Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangilia kwa Tumaini la Ufalme!

Shangilia kwa Tumaini la Ufalme!

Shangilia kwa Tumaini la Ufalme!

ILIKUWA sherehe yenye furaha kukiwa na hudhurio la watu 5,784 waliokusanyika Machi 10, 2001, katika sehemu tatu zilizo katika Jimbo la New York zinazotumiwa na familia kubwa ya Betheli. Sherehe hiyo ilikuwa kuhitimu kwa darasa la 110 la shule ya mishonari ya Gileadi.

Carey Barber, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, aliwakaribisha wote na kufungua programu kwa kusema: “Tunafurahi kujua kwamba sasa wanafunzi wa madarasa 110 ya Gileadi wamezoezwa kuwa mishonari na kutumwa katika maeneo mbalimbali kote duniani.”

Jinsi Unavyoweza Kudumisha Shangwe

Baada ya maneno ya Ndugu Bar­ber ya kufungua programu, Don Adams alihutubia wahudhuriaji, kutia ndani wanafunzi 48 waliokuwa wakihitimu, kupitia hotuba yenye kichwa “Baraka za Yehova Hututajirisha.” Akitegemeza hotuba yake juu ya andiko la Mithali 10:22, aliwakumbusha wahudhuriaji kwamba Yehova hutegemeza na kuwabariki watumishi wake wanapotanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwao. Aliwatia moyo wanafunzi wakubali migawo yao wakiwa na nia kama ya mtume Paulo alipoombwa ‘avuke na kuingia Makedonia akasaidie.’ (Matendo 16:9) Ijapokuwa kulikuwa na magumu mengi, Paulo alinufaika sana kwa sababu ya kuwa na nia ya kuhubiri mahali alipotumwa.

Wanafunzi waliokuwa wakihitimu walikuwa wamemaliza kipindi cha miezi mitano cha kujifunza Biblia na kuzoezwa ili kuwa tayari kwa kazi ya mishonari. Hata hivyo, Daniel Syd­lik, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, aliwatia moyo waendelee kujifunza. Akizungumzia kichwa “Mwe Wanafunzi wa Kweli,” alisema hivi: “Kuwa mwanafunzi kwamaanisha kutii maneno ya Yesu daima. Kunatia ndani kuwa na nia ya kusikiliza maneno yake, ujumbe wake, na mafundisho yake daima.” Alisema kwamba wanafunzi wa Kristo hawafanyi maamuzi bila kusikiliza sauti ya Bwana-mkubwa wao; hekima ya Mungu inahusiana sana na maisha ya Kristo. (Wakolosai 2:3) Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kusikia maneno ya Yesu kwa mara moja tu na kukata kauli kwamba anajua kila neno kumhusu, kwa hiyo Ndugu Syd­lik aliwatia moyo wahitimu waendelee kujifunza, kutumia na kufundisha kweli ya Kikristo, ambayo hutokeza uhuru.—Yohana 8:31, 32.

Ili kudumisha shangwe katika utumishi wa Mungu, lazima mtu awe tayari kukubali nidhamu na sahihisho. “Je Mafigo Yako Yatakusahihisha?” ndilo swali lililozushwa na mfunzi wa Gileadi Law­rence Bow­en. Alieleza kwamba katika Biblia, mafigo ya mfano yanahusianishwa na mawazo na hisia za ndani za mtu. Yanaweza kumsahihisha mtu ikiwa shauri lililopuliziwa kutoka kwa Neno la Mungu limepenya kabisa kwenye utu wake. (Zaburi 16:7; Yeremia 17:10) Mwenendo wa mtu mwaminifu unaweza kugusa sana hisia za Yehova. Baada ya kusoma andiko la Mithali 23:15, 16, msemaji aliuliza hivi: “Je mafigo yako yatakusahihisha?” Aliongezea: “Tunatumaini kwamba ­yatakusahihisha, na hivyo kumfurahisha sana Yehova. Utakuwa umegusa hisia zake za ndani kabisa. Naam, utafurahisha mafigo ya Mungu unapodumu katika migawo yako kwa uaminifu.”

