Ona video zinazopatikana

Kuomba Musamaha—Kunasaidiaka Kufanya Amani

Kuomba Musamaha—Kunasaidiaka Kufanya Amani

Kuomba Musamaha​—Kunasaidiaka Kufanya Amani

DEBORAH Tannen, muandikaji mwenye kujulikana sana na mwenye elimu ya tabia za watu wa ku masomo ya juu ya Georgetown mu Washington, D.C.aliandika hivi: “Kuomba musamaha kunasaidiaka sana. Kunasaidiaka kumaliza hali ya kukosa kuelewana bila kutumia jeuri, kunaunganishaka mataifa yenye haielewane, kunasaidiaka serikali zionyeshe kama zinaelewa magumu yenye zimeletea raia wake, kunasaidiaka watu wakuwe tena marafiki.”

Biblia inaonyesha kama mara mingi kuomba musamaha kwa moyo wote kunasaidiaka mutu akuwe tena na uhusiano muzuri pamoya na wengine. Kwa mufano, mu mufano wake wa mwana mupotevu, Yesu alionyesha kama wakati ule mwana mupotevu aliomba musamaha, baba yake alikuwa tayari kumukaribisha. (Luka 15:17-24) Kwa kweli, mutu anapaswa kuwa tayari kujishusha na kuomba musamaha. Kusema kweli, kama uko munyenyekevu, itakuwa mwepesi kwako kuomba musamaha.

Kuomba Musamaha Kunasaidiaka Sana

Mufano wa Abigaili, mwanamuke Mwisraeli wa zamani, unatufundisha kama kuomba musamaha kunasaidiaka sana, hata kama aliomba musamaha juu ya makosa yenye bwana yake alifanya. Wakati Daudi, mwenye alifikia kuwa mufalme wa Israeli, alikuwa mu jangwa, yeye na wanaume wake walilinda kondoo wa Nabali, bwana ya Abigaili. Lakini wakati wanaume wa Daudi waliomba Nabali awapatie mukate na maji, Nabali aliwafukuza na kuwatukana sana. Daudi alikasirika sana na akakamata wanaume wake 400 ili waende kuua Nabali na nyumba yake yote. Wakati Abigaili alisikia ile habari, alienda kukutana na Daudi. Wakati Abigaili aliona Daudi, alianguka uso chini ku miguu yake. Kisha akasema hivi: “Bwana wangu, acha lawama ikuwe juu yangu; acha mutumishi wako mwanamuke azungumuze na wewe, na usikilize maneno ya mutumishi wako mwanamuke.” Kisha Abigaili akafasiria Daudi namna mambo ilitendeka na akamupatia chakula na maji. Daudi akasema: “Panda uende kwa amani kwenye nyumba yako. Angalia, nimekusikiliza, na nitatimiza ombi lako.”​—1 Samweli 25:2-35.

Unyenyekevu wa Abigaili na maneno yake ya kuomba musamaha kwa ajili ya tabia ya mubaya ya bwana yake, iliokoa watu wa nyumba yake. Na hata Daudi alimushukuru juu alimuzuia asimwange damu. Hata kama haiko Abigaili njo alikoseaka Daudi na wanaume wake, Abigaili alikubali kubeba makosa ya familia yake na akafanya amani pamoya na Daudi.

Mutume Paulo naye alijua ni wakati gani ilikuwa lazima kuomba musamaha. Wakati fulani alipaswa kujitetea mbele ya Sanhedrini, tribinali kubwa ya Wayahudi. Kuhani mukubwa Anania alikasirika sana wakati alisikia maneno ya kweli yenye Paulo alisema, na akaomba wale wenye walikuwa wanasimama pembeni ya Paulo wamupige ku kinywa. Wakati Paulo alisikia vile, alimuambia hivi: “Mungu atakupiga, wewe ukuta wenye umepakwa rangi nyeupe. Je, unakaa ili kunihukumu kulingana na Sheria na wakati uleule unavunja Sheria hiyo kwa kuamuru nipigwe?” Wakati watu wenye walikuwa pale walimushitaki Paulo kuwa amemutukana kuhani mukubwa, palepale Paulo alikubali kosa yake na akasema hivi: “Ndugu, sikujua kama yeye ni kuhani mukubwa. Kwa maana imeandikwa, ‘Haupaswe kusema mubaya juu ya mutawala wa watu wako.’”​—Matendo 23:1-5.

Paulo alikuwa na sheria ya kusema kama mutu mwenye amewekwa kuwa muamuzi hapaswe kutenda kwa jeuri. Lakini aliomba musamaha, juu bila kujua alizungumuza na kuhani mukubwa mu njia yenye ingeonekana kuwa ya kukosa heshima. * Juu Paulo aliomba musamaha, Sanhedrini ilikuwa tayari kumusikiliza. Na juu Paulo alijua jambo yenye ilikuwa naleta mugawanyiko kati ya watu wenye walifanyiza Sanhedrini, aliwaambia kama alishitakiwa kwa sababu aliamini ufufuo. Kwa hiyo, mugawanyiko mukubwa ukatokea na Wafarisayo wakakuwa upande wa Paulo.​—Matendo 23:6-10.

