Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yakobo Alithamini Mambo ya Kiroho

Yakobo Alithamini Mambo ya Kiroho

Yakobo Alithamini Mambo ya Kiroho

MAISHA ya Yakobo yamejaa mizozo na majanga. Analazimika kukimbia kuokoa maisha yake kwa sababu ya hasira ya ndugu-pacha wake ya kutaka kumuua. Badala ya kumwoa msichana anayempenda, Yakobo anadanganywa kumwoa msichana mwingine kwanza na anaishia kuwa na wake wanne na matatizo mengi. (Mwanzo 30:1-13) Anamtumikia mtu anayemtumia vibaya kwa miaka 20. Anapigana mweleka na malaika na anapata madhara ya kudumu. Msichana wake analalwa kinguvu, wanawe wanasababisha mauaji makubwa, naye anaomboleza kwa sababu ya kifo chenye kuhuzunisha cha mwana na mke wake mpendwa. Analazimika kuhama akiwa mzee ili kuepuka njaa, naye anakiri kwamba siku zake zilikuwa “chache, tena za taabu.” (Mwanzo 47:9) Ingawa anapatwa na matatizo hayo yote Yakobo ni mtu wa kiroho anayemtumaini Mungu. Je, anastahili kuonyesha imani kama hiyo? Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza baadhi ya mambo yaliyompata Yakobo?

Alikuwa Tofauti Sana na Ndugu Yake

Yakobo aligombana na ndugu yake hasa kwa sababu yeye alithamini mambo ya kiroho, lakini Esau aliyadharau. Yakobo alipendezwa na ahadi ya agano iliyotolewa kwa Abrahamu naye alijitoa kutunza familia ambayo Mungu alikusudia irithi ahadi hizo. Kwa hiyo Yehova “alimpenda.” Yakobo alikuwa mtu “asiye na lawama” maneno yanayomaanisha ubora wa kiadili. Tofauti na Yakobo, Esau hakujali sana urithi wake wa kiroho ambao alimuuzia Yakobo kwa kitu kidogo sana. Wakati Yakobo kwa kibali cha Mungu alipodai haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza na kupata urithi wa kiroho ambao ungalikuwa wa ndugu yake, Esau alipandwa na hasira ya kulipiza kisasi. Yakobo aliondoka na kuacha wapendwa wake wote, lakini mambo yaliyompata baadaye hakika yalifanya asivunjike moyo.—Malaki 1:2, 3; Mwanzo 25:27-34; 27:1-45, NW.

Katika ndoto, Mungu alimwonyesha Yakobo malaika waliokuwa wakipanda na kushuka ngazi, au mawe yaliyokuwa yamepangwa kama ngazi, kati ya mbingu na dunia naye akamwambia kwamba angemlinda Yakobo na uzao wake. “Na katika wewe, na katika uzao wako jamaa zote za dunia watabarikiwa. Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia.”—Mwanzo 28:10-15.

Maneno hayo yanatia moyo kama nini! Yehova alithibitisha kwamba ahadi zilizotolewa kwa Abrahamu na Isaka zingetajirisha familia ya Yakobo kiroho. Yakobo alitambua kwamba malaika wanaweza kuwahudumia wale walio na kibali cha Mungu, naye alihakikishiwa ulinzi wa kimungu. Kwa kuonyesha shukrani, Yakobo aliweka nadhiri ya kuwa mwaminifu kwa Yehova.—Mwanzo 28:16-22.

Kwa vyovyote vile, Yakobo hakunyakua urithi wa Esau. Kabla wavulana hao wawili hawajazaliwa, Yehova alisema kwamba ‘mkubwa angemtumikia mdogo.’ (Mwanzo 25:23) Huenda mtu akajiuliza, ‘Je, haingalikuwa rahisi Mungu kufanya Yakobo azaliwe kwanza?’ Mambo yaliyotukia baadaye yanatufundisha kweli muhimu. Mungu hawabariki wale wanaohisi kwamba wana haki ya kupata baraka, lakini yeye huonyesha fadhili isiyostahiliwa kwa wale anaochagua. Kwa hiyo, Yakobo ndiye aliyepata haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza, wala si ndugu yake mkubwa ambaye hakuithamini. Vivyo hivyo, Waisraeli wa kiroho walichukua mahali pa Wayahudi wa asili kwa sababu Wayahudi hao walionyesha mtazamo kama wa Esau wakiwa taifa. (Waroma 9:6-16, 24) Hatuwezi kurithi uhusiano mzuri pamoja na Yehova bila jitihada yoyote, hata kama mtu amezaliwa katika mazingira au familia inayomwogopa Mungu. Wale wote wanaotaka kupata baraka za Mungu wanapaswa kujitahidi kuwa watu wanaomwogopa Mungu, ambao wanathamini kikweli mambo ya kiroho.