Hotuba ya mwisho kwenye programu ilitolewa na Mark Nou­mair, ambaye alikuwa mishonari nchini Kenya kabla hajawa mfunzi wa Gileadi. Hotuba yake iliyokuwa na kichwa “Ni Afadhali Kujionea kwa Macho” ilikazia umuhimu wa kusitawisha uradhi. Kupatana na andiko la Mhubiri 6:9, Ndugu Nou­mair alipendekeza: “Kubali mambo jinsi yalivyo. Huko ndiko ‘kuona kwa macho.’ Badala ya kuota juu ya jambo fulani unalotaka kufanya lakini haulifanyi, jitahidi kufanya yote uwezayo katika hali zako za sasa. Kuishi huku ukiota ndoto za mchana, kutarajia mambo usiyoweza kupata, au kufikiria sana mambo mabaya yanayokupata katika mgawo wako kutakufanya tu ukose uradhi. Naam, hata tuwe tunaishi wapi ama hali ziweje, kusitawisha uradhi wa kimungu katika hali zetu hufanya tuwe na mtazamo wenye shangwe tunapomtumikia Muumba wetu Mtukufu.

Mambo Yenye Kufurahisha Katika Utumishi wa Ufalme na Katika Gileadi

Baada ya mashauri hayo ya busara kupitia hotuba hizo, wanafunzi walieleza mambo fulani waliyofurahia walipokuwa katika huduma wakati wa mtaala wao wa miezi mitano. Chini ya mwelekezo wa Wal­lace Liv­er­ance, msajili wa Shule ya Gileadi, wanafunzi waliokuwa wakihitimu walisimulia jinsi walivyojipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu. (2 Wakorintho 4:2) Watu fulani walipendezwa na ujumbe wao. Mambo yaliyosimuliwa na wanafunzi yalionyesha jinsi mafunzo ya Biblia yalivyoanzishwa na watu wanyofu waliokutana nao barabarani, katika huduma ya nyumba kwa nyumba, na katika sehemu nyinginezo. Katika pindi mbalimbali, watu wenye kupendezwa walisema kwamba vichapo vya tengenezo la Yehova ambavyo vinategemea Biblia vilikuwa na ukweli. Mwenye nyumba mmoja alipendezwa sana na mstari fulani wa Biblia. Sasa anajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

Baada ya hapo, Joel Adams aliwahoji wahitimu wa Gileadi wa miaka iliyopita. Kichwa cha mazungumzo yake kilikuwa “Usiache Kujifunza, Usiache Kumtumikia Yehova.” Waliohojiwa waliwapa mishonari wapya mashauri ya wakati ufaao. Akikumbuka wakati ambapo alikuwa mshiriki wa darasa la 26 la Gileadi, Har­ry John­son alisema: “Tulifundishwa kwamba sikuzote Yehova amewaongoza watu wake na atazidi kuwaongoza. Uhakika huo umenitia moyo miaka yote.” Wil­liam ­Nonkes, mshiriki wa darasa la 53 la Gileadi, aliwashauri hivi wahitimu: “Zaidi ya yote, kumbukeni kanuni za Biblia na kuzitumia katika maamuzi yote mtakayofanya maishani mwenu sasa na milele. Mkifanya hivyo, hamtaacha mgawo wenu, naye Yehova atawabariki sana.”

Katika programu hiyo Rich­ard Rian alichagua hotuba yenye kichwa “Twaimarishwa Kufanya Mapenzi ya Yehova.” Kati ya watu aliowahoji kulikuwemo John Kurtz, mhitimu wa darasa la 30, ambaye ametumikia nchini Hispania akiwa mishonari kwa muda wa miaka zaidi ya 41. Alipoulizwa juu ya utaratibu wa masomo ya Gileadi, Ndugu Kurtz alisema: “Biblia ndicho kitabu kikuu cha mafundisho. Kisha tuna vifaa vya kujifunzia Biblia ambavyo hutusaidia kuielewa. Vifaa hivyo vinapatikana kwa wote. Hakuna mafundisho ya siri yanayofundishwa katika Gileadi. Mimi hukazia jambo hili daima kwa sababu wote wanaweza kupata kwa urahisi habari inayofundishwa Gileadi.”

