Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sikuzote Unahitaji Amri ya Biblia?

Je, Sikuzote Unahitaji Amri ya Biblia?

Je, Sikuzote Unahitaji Amri ya Biblia?

ULIPOKUWA mtoto mchanga, inaelekea wazazi wako walikuwekea sheria nyingi. Ulipoendelea kukua, ulitambua kwamba walifanya hivyo kwa faida yako. Na ukiwa mtu mzima, huenda bado unaishi kulingana na kanuni fulani walizokufundisha, hata ingawa huko tena chini ya mamlaka yao.

Baba yetu wa mbinguni, Yehova, hutupa amri fulani za moja kwa moja kupitia Neno lake, Biblia. Kwa mfano, anakataza ibada ya sanamu, uasherati, uzinzi, na wizi. (Kutoka 20:1-17; Matendo 15:28, 29) Tunapoendelea ‘kukua katika mambo yote,’ tunatambua kwamba Yehova anatafuta faida yetu na kwamba amri zake hazituzuii kupita kiasi.—Waefeso 4:15; Isaya 48:17, 18; 54:13.

Hata hivyo, kuna hali nyingi ambapo hakuna amri ya moja kwa moja. Katika hali hizo, wengine hufikiri kwamba kwa kuwa hakuna sheria ya moja kwa moja kutoka katika Biblia, basi wako huru kufanya wanavyopenda. Wanasema kwamba ikiwa Mungu angeona ni lazima, angeonyesha mapenzi yake kupitia amri ya moja kwa moja.

Wale wanaofikiri hivyo mara nyingi hufanya maamuzi yasiyo ya hekima nao baadaye huwa na majuto makubwa. Wanakosa kutambua kwamba mbali na sheria, Biblia pia ina mambo yanayoonyesha maoni ya Mungu. Tunapojifunza Biblia na kujua maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali, tunasitawisha dhamiri iliyozoezwa na Biblia na tunasaidiwa kufanya maamuzi yanayopatana na njia zake. Tunapofanya hivyo, tunaufurahisha moyo wake nasi hupata faida zinazotokana na kufanya maamuzi yenye hekima.—Waefeso 5:1.

Mifano ya Biblia Yenye Kutokeza

Tunaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu watumishi wa Mungu nyakati za zamani, tunaona hali ambazo walifikiria maoni ya Yehova hata wakati ambapo hawakuwa chini ya amri ya moja kwa moja. Fikiria mfano wa Yosefu. Wakati alipokuwa akikabiliana na ushawishi usio wa adili wa mke wa Potifa, hapakuwa na sheria ya Mungu iliyoandikwa ambayo ilikataza uzinzi. Ingawa hivyo, hata bila sheria ya moja kwa moja, Yosefu alitambua kwamba kufanya uzinzi ni ‘kumtendea Mungu’ dhambi na pia dhamiri yake mwenyewe. (Mwanzo 39:9) Inaonekana Yosefu alitambua kwamba kufanya uzinzi ni kinyume cha maoni na mapenzi ya Mungu, kama yalivyoonyeshwa katika Edeni.—Mwanzo 2:24.

Fikiria mfano mwingine. Kwenye Matendo 16:3, tunajifunza kwamba kabla ya kumchukua Timotheo katika safari zake za Kikristo, Paulo alimtahiri. Hata hivyo, katika mstari wa 4 tunasoma kwamba baadaye Paulo na Timotheo walisafiri kupitia majiji wakiwapa “maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu.” Kati ya maagizo hayo kulikuwa na uamuzi kwamba Wakristo hawakuwa tena chini ya sheria ya kutahiriwa! (Matendo 15:5, 6, 28, 29) Kwa nini Paulo alihisi kwamba Timotheo alipaswa kutahiriwa? “Kwa sababu ya Wayahudi waliokuwa katika sehemu hizo, kwa maana wote walijua kwamba baba [ya Timotheo] ni Mgiriki.” Paulo hakutaka kuwakwaza au kuwakasirisha bure. Alitaka sana Wakristo waendelee “[kujipendekeza] kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.”—2 Wakorintho 4:2; 1 Wakorintho 9:19-23.

