Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unataka Kubaki na Pesa Zako au Uhai Wako?

Je, Unataka Kubaki na Pesa Zako au Uhai Wako?

Je, Unataka Kubaki na Pesa Zako au Uhai Wako?

Huenda umesikia kuhusu majambazi waliowaelekezea watu bunduki, na kudai: “Pesa zako au uhai wako!” Leo, twafahamu dai hilo linalojulikana sana kwa sababu ya jambo gumu linalotutatanisha sote—hasa sisi ambao tunaishi katika nchi zenye utajiri. Hata hivyo, sasa si jambazi anayedai hivyo, bali ni jinsi jamii inavyokazia sana pesa na mafanikio ya kimwili.

KWA sababu ya kukaziwa sana kwa vitu hivyo, watu wamekuwa na masuala na mahangaiko mapya. Pesa na vitu vya kimwili vyapasa kufuatiwa kwa kadiri gani? Je, tunaweza kuridhika na vitu vichache vya kimwili? Je, kwa kweli watu wanapoteza “uhai ulio halisi” kusudi wapate vitu vya kimwili? Je, pesa zaweza kufanya uwe na maisha yenye furaha?

Kutamani Pesa Kupita Kiasi

Kati ya tamaa za mwanadamu zinazofaa na zisizofaa—upendo wa pesa ndio wa kwanza. Tofauti na tamaa ya ngono na ya chakula, tamaa ya pesa inayopita kiasi yaweza kuendelea bila kukoma. Tamaa hiyo haiishi hata mtu anapozeeka. Katika visa vingi kwa kweli uzee waweza kufanya mtu awe na tamaa na mahangaiko zaidi kuhusu pesa na vitu ambavyo pesa zaweza kununua.

Pupa ya pesa inaonekana kuwa inaongezeka. Mchezaji mmoja maarufu katika sinema fulani mashuhuri alisema hivi: “Pupa hunufaisha. Pupa ni nzuri.” Ijapokuwa wengi walirejezea miaka ya 1980 kuwa Kipindi cha Pupa, mambo yaliyotukia kabla na baada ya hapo yanaonyesha kwamba mtazamo wa wanadamu kuelekea pesa haujabadilika sana katika miaka ambayo imepita.

Labda jambo ambalo ni jipya ni kwamba watu wengi sana hupata fursa za kutosheleza mara moja tamaa ya kupata pesa zaidi. Inaonekana kwamba watu wengi ulimwenguni mara nyingi hutumia nishati yao nyingi kutengeneza na kujipatia vitu vya kimwili kwa wingi zaidi. Huenda ukakubali kwamba mara nyingi kuwa na vitu vya kimwili na kutumia pesa kumekuwa jambo linalofikiriwa sana na linalofanywa kwa bidii katika maisha ya kisasa.

Lakini je, watu wamepata furaha zaidi kwa kufanya hivyo? Kwa kujibu swali hilo, Mfalme Solomoni mwenye hekima na utajiri mwingi aliandika hivi miaka 3,000 iliyopita: “Apendaye fedha hatashiba fedha, wala apendaye wingi hatashiba nyongeza. Hayo pia ni ubatili.” (Mhubiri 5:10) Masomo ya kisasa yanayohusu mambo ya kijamii yanafikia mikataa hiyo isiyo ya kawaida.

Pesa na Furaha

Mojawapo ya ugunduzi wenye kushangaza zaidi kuhusu tabia ya wanadamu ni kwamba kulundika pesa na vitu vya kimwili hakutokezi furaha na uradhi. Watafiti wengi wametambua kwamba mtu anapopata utajiri wa kiasi fulani, furaha na uradhi wake hautegemei vitu vya kimwili alivyo navyo.

Hivyo, kufuatia pesa na vitu vya kimwili kupita kiasi hufanya wengi wajiulize, ‘Inaonekana tunafurahia kila kitu kipya tunachonunua; lakini, kwa nini baada ya kufanya mambo yote hayo, furaha hiyo haileti uradhi zaidi?’

Katika kitabu chake Happy People, mwandishi Jonathan Freedman asema kwamba watu wakiwa na pesa za mahitaji ya lazima, kuongeza mapato yao hakuhusiani na kuongezeka kwa furaha yao. Wengi wametambua kwamba jambo linalofanya watu wawe na furaha ni kufuatia mambo ya kiroho, mambo yanayofaa maishani, na kanuni za kiadili. Jambo la maana pia ni kuwa na uhusiano mzuri na wengine na kujiepusha na mahitilafiano au hali zinazoweza kutuzuia kufurahia vitu tulivyo navyo.

Wengi huona kwamba matatizo mengi ya sasa ya kijamii husababishwa hasa na mwelekeo wa kujaribu kutumia ufanisi wa kimwili kutatua matatizo ambayo kwa kweli ni ya moyoni. Maripota fulani wa mambo ya kijamii wanataja kwamba kwa ujumla kuna hali ya shaka na kutoridhika. Pia wanasema kwamba watu wengi katika nchi zenye utajiri huwaendea matabibu au kutafuta kusudi la maisha na amani ya akili kutoka kwa walimu wa dini ya Kihindu, madhehebu, na vikundi vinavyodai kutoa tiba. Hilo lathibitisha kwamba vitu vya kimwili haviwezi kufanya maisha yawe na kusudi.

Pesa Zinapokuwa na Uwezo na Zinapokosa Uwezo

Ni kweli kwamba pesa zina uwezo. Zaweza kununua nyumba nzuri, mavazi yenye kupendeza, na fanicha safi sana. Pia zaweza kufanya mtu avutie, atimize tamaa fulani, au apate sifa bandia, na kuwa na marafiki wachache wa muda walio tayari kumfanyia mambo fulani. Lakini uwezo wa pesa unaishia hapo tu. Pesa haziwezi kununua kitu tunachohitaji zaidi—upendo wa rafiki mmoja wa kweli, amani ya akili, faraja kidogo tunapokaribia kufa. Na wale wanaothamini uhusiano wao pamoja na Muumba, pesa haziwezi kununua kibali cha Mungu.

Mfalme Solomoni, aliyefurahia vitu vyote vinavyoweza kununuliwa na pesa katika siku zake, alitambua kwamba kutegemea vitu vya kimwili hakuleti furaha ya kudumu. (Mhubiri 5:12-15) Pesa zinaweza kupotea benki zinapoporomoka au wakati wa inflesheni. Mali kama vile nyumba na mashamba zaweza kuharibiwa na dhoruba kali. Ingawa bima hugharimia kwa kiasi fulani hasara ya vitu vilivyoharibiwa, haiwezi kutoa kitulizo cha kihisia-moyo. Hisa na dhamana zaweza kupoteza thamani mara moja uchumi unapoporomoka kwa ghafula. Hata kazi yenye mshahara mnono inaweza kupotea kwa ghafula.

Kwa hiyo basi, twawezaje kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu pesa? Pesa au vitu vya kimwili vyapasa kuwa vya maana kadiri gani maishani mwetu? Tafadhali chunguza jambo hilo zaidi ili uone jinsi unavyoweza kupata kitu fulani chenye thamani ya kweli—“uhai ulio halisi.”

[Picha katika ukurasa wa 4]

Vitu vya kimwili havileti furaha ya kudumu