Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nimeifanya Roho Takatifu Kuwa Msaidizi Wangu wa Kibinafsi?

Je, Nimeifanya Roho Takatifu Kuwa Msaidizi Wangu wa Kibinafsi?

Je, Nimeifanya Roho Takatifu Kuwa Msaidizi Wangu wa Kibinafsi?

WANATHEOLOJIA, mbali na watu wengine kwa ujumla, wana maoni mbalimbali kuhusu roho takatifu ya Mungu. Hata hivyo, si lazima kuwe na hali hiyo ya kukosa uhakika. Biblia hueleza waziwazi juu ya roho takatifu. Hiyo si mtu, kama wengine wanavyodai; ni kani ya utendaji yenye nguvu ambayo Mungu hutumia kutekeleza kusudi lake.—Zaburi 104:30; Matendo 2:33; 4:31; 2 Petro 1:21.

Kwa kuwa roho takatifu yahusiana sana na kutimizwa kwa makusudi ya Mungu, twapaswa kupatanisha maisha yetu nayo. Twapaswa kuifanya kuwa msaidizi wetu wa kibinafsi.

Msaidizi—Kwa Nini Anahitajiwa?

Akitazamia wakati ambapo angeondoka duniani, Yesu aliwahakikishia hivi wafuasi wake: “Nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji mwingine awe pamoja nanyi milele.” Tena: “Mimi ninawaambia nyinyi kweli, ni kwa manufaa yenu mimi ninaenda zangu. Kwa maana nisipoenda zangu, msaidiaji hatakuja kwenu kwa vyovyote; bali nikishika njia kwenda zangu, hakika nitamtuma yeye kwenu.”— Yohana 14:16, 17; 16:7.

Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi muhimu kwa kuwaagiza hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Hiyo haingekuwa kazi rahisi kwa kuwa ingetimizwa chini ya upinzani.—Mathayo 10:22, 23.

Mbali na upinzani kutoka nje, kungekuwako pia mgongano wa kiwango fulani kutanikoni. ‘Sasa nawahimiza nyinyi akina ndugu,’ Paulo akawaandikia Wakristo wa Roma yapata mwaka wa 56 W.K., “mfulize kuangalia wale wasababishao migawanyiko na sababu za kukwaza kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, na mwaepuke.” (Waroma 16:17, 18) Hali hiyo ingekuwa mbaya zaidi baada ya mitume kufa. Paulo alionya hivi: “Mimi najua kwamba baada ya kwenda zangu mbwa-mwitu wenye kuonea wataingia miongoni mwenu na hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka miongoni mwenu nyinyi wenyewe wanaume watainuka na kusema mambo yaliyopotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”—Matendo 20:29, 30.

Msaada wa Mungu ulihitajiwa ili kushinda vizuizi hivyo. Mungu alifanya hivyo kupitia Yesu. Baada ya kufufuliwa, siku ya Pentekoste 33 W.K., wafuasi wake wapatao 120 “wote wakawa wenye kujazwa roho takatifu.”—Matendo 1:15; 2:4.

Wanafunzi walitambua kwamba roho takatifu iliyomwagwa pindi hiyo ilikuwa msaada ambao Yesu alikuwa ameahidi. Bila shaka, sasa walielewa vizuri zaidi utambulisho ambao Yesu alitoa: “Msaidiaji, roho takatifu, ambayo Baba atapeleka katika jina langu, hiyo itawafundisha nyinyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yohana 14:26) Pia aliiita, ‘msaidiaji, roho ya ile kweli.’—Yohana 15:26.

Roho Ni Msaidizi Jinsi Gani?

Roho ingetumika kuwa msaidizi katika njia mbalimbali. Kwanza, Yesu aliahidi kwamba ingewakumbusha wanafunzi wake mambo aliyowaambia. Alimaanisha kwamba ingewasaidia kukumbuka zaidi ya maneno tu. Roho ingewasaidia waelewe mambo yenye kina na waone umuhimu wa yale aliyofundisha. (Yohana 16:12-14) Kwa ufupi, roho ingewasaidia wanafunzi wake waelewe vizuri zaidi ile kweli. Baadaye mtume Paulo aliandika hivi: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua kupitia roho yake, kwa maana roho huchunguza ndani ya mambo yote, hata mambo yenye kina kirefu ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Ili wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu wawafundishe wengine ujuzi sahihi, walihitaji kuwa na uelewevu wenye misingi imara.

