Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni kwa nini Biblia inasema kwamba mtu anapaswa kupiga mayowe akitishwa kulalwa kinguvu?

Mtu ambaye hajawahi kushambuliwa kikatili ili kulalwa kinguvu (kubakwa) hawezi kuelewa jinsi jambo hilo linavyoweza kuharibu maisha ya mtu. Tukio hilo ni lenye kuogofya sana hivi kwamba linaweza kumfadhaisha mtu aliyeshambuliwa kwa maisha yake yote. * Mwanamke mmoja kijana Mkristo aliyeshambuliwa miaka michache iliyopita anasema hivi: “Siwezi kueleza woga niliokuwa nao usiku ule; wala mfadhaiko ambao nimepambana nao tangu wakati huo.” Si ajabu kwamba wengi hawataki hata kufikiria jambo hili lenye kutisha. Hata hivyo, kulalwa kinguvu si jambo la kuwazia, bali ni jambo linalowakumba watu katika ulimwengu huu mwovu.

Biblia inataja waziwazi visa fulani vya kale ambavyo watu walilala wengine kinguvu au walijaribu kuwalala kinguvu. (Mwanzo 19:4-11; 34:1-7; 2 Samweli 13:1-14) Lakini pia inatoa ushauri kuhusu kile ambacho mtu anapaswa kufanya anapotishwa kulalwa kinguvu. Maagizo ya Sheria kuhusu jambo hilo yanapatikana katika Kumbukumbu la Torati 22:23-27. Maagizo hayo yanahusu visa viwili. Katika kisa cha kwanza mwanamume alimpata mwanamke kijana mjini, akalala naye. Lakini mwanamke huyo hakupiga mayowe au kelele ili apate msaada. Basi, alikuwa na hatia, ‘kwa kuwa hakupiga ukelele, naye alikuwa ndani ya mji.’ Kama angalipiga mayowe huenda watu waliokuwa karibu wangaliweza kumwokoa. Katika kisa cha pili, mwanamume alimpata mwanamke kijana kondeni, “akamtenza nguvu, akalala naye.” Huyo mwanamke ‘akalia, lakini hapakuwa na mtu wa kumwokoa.’ Tofauti na mwanamke wa kwanza, ni wazi kwamba mwanamke huyu hakukubali kulala na yule aliyemshambulia. Alijitahidi juu chini kumzuia mshambuliaji huku akipiga kelele ili apate msaada, lakini yule mtu alimshinda nguvu. Mayowe yanaonyesha kwamba hakukubali tendo hilo; hakuwa na hatia.

Kanuni za Sheria ya Musa zinawaongoza Wakristo leo ijapokuwa hawako chini ya sheria hiyo. Masimulizi hayo yanakazia kwamba ni muhimu kumpinga mshambuliaji na kupiga kelele ili kupata msaada. Kupiga mayowe mtu anapojaribu kukulala kinguvu bado kunaonwa kuwa jambo la hekima kufanya. Mtaalamu mmoja wa kuzuia uhalifu alisema hivi: “Silaha bora ya mwanamke anayeshambuliwa bado ni kupiga mayowe.” Wengine wanaweza kumsikia mwanamke anayepiga mayowe na kumsaidia, au mayowe yanaweza kumshtua mshambuliaji hivi kwamba atoroke. Mwanamke kijana Mkristo aliyetishwa kulalwa kinguvu alisema hivi: “Nilipiga mayowe kwa nguvu zangu zote, akarudi nyuma. Aliponikaribia tena, nikapiga mayowe tena na kukimbia. Zamani nilifikiri, ‘Kupiga mayowe kutanisaidiaje mwanamume mwenye nguvu akinishika akiwa na lengo moja tu?’ Lakini nimejua kwamba kupiga mayowe kuna faida kubwa!”

Hata mwanamke akishindwa kumzuia mtu asimlale kinguvu, kupambana kwake na mayowe yake si bure. Badala yake, jambo hilo linaonyesha kwamba alifanya yote aliyoweza ili kuzuia asilalwe kinguvu. (Kumbukumbu la Torati 22:26) Ijapokuwa amelalwa kinguvu, anaweza kuwa na dhamiri njema, anaweza kujiheshimu, na kujua kwamba yeye ni safi machoni pa Mungu. Huenda tukio hilo lenye kutisha likamdhuru kihisia, lakini kujua kwamba alifanya aliyoweza kumzuia mshambuliaji kutamsaidia sana kupona hatua kwa hatua.

Tunapojifunza jinsi ya kutumia kanuni zilizo katika Kumbukumbu la Torati 22:23-27, ni lazima tutambue kwamba simulizi hili fupi halitaji hali zote zinazoweza kutokea. Kwa mfano, andiko hilo halitaji mwanamke bubu asiyeweza kupiga kelele, wala mwanamke aliyezimia, au aliyepigwa na bumbuazi kwa sababu ya woga hivi kwamba alishindwa kupiga kelele au mwanamke asiyeweza kupiga kelele kwa sababu ya kuzibwa mdomo kwa mkono au kwa kitambaa. Hata hivyo, kwa kuwa Yehova anajua mambo yote, kutia ndani nia za watu, anaelewa hali ya wale waliokumbwa na msiba huo naye huwatendea kwa haki, kwa kuwa “njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Anajua kile kilichotukia na jitihada za yule aliyeshambuliwa za kuzuia asilalwe kinguvu. Kwa hiyo, mwanamke aliyelalwa kinguvu ambaye hakuweza kupiga mayowe lakini alifanya yote aliyoweza kumzuia mbakaji, anaweza kuacha mambo mikononi mwa Yehova.—Zaburi 55:22; 1 Petro 5:7.

Hata wakijua hayo, baadhi ya wanawake Wakristo ambao wameshambuliwa kwa ukatili na kulalwa kinguvu wana uchungu moyoni daima kwa sababu wanahisi kwamba wana hatia. Wanahisi kwamba wangaliweza kufanya zaidi ili kuzuia wasilalwe kinguvu. Hata hivyo, badala ya kujilaumu, wanaweza kutoa sala kwa Yehova, kumwomba msaada, na kutegemea fadhili zake zenye upendo.—Kutoka 34:6; Zaburi 86:5.

Kwa hiyo, wanawake Wakristo ambao wana uchungu moyoni kwa sababu ya kulalwa kinguvu wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anaelewa kabisa uchungu wao. Neno la Mungu linawahakikishia hivi: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:18) Wanaweza kusaidiwa pia kushinda mfadhaiko kwa kukubali fadhili na utegemezo wa waamini wenzao katika kutaniko la Kikristo. (Ayubu 29:12; 1 Wathesalonike 5:14) Isitoshe, iwapo wale walioshambuliwa wanajitahidi kukaza fikira kwenye mawazo yenye kujenga watapata “amani ya Mungu izidiyo fikira yote.”—Wafilipi 4:6-9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ijapokuwa makala hii inazungumzia kulalwa kinguvu kwa wanawake, kanuni zinazozungumziwa zinawahusu pia wanaume wanaotishwa kulalwa kinguvu.