Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema Yazaa Matunda Huko São Tomé na Príncipe

Habari Njema Yazaa Matunda Huko São Tomé na Príncipe

Habari Njema Yazaa Matunda Huko São Tomé na Príncipe

YAELEKEA watu wengi hawajasikia kuhusu São Tomé na Príncipe. Kwa kawaida visiwa hivi havionyeshwi katika broshua zinazotangaza sehemu mbalimbali za kwenda likizo. Kwenye ramani ya dunia, visiwa hivi ni kama vidoa tu kwenye Ghuba ya Guinea iliyo magharibi mwa pwani ya Afrika. Kisiwa cha São Tomé kiko karibu sana na ikweta nacho kile cha Príncipe kiko kaskazini mashariki ya São Tomé. Kwa sababu ya hali ya hewa ya mvua na unyevunyevu, milima ambayo urefu wake ni zaidi ya meta 2,000, imefunikwa na misitu ya mvua iliyositawi sana.

Watu wa visiwa hivi vya kitropiki, ambavyo vimezungukwa na maji ya bluu na fuo zenye michikichi, ni wachangamfu na wenye urafiki. Utamaduni wa watu hao unapendeza kwa kuwa wana asili ya Kiafrika na Kizungu. Wakaaji 170,000 wa visiwa hivi hukuza kakao, zao kuu ambalo huuzwa nchi za nje, na wengine ni wakulima au wavuvi. Katika miaka ya hivi karibuni imekuwa vigumu hata kupata chakula cha kila siku.

Hata hivyo, kuna jambo moja lililotukia miaka ya 1990 ambalo liliathiri sana maisha ya wakaaji wa visiwa hivi ambao wanaendelea kuongezeka. Mnamo Juni 1993, Mashahidi wa Yehova walisajiliwa kisheria na serikali ya São Tomé na Príncipe na hivyo kukomesha magumu ya muda mrefu ambayo mara nyingi yaliwakabili katika visiwa hivi.

Mbegu Zilizopandwa Chini ya Magumu

Yaonekana kwamba Shahidi wa kwanza alikuja kwenye visiwa hivi mapema miaka ya 1950 wakati wafungwa kutoka nchi nyingine za Afrika zilizotawaliwa na Wareno walipoletwa visiwani humo kufanya kazi katika kambi za kazi ngumu. Shahidi huyo Mwafrika, aliyekuwa painia au mhudumu wa wakati wote, alifukuzwa nchini Msumbiji kwa sababu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika nchi hiyo. Ingawa Shahidi huyo alikuwa peke yake, alihubiri kwa bidii, na baada ya miezi sita watu wengine 13 wakaijiunga naye kueneza habari njema. Baadaye, Mashahidi wengine walifika visiwani humo baada ya kufukuzwa kutoka Angola. Walipokuwa kifungoni, walitumia kila nafasi kuwahubiria wenyeji habari njema.

Kufikia mwaka wa 1966, ndugu wote waliokuwa wakitumikia kifungo chao kisiwani São Tomé walikuwa wamerudi huko Afrika bara. Wahubiri wachache wa Ufalme waliobaki waliendelea kuhubiri kwa ujasiri. Walinyanyaswa, wakapigwa, na kutiwa gerezani kwa sababu walikutana pamoja kujifunza Biblia, na hakukuwa na mtu wa kuwatembelea au kuwatia moyo. Visiwa hivi vilipata uhuru kutoka Ureno mwaka wa 1975 na hatua kwa hatua mbegu za kweli ya Ufalme zikaanza kuzaa matunda.

Upanuzi na Ujenzi

Mwezi ambao Mashahidi wa Yehova walisajiliwa kisheria mwaka wa 1993, kulikuwa na kilele cha watangazaji wa Ufalme 100. Mwaka huohuo, mapainia wa pekee waliwasili kutoka Ureno. Wenyeji waliwapenda kwa sababu ya jitihada waliyofanya kujifunza Kikrioli kinachotokana na Kireno. Wakati huo hangaiko lao kuu lilikuwa kutafuta uwanja wa kujenga Jumba la Ufalme. Alipopata habari hizo, dada mmoja aitwaye Maria alitoa nusu ya ardhi ambapo nyumba yake ndogo imejengwa. Uwanja huo ulikuwa mkubwa vya kutosha kujenga Jumba kubwa la Ufalme. Maria hakujua kwamba wasitawishaji wa ardhi wenye tamaa walikuwa wakiutaka, kwa kuwa jamaa zake wote walikuwa wamekufa. Siku moja mfanyabiashara fulani mashuhuri alikuja kuzungumza na Maria.

