Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mikusanyiko—Uthibitisho Wenye Shangwe wa Udugu Wetu

Mikusanyiko—Uthibitisho Wenye Shangwe wa Udugu Wetu

Simameni Mkiwa Kamili na kwa Usadikisho Imara

Mikusanyiko—Uthibitisho Wenye Shangwe wa Udugu Wetu

JOSEPH F. RUTHERFORD mwenye umri wa miaka 50 na ambaye ana afya mbaya baada ya kufungwa gerezani isivyo haki kwa muda wa mwaka mmoja hivi, anatumikia kwa furaha akiwa mhudumu wa hoteli. Akiwa amewabebea masanduku yao, yeye huwapeleka Wakristo wenzake kwenye vyumba vyao vya hoteli. Watu wawili ambao walikuwa wamefungwa pamoja naye hapo awali—Wanafunzi wa Biblia wenzake—wanagawa vyumba kwa watu wengi wanaosubiri kupata mahali pa kulala. Shughuli zinaendelea hadi baada ya saa sita usiku. Watu wote waliopo hapo wanachangamka. Kuna sherehe gani?

Ni mwaka wa 1919, na Wanafunzi wa Biblia (ambao sasa wanajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova) wanapata kitulizo baada ya kunyanyaswa vikali. Ili kuimarisha ndugu zao, wanafanya mkusanyiko huko Cedar Point, Ohio, Marekani, kuanzia Septemba 1 hadi 8, mwaka wa 1919. Siku ya mwisho ya mkusanyiko huo, umati uliosisimuka wa wahudhuriaji 7,000 wanamsikiliza kwa makini Ndugu Rutherford anapowatia moyo kwa maneno haya: “Wewe ni balozi wa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana, unayewatangazia watu . . . ufalme wenye utukufu wa Bwana.”

Watu wa Yehova walianza kukusanyika zamani wakati wa Waisraeli. (Kutoka 23:14-17; Luka 2:41-43) Mikusanyiko hiyo ilikuwa pindi zenye furaha, ambapo wote waliohudhuria walisaidiwa kufikiria Neno la Mungu. Vivyo hivyo, mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa hukazia sana mambo ya kiroho. Mikusanyiko hiyo yenye shangwe, ni uthibitisho ulio wazi kwa watazamaji walio na mioyo minyofu kwamba Mashahidi wameunganishwa na vifungo vyenye nguvu vya udugu wa Kikristo.

Jitihada za Kuhudhuria

Wakristo wa siku za kisasa wanatambua kwamba mikusanyiko yao hutokeza fursa za kufundishwa Neno la Mungu na kupata burudisho la kiroho. Wao huona mikusanyiko hiyo kuwa njia muhimu sana ya kuwasaidia ‘wasimame wakiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.’ (Wakolosai 4:12) Kwa hiyo, Mashahidi huunga mkono mikusanyiko hiyo kwa moyo wote na kujitahidi vilivyo kuihudhuria.

Wengine wanahitaji kudhihirisha imani na kushinda vizuizi vilivyo kama mlima ili wahudhurie mikusanyiko hiyo. Kwa mfano, fikiria Shahidi mmoja mzee nchini Austria. Ingawa ana ugonjwa wa sukari na anahitaji kudungwa sindano ya insulini kila siku, alihakikisha kwamba amehudhuria siku zote za mkusanyiko wa wilaya nchini mwake. Nchini India, familia kubwa ya Mashahidi ambao ni maskini sana waliona ikiwa vigumu sana kuhudhuria mkusanyiko fulani. Mshiriki mmoja wa familia hiyo aliwasaidia. “Kwa kuwa sikutaka tukose mkusanyiko huo,” asema, “niliuza vipuli vyangu vya dhahabu ili tupate nauli. Jitihada nilizofanya hazikuwa za bure kwa kuwa, ushirika pamoja na akina ndugu na mambo yaliyoonwa yalijenga imani yetu.”

Nchini Papua New Guinea, kikundi cha watu wenye kupendezwa ambao hawajabatizwa walikuwa wameazimia kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya kwenye jiji kuu. Walienda kwa mwanakijiji mmoja aliyekuwa na gari na kumwuliza angewatoza pesa ngapi kuwasafirisha hadi kwenye mkusanyiko. Kwa kuwa kiasi walichokuwa nacho hakikutosha nauli yao, waliamua kufanya kazi ya kukarabati chumba cha kupikia cha mtu huyo. Kwa hiyo waliweza kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya na kunufaika na programu nzima.

Umbali hauwezi kuwazuia Mashahidi wa Yehova kuhudhuria mikusanyiko. Mnamo mwaka wa 1978, mjumbe mmoja kijana kutoka Poland, alisafiri mwendo wa kilometa 1,200 kwa baiskeli ili kuhudhuria mkusanyiko huko Lille, Ufaransa. Wakati wa kiangazi cha mwaka wa 1997, Mashahidi wawili kutoka Mongolia walisafiri mwendo wa kilometa 1,200 ili kuhudhuria mkusanyiko wa Kikristo huko Irkutsk, Urusi.

Wonyesho wa Udugu wa Kweli

Watu wenye maoni yaliyosawazika huona waziwazi umoja na udugu unaodhihirishwa na Mashahidi kwenye mikusanyiko yao. Wengi wamevutiwa kuona kwamba hakuna ubaguzi miongoni mwa watu wanaohudhuria mkusanyiko na kwamba kuna uchangamfu wa kweli hata miongoni mwa wale ambao huenda wanakutana kwa mara ya kwanza.

Katika mkusanyiko wa kimataifa uliofanywa hivi majuzi nchini Australia, kiongozi mmoja wa watalii aliyeandamana kwa muda wa juma moja na wajumbe wa mkusanyiko waliokuwa wakizuru, alitaka kushirikiana nao kwa muda mrefu zaidi ili kufurahia ushirika wao. Alivutiwa na upendo na umoja miongoni mwao na hangeweza kuamini kwamba wangeweza kupatana jinsi hiyo, kwa kuwa wengi wao hawakuwa wanajuana. Wakati wake wa kuondoka ulipowadia, aliwaomba wamsikilize. Akiwazungumzia kwa kuwaita “ndugu na dada,” alianza kuwashukuru lakini hakuweza kumaliza, kwa kuwa alizidiwa na hisia na akaanza kulia.

Mnamo mwaka wa 1997, kwa mara ya kwanza Sri Lanka ilifanya mkusanyiko wa wilaya katika lugha tatu kwenye uwanja mkubwa. Hotuba zote zilitolewa sawia katika Kiingereza, Kisinhala, na Kitamil. Katika ulimwengu wenye misukosuko ya kikabila inayozidi kuongezeka, watu walitambua kwa urahisi mkusanyiko huo uliofanywa na watu wa kabila tatu tofauti-tofauti. Polisi mmoja alimwuliza ndugu fulani hivi: “Ni nani anayesimamia mkusanyiko huu—ni Wasinhala, Watamil, au Waingereza?” Ndugu huyo alimjibu, “Hakuna. Sote tunafanya mambo yote pamoja.” Polisi huyo alishangaa sana. Watu wote wa kutoka vikundi hivyo vitatu wenye kusema lugha tofauti walipoungana kusema “Ameni” katika sala ya mwisho, sauti zao zilivuma uwanjani, na papo hapo wote wakapiga makofi kwa pamoja. Kila mtu alitokwa na machozi. Naam, kwa kweli mikusanyiko ni uthibitisho wenye shangwe wa udugu wetu.—Zaburi 133:1. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ona ukurasa wa 66-77, 254-282 wa kitabu Mashahidi wa YehovaWapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.