Pili, Yesu alifundisha wanafunzi wake wasali mara nyingi. Ikiwa nyakati fulani wangekosa kujua jambo la kusali, roho ingeweza kuwaombea au ingewasaidia. “Kwa namna hiyo roho pia hujiunga kutoa msaada kwa ajili ya udhaifu wetu, kwa maana tatizo la tupasalo kusali kwa ajili yalo kama tuhitajivyo hatujui, lakini hiyo roho yenyewe hutuombea pamoja na upigaji-kite usiotamkwa.”—Waroma 8:26.

Tatu, ingewasaidia wanafunzi wa Yesu kutetea ile kweli hadharani. Aliwaonya hivi: “Watawakabidhi nyinyi kwenye mahakama za mtaa, nao watawapiga nyinyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtaburutwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa. Hata hivyo, wakati wawakabidhipo nyinyi, msiwe wenye kuhangaikia jinsi gani au jambo gani mtakalosema; kwa maana lile mtakalosema litapewa kwenu katika saa hiyo; kwa maana wanaosema si nyinyi tu, bali ni roho ya Baba yenu isemayo kupitia nyinyi.”—Mathayo 10:17-20.

Pia roho takatifu ingesaidia kutambulisha kutaniko la Kikristo na kuchochea washiriki wake wafanye maamuzi ya kibinafsi yenye hekima. Acheni tuzungumzie kindani zaidi mambo hayo mawili kuhusu habari hiyo na kuona yana maana gani kwetu leo.

Kutumika Kama Alama ya Utambulisho

Kwa karne nyingi Wayahudi walitumikia chini ya Sheria ya Kimusa wakiwa watu walioteuliwa na Mungu. Kwa kuwa walimkataa Yesu kuwa Mesiya, alitabiri kwamba punde si punde wao pia wangekataliwa: “Je, hamkusoma kamwe katika Maandiko, ‘Jiwe walilolikataa wajenzi ndilo limekuwa jiwe la pembeni lililo kuu. Kutoka kwa Yehova hilo limekuja kuwa, nalo ni la kustaajabisha machoni petu’? Hiyo ndiyo sababu nawaambia nyinyi, Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa kwa taifa lenye kutokeza matunda yao.” (Mathayo 21:42, 43) Baada ya kutaniko la Kikristo kuanzishwa kwenye Pentekoste 33 W.K., wafuasi wa Kristo wakawa “taifa lenye kutokeza matunda yao.” Kuanzia wakati huo na kuendelea kutaniko hili likawa njia ya Mungu ya mawasiliano. Ili watu watambue kwamba Mungu alikuwa amehamisha kibali chake, Mungu aliandaa alama ya utambulisho iliyo dhahiri.

Kwenye Pentekoste, roho takatifu iliwawezesha wanafunzi kusema kwa lugha ambazo hawakuwa wamepata kujifunza na kufanya watazamaji washangae na kuuliza hivi: “Ni jinsi gani sisi, kila mmoja wetu, tunasikia lugha yake mwenyewe ambayo katika hiyo tulizaliwa?” (Matendo 2:7, 8) Uwezo wa kuzungumza katika lugha wasizojua, pamoja na “mambo mengi ya ajabu na ishara [ambazo] zikaanza kutukia kupitia mitume,” ulifanya watu wapatao elfu tatu kutambua kwamba kwa kweli roho ya Mungu ilikuwa ikitenda.—Matendo 2:41, 43.

Pia, kwa kutokeza “matunda ya roho”—upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti—wanafunzi wa Kristo walitambuliwa waziwazi kuwa watumishi wa Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hakika, upendo, ulitambulisha waziwazi kutaniko la Kikristo la kweli. Yesu alitabiri hivi: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—Yohana 13:34, 35.

Washiriki wa kutaniko la Kikristo la mapema walikubali kuongozwa na roho takatifu ya Mungu na kutumia ifaavyo msaada iliyotoa. Ingawa Wakristo leo wanatambua kwamba Mungu hafufui wafu na kufanya miujiza kama alivyofanya katika karne ya kwanza, wanaruhusu matunda ya roho ya Mungu yawatambulishe kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.—1 Wakorintho 13:8.

Msaidizi Katika Kufanya Maamuzi ya Kibinafsi

Biblia iliandikwa kupitia roho takatifu. Kwa hiyo, tunapokubali kushawishiwa na Biblia, ni kana kwamba tunafundishwa na roho takatifu. (2 Timotheo 3:16, 17) Inaweza kutusaidia tufanye maamuzi yenye hekima. Lakini je, tunairuhusu itusaidie?