“Mambo ninayosikia kukuhusu si mazuri!” akamwonya. “Ninasikia kwamba umetoa ardhi yako bila malipo. Je, hujui kwamba ardhi hiyo ina thamani kubwa sana kwa kuwa iko katika jiji?”

“Kama ningekubali kukuuzia ardhi hiyo, ungenipa pesa ngapi?” Maria akamwuliza. Mtu huyo alipokosa kujibu, Maria aliendelea kusema: “Hata kama ungenipa pesa zote katika ulimwengu, hazingetosha kwa sababu pesa haziwezi kununua uhai.”

“Huna watoto, sivyo”? mtu huyo akauliza.

Ili kukomesha mazungumzo hayo, Maria alisema: “Ardhi hii ni ya Yehova. Alinikopesha kwa miaka mingi sana nami sasa nimemrudishia. Ninatarajia kuishi milele.” Kisha akamwuliza mtu huyo: “Je, unaweza kutoa uhai wa milele?” Bila kusema lolote mtu huyo aligeuka na kwenda zake.

Matokeo yalikuwa kwamba, jengo zuri la orofa mbili lilijengwa kwa msaada wa ndugu wenye ustadi kutoka Ureno. Jengo hilo lina sehemu iliyo chini ya ardhi, Jumba kubwa la Ufalme, na vyumba vya kuishi. Pia lina madarasa ya kufanyia shule za wazee, watumishi wa huduma, na mapainia. Sasa makutaniko mawili yanafanyia mikutano yao katika jumba hilo, na kulifanya kuwa kituo bora cha kuelimisha watu kwa ajili ya ibada safi katika jiji kuu.

Katika jiji la Mé-Zochi, kulikuwa na kutaniko la wahubiri 60 wenye bidii. Wahubiri hao walihitaji sana Jumba la Ufalme linalofaa kwa sababu mikutano ilifanyiwa katika Jumba la Ufalme la muda lililokuwa katika shamba la ndizi. Baraza la jiji lilijulishwa jambo hilo, na maofisa fulani wenye huruma wakatoa uwanja mzuri kwenye barabara kuu. Jumba zuri la Ufalme lilijengwa kwa muda wa miezi miwili kwa msaada wa ndugu kutoka Ureno, waliotumia ule mpango wa kujenga unaochukua muda mfupi. Wenyeji hawakuamini waliyoona. Mhandisi mmoja kutoka Sweden aliyehusika katika ujenzi fulani jijini alishangaa alipowaona ndugu na dada wakifanya kazi. “Siamini!” akasema. “Mashahidi wa Yehova hapa jijini Mé-Zochi wanatumia mpango wa kujenga unaochukua muda mfupi! Tunapaswa kufanya vivyo hivyo kuhusiana na mjengo wetu.” Watu 232 walihudhuria kuwekwa wakfu kwa Jumba la Ufalme Juni 12, 1999. Jumba hilo linawavutia sana wageni wanaotembelea jiji la Mé-Zochi.

Kusanyiko la Kipekee

Mashahidi wa Yehova katika visiwa vya São Tomé na Príncipe walishuhudia tukio la kipekee wakati Kusanyiko la kwanza la Wilaya la siku tatu lenye kichwa “Ufundishaji wa Kimungu” lilipofanywa Januari 1994 visiwani humo. Lilifanywa katika jumba bora zaidi nchini lenye mfumo wa kusafisha hewa. Je, unaweza kuwazia jinsi watangazaji wa Ufalme 116 walivyofurahi kuona wahudhuriaji 405 na kwa mara ya kwanza wakatazama drama za Biblia na kupokea vichapo vipya kusanyikoni? Watu 20 waliokuwa wamejiweka wakfu walibatizwa kwenye ufuo fulani wa kitropiki.

Watu walivutiwa sana na beji za pekee zilizovaliwa na wajumbe. Wageni 25 waliotoka Ureno na Angola walifanya kusanyiko hilo lionekane kuwa la kimataifa. Uhusiano mchangamfu wa upendo wa Kikristo ulisitawi haraka, na wengi walitokwa na machozi walipoagana baada ya kusanyiko kumalizika.—Yohana 13:35.

