Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Mkiwa Imara Kama Ambao Mnaona Yeye Asiyeonekana!

Endeleeni Mkiwa Imara Kama Ambao Mnaona Yeye Asiyeonekana!

Endeleeni Mkiwa Imara Kama Ambao Mnaona Yeye Asiyeonekana!

“[Musa] aliendelea akiwa imara kama ambaye anaona Yeye asiyeonekana.”—Waebrania 11:27.

1. Yesu alisema jambo gani lenye kutokeza kuhusu Mungu kwenye Mahubiri yake ya Mlimani?

YEHOVA ni Mungu asiyeonekana. Musa alipoomba aone utukufu Wake, Yehova alijibu: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.” (Kutoka 33:20) Naye mtume Yohana aliandika: “Hakuna mtu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (Yohana 1:18) Yesu Kristo alipokuwa mwanadamu duniani, hata yeye hangeweza kumwona Mungu. Hata hivyo, kwenye Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema: “Wenye furaha ni wenye kutakata moyoni, kwa kuwa wao watamwona Mungu.” (Mathayo 5:8) Yesu alimaanisha nini?

2. Kwa nini hatuwezi kumwona Mungu kwa macho yetu halisi?

2 Maandiko humtaja Yehova kuwa Roho asiyeonekana. (Yohana 4:24; Wakolosai 1:15; 1 Timotheo 1:17) Hivyo, Yesu hakuwa akisema kwamba sisi wanadamu tunaweza kwa kweli kumwona Yehova kwa macho yetu halisi. Ni kweli kwamba Wakristo watiwa-mafuta watamwona Yehova Mungu mbinguni baada ya kufufuliwa wakiwa viumbe wa roho. Lakini wanadamu wenye “kutakata moyoni” walio na tumaini la kuishi milele katika dunia wanaweza “kumwona” Mungu pia. Inawezekanaje?

3. Wanadamu wanawezaje kufahamu baadhi ya sifa za Mungu?

3 Tunajifunza jambo fulani kumhusu Yehova kwa kuchunguza kwa makini vitu alivyoumba. Hivyo, huenda tukavutiwa na nguvu zake na kuchochewa kutambua kwamba yeye ndiye Mungu Muumba. (Waebrania 11:3; Ufunuo 4:11) Kuhusiana na hilo mtume Paulo aliandika: “Kwa maana sifa [za Mungu] zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.” (Waroma 1:20) Kwa hiyo, maneno ya Yesu juu ya kumwona Mungu hutia ndani uwezo wa kufahamu baadhi ya sifa za Yehova. Kuona huko kwategemea ujuzi sahihi na hufahamika kiroho kwa ‘macho ya moyo.’ (Waefeso 1:18) Maneno na matendo ya Yesu pia yanafunua mengi kumhusu Mungu. Hivyo, Yesu alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Yesu alidhihirisha kikamili utu wa Yehova. Hivyo, kujua maisha na mafundisho ya Yesu kunaweza kutusaidia kuona, au kufahamu, baadhi ya sifa za Mungu.

Hali ya Kiroho Ni Muhimu

4. Leo wengi wanadhihirishaje kwamba si watu wa kiroho?

4 Leo, imani na hali ya kweli ya kiroho ni haba kwelikweli. Paulo alisema: “Imani si miliki ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Wengi wamejiingiza sana katika kufuatia mambo ya kibinafsi na hawana imani katika Mungu. Mwenendo wao wenye dhambi na kutokuwa watu wa kiroho huwazuia kumwona kwa macho ya uelewevu, kwa kuwa mtume Yohana aliandika: “Yeye ambaye atenda baya hajaona Mungu.” (3 Yohana 11) Kwa sababu watu hao hawamwoni Mungu kwa macho halisi, wanatenda kana kwamba Mungu haoni wanayofanya. (Ezekieli 9:9) Wao hudharau mambo ya kiroho, hivyo hawawezi kupata “kumjua Mungu.” (Mithali 2:5) Basi, kwa kufaa Paulo aliandika: “Mtu wa kimwili hayapokei mambo ya roho ya Mungu, kwa maana hayo ni upumbavu kwake; naye hawezi kupata kuyajua, kwa sababu hayo huchunguzwa kiroho.”—1 Wakorintho 2:14.