Akaribishwa na Labani

Alipofika Padan-aramu kutafuta mke kati ya watu wa jamaa yake, Yakobo alikutana na binamu yake Raheli, binti ya Labani, kwenye kisima. Yakobo aliondoa jiwe nzito lililofunika kisima hicho na kuwanywesha maji wanyama ambao Raheli alikuwa akichunga. * Raheli alikimbia nyumbani kutoa habari kuhusu kufika kwa Yakobo, naye Labani akaharakisha kwenda kukutana naye. Lazima Labani awe alikata tamaa ikiwa alitazamia kupata mali kama ile familia yao ilipata kutoka kwa mtumishi wa Abrahamu, kwa kuwa Yakobo alikuja mikono mitupu. Lakini yaonekana Labani aliona jinsi ambavyo angeweza kujinufaisha kwa kumtumia vibaya Yakobo aliyekuwa mfanyakazi mwenye bidii.—Mwanzo 28:1-5; 29:1-14.

Yakobo alisimulia mambo yaliyompata. Haifahamiki kama alitaja ujanja aliotumia ili kupata haki ya mzaliwa wa kwanza, lakini baada ya kusikia “maneno hayo yote,” Labani alisema hivi: ‘Wewe kweli ndiwe mfupa wangu na nyama yangu.’ Msomi mmoja alisema kwamba huenda maneno hayo yalimaanisha kuwa Yakobo alikaribishwa kwa uchangamfu kukaa nyumbani kwake, au Labani alikuwa anakiri kwamba alilazimika kumlinda Yakobo kwa kuwa alikuwa mtu wa ukoo. Vyovyote vile, Labani alianza kufikiria mara moja jinsi angeweza kumtumia vibaya mpwa wake.

Labani alianzisha jambo ambalo lingesababisha hali ya kutoelewana kwa muda wa miaka 20 iliyofuata. “Kwa sababu wewe ni ndugu yangu, basi, je! unitumikie bure?” akauliza. “Niambie mshahara wako utakuwa nini?” Ingawa Labani alijifanya kuwa mjomba mwema, alipuuza uhusiano wake wa kiukoo pamoja na Yakobo na kufanya mapatano ya kazi pamoja naye. Kwa kuwa Yakobo alimpenda Raheli, alijibu: “Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo.”—Mwanzo 29:15-20.

Ahadi ya ndoa ilifanywa kwa kulipa mahari kwa familia ya bibi-arusi. Baadaye Sheria ya Musa iliweka malipo ya shekeli 50 za fedha kwa ajili ya mabikira walioshawishiwa. Msomi Gordon Wenham anasadiki kwamba hayo ndiyo yaliyokuwa “malipo ya juu zaidi ya mahari,” lakini malipo mengi ya mahari yalikuwa ya “chini zaidi.” (Kumbukumbu la Torati 22:28, 29) Kwa kuwa Yakobo hangeweza kupata malipo hayo, alikubali kumtumikia Labani kwa muda wa miaka saba. Wenham aendelea kusema, “Kwa kuwa nyakati za Wababuloni wa kale wafanyakazi wa muda walipokea kati ya nusu shekeli na shekeli moja kwa mwezi (kutoka shekeli 42 mpaka 84 kwa miaka saba kamili), Yakobo alikubali kumpa Labani kiasi kikubwa sana cha mahari ili kumwoa Raheli.” Labani alikubali kwa furaha.—Mwanzo 29:19.