Waandishi wa habari kutoka idhaa ya Redio ya Taifa walikuja na kumhoji mwangalizi wa kusanyiko. Pia walitangaza sehemu kadhaa za hotuba zilizotolewa. Hiyo ilikuwa pindi ya pekee kwelikweli, nayo ilisaidia Mashahidi hao waaminifu ambao wameishi mbali kwa muda mrefu wajihisi wako karibu na tengenezo la Yehova linaloonekana.

Kuzaa Matunda kwa Utukufu wa Yehova

Ujumbe wa Ufalme unapozaa matunda, hufanya watu wawe na mwenendo mzuri ambao humtukuza na kumletea Yehova heshima. (Tito 2:10) Msichana mmoja tineja alifurahia mambo aliyokuwa akijifunza katika Biblia kila juma. Hata hivyo, baba yake alimkataza asihudhurie mikutano ya kutaniko. Alipomweleza kwa heshima umuhimu wa mikutano ya Kikristo na tamaa yake ya kuihudhuria, alimfukuza nyumbani mara moja. Yaonekana, alifikiri msichana huyo angefanya kama vijana wengine wengi wanavyofanya, yaani, kuanza kuishi mara moja na mwanamume ambaye angemtegemeza. Baba yake aliposikia kwamba msichana huyo alikuwa akiishi maisha mazuri na safi kiadili akiwa Mkristo, alichochewa kumkubali arudi nyumbani na kumpa uhuru kamili wa kumtumikia Yehova.

Mfano mwingine unahusu mtu mmoja aliyekuwa kiongozi wa kikundi fulani cha wanamuziki. Alikatishwa tamaa na maisha yake yasiyo ya adili. Alipokuwa akitafuta kujua kusudi la maisha, alikutana na Mashahidi. Alipoanza kuishi kupatana na viwango vya maadili vya Biblia, watu wengi mjini walianza kuzungumza juu yake. Muda si muda, akaona anahitaji kuacha mashirika yote yasiyofaa. (1 Wakorintho 15:33) Kisha akachukua hatua muhimu ya kubatizwa ili kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova.

Vijana kadhaa waliokuwa wakitafuta dini ya kweli, walizungumza na makasisi wa vikundi kadhaa vya kiinjili, lakini makasisi hao waliwatatanisha na kuwakatisha tamaa hata zaidi. Hivyo, wakawa wazururaji wenye jeuri waliodhihaki jambo lolote lililohusiana na dini.

Siku moja, mishonari fulani ambaye ni Shahidi wa Yehova, alipitia mahali vijana hao walipokuwa akiwa njiani kwenda kuongoza funzo la Biblia. Vijana hao walitaka mishonari huyo awajibu maswali kadhaa nao wakampeleka nyuma ya nyumba fulani ambako alipewa kiti kidogo akalie. Walimrushia maswali mengi kuhusu mambo kama vile nafsi, moto wa mateso, maisha ya mbinguni, na mwisho wa ulimwengu. Shahidi huyo aliwajibu maswali yao yote akitumia Biblia aliyopewa na kiongozi wa genge hilo. Muda wa saa moja baadaye, kiongozi huyo anayeitwa Law, alimwambia mishonari huyo hivi: “Tulipokuomba uje kujibu maswali, tulikuwa na nia ya kukudhihaki kama tunavyowadhihaki watu wa dini nyingine. Tulifikiri kwamba hakuna mtu anayeweza kujibu maswali hayo. Lakini wewe uliyajibu ukitumia Biblia tu! Nieleze, ninawezaje kujifunza zaidi kuihusu Biblia?” Law alianza kujifunza Biblia na muda mfupi baadaye akaanza kuhudhuria mikutano. Muda si muda aliachana na genge hilo na kuacha maisha ya jeuri. Katika muda wa mwaka mmoja, Law aliweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Sasa yeye ni mtumishi wa huduma.

Desturi moja ya kienyeji ambayo imekita mizizi ni kwamba wanaume na wanawake huishi pamoja tu bila kufunga ndoa. Wengi wameishi pamoja kwa miaka mingi na wamezaa watoto. Wanaona ni vigumu kukubali maoni ya Mungu kuhusu ndoa. Inafurahisha kuona jinsi Neno la Mungu lilivyomsaidia mtu fulani kushinda tatizo hilo.—2 Wakorintho 10:4-6; Waebrania 4:12.

