Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanya Maamuzi Ni Jambo Gumu Lisiloweza Kuepukika

Kufanya Maamuzi Ni Jambo Gumu Lisiloweza Kuepukika

Kufanya Maamuzi Ni Jambo Gumu Lisiloweza Kuepukika

NAPOLEON BONAPARTE, maliki wa Ufaransa wa karne ya 19, alisema hivi wakati mmoja: “Hakuna jambo lililo gumu au lenye thamani zaidi kuliko kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi.” Yaelekea utakubaliana na maneno hayo, kwa kuwa watu kwa ujumla huthamini sana kuwa na uwezo wa kuongoza maisha yao. Wakati huohuo, watu wamejifunza kwamba nyakati nyingine ni vigumu sana kufanya maamuzi.

Hatuwezi kuepuka kufanya maamuzi, yawe rahisi au yawe magumu. Inatubidi kufanya maamuzi kila siku. Baada ya kuamka asubuhi, lazima tuamue tutavaa nini, ni kiamsha kinywa gani tutakachokula, na pia tuamue jinsi tutakavyoshughulika na mambo mbalimbali mchana kutwa. Mengi ya maamuzi hayo si muhimu sana. Mara nyingi hatuyafikirii sana. Ni mara chache tutakosa usingizi hata kama maamuzi hayo ni ya hekima au si ya hekima.

Kwa upande mwingine, maamuzi mengine ni muhimu sana. Lazima vijana wengi katika ulimwengu wa sasa waamue ni miradi ya aina gani watakayofuatia. Huenda ikawabidi kuamua watasomea nini na kwa muda gani. Baadaye wengi wao wataamua kama watafunga ndoa au watabaki waseja. Wale wanaotaka kufunga ndoa lazima waamue: ‘Je, nina umri wa kutosha na nimekomaa vya kutosha kufunga ndoa? Ninataka mwenzi wa aina gani, au jambo lililo muhimu zaidi, ninahitaji mwenzi wa aina gani?’ Kuchagua mwenzi wa ndoa ni uamuzi unaoweza kuathiri sana maisha yetu.

Tunapaswa kufanya maamuzi ya hekima kuhusiana na mambo muhimu, kwa kuwa furaha yetu inategemea sana maamuzi tunayofanya. Huenda wengine wakahisi kwamba wana uwezo wa kufanya maamuzi hayo na huenda wakakataa kusaidiwa. Je, ni jambo la hekima kufanya hivyo? Acheni tuone.

[Picha katika ukurasa wa 3 zimeandaliwa na]

Napoleon: From the book The Pictorial History of the World