Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Midomo ya Kweli Itathibitishwa Milele’

‘Midomo ya Kweli Itathibitishwa Milele’

‘Midomo ya Kweli Itathibitishwa Milele’

KAMA moto unavyoweza kuteketeza msitu ndivyo na kiungo hiki kinavyoweza kuharibu kabisa maisha ya mtu. Kinaweza kujaa sumu, na vilevile kuwa “mti wa uzima.” (Mithali 15:4) Kiungo hiki kinaweza kusababisha mauti au uzima. (Mithali 18:21) Ulimi ni kiungo kidogo lakini chenye nguvu sana hivi kwamba kinaweza kuutia mwili wote doa. (Yakobo 3:5-9) Hivyo ni jambo la hekima kuulinda ulimi.

Katika sehemu ya pili ya sura ya 12 ya kitabu cha Biblia cha Mithali, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale anatoa shauri zuri linaloweza kutusaidia kuudhibiti usemi wetu. Kwa kutumia mithali fupi zilizojaa maana, mfalme huyo mwenye hekima anaonyesha kwamba usemi unaweza kuwa na matokeo fulani na kufunua mengi kuhusu sifa za yule anayesema. Shauri la Sulemani lililoongozwa kwa roho ya Mungu ni muhimu sana kwa yeyote anayetaka ‘kuweka mngojezi mlangoni pa midomo yake.’—Zaburi 141:3.

‘Kosa Linalotia Mtu Mtegoni’

Sulemani anasema, “Katika kosa la midomo kuna mtego kwa mbaya; bali mwenye haki atatoka katika taabu.” (Mithali 12:13) Kusema uongo ni dhambi ya midomo ambayo inaweza kuwa kama mtego wenye kuua kwa wale wanaouzoea. (Ufunuo 21:8) Kusema uongo kunaweza kuonekana kama njia rahisi ya kuepuka adhabu au hali mbaya. Mara nyingi mtu anaposema uongo analazimika kusema uongo tena. Kama vile mtu anayeanza kucheza kamari kwa pesa kidogo anavyoshawishika kutumia pesa nyingi zaidi akijaribu kuokoa zile alizopoteza, ndivyo mtu anayesema uongo hujikuta amenaswa katika mtego mbaya wa kusema uongo tena na tena.

Kosa la midomo humtia mtu mtegoni katika maana ya kwamba anayewadanganya wengine huishia kujidanganya mwenyewe. Kwa mfano, huenda mtu mwongo akafikiri kwamba anajua mengi na ni mwerevu sana, ilhali anajua machache sana. Hivyo basi anaanza kujidanganya. Kwa kweli, ‘yeye hujipendekeza machoni pake kuwa upotovu wake hautaonekana na kuchukiwa.’ (Zaburi 36:2) Uongo unakuwa mtego ulioje! Kwa upande mwingine, mwadilifu hatajiingiza katika hali hiyo ngumu. Hata akipatwa na shida, hatadanganya.

‘Matunda Yanayoshibisha’

Mtume Paulo anaonya, “Msiongozwe vibaya: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Wagalatia 6:7) Bila shaka, kanuni hii inahusu usemi na matendo yetu. Sulemani anasema: “Mtu atashiba mema kwa matunda ya kinywa chake; na atarudishiwa matendo ya mikono yake.”Mithali 12:14.

Kinywa ‘kinachonena hekima’ huzaa matunda yanayoshibisha. (Zaburi 37:30) Tunahitaji ujuzi ili kuwa na hekima na hakuna binadamu anayejua kila kitu. Kila mtu anahitaji kusikiliza shauri zuri na kulitii. Mfalme wa Israeli anasema: “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.”Mithali 12:15.

Yehova hutupatia shauri zuri kupitia Neno lake na tengenezo lake, akitumia vichapo vinavyotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45; 2 Timotheo 3:16) Ni jambo la upumbavu kama nini kukataa shauri zuri na kusisitiza kufanya mambo kwa njia tunayoona ni sawa! ‘Lazima tuwe wepesi sana juu ya kusikia’ wakati Yehova ambaye ‘huwafundisha wanadamu,’ anapotushauri kupitia njia yake ya mawasiliano.—Yakobo 1:19; Zaburi 94:10.

Wenye hekima na wapumbavu huitikiaje wanapotukanwa au kuchambuliwa isivyofaa? Sulemani anajibu: “Ghadhabu ya mpumbavu hujulika mara [“siku hiyohiyo,” “NW”]; bali mtu mwerevu husitiri aibu.”Mithali 12:16.

Mpumbavu anapotukanwa, hujibu kwa haraka na kwa hasira “siku hiyohiyo.” Lakini mtu mwenye busara huomba roho ya Mungu ili aweze kujidhibiti. Yeye hutafakari shauri la Neno la Mungu na kutafakari kwa shukrani maneno haya ya Yesu: “Yeyote akupigaye kofi kwenye shavu lako la kuume, mgeuzie lile jingine pia.” (Mathayo 5:39) Kwa sababu hataki ‘kurudisha ovu kwa ovu kwa yeyote,’ mtu mwenye busara huzuia kinywa chake asinene bila kufikiri. (Waroma 12:17) Vivyo hivyo, tusipotilia maanani hali yoyote yenye kuaibisha inayoweza kutupata, tutajiepusha na ugomvi.