Antonio alijua kwamba alipaswa kuhalalisha ndoa yake naye akapanga kufanya hivyo baada ya kuvuna mahindi na hivyo kupata pesa za kugharimia karamu ya ndoa. Usiku mmoja kabla tu ya kuvuna, wezi walikuja na kuiba mahindi yake. Aliamua kungoja mavuno ya mwaka uliofuata, nayo pia yakaibwa. Aliposhindwa kwa mara nyingine kupata pesa za kugharimia arusi yake, Antonio alitambua mpinzani wake alikuwa nani hasa. “Sitakubali Shetani anichezee tena,” akasema. “Katika muda wa mwezi mmoja na nusu tutafunga ndoa, iwe kutakuwa na karamu au la!” Hivyo walifunga ndoa, nao walishangaa marafiki wao walipotoa kuku, mabata, na mbuzi kwa ajili ya karamu ya ndoa. Baada ya kuhalalisha ndoa yao, Antonio na mke wake—pamoja na watoto wao sita walibatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova.

Kisiwa cha Príncipe

Katika miaka ya hivi majuzi, kisiwa cha Príncipe chenye wakaaji 6,000 kimetembelewa mara kwa mara na waangalizi wa mzunguko na mapainia kutoka São Tomé. Wakaaji wa kisiwa hicho waliwakaribisha vizuri sana nao walikuwa tayari kusikiliza ujumbe wa Mashahidi. Baada ya mtu mmoja kusoma trakti aliyoachiwa, aliwatafuta mapainia hao siku iliyofuata naye akajitoa kuwasaidia kugawanya trakti. Mapainia hao walimweleza kwamba wao ndio waliopaswa kufanya kazi hiyo, lakini mtu huyo akasisitiza kwamba alipaswa kuandamana nao nyumba kwa nyumba ili aweze kuwajulisha kwa wenye nyumba na kuwashauri wawasikilize Mashahidi kwa makini. Mwishowe, mtu huyo aliondoka baada ya kuwapongeza mapainia hao kwa kazi muhimu waliyokuwa wakifanya.

Katika mwaka wa 1998 mapainia wawili walihamia Príncipe kutoka São Tomé, na muda si muda wakawa wanaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 17. Kazi iliendelea kupanuka, na baada ya muda mfupi Funzo la Kitabu la Kutaniko lilikuwa na wastani wa wahudhuriaji 16, na zaidi ya watu 30 walihudhuria hotuba ya watu wote. Baraza la jiji lilijulishwa kuhusu uhitaji wa mahali pa kukutania, na jambo la kufurahisha ni kwamba ndugu walipewa uwanja wa kujenga Jumba la Ufalme. Ndugu kutoka São Tomé walijitolea kujenga Jumba la Ufalme dogo ambalo lina makao ya mapainia wawili wa pekee.

Bila shaka, habari njema inazaa matunda mengi na inazidi kuenezwa katika visiwa hivi vya mbali. (Wakolosai 1:5, 6) Mnamo Januari 1990, kulikuwa na wahubiri 46 huko São Tomé na Príncipe. Katika mwaka wa utumishi wa 2002, kulikuwa na kilele cha watangazaji wa Ufalme 388! Zaidi ya asilimia 20 ya wahubiri ni watumishi wa wakati wote, na mafunzo ya Biblia ya nyumbani yapatayo 1,400 yanaongozwa. Katika mwaka wa 2001, watu 1,907 walihudhuria Ukumbusho, na hicho kilikuwa kilele kisichokuwa na kifani. Naam, katika visiwa hivi vya kitropiki, neno la Yehova linaenea haraka na linatukuzwa.—2 Wathesalonike 3:1.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Vipindi vya Redio Vinavyopendwa Sana

Kati ya vichapo vinavyothaminiwa sana katika visiwa hivi ni Maswali Ambayo Vijana Huuliza-Majibu Yafanyayo Kazi. * Baada ya kila majuma mawili, kunakuwa na kipindi cha dakika 15 chenye kichwa hicho kwenye idhaa ya Redio ya Taifa. Inasisimua kama nini kumsikia mtangazaji akiuliza, “Vijana, mnajuaje kama ni upendo halisi au shauku ya kipumbavu?” kisha anasoma sehemu fulani ya kitabu hicho! (Ona sura ya 31.) Kipindi kingine kama hicho huzungumzia sehemu zilizoteuliwa za kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 33 Vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 33 Vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Jumba la Ufalme la kwanza huko São Tomé mwaka wa 1994

[Picha katika ukurasa wa 10]

1. Jumba la Ufalme lililojengwa kwa muda mfupi huko Mé-Zochi

2. Lile kusanyiko la wilaya la pekee lilifanywa katika jumba hili

3. Watu wenye furaha wanaotaka kubatizwa kwenye kusanyiko

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

Globe: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.