Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Vijana kwa Mafundisho ya Wakati Unaofaa

Kuwasaidia Vijana kwa Mafundisho ya Wakati Unaofaa

Simameni Mkiwa Kamili na kwa Usadikisho Imara

Kuwasaidia Vijana kwa Mafundisho ya Wakati Unaofaa

EPAFRASI alikuwa Mkristo wa karne ya kwanza aliyesafiri hadi Roma. Hata hivyo, alikuwa akifikiria mambo aliyokuwa ameyaacha huko Kolosai, mji mmoja huko Asia Ndogo. Alikuwa amehubiri habari njema huko Kolosai na bila shaka alikuwa amewasaidia baadhi ya Wakolosai kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. (Wakolosai 1:7) Epafrasi aliwahangaikia sana waamini wenzake huko Kolosai, kwa hiyo mtume Paulo aliwaandikia hivi akiwa Roma: “Epafrasi . . . awapelekea nyinyi salamu zake, akijikakamua mwenyewe sikuzote kwa ajili yenu katika sala zake, ili nyinyi mwishowe mpate kusimama mkiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.”—Wakolosai 4:12.

Baba na mama Wakristo wa siku hizi vilevile wanatoa sala kwa bidii ili watoto wao wadumishe hali nzuri ya kiroho. Wazazi hao wanajitahidi kufundisha watoto wao kumpenda Mungu kwa moyo ili wasimame imara katika imani.

Vijana wengi Wakristo wameomba msaada kushughulikia magumu wanayokabili shuleni na penginepo. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 15 alisema hivi: “Matatizo yetu yanazidi kuwa mabaya. Maisha yanatisha. Tunahitaji msaada!” Je, maombi ya vijana hao na sala za wazazi wanaomcha Mungu zimejibiwa? Ndiyo! Mafundisho ya Biblia yameandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Vichapo kadhaa vinatajwa hapa, ambavyo vimewasaidia mamia ya maelfu ya vijana ‘kusimama wakiwa kamili na kwa usadikisho imara.’ Acheni tuzingatie vichapo vichache kati ya hivyo.

‘Tazama, Mashahidi Wapya 15,000!’

Mnamo Agosti 1941, wasikilizaji 115,000 walikusanyika huko St. Louis, Missouri, Marekani, ili wahudhurie mkusanyiko mkubwa kushinda mikusanyiko yote ambayo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefanya kufikia wakati huo. Katika siku yake ya mwisho—“Siku ya Watoto”—watoto wapatao 15,000 waliketi karibu na jukwaa wakimsikiliza kwa makini Joseph F. Rutherford alipotoa hotuba yenye kichwa “Watoto wa Mfalme.” Alipokuwa karibu kumaliza hotuba yake, Rutherford aliyekuwa na umri wa miaka 71, aliwaambia watoto hao hivi, akisema nao kama baba:

“Nyinyi nyote . . . watoto mliokubali . . . kutii Mungu na Mfalme wake, tafadhalini simameni.” Watoto wote wakasimama. Ndugu Rutherford alisema hivi: “Tazama, mashahidi wa Ufalme wapya zaidi ya 15,000!” Wasikilizaji walipiga makofi. Msemaji aliongeza kusema: “Nyinyi nyote ambao mtafanya mwezayo kuwaambia wengine juu ya ufalme wa Mungu na baraka zinazoambatana nao . . . , tafadhalini semeni Ndiyo.” Watoto waliitikia kwa kusema “Ndiyo!” kwa sauti kubwa. Kisha alionyesha kitabu kipya chenye kichwa Children (Watoto), na wasikilizaji waliitikia kwa kupiga makofi kwa muda mrefu.

Baada ya hotuba hiyo yenye kusisimua, vijana hao walipanga mstari mrefu kwenda jukwaani ambapo Ndugu Rutherford aliwapa kila mmoja nakala moja ya kitabu hicho kipya kama zawadi. Wasikilizaji walilia machozi walipowaona watoto hao. Mwanamume mmoja aliyeshuhudia tukio hilo alisema hivi: “Ni mtu mwenye moyo mgumu pekee, ambaye hangeguswa kuona watoto [walioonyesha] imani na tumaini thabiti katika Mungu wao, Yehova.”