‘Ulimi Wenye Afya’

Kosa la midomo linaweza kusababisha madhara makubwa katika kikao cha hukumu. Mfalme wa Israeli anasema: “Atamkaye maneno ya kweli hufunua haki; bali shahidi wa uongo hutamka hila.” (Mithali 12:17) Shahidi wa kweli hutamka ukweli kwa sababu ushuhuda wake unategemeka na ni wenye kuaminika. Maneno yake huchangia kutekelezwa kwa haki. Lakini, shahidi wa uongo hudanganya na huchangia kupotoshwa kwa haki.

Sulemani anaendelea kusema: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mithali 12:18) Maneno yanaweza kuchoma kama upanga, kuvunja urafiki, na kusababisha matatizo. Au yanaweza kuwa yenye kufurahisha na kupendeza, na kufanya urafiki udumu. Kuwatusi wengine, kuwapigia kelele, kuwachambua daima, na kuwakashifu, ni mambo yanayochoma na kusababisha maumivu makali ya kihisia-moyo. Inafaa kama nini kurekebisha makosa yoyote ambayo huenda tukafanya kuhusiana na hayo kwa kuomba msamaha kwa unyofu!

Katika nyakati hizi ngumu tunamoishi haishangazi kwamba wengi ‘wamevunjika moyo’ na ‘kupondeka roho.’ (Zaburi 34:18) Tunatumia nguvu ya maneno yenye afya ‘kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo’ na ‘kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) Naam, maneno yenye huruma yanaweza kuwatia moyo matineja wanaokabiliana na msongo wa marika wenye kudhuru. Kuzungumza kwa kuwajali walio wazee kwa umri huwahakikishia kwamba wanahitajiwa na wanapendwa. Bila shaka maneno ya fadhili yanaweza kuwachangamsha walio wagonjwa. Hata inakuwa rahisi kukubali karipio linapotolewa “katika roho ya upole.” (Wagalatia 6:1) Jinsi ulivyo wenye afya ulimi wa yule anayeutumia kuwahubiria wenye kusikiliza habari njema za Ufalme wa Mungu!

‘Mdomo Unaothibitishwa Milele’

Akitumia neno “mdomo” katika maana sawa na “ulimi,” Sulemani anasema hivi: “Mdomo wa kweli utathibitishwa milele; bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu.” (Mithali 12:19) Katika Kiebrania, maneno “mdomo wa kweli” yako katika umoja na yanamaanisha mengi zaidi ya kusema kweli. “Maneno hayo yanamaanisha sifa kama vile uthabiti, hali ya kudumu, na kutegemeka,” kinasema kichapo kimoja cha kitaalamu. ‘Usemi wa aina hiyo utadumu milele kwa sababu unategemeka, tofauti na ulimi wa uongo ambao unaweza kudanganya kwa muda lakini usioweza kudumu unapojaribiwa.’

Mfalme mwenye hekima anasema, “Hila imo mioyoni mwao wafikirio uovu; bali wafanyao mashauri ya amani, kwao kuna furaha.” Mfalme huyo anaendelea kusema: “Mwenye haki hatapatikana na msiba wowote; bali wasio haki watajazwa mabaya.”Mithali 12:20, 21.

Wanaopanga hila wanaweza tu kusababisha maumivu na mateso. Lakini, washauri wa amani wanapata uradhi kwa kufanya mambo yanayofaa. Pia wanafurahia matokeo mazuri ya kufanya hivyo. Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba wanapata kibali cha Mungu kwa kuwa “midomo ya uongo ni chukizo kwa BWANA; bali watendao uaminifu ndio furaha yake.”Mithali 12:22.

‘Usemi Unaositiri Maarifa’

Mfalme wa Israeli anasema hivi anapoonyesha tofauti nyingine kati ya mtu anayetumia maneno kwa uangalifu na yule asiyefanya hivyo: “Mwanadamu mwenye busara husitiri maarifa; bali moyo wa wapumbavu hutangaza upumbavu.”Mithali 12:23.

Mtu mwenye busara anajua wakati wa kuzungumza na wakati wa kunyamaza. Anasitiri maarifa kwa kujidhibiti asijionyeshe kuwa anajua mengi. Hiyo haimaanishi kwamba yeye husitiri maarifa wakati wote, bali hueleza anayoyajua kwa njia ya busara. Tofauti na mtu mwenye busara, mpumbavu husema bila kufikiri na hufunua upumbavu wake. Kwa hiyo, maneno yetu na yawe machache na tuepuke kutumia ulimi wetu kwa majivuno.

