Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Yesu Alivyozaliwa na Sababu Iliyofanya Azaliwe

Jinsi Yesu Alivyozaliwa na Sababu Iliyofanya Azaliwe

Jinsi Yesu Alivyozaliwa na Sababu Iliyofanya Azaliwe

“HAIWEZEKANI!” Watu wengi ambao si Wakristo wangesema hivyo baada ya kusikia simulizi kuhusu kuzaliwa kwa Yesu. Wanahisi kwamba ni jambo lisilopatana na sayansi kuamini kwamba msichana bikira angeweza kupata mimba na kuzaa mwana bila baba wa kibinadamu. Unaonaje?

Mnamo mwaka wa 1984, gazeti The Times la London lilichapisha barua iliyoeleza jambo hilo ikisema: “Ni jambo lisilopatana na akili kutumia sayansi kuwa msingi wa kupinga miujiza. Kuamini kwamba miujiza haiwezi kutokea ni sawa na kuamini kwamba inaweza kutokea.” Barua hiyo ilitiwa sahihi na maprofesa 14 wa sayansi kutoka vyuo vikuu vya Uingereza. Walisema: “Tunakubali kwa nia moja kwamba kujifungua kwa bikira, miujiza inayosimuliwa katika Injili, na kufufuliwa kwa Kristo ni matukio halisi.”

Hata hivyo, inaeleweka kwamba mtu anaweza kushangaa anaposikia kwa mara ya kwanza kwamba Yesu alizaliwa na bikira. Mamake Yesu aliyekuwa bikira alishangaa wakati malaika wa Mungu alipomwambia: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu.” Maria aliuliza hivi: “Hilo litakuwaje, kwa kuwa huwa sifanyi ngono na mwanamume?” Kisha malaika akamweleza kwamba Mungu atafanya muujiza huo kupitia roho Yake takatifu, na kuongeza kusema: “Kwa Mungu hakuna tangazo lolote litakalokuwa lisilowezekana.” (Luka 1:31, 34-37) Ni wazi kwamba Yule ambaye aliumba mwanadamu akiwa na uwezo wa ajabu wa kuzaa angeweza pia kufanya Yesu azaliwe na bikira. Ikiwa Mungu aliumba ulimwengu pamoja na vipimo vyake vilivyo sahihi kabisa, angeweza pia kutumia yai la Maria na kutokeza Mwana mkamilifu wa kibinadamu.

Kwa Nini Ilikuwa Lazima Yesu Azaliwe?

Yosefu, mwanamume mwenye kumwogopa Mungu alikuwa amemchumbia Maria wakati alipopata mimba. Kupitia ndoto, Malaika wa Mungu alimweleza Yosefu sababu kuu iliyofanya mchumba wake bikira apate mimba. Malaika huyo alisema: “Usiogope kumpeleka Maria mke wako nyumbani, kwa maana kile ambacho kimezaliwa ndani yake ni kwa roho takatifu. Yeye atazaa mwana, nawe lazima umwite jina lake Yesu, kwa maana yeye ataokoa watu wake kutoka katika dhambi zao.” (Mathayo 1:20, 21) Jina Yesu katika Kiebrania linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.” Jina hilo linatukumbusha kwamba tunahitaji kuokolewa kutoka kwa dhambi na kifo na pia hutukumbusha mpango wa Yehova Mungu wa kutuokoa kupitia Yesu.

Kwa sababu mtu wa kwanza, Adamu, alifanya dhambi, wazao wake wote walizaliwa wakiwa hawajakamilika na wakiwa na mwelekeo wa kuvunja sheria za Mungu. (Waroma 5:12) Wazao wa Adamu wangekombolewaje kutoka kwa dhambi na kuwa wakamilifu? Uhai wa mwanadamu mwingine mkamilifu unaolingana na ule ambao Adamu alipoteza ulihitajiwa ili haki itekelezwe. Ndiyo sababu Mungu alifanya mwanadamu mkamilifu Yesu, azaliwe kimuujiza, na ndiyo sababu Yesu aliruhusu maadui wake wamwue. (Yohana 10:17, 18; 1 Timotheo 2:5, 6) Baada ya Yesu kufufuliwa na kupaa mbinguni, angeweza kusema hivi kwa uhakika: “Nikawa mfu, lakini, tazama! mimi niko hai milele na milele, nami nina funguo za kifo na za Hadesi [kaburi la wanadamu].”—Ufunuo 1:18.