Yakobo aliona miaka saba kama “siku chache tu” kwa kuwa alimpenda Raheli sana. Baada ya hapo, alidai apewe bibi-arusi wake aliyefunikwa kwa shela, pasipo kujua hila ya Labani. Wazia jinsi alivyoshtuka asubuhi iliyofuata alipogundua kwamba alikuwa amelala na Lea, wala si dada yake Raheli! Yakobo aliuliza: “Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya?” Labani akamjibu: “Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine.” (Mwanzo 29:20-27) Akiwa amenaswa bila kujua la kufanya, Yakobo alilazimika kukubali matakwa hayo ikiwa alimtaka Raheli.

Tofauti na ile miaka saba ya kwanza, miaka saba iliyofuata ilikuwa yenye uchungu sana. Je, Yakobo angeweza kumsamehe Labani kwa sababu ya kumtendea kikatili? Namna gani Lea, ambaye alishiriki ukatili huo? Bila shaka, Labani hakujali hata kidogo magumu ambayo yangewapata Lea na Raheli wakati ujao kwa sababu ya tendo lake. Alijali tu masilahi yake. Raheli ambaye aliendelea kuwa tasa, alimwonea wivu na pia kumwekea kinyongo dada yake Lea alipozaa wana wanne baada ya muda mfupi. Ndipo Raheli, aliyetaka sana kupata watoto, akaamua kutoa kijakazi wake ili apate watoto kupitia kwake, naye Lea akafanya vivyo hivyo ili kushindana naye. Yakobo alijikuta akiwa na wake wanne, watoto 12, na familia isiyo na furaha. Hata hivyo, Yehova alikuwa akimfanya Yakobo kuwa taifa kubwa.—Mwanzo 29:28–30:24.

Atajirishwa na Yehova

Ingawa Yakobo alipata majaribu, aliona kwamba Mungu alikuwa pamoja naye kama alivyoahidi. Labani aliona jambo hilo pia kwa kuwa wale wanyama wachache aliokuwa nao Yakobo alipofika, waliongezeka sana chini ya utunzaji wa mpwa wake. Kwa kuwa Labani hakutaka Yakobo aende, alimwomba amweleze mshahara ambao angetaka alipwe ili aendelee kumtumikia. Naye Yakobo akaomba apewe wanyama wenye rangi isiyo ya kawaida waliozaliwa katika kundi la Labani. Inasemekana kwamba katika eneo hilo, kwa kawaida kondoo walikuwa na rangi nyeupe, nao mbuzi walikuwa na rangi nyeusi au rangi ya kahawia; ni wachache waliokuwa na madoadoa. Kwa hiyo, huku akifikiri kwamba angemlipa Yakobo mshahara mdogo kwa kumpa wanyama wasio na rangi ya kawaida, Labani alikubali kwa furaha na mara moja akaondoa wanyama wote wa Yakobo wenye alama zisizo za kawaida ili wasichanganyike na wale wake ambao Yakobo alikuwa anawatunza. Bila shaka, aliamini kwamba Yakobo hangenufaika sana na mapatano hayo, na hangepata ile asilimia 20 ya wana-mbuzi na wana-kondoo ambayo ilikuwa mshahara wa wachungaji wa kale. Lakini Labani alijidanganya, kwa kuwa Yehova alikuwa pamoja na Yakobo.—Mwanzo 30:25-36.

Chini ya mwongozo wa Mungu, wanyama ambao Yakobo alizalisha walikuwa wenye afya, na wenye rangi ya kupendeza. (Mwanzo 30:37-42) Maoni ya Yakobo kuhusu uzalishaji wa mifugo hayakuwa sahihi. Hata hivyo, “kulingana na sayansi, wanyama hao wangeweza kuzaliwa kwa mchanganyiko wa mbegu ya . . . wanyama wa rangi moja wenye chembe za urithi ambazo zingeweza kutokeza wanyama wa rangi mbalimbali,” asema msomi Nahum Sarna, na “wanyama hao wanatambulikana kwa . . . nguvu zao zinazotokana na mchanganyiko wa chembe za urithi.”