5. Watu ambao wanazingatia mambo ya kiroho wanafahamu jambo gani?

5 Hata hivyo, ikiwa tunazingatia mambo ya kiroho, tutakumbuka daima kwamba ingawa Yehova si Mungu wa kutafutatafuta makosa, yeye hujua tunapotenda kulingana na mawazo yetu na tamaa zetu mbaya. Naam, “njia za mwanadamu zi mbele za macho ya BWANA, na mienendo yake yote huitafakari.” (Mithali 5:21) Iwapo tunafanya dhambi, tunachochewa kutubu na kutafuta msamaha wa Yehova kwa sababu tunampenda na hatutaki kumhuzunisha.—Zaburi 78:41; 130:3.

Ni Nini Hutufanya Tuwe Imara?

6. Inamaanisha nini kuwa imara?

6 Ingawa hatuwezi kumwona Yehova kwa macho yetu, acheni sikuzote tukumbuke kwamba yeye anatuona. Kujua kwamba yeye yuko na kuwa na imani kwamba yeye yu karibu na wote wamwitao kutatusaidia tuwe imara, thabiti, na tusioondoleka katika uaminifu wetu kwake. (Zaburi 145:18) Tunaweza kuwa kama Musa ambaye Paulo aliandika hivi kumhusu: “Kwa imani aliondoka Misri, lakini bila kuihofu hasira ya mfalme, kwa maana aliendelea akiwa imara kama ambaye anaona Yeye asiyeonekana.”—Waebrania 11:27.

7, 8. Ni nini kilichompa Musa ujasiri mbele ya Farao?

7 Alipotekeleza utume aliopewa na Mungu wa kuwaongoza Waisraeli kutoka utumwani Misri, Musa alienda mara nyingi mbele ya Farao mkatili katika ua wa kifalme uliojaa wakuu wa kidini na kijeshi. Yaelekea kuta za jumba la kifalme zilikuwa na sanamu. Ingawa haonekani, Yehova alikuwa halisi kwa Musa, tofauti na sanamu zote zilizowakilisha miungu isiyo na uhai ya Misri. Si ajabu kwamba Musa hakutishwa na Farao!

8 Ni nini kilichompa Musa ujasiri wa kwenda mbele ya Farao tena na tena? Maandiko yanatuambia kwamba “huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Ni wazi kwamba hali yake ya kiroho yenye nguvu na imani kwamba Mungu alikuwa pamoja naye zilimpa Musa nguvu alizohitaji kumwakilisha ‘Yeye asiyeonekana’ mbele za mfalme mkatili wa Misri. Ni katika njia zipi wale ‘wanaomwona’ yeye asiyeonekana hudhihirisha imani kwake leo?

9. Ni kwa njia gani moja tunaweza kuendelea tukiwa imara?

9 Njia moja ya kuonyesha imani na kuendelea kuwa imara kama ambaye anamwona Yeye asiyeonekana ni kuhubiri kwa ujasiri licha ya upinzani. Yesu aliwaonya wanafunzi wake: “Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” (Luka 21:17) Pia aliwaambia: “Mtumwa si mkubwa zaidi kuliko bwana-mkubwa wake. Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia.” (Yohana 15:20) Maneno ya Yesu yalitimia punde baada ya kifo chake wakati wafuasi wake waliponyanyaswa kwa kutishwa, kukamatwa, na kupigwa. (Matendo 4:1-3, 18-21; 5:17, 18, 40) Ingawa mnyanyaso ulikuwa mwingi, mitume wa Yesu na wanafunzi wake wengine waliendelea kuhubiri habari njema kwa ujasiri.—Matendo 4:29-31.

