilo, Yesu alifunua njia moja ya kupambanua kati ya namna mbalimbali za Ukristo bandia na Ukristo wa kweli. Kwanza, alionya hivi: “Iweni wenye kulinda kuhusu manabii wasio wa kweli ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwa-mwitu walafi.” Kisha akaongezea hivi: “Kwa matunda yao mtawatambua.” (Mathayo 7:15-23) Wafuasi wa kweli wa Yesu hufanya yale aliyofundisha, nao hutambuliwa kwa urahisi kwa matunda yao mazuri. Kama alivyofanya Yesu mwenyewe, wanatembelea watu ili kuwaeleza juu ya Ufalme wa Mungu kwa kutumia Maandiko. Wanafuata kielelezo cha Yesu, na hivyo kujiepusha na ugomvi wa kisiasa na wa kijamii. Wanakubali Biblia kuwa Neno la Mungu na kuiheshimu kuwa ile kweli. Wanajulisha jina la Mungu. Na kwa kuwa wanajitahidi kuonyesha upendo ambao Mungu anafundisha, hawaendi vitani. Badala yake, kila mmoja anamwona mwenzake kuwa ndugu.—Luka 4:43; 10:1-9; Yohana 13:34, 35; 17:16, 17, 26.

Kulingana na Maandiko, inawezekana “[ku]pambanua kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.” (Malaki 3:18) Leo, waabudu wa kweli wameungana katika wazo na tendo, kama walivyofanya Wakristo wa karne ya kwanza. (Waefeso 4:4-6) Unapotambua kikundi hicho cha Wakristo wa kweli, kwa nini udadisi itikadi za watu wengine?

Jihadhari na Walimu Bandia

Biblia hukiri kwamba hata baada ya kujifunza kweli ya Biblia, mtu aweza kuchafuliwa kiroho na mafundisho bandia. Mtume Paulo alionya hivi: “Jihadharini: labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” (Wakolosai 2:8) Andiko hili latoa ufafanuzi ulio wazi kama nini! Kama wanyama wanaotaka kukunasa na kukumeza, walimu bandia wanaweza kutokeza hatari halisi.

Ni kweli kwamba Paulo alijua yale ambayo wengine waliamini. Wakati fulani alianza hotuba kwa kusema hivi: “Wanaume wa Athene, naona kwamba katika mambo yote mwaonekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuhofu miungu kuliko wengine walivyo. Kwa mfano, nilipokuwa nikipita njiani na kutazama kwa uangalifu vitu vyenu vya kupewa heshima inayozidi nilikuta pia madhabahu ambayo juu yayo ilikuwa imeandikwa ‘Kwa Mungu Asiyejulikana.’” (Matendo 17:22, 23) Hata hivyo, Paulo hakulisha akili yake kwa ukawaida falsafa za wasemaji Wagiriki.

Kuna tofauti kati ya kufahamu asili na itikadi za dini bandia na kujilisha itikadi hizo. * Yehova amemweka “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aandae mafundisho yanayotegemea Neno lake. (Mathayo 4:4; 24:45) Paulo mwenyewe aliandika hivi: “Hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu. Au je, ‘tunamchochea Yehova kwenye wivu’?”—1 Wakorintho 10:20-22.

Huenda baadhi ya walimu bandia walikuwa Wakristo wa kweli hapo awali, lakini wakati fulani wakageukia kosa na kuacha kweli. (Yuda 4, 11) Hatupaswi kushangazwa na jambo hilo. Baada ya kuzungumza juu ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anayewakilisha kundi la Wakristo watiwa-mafuta, Yesu alizungumza juu ya “mtumwa mwovu,” jamii ya walalamikaji wanaosema kwamba, “bwana-mkubwa wangu anakawia,” na kuanza kupiga watumwa wenzake. (Mathayo 24:48, 49) Mara nyingi, watu hawa na wafuasi wao hawana mafundisho dhahiri yaliyo yao wenyewe: wanapenda tu kuharibu imani ya wengine. Mtume Yohana aliandika hivi kuwahusu: “Ikiwa yeyote aja kwenu na haleti ufundishaji huu, msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kusema salamu kwake.”—2 Yohana 10; 2 Wakorintho 11:3, 4, 13-15.

Inafaa watu wenye moyo mweupe wanaotafuta ile kweli wafikirie kwa makini yale wanayosikia kutoka kwa dini tofauti-tofauti. Halafu, Mungu atabariki watu wenye moyo mnyofu wanaotafuta ile kweli. Biblia husema hivi kuhusu hekima ya kimungu: ‘Ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapopata kumjua Mungu.’ (Mithali 2:4, 5) Baada ya kupata ujuzi huo kuhusu Mungu kupitia Biblia na kutaniko la Kikristo, na kuona jinsi Yehova anavyobariki wale wanaoongozwa na ujuzi huo, Wakristo wa kweli hawaendelei kusikiliza mafundisho bandia ya kidini.—2 Timotheo 3:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., kina habari ya msingi kuhusu historia na mafundisho ya dini nyingi za ulimwengu.