Alipoona matokeo, Labani alijaribu kubadili mapatano kuhusu wanyama waliopaswa kuwa wa mpwa wake—wenye mistari-mistari, madoa-doa ya rangi, au wenye mabaka. Alikuwa akijaribu kujinufaisha, lakini hata ingawa Labani alibadili-badili mapatano hayo, Yehova alihakikisha kwamba sikuzote Yakobo amefanikiwa. Labani alisaga meno yake tu. Baada ya muda mfupi, Yakobo alikuwa na mali nyingi, makundi ya wanyama, watumishi, ngamia, na punda, si kwa sababu ya werevu wake, bali kwa sababu Yehova alikuwa pamoja naye. Baadaye aliwaambia hivi Raheli na Lea: “Baba yenu amenidanganya, akabadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hakumwacha kunidhuru. . . . Hivi Mungu akamnyang’anya mali yake baba yenu na kunipa mimi.” Pia Yehova alimhakikishia Yakobo kwamba Aliona yote ambayo Labani alikuwa akifanya lakini Yakobo hakuhitaji kuwa na wasiwasi. Mungu alimwambia, “Rudi uende mpaka nchi yako, na kwa jamaa zako, nami nitakutendea mema.”—Mwanzo 31:1-13; 32:9.

Baada ya kumwacha Labani mwenye udanganyifu, Yakobo alirudi nyumbani. Ingawa miaka 20 ilikuwa imepita bado alikuwa anamwogopa Esau, na hasa aliposikia kwamba alikuwa njiani akija na wanaume mia nne. Yakobo angefanyaje? Kwa kuwa sikuzote Yakobo alimtumaini Mungu, yeye alitenda kwa imani. Alisali, na kukiri kwamba hakustahili ukarimu wa Yehova na akamsihi aikomboe familia yake kutoka kwa mkono wa Esau kwa msingi wa ahadi Zake.—Mwanzo 32:2-12.

Kisha jambo lisilotarajiwa likatukia. Mtu asiyejulikana ambaye baadaye Yakobo alimtambua kuwa malaika, alipigana mweleka naye usiku na kwa mguso mmoja, akategua paja la Yakobo. Yakobo alikataa kumwachilia mpaka malaika huyo ambariki kwanza. Baadaye nabii Hosea alisema kwamba Yakobo “alilia ili apate kujiombea kibali kwa bidii.” (Hosea 12:2-4, NW; Mwanzo 32:24-29) Yakobo alijua kwamba malaika walikuwa wametokea hapo zamani kuhusiana na kutimizwa kwa agano la Abrahamu kupitia uzao wake. Kwa hiyo akajikakamua sana kupigana mweleka na kupata baraka. Wakati huo, Mungu alibadili jina lake na kumwita Israeli, linalomaanisha “Anayeshindana na Mungu” au “Mungu Hushindana.”

Je, U Tayari Kupigana Mweleka?

Yakobo alikabili na kushinda matatizo mengine mbali na kukutana na Esau na kupigana mweleka na malaika. Hata hivyo, matukio ambayo tumezungumzia hapa yanaonyesha Yakobo alikuwa mtu wa aina gani. Ingawa Esau hangeweza kuvumilia njaa kidogo ili ahifadhi haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza, Yakobo alipambana katika maisha yake yote ili kupata baraka, na hata akapigana mweleka na malaika. Mungu alimwongoza na kumlinda Yakobo kama alivyoahidi, naye akawa baba wa taifa kubwa na babu wa Mesiya.—Mathayo 1:2, 16.

Je, uko tayari kujitahidi ili kupata kibali cha Yehova kana kwamba unapigana mweleka? Leo wale wanaotaka kufanya mapenzi ya Mungu wanapata magumu na mikazo mingi maishani, na nyakati nyingine wanahitaji kujitahidi sana kufanya maamuzi yanayofaa. Hata hivyo, kielelezo kizuri cha Yakobo kinatuchochea sana kushikamana na tumaini la kupata thawabu ambayo Yehova ametuahidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Pindi hiyo inafanana na wakati Rebeka, mama yake Yakobo, alipowanywesha ngamia wa Eliezeri. Kisha Rebeka alikimbia nyumbani na kutoa habari kuhusu kufika kwa mgeni. Labani alipoona vitu vya dhahabu ambavyo dada yake alipewa kama zawadi, akakimbia kumlaki Eliezeri.—Mwanzo 24:28-31, 53.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yakobo alipambana katika maisha yake yote ili apate baraka