10. Uhakika wetu kwamba Yehova anatulinda hutusaidiaje katika huduma?

10 Kama Musa, wafuasi wa mapema wa Yesu hawakutishwa na adui zao wengi wenye kuonekana. Wanafunzi wa Yesu walikuwa na imani katika Mungu, na kwa sababu hiyo wakaweza kuvumilia mnyanyaso huo mkali. Naam, waliendelea kuwa imara kama ambaye anamwona Yeye asiyeonekana. Leo, sisi huwa jasiri na wasioogopa katika kazi yetu ya kuhubiri Ufalme kwa kuwa sikuzote tunafahamu kwamba Yehova anatulinda. Neno la Mungu linasema kwamba “kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.” (Mithali 29:25) Hivyo, sisi haturudi nyuma kwa kuogopa kunyanyaswa; wala hatuaibikii huduma yetu. Imani yetu hutuchochea kutoa ushahidi kwa ujasiri kwa jirani zetu, wafanyakazi wenzetu, wanashule wenzetu, na wengineo.—Waroma 1:14-16.

Yeye Asiyeonekana Anaongoza Watu Wake

11. Kulingana na Petro na Yuda, baadhi ya watu walioshirikiana na kutaniko la Kikristo walidhihirishaje kwamba hawakuwa na hali nzuri ya kiroho?

11 Imani hutusaidia kuona kwamba Yehova ndiye anayeongoza tengenezo lake la kidunia. Hivyo tunaepuka kuwachambua wale wenye majukumu kutanikoni. Mtume Petro na Yuda, ndugu wa kambo wa Yesu, walionya juu ya watu fulani ambao hawakuwa na hali nzuri ya kiroho ambao walisema maneno yenye kuudhi juu ya wanaume wenye kuongoza miongoni mwa Wakristo. (2 Petro 2:9-12; Yuda 8) Je, watu hao wenye kutafutatafuta makosa wangalisema namna hiyo mbele za Yehova kama wangalikuwa wanamwona kihalisi? La, hasha! Lakini kwa kuwa Mungu haonekani, watu hao wa kimwili hawakufikiria kwamba wanawajibika mbele zake.

12. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea wale wenye kuongoza kutanikoni?

12 Ni kweli kwamba kutaniko la Kikristo limefanyizwa na watu ambao si wakamilifu. Wale wanaotumikia wakiwa wazee hufanya makosa ambayo nyakati nyingine yanaweza kutuathiri sisi binafsi. Hata hivyo, Yehova anatumia wanaume hao kuchunga kundi lake. (1 Petro 5:1, 2) Wanaume na wanawake wanaozingatia mambo ya kiroho hutambua kwamba hiyo ni njia moja ambayo Yehova hutumia kuongoza watu wake. Kwa hiyo, tukiwa Wakristo, sisi huepuka kuwa wenye kuchambua, kulalamika, nasi huonyesha heshima kwa mipango ya kitheokrasi ya Mungu. Kwa kuwatii wale wenye kuongoza miongoni mwetu, tunaonyesha kwamba tunamwona Yeye asiyeonekana.—Waebrania 13:17.

Kumwona Mungu Kuwa Mfunzi Wetu Mkuu

13, 14. Kumwona Yehova kuwa Mfunzi Mkuu humaanisha nini kwako?

13 Kuna sehemu nyingi ambayo inahitaji tuwe na ufahamu wa kiroho. Isaya alitabiri hivi: “Macho yako yatamwona Mfunzi wako Mkuu.” (Isaya 30:20, NW) Inahitaji imani kutambua kwamba Yehova ndiye anayetufunza kupitia tengenezo lake la kidunia. (Mathayo 24:45-47) Kumwona Mungu kuwa Mfunzi wetu Mkuu humaanisha mengi zaidi ya kuwa na mazoea mazuri ya kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Humaanisha kutumia kikamili maandalizi ya kiroho ya Mungu. Kwa mfano, tunahitaji kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mwongozo ambao Yehova hutoa kupitia Yesu ili tusipeperushwe mbali kiroho.—Waebrania 2:1.