Sulemani anaendelea kuonyesha tofauti ya mambo mbalimbali, na sasa anatoa hoja yenye kuvutia kuhusu bidii na uvivu. Anasema: “Mkono wa mwenye bidii utatawala; bali mvivu atalipishwa kodi.” (Mithali 12:24) Kufanya kazi kwa bidii kunaweza kuleta mafanikio na kumwezesha mtu kujitegemea kifedha, ilhali uvivu unaweza kufanya mtu awe mtumwa. Msomi mmoja anasema kwamba, “baada ya muda mvivu atakuwa mtumwa wa mtu mwenye bidii.”

‘Neno Linalofurahisha’

Mfalme Sulemani anazungumza tena juu ya usemi akizingatia hasa utu wa wanadamu. Anasema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.”Mithali 12:25.

Kuna mahangaiko mengi sana yanayoweza kuinamisha moyo kwa huzuni. Maneno yenye kutia moyo ya mtu mwenye huruma yanaweza kuinua moyo na kuufanya ufurahi. Lakini wengine watajuaje mahangaiko tuliyo nayo moyoni tusipowaeleza? Naam, tunapokuwa na huzuni au tumeshuka moyo, tunahitaji kuzungumza na mtu mwenye huruma anayeweza kutusaidia. Isitoshe, unapoeleza jinsi unavyohisi unapunguza maumivu ya moyoni. Kwa hiyo, inafaa kuzungumza na mwenzi wa ndoa, mzazi, au rafiki mwenye huruma na mwenye sifa za kiroho.

Biblia ina maneno mazuri sana yanayotia moyo. Kwa hiyo lazima tumkaribie Mungu kwa kutafakari kwa shukrani Neno lake lililoongozwa kwa roho yake. Bila shaka, kutafakari huko kunaweza kuufurahisha moyo ulio na mahangaiko na kuyatia nuru macho yetu yenye huzuni. Mtunga-zaburi anathibitisha hilo kwa kusema: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya BWANA ni safi, huyatia macho nuru.”—Zaburi 19:7, 8.

Njia Yenye Kuthawabisha

Mfalme wa Israeli anasema hivi kutofautisha njia ya mwenye haki na mwovu: “Mwenye haki ni kiongozi cha mwenzake; bali njia ya wasio haki huwakosesha.” (Mithali 12:26) Mwenye haki huwa mwangalifu kuhusu malisho yake, yaani, washirika na marafiki anaochagua. Anawachagua kwa hekima akijitahidi kuepuka uhusiano unaoweza kumletea madhara. Waovu hawafanyi hivyo bali hukataa shauri na kusizitiza kufanya mambo kwa njia wanayoona ni sawa. Nao hupotoshwa na kukosa mwelekeo.

Mfalme Sulemani anatumia njia nyingine kuonyesha tofauti kati ya mtu mvivu na mtu mwenye bidii. Anasema: “Mtu mvivu hapiki mawindo yake; bali mwenye bidii anazo mali za thamani.” (Mithali 12:27) “Mtu mvivu” “hapiki” au “kuchoma” mawindo yake. (New International Version) Kwa sababu hiyo hawezi kumaliza anachoanza. Kwa upande mwingine bidii huleta utajiri.

Kwa kuwa uvivu una madhara mengi sana, mtume Paulo alilazimika kuwaandikia Wakristo wenzake huko Thesalonike ili kuwarekebisha baadhi yao waliokuwa ‘wakitembea bila utaratibu,’ wasiofanya kazi hata kidogo bali wakijiingiza katika mambo yasiyowahusu. Watu hao walikuwa mzigo kifedha kwa wengine. Kwa hiyo Paulo aliwashauri waziwazi na kuwahimiza ‘wafanye kazi kwa utulivu na kula chakula ambacho wao wenyewe walichuma.’ Na kama hawangetii shauri hilo lenye nguvu, basi wengine kutanikoni wangefuata shauri la Paulo la “kujiondoa” kutoka kwao, yaani, kujiepusha nao, yaelekea katika mambo ya kijamii.—2 Wathesalonike 3:6-12.

Tunapaswa kutii shauri la Sulemani la kuwa wenye bidii na wenye kutumia ulimi wetu kwa njia inayofaa. Na tujitahidi kutumia kiungo hicho kidogo ili kuleta afya na shangwe na kujiepusha na makosa yanayosababishwa na midomo huku tukifuatia mwenendo wa uadilifu. Sulemani anatuhakikishia hivi: “Katika njia ya haki kuna uhai; wala hakuna mauti katika mapito yake.”Mithali 12:28.

[Picha katika ukurasa wa 27]

“Yeye aliye na hekima husikiliza shauri”

[Picha katika ukurasa wa 28]

“Ulimi wa mwenye haki ni afya”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unaweza kupata faraja kwa kuzungumza na rafiki unayemwamini

[Picha katika ukurasa wa 30]

Kutafakari Neno la Mungu kwa shukrani huufurahisha moyo