Kwa kuwa ana funguo za mfano za kifo na Hadesi, Yesu anawafungulia njia wanadamu wenye dhambi ili wapate tena kile ambacho Adamu alipoteza. Yesu alisema: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai; na kila mtu aliye hai na hudhihirisha imani katika mimi hatakufa hata kidogo kabisa.” (Yohana 11:25, 26) Ni ahadi nzuri kama nini! Hata hivyo, kuna sababu kuu hata zaidi iliyofanya Yesu azaliwe.

Sababu Kuu Zaidi

Maisha ya Yesu hayakuanza katika tumbo la uzazi la Maria. Alisema hivi waziwazi: “Nimeteremka kutoka mbinguni.” (Yohana 6:38) Yesu alikuwa ameishi mbinguni pamoja na Baba yake tangu mwanzo wa uumbaji. Kwa kweli, Biblia humtaja kuwa “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufunuo 3:14) Akiwa mbinguni, Yesu alishuhudia uasi wa malaika mwovu aliyepotosha wanadamu wa kwanza na kufanya wakatae utawala wa Mungu. Hilo lilimpa Yesu sababu kuu zaidi ya kutaka kuzaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu, Mwana wa Mungu. Sababu hiyo ni ipi?

Alitaka kuthibitisha kwamba Baba yake wa mbinguni ana haki ya kuutawala ulimwengu. Kwa kudumu akiwa mwaminifu tangu kuzaliwa hadi kufa, Yesu alionyesha kwamba alikuwa tayari kujitiisha chini ya utawala wa Yehova kwa viumbe Wake. Kabla hajauawa na maadui wa Mungu, Yesu alitaja waziwazi sababu iliyofanya awe na nia ya kutoa uhai wake kuwa dhabihu. Alisema kwamba alitaka ulimwengu ujue kwamba alimpenda Baba. (Yohana 14:31) Ikiwa wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, wangekuwa na upendo kama huo, wangekuwa waaminifu chini ya jaribu dogo lililowapata.—Mwanzo 2:15-17.

Pia uaminifu wa Yesu ulithibitisha kwamba malaika mwovu, Shetani, ni mwongo. Shetani alikuwa amemchongea Mungu na mwanadamu kwa kusema mbele ya malaika walio mbinguni hivi: “Yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:1, 4) Shetani alidai kwamba wanadamu wote wangemkana Mungu uhai wao unapokuwa hatarini.

Masuala hayo ambayo yametajwa yalipinga haki ya Mungu ya kuwa mtawala. Ili kuyatatua, Yesu alikubali kuzaliwa akiwa mwanadamu na kuwa mwaminifu hadi kifo.

Kwa hiyo, sababu kuu iliyofanya Yesu azaliwe duniani, kama alivyosema ni ili ‘atoe ushahidi juu ya ile kweli.’ (Yohana 18:37) Alitoa ushahidi huo kupitia maneno na matendo na kuonyesha kwamba utawala wa Mungu ni wa uadilifu kabisa na kwamba kujitiisha chini ya utawala huo huleta furaha ya kudumu. Pia Yesu alisema kwamba alikuja ulimwenguni kutoa uhai wake wa kibinadamu kuwa “fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi,” na kuwapatia wanadamu wenye dhambi fursa ya kuwa wakamilifu na kupata uhai udumuo milele. (Marko 10:45) Ili wanadamu waelewe mambo hayo muhimu, ilikuwa lazima kuwe na maandishi yanayohusu kuzaliwa kwa Yesu. Isitoshe, tunaweza kujifunza habari muhimu kutokana na mambo yaliyotukia wakati wa kuzaliwa kwa Yesu, kama tutakavyoona katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wazao wa Adamu wangekombolewaje kutoka kwa dhambi?