14 Nyakati nyingine inahitaji jitihada za pekee ili kunufaika kikamili kutokana na chakula cha kiroho. Kwa mfano, huenda tukawa na mwelekeo wa kusoma kijuujuu tu masimulizi fulani ya Biblia tunayoona kuwa magumu kueleweka. Tunaposoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! labda tunakosa kusoma makala fulani kwa sababu hatupendezwi na habari inayozungumziwa. Au huenda tukaruhusu akili zetu zitangatange wakati wa mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, tunaweza kuendelea kuwa macho iwapo tunafikiria kwa makini mambo yanayozungumziwa. Uthamini wetu mkubwa kwa mafundisho ya kiroho tunayopokea huonyesha kwamba sisi humtambua Yehova kuwa Mfunzi wetu Mkuu.

Lazima Tutoe Hesabu

15. Watu wengine wametendaje kana kwamba Yehova hawaoni?

15 Imani katika Yeye asiyeonekana ni muhimu hasa kwa sababu uovu umeenea sana ‘siku hizi za mwisho.’ (Danieli 12:4) Ukosefu wa unyofu na ngono haramu zimeenea sana. Bila shaka, ni jambo la hekima kukumbuka kwamba Yehova huona matendo yetu hata wakati ambapo wanadamu hawawezi kutuona. Wengine wamekosa kutambua jambo hilo. Ikiwa wengine hawawaoni, wanaweza kufanya mambo yasiyopatana na Maandiko. Kwa mfano, wengine wameshawishiwa kutazama vitumbuizo na ponografia yenye kudhuru kupitia Internet, televisheni, na vifaa vingine vya tekinolojia ya kisasa. Kwa kuwa mambo kama hayo yanaweza kufanywa faraghani, watu wengine wanatenda kana kwamba Yehova haoni yale wanayofanya.

16. Ni nini chapasa kutusaidia kufuata viwango vya juu vya Yehova?

16 Inafaa kukumbuka maneno ya mtume Paulo: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:12) Tunahitaji kufahamu kwamba kila wakati tunapofanya dhambi, tunaifanya dhidi ya Yehova. Kujua hilo kwapasa kutusaidie kufuata viwango vyake vya juu na kuepuka mwenendo mchafu. Biblia hutukumbusha: “Hakuna kiumbe kisichokuwa dhahiri machoni pake, bali vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.” (Waebrania 4:13) Ni kweli kwamba lazima tumtolee Mungu hesabu, lakini hapana shaka kwamba tunafanya mapenzi ya Yehova na kufuata viwango vyake vya uadilifu kwa sababu tunampenda sana. Kwa hiyo, acheni tutumie busara katika mambo kama vitumbuizo tunavyochagua na jinsi tunavyojiendesha na watu wa jinsia tofauti.

17. Yehova hututazama akiwa na maoni gani?

17 Yehova anapendezwa nasi sana, lakini hilo halimaanishi kwamba anangojea tufanye makosa ili aweze kutuadhibu. Badala yake, yeye hututazama akiwa na hangaiko lenye upendo, kama lile la baba ambaye anataka kuwapa thawabu watoto wake watiifu. Inafariji kama nini kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni anapendezwa na imani yetu, naye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii”! (Waebrania 11:6) Na tuonyeshe imani kamili katika Yehova na ‘kumtumikia kwa moyo mkamilifu.’—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

18. Kwa sababu Yehova hututazama na huona uaminifu wetu, Maandiko hutuhakikishia nini?

18 Andiko la Mithali 15:3 lasema: “Macho ya BWANA yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.” Naam, Mungu huwachunguza watu wabaya na kuwatendea kupatana na mwenendo wao. Hata hivyo, iwapo sisi ni miongoni mwa wale ‘wema,’ tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova huona matendo yetu ya uaminifu. Inaimarisha imani kama nini kujua kwamba ‘kazi yetu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana’ na kwamba yeye asiyeonekana ‘hatasahau kazi yetu na upendo tulioonyesha kwa ajili ya jina lake’!—1 Wakorintho 15:58; Waebrania 6:10.