Mufano wa Paulo na Abigaili unatufundisha nini? Wote wawili waliomba musamaha kwa moyo wote na ile ilifanya wengine wakuwe tayari kuwasikiliza. Kwa hiyo, kuomba musamaha kunaweza kusaidia kufanya amani. Kama tunakubali makosa yetu na tunaomba musamaha juu ya mambo yenye tulifanya, ile inaweza kufanya wengine wakuwe tayari kutusikiliza.

‘Lakini Sikufanya Kitu ya Mubaya’

Wakati tunafikia kujua kama mambo yenye tulisema ao kufanya ilikwaza mutu fulani, tunaweza kuwaza kama ule mutu anatafutaka tu makosa kwenye haiko ao anakasirikaka mbio. Lakini, Yesu Kristo alishauria hivi wanafunzi wake: “Basi, kama unaleta zawadi yako kwenye mazabahu na pale unakumbuka kama ndugu yako iko na jambo fulani juu yako, acha zawadi yako pale mbele ya mazabahu, na uende. Fanya kwanza amani na ndugu yako, na kisha urudie na utoe zawadi yako.”​—Matayo 5:23, 24.

Tuseme ndugu fulani anawaza kama umemukwaza. Mu hali ya vile, Yesu alisema kama unapaswa kuenda na ‘kufanya kwanza amani na ndugu yako.’ Ikuwe unawaza kama ulimukwaza ao hapana, unapaswa tu kufanya vile. Kulingana na maandishi ya Kigiriki, maneno yenye Yesu alitumia hapa, ‘inaonyesha kama ngambo zote mbili zinapaswa kutafuta kupatana kisha kukosana.’ (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) Inawezekana wote wawili walikosea juu wote hawakamilike, na wote wanafanyaka makosa. Njo maana inaomba wote wawili wajikaze kupatana.

Jambo ya maana haiko kutafuta kujua nani njo iko na kosa na nani njo hana kosa, lakini ni kuwa wa kwanza kufanya amani. Wakati mutume Paulo aliona kama Wakristo Wakorinto walikuwa wanapelekana ku tribinali za ulimwengu juu ya mambo ya kipekee sawa vile juu ya kukosa kuelewana juu ya makuta, aliwashauria hivi: “Sababu gani musikubali wengine wawakosee ninyi? Na tena, sababu gani hamukubali wengine wawapunje ninyi?” (1 Wakorinto 6:7) Hata kama Paulo alisema ile maneno juu ya kutia Wakristo moyo juu wasikuwe wanapelekana ku tribinali za ulimwengu, mu maneno yake muko hii kanuni ya maana: Amani kati ya Wakristo ni jambo ya maana zaidi kuliko kujua nani njo iko na kosa na nani njo hana kosa. Kuchunga ile kanuni mu kichwa kutafanya ikuwe mwepesi kwetu kuomba musamaha juu ya kosa yenye mutu anawaza kama tumemutendea.

Tuombe Musamaha kwa Moyo Wote

Watu fulani wanatumiaka kupita kiasi maneno ya kuomba musamaha. Kwa mufano mu inchi ya Japani, neno sumimasen, ni neno ya kuomba musamaha. Lakini inatumiwaka sana. Na hata mutu anaweza kuitumia juu ya kusema aksanti ili kuonyesha kama anajisikia mubaya juu haweze kurudisha wema wenye walimufanyia. Juu ile neno inatumiwaka mu hali za mingi, watu fulani wanaweza kuona kama inatumiwa kupita kiasi na wanaweza kujiuliza kama wenye kuitumia wanaisema kwa moyo wote kabisa ao ilishakakuwa tu wimbo. Hata mu luga zingine, maneno ya kuomba musamaha inaweza kutumiwa kupita kiasi.