Katika mkusanyiko huo wa ajabu, vijana 1,300 walionyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova kupitia ubatizo. Wengi wao wamesimama imara katika imani hadi leo. Baadhi yao huimarisha makutaniko mahali wanapoishi, wengine wamejitolea kutumikia huko Betheli, au wanatumikia katika nchi za kigeni kama wamishonari. Ndiyo, “Siku ya Watoto” na kitabu Children kilikuwa na uvutano wenye kudumu kwa vijana wengi!

“Vinakuja kwa Wakati Unaofaa”

Katika miaka ya 1970, Mashahidi wa Yehova walichapisha vitabu vingine vitatu vilivyovutia mioyo ya mamia ya maelfu ya vijana. Vitabu hivyo vitatu vilikuwa Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, Kupata Faida Zote za Ujana Wako, na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Katika mwaka wa 1982 mfululizo wa habari wa “Vijana Huuliza . . .” ulianza kuchapishwa katika gazeti la Amkeni! Sehemu hizo zimegusa vijana na wazee. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 14 alisema hivi: “Kila usiku mimi humshukuru Mungu kwa habari hizo.” Kijana mwenye umri wa miaka 13 alisema: “Napenda mfululizo wa ‘Vijana Huuliza,’ inaonekana unakuja kwa wakati unaofaa.” Wazazi na wazee Wakristo waliowekwa wanakubali kwamba sehemu hizo zimekuja kwa wakati unaofaa na ni zenye faida.

Kufikia mwaka wa 1989, sehemu 200 hivi za “Vijana Huuliza . . .” zilikuwa zimechapishwa katika Amkeni! Katika Mkusanyiko wa Wilaya wa “Ujitoaji wa Kimungu” wa mwaka huo kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kilitolewa. Je, kitabu hicho kimewasaidia vijana wasimame imara katika imani? Vijana watatu waliandika hivi: “Kitabu hicho kimetusaidia sana kuelewa matatizo yetu na kujua jinsi ya kuyakabili. Asanteni sana kwa kujali hali yetu.” Vijana wengi kotekote duniani waliosoma kitabu hicho wanakubaliana na maoni hayo.

“Kilitosheleza Njaa Yetu”

Katika mwaka wa 1999, Mashahidi wa Yehova walitoa video Young People Ask—How Can I Make Real Friends? (Vijana Huuliza—Ninawezaje Kupata Marafiki wa Kweli?), ambayo ni kifaa kingine kilichotolewa kwa wakati unaofaa ili kuelimisha vijana. Wengi waliipenda sana. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 14 alisema: “Ujumbe wa video hiyo uliingia moyoni mwangu moja kwa moja.” Mama mmoja asiye na mwenzi alitaarifu hivi: “Video hiyo itakuwa sehemu ya kawaida ya chakula chetu cha kiroho.” “Inachangamsha moyo kujua kwamba Rafiki yetu bora, Yehova, anawapenda na kuwajali kwelikweli vijana katika tengenezo lake la ulimwenguni pote,” mwanamke mmoja kijana alisema.

Video hiyo imekuwa na matokeo gani? Vijana wanasema hivi: “Imenisaidia kuchagua marafiki wazuri, kushirikiana na wengi zaidi kutanikoni, na kumfanya Yehova kuwa rafiki yangu.” “Imenisaidia kuwa na ujasiri ninapokuwa pamoja na marika wangu.” “Imeimarisha azimio langu la kumtumikia Yehova kadiri niwezavyo.” Na wenzi wawili wa ndoa waliandika hivi: “Tunashukuru kwa moyo wote kwa ‘chakula’ hicho. Kilitosheleza njaa yetu.”

Washiriki waliotiwa mafuta wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” wametii agizo la Mungu la kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati wake kwa wote watakaokikubali. Na ni furaha iliyoje kuona jinsi elimu hiyo ya Kimaandiko inavyowasaidia vijana ‘kusimama wakiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu’!