Kumruhusu Yehova Atuchunguze

19. Imani yenye nguvu katika Yehova huleta manufaa gani?

19 Sisi watumishi waaminifu wa Yehova tu wenye thamani sana kwake. (Mathayo 10:29-31) Ingawa haonekani, anaweza kuwa halisi kwetu, nasi tunathamini uhusiano wetu wenye thamani pamoja naye. Kuwa na mtazamo kama huo kuelekea Baba yetu wa mbinguni hutunufaisha sana. Imani yetu thabiti hutusaidia kuwa na moyo safi na dhamiri nzuri mbele za Yehova. Imani bila unafiki pia inatuzuia tusiishi maisha maradufu. (1 Timotheo 1:5, 18, 19) Imani yetu yenye nguvu katika Mungu ni kielelezo chema na inaweza kuwa na matokeo mazuri juu ya wale wanaotuzunguka. (1 Timotheo 4:12) Isitoshe, imani hiyo hufanya mtu asitawishe mwenendo unaokubaliwa na Mungu na kufanya moyo wa Yehova ufurahi.—Mithali 27:11.

20, 21. (a) Kwa nini ni jambo lenye manufaa kumruhusu Yehova atuchunguze? (b) Tunaweza kutumiaje Zaburi 139:23, 24?

20 Iwapo tuna hekima kwelikweli, tunafurahi kwamba Yehova hutuchunguza. Tunataka atuone na pia achunguze kikamili mawazo na matendo yetu. Katika sala, ni vema kumruhusu Yehova atuchunguze na kuona kama tuna maelekeo yasiyofaa. Bila shaka yeye anaweza kutusaidia kuvumilia matatizo yetu na kufanya marekebisho yanayohitajiwa. Kwa kufaa, mtunga-zaburi Daudi aliimba: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu; uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu, ukaniongoze katika njia ya milele.”—Zaburi 139:23, 24.

21 Daudi alimsihi Yehova amchunguze aone kama iko ‘njia yoyote iletayo majuto’ ndani yake. Kama mtunga-zaburi, je, hatutamani Mungu achunguze mioyo yetu na kuona kama tuna nia mbaya? Basi, kwa imani acheni tumwombe Yehova atuchunguze. Lakini vipi ikiwa tuna wasiwasi kuhusu kosa fulani au kuna jambo fulani linalotuumiza? Basi, acheni tuendelee kusali kwa bidii kwa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, na kufuata kwa unyenyekevu mwongozo wa roho yake takatifu na ushauri wa Neno lake. Tunaweza kuwa na hakika kwamba atatusaidia kufuata mwenendo ambao utatuongoza kwenye uhai udumuo milele.—Zaburi 40:11-13.

22. Yatupasa kuwa na azimio gani kuhusiana na staha kwa Yeye asiyeonekana?

22 Naam, Yehova atatubariki kwa uhai udumuo milele tukiyatimiza matakwa yake. Bila shaka, ni lazima tutambue uwezo na mamlaka yake, kama vile mtume Paulo alivyofanya alipoandika: “Kwa Mfalme wa umilele, asiyefisidika, asiyeonekana, Mungu pekee, kuwe heshima na utukufu milele na milele. Ameni.” (1 Timotheo 1:17) Sikuzote na tumwonyeshe Yehova staha hiyo ya kutoka moyoni. Na hata iweje, acheni tuwe thabiti katika azimio letu la kuendelea kuwa imara kama ambao wanaona Yeye asiyeonekana.

Unaweza Kujibuje?

• Wanadamu wanaweza kumwona Mungu jinsi gani?

• Ikiwa Yehova ni halisi kwetu, tutatendaje tukinyanyaswa?

• Inamaanisha nini kumwona Yehova kuwa Mfunzi wetu Mkuu?

• Kwa nini tutake kuchunguzwa na Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Musa hakutishwa na Farao bali alitenda kana kwamba angeweza kumwona Yehova, Mungu asiyeonekana

[Picha katika ukurasa wa 21]

Na tusitende kamwe kana kwamba Yehova hawezi kuona yale tunayofanya

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunatafuta kwa bidii kumjua Mungu kwa sababu sisi humwona kuwa Mfunzi wetu Mkuu