Ni jambo ya maana kuomba musamaha kwa moyo wote, hata ikuwe tunasemaka luga gani. Sauti yetu inapaswa kuonyesha kama tunahuzunika kabisa juu ya mambo yenye tulifanya. Mu mahubiri yake ya ku mulima, Yesu Kristo aliambia hivi wanafunzi wake: “Muache tu neno lenu ‘Ndiyo’ limaanishe ndiyo, na ‘Hapana’ yenu imaanishe hapana, kwa maana lenye kupita hayo linatoka kwa ule muovu.” (Matayo 5:37) Kama unaomba musamaha ufanye vile kwa moyo wote! Tukamate mufano: Kwenye uwanja wa ndege (aéroport), mwanaume fulani iko ku mustari, kisha muzigo yake inagonga mwanamuke mwenye iko pembeni yake. Ule mwanaume anamuomba musamaha. Kisha dakika fulani, wakati watu wanasogea ku mustari, ile muzigo inagonga tena ule mwanamuke. Kwa heshima, ule mwanaume anaomba tena musamaha. Wakati ile muzigo inagonga tena ule mwanamuke kwa mara ya tatu, mutu mwenye alikuwa anasafiri na ule mwanamuke akamuambia kama ikiwa ile musamaha yake ilikuwa natoka kabisa ku moyo, alipaswa kujikaza juu muzigo yake isiguse tena ule mwanamuke. Ile inatufundisha kama wakati tunaomba musamaha kwa moyo wote, tunapaswa pia kujikaza tusirudilie ile kosa.

Kuomba musamaha maana yake kukubali makosa yenye tulifanya, kuomba huruma, na kujikaza kutengeneza mambo. Mutu mwenye alikosewa naye anapaswa kuwa tayari kusamehe mwenzake mwenye ameomba musamaha. (Matayo 18:21, 22; Marko 11:25; Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13) Juu wote wawili hawakamilike, wakati fulani haikuwake mwepesi kufanya amani. Lakini, kuomba musamaha kunasaidiaka sana kurudisha amani.

Wakati Haifae Kuomba Musamaha

Ni kweli kwamba kuomba musamaha kunatulizaka mambo na kunaletaka amani. Lakini mutu mwenye hekima hapaswe kuomba musamaha wakati haifae kufanya vile. Tuseme shida ni juu uko muaminifu kwa Mungu. Wakati Yesu alikuwa ku dunia, “alijinyenyekeza mwenyewe na kuwa mutiifu mupaka kifo, ndiyo, kifo kwenye muti wa mateso.” (Wafilipi 2:8) Lakini, hakuomba musamaha juu ya mambo yenye alikuwa anaamini juu tu wamupunguzie mateso. Na Yesu hakuomba musamaha wakati kuhani mukubwa alimuambia hivi: “Ninakuapisha mbele ya Mungu mwenye kuishi utuambie kama wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu!” Kuliko kuomba musamaha juu ya woga, Yesu alisema hivi kwa uhodari: “Wewe mwenyewe umesema. Lakini ninawaambia ninyi: Kuanzia sasa mutaona Mwana wa binadamu akiwa amekaa kwenye mukono wa kuume wa nguvu, na akikuja juu ya mawingu ya mbinguni.” (Matayo 26:63, 64) Yesu hakufikiria hata kidogo kuvunja ushikamanifu wake kwa Baba yake, Yehova, juu tu ya kufanya amani na kuhani mukubwa.

Wakristo wanaheshimiaka wenye mamlaka. Lakini, hawana sababu ya kuomba musamaha juu ya kumutii Mungu na juu ya kupenda ndugu zao.​—Matayo 28:19, 20; Waroma 13:5-7.

Hakutakuwaka Tena Mambo Yenye Inavuruga Amani

Leo, tunafanyaka makosa juu tuliriti zambi na hali ya kutokamilika kutoka kwa Adamu, muzazi wetu wa kwanza. (Waroma 5:12; 1 Yohana 1:10) Adamu alifanya zambi wakati alikosa kumutii Mungu, Muumbaji wake. Lakini ku mwanzo, Adamu na Eva walikuwa wakamilifu na hawakukuwa na zambi. Na Mungu ameahidi kama atarudishia wanadamu ile hali ya ukamilifu yenye Adamu na Eva walipoteza. Atamaliza zambi na magumu yote yenye zambi imetuletea.​—1 Wakorinto 15:56, 57.

Wazia namna mambo itakuwa! Yakobo, ndugu ya Yesu, alisema hivi wakati alitoa mashauri kuhusu namna ya kutumia ulimi: “Kama mutu yeyote hajikwae katika neno, huyo ni mutu mukamilifu, mwenye anaweza kuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2) Mutu mukamilifu iko na uwezo wa kutumia ulimi wake bila kukosea. Kwa hiyo, hana lazima ya kuomba musamaha juu ya mambo yenye alisema. “Anaweza kuongoza kwa lijamu mwili wake wote.” Hali itakuwa muzuri sana wakati tutakuwa wakamilifu! Ile wakati, hakutakuwa mambo yenye itavuruga amani kati ya watu. Lakini mbele ile wakati ifike, kama tunakosea mutu, tukuwe tunaomba musamaha kwa moyo wote juu amani isipotee.

[Maelezo ya chini]

^ Pengine Paulo hakutambua kuhani mukubwa juu hakukuwa naona muzuri.

[Picha]

Mufano wa Paulo unaweza kutufundisha nini?

[Picha]

Wakati watu wote watakuwa wakamilifu, hakutakuwa mambo yenye itavuruga amani