Kwa mfano, tunachagua kazi ya aina gani? Roho takatifu itatuwezesha tuone kazi tunayoelekea kupata kwa maoni ya Yehova. Lazima kazi yetu ipatane na kanuni za Biblia, na ikiwezekana yapasa kutusaidia tufuatie miradi ya kitheokrasi. Mshahara au umashuhuri wa kazi si jambo la maana. Jambo la maana zaidi ni kama inatuandalia mahitaji ya maisha na kutupa wakati na fursa ya kutosha kutimiza wajibu wetu mbalimbali wa Kikristo.

Ni jambo la kawaida na linalofaa kutamani kufurahia maisha. (Mhubiri 2:24; 11:9) Kwa hiyo Mkristo mwenye usawaziko aweza kufuatia tafrija ili kujiburudisha na kujifurahisha. Lakini apaswa kuchagua tafrija ambayo itamwezesha kudhihirisha matunda ya roho, si ile inayokazia “kazi za mwili.” Paulo aeleza hivi: “Sasa kazi za mwili ni dhahiri, nazo ni uasherati, ukosefu wa usafi, mwenendo mlegevu, ibada ya sanamu, zoea la uwasiliani-roho, uadui, zogo, wivu, hasira za ghafula, magomvi, migawanyiko, mafarakano, husuda, vipindi vya kulewa, sherehe zenye kelele za ulevi na ulafi, na mambo kama haya.” Pia twapaswa kuepuka kuwa “wenye majisifu ya bure, wenye kuchochea shindano juu ya mtu na mwenzake, tukihusudiana.”—Wagalatia 5:16-26.

Ndivyo ilivyo kuhusu kuchagua marafiki. Ni jambo la hekima kuwachagua kulingana na hali ya kiroho, si kulingana na sura ya nje au mali. Bila shaka Daudi alikuwa rafiki ya Mungu, kwa kuwa Mungu alisema kwamba yeye ni “mwanamume mwenye kukubalika kwa moyo [wake].” (Matendo 13:22) Bila kuangalia sura ya nje, Mungu alimchagua Daudi kuwa mfalme wa Israeli, kulingana na kanuni hii: “BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.”—1 Samweli 16:7.

Urafiki wa maelfu umevunjika, kwa sababu ulitegemea sura ya nje au mali. Urafiki unaotegemea utajiri usiotegemeka waweza kuvunjika kwa ghafula. (Mithali 14:20) Neno la Mungu lililopuliziwa kwa roho hutushauri kwamba tunapochagua marafiki, twapaswa kuchagua wale wanaoweza kutusaidia kumtumikia Yehova. Hutuambia tuwe tunatoa badala ya kupokea kwa sababu kutoa hutokeza shangwe kubwa zaidi. (Matendo 20:35) Kati ya mambo yenye thamani zaidi tunayoweza kuwapa marafiki wetu ni wakati na shauku.

Kwa Mkristo anayetafuta mwenzi wa ndoa, Biblia huandaa shauri lililopuliziwa kwa roho. Ni kana kwamba inasema: ‘Usitazame tu uso na umbo. Tazama miguu.’ Miguu? Naam, katika maana hii: Je, inatumiwa kufanya kazi ya Yehova ya kuhubiri habari njema, na kwa njia hiyo ni mizuri machoni pake? Je, imevikwa ujumbe wa ile kweli na habari njema za amani? Twasoma hivi: “Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima miguu yake aletaye habari njema, yeye aitangazaye amani, aletaye habari njema ya mambo mema, yeye autangazaye wokovu, auambiaye Sayuni, Mungu wako anamiliki.”—Isaya 52:7; Waefeso 6:15.

Kwa kuwa tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” twahitaji msaada katika kufanya mapenzi ya Mungu. (2 Timotheo 3:1) Roho takatifu ya Mungu, ikiwa msaidizi, ilitegemeza sana kazi ya Wakristo katika karne ya kwanza, kutia ndani kuwa msaidizi wao wa kibinafsi. Njia kuu ambayo sisi pia twaweza kufanya roho takatifu iwe msaidizi wetu wa kibinafsi ni kwa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu ambalo liliandikwa kupitia roho takatifu. Je, tumefanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 23]