Ndugu Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alimalizia programu hiyo ya kiroho kwa kuzungumzia hotuba yenye kichwa “Twasonga Mbele Tukiwa Chini ya Mabawa ya Yehova.” Alieleza jinsi ambavyo Biblia inafananisha ulinzi na utegemezo ambao Mungu huwapa watumishi wake waaminifu na mabawa ya tai. (Kumbukumbu la Torati 32:11, 12; Zaburi 91:4) Nyakati nyingine tai hutandaza mabawa yake kwa muda wa saa nyingi kusudi alinde makinda yake. Nyakati nyingine, huenda tai mzazi akafunika makinda yake kwa mabawa ili kuyalinda na upepo baridi. Vivyo hivyo, kwa kupatana na kusudi lake, Yehova anaweza kuwalinda watumishi wake waaminifu, hasa wanapokabili majaribu ya kiroho. Yehova haruhusu watumishi wake wajaribiwe kupita vile wawezavyo kuhimili, bali hufanya njia ya kutokea ili waweze kuvumilia. (1 Wakorintho 10:13) Ndugu Lösch alimalizia kwa kusema: “Ili tuendelee kulindwa kiroho, lazima tudumu chini ya mabawa ya Yehova. Hii yamaanisha kwamba hatupaswi kusitawisha roho ya kujitegemea. Acheni sikuzote tuendelee kuwa karibu na Yehova na tengenezo lake lililo kama mama, na tusijitenge na mwelekezo na shauri lake lenye upendo.”

Mwenyekiti alisoma salamu za watu kutoka sehemu zote za ulimwengu zilizotumwa kwa barua ili kuwatakia mema wahitimu hao. Kisha wakati wa kutoa diploma ukawadia. Shule ya Gileadi ilipoanzishwa, ilikusudiwa iwe na madarasa machache tu kwa muda wa miaka mitano. Lakini kwa muda wa miaka 58, Yehova Mungu amehakikisha kwamba shule hiyo imeendelea kufanywa. Kama alivyosema Ndugu Bar­ber katika maneno yake ya utangulizi: “Wahitimu wa Gileadi wamekuwa na sifa nzuri kama nini tangu mwaka wa 1943 wakati shule ya Gileadi ilipoanzishwa! Jitihada zao za pamoja zimefanya mamia ya maelfu ya watu wapole duniani waje kwenye tengenezo tukufu la Yehova.” Naam, shule hii ya mishonari imefanya mamilioni ya watu washangilie kwa kuwa na tumaini la Ufalme.

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi ­zilizowakilishwa: 8

Idadi ya nchi ­walikotumwa: 18

Jumla ya wanafunzi: 48

Wastani wa umri: 34

Wastani wa miaka katika kweli: 18

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13

[Picha katika ukurasa wa]

Darasa la 110 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha ifuatayo, nambari za safu zaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Vacek, E.; Madelin, L.; Evans, G.; Watanabe, K. (2) Trafford, P.; Turfa, J.; Wilson, P.; Williams, R.; ­Weber, A. (3) Johnson, T.; Hanau, K.; Mourlhou, F.; Charpentier, F.; Peckham, R.; Androsoff, P. (4) ­Seegers, T.; Seegers, D.; Bailey, P.; Bailey, M.; Madelin, K.; Lippold, E.; Lippold, T. (5) Evans, N.; Gold, R.; Bollmann, I.; Vacek, R.; ­Oundjian, J.; Wilson, N. (6) Turfa, J.; Zuidema, L.; Zuidema, R.; Bengtsson, C.; ­Bengtsson, J.; Galano, M.; ­Galano, L. (7) Peckham, T.; Mourlhou, J.; Charpentier, C.; Gold, M.; Bollmann, R.; Oundjian, F. (8) Weber, R.; Johnson, B.; Hanau, D.; Watanabe, Y.; Williams, R.; Trafford, G.; Androsoff, T.