Hayo ndiyo yaliyokuwa maoni ya Paulo na Timotheo. Hebu soma Waroma 14:15, 20, 21 na 1 Wakorintho 8:9-13; 10:23-33, uone jinsi Paulo alivyohangaikia sana hali ya kiroho ya wengine, hasa wale ambao wangeweza kukwazwa na jambo ambalo, kwa kweli, halikuwa kosa. Na Paulo aliandika hivi kumhusu Timotheo: “Sina mtu mwingine yeyote aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mambo yenu. Kwa maana wengine wote wanatafuta faida zao wenyewe, wala si zile za Kristo Yesu. Lakini ninyi mnaujua uthibitisho alioutoa juu yake mwenyewe, kwamba kama mtoto na baba yake yeye alitumika pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Wafilipi 2:20-22) Wanaume hao wawili Wakristo walituwekea mfano mzuri kama nini tunaoweza kuiga leo! Badala ya kutafuta mapendezi yao wenyewe wakati ambapo hakukuwa na amri ya moja kwa moja kutoka kwa Mungu, waliiga upendo wa Yehova na Mwana wake kwa kufikiria jinsi ambavyo maamuzi yao yangewaathiri wengine kiroho.

Hebu mfikirie Yesu Kristo, mfano bora tunaoweza kuiga. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, alieleza waziwazi kwamba yule anayeelewa maana ya amri za Mungu atatii hata mambo ambayo hayaamuriwi au kukatazwa moja kwa moja. (Mathayo 5:21, 22, 27, 28) Yesu, Paulo, Timotheo, na Yosefu hawakuwa na maoni ya kwamba ikiwa hakuna sheria ya moja kwa moja kutoka kwa Mungu, mtu anaweza kufanya anavyopenda. Ili kuwa na maoni kama ya Mungu, wanaume hao waliishi kupatana na amri mbili ambazo Yesu alisema kuwa ndizo kuu kuliko zote—kumpenda Mungu na kumpenda jirani.—Mathayo 22:36-40.

Namna Gani Wakristo Leo?

Ni wazi kwamba hatupaswi kuiona Biblia kama kitabu cha sheria—tukitarajia kwamba kila wajibu utajwe waziwazi. Tunapochagua kufanya mambo kupatana na maoni ya Yehova, hata wakati ambapo hakuna sheria ya moja kwa moja inayoongoza matendo yetu, tunaufurahisha sana moyo wake. Yaani, badala ya kuambiwa sikuzote mambo ambayo Mungu anataka tufanye, tunaweza “kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.” (Waefeso 5:17; Waroma 12:2) Kwa nini kufanya hivyo humfurahisha Yehova? Kwa sababu kwa kufanya hivyo tunaonyesha kwamba hatuhangaikii sana mapendezi na haki zetu wenyewe kama tunavyohangaikia kumpendeza. Tunaonyesha kwamba tunauthamini sana upendo wake hivi kwamba tunataka kuuiga, na kuchochewa na upendo huo. (Methali 23:15; 27:11) Pia, kutenda kulingana na Maandiko hutufanya tuwe na afya nzuri kiroho na wakati mwingine kimwili.

Na tuone jinsi kanuni hiyo inavyoweza kutumiwa katika mambo ya kibinafsi.

Kuchagua Vitumbuizo

Hebu wazia kijana anayetaka kununua kanda fulani ya muziki. Muziki ambao amesikia kwenye kanda hiyo unamvutia sana, lakini hana uhakika kwa sababu upande wa nyuma wa kifuniko cha kanda hiyo unataja ngono na mambo machafu waziwazi. Pia, anajua kwamba nyimbo nyingi za mwanamuziki huyo huonyesha hasira na jeuri. Kwa kuwa anampenda Yehova, kijana huyo anahangaikia maoni na hisia Zake kuhusu jambo hilo. Anaweza kujuaje mapenzi ya Mungu?

Katika barua aliyowaandikia Wagalatia, Paulo anaorodhesha matendo ya mwili na matunda ya roho ya Mungu. Huenda unajua matunda ya roho ya Mungu: upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia. Lakini matendo ya mwili yanatia ndani nini? Paulo anaandika: “Sasa matendo ya mwili ni wazi, nayo ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda, vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo. Kuhusu mambo hayo mimi ninawaonya ninyi kimbele, kama vile nilivyowaonya kimbele, kwamba wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-23.

Ona maneno ya mwisho kabisa katika orodha hiyo—“mambo kama hayo.” Paulo hakuandika orodha kamili ya kila jambo linaloweza kuonwa kuwa tendo la mwili. Haimaanishi kwamba mtu anaweza kudai hivi, ‘Maandiko yananiruhusu kutenda jambo lolote ambalo halipo katika orodha ya Paulo ya matendo ya mwili.’ Badala yake, wasomaji wanapaswa kutumia nguvu zao za ufahamu ili kutambua mambo ambayo huenda hayako kwenye orodha hiyo lakini ni “kama hayo.” Wale wanaofanya pasipo kutubu matendo “kama hayo” ambayo hayajatajwa, hawatarithi baraka za Ufalme wa Mungu.

Kwa hiyo, tunahitaji kufahamu, au kutambua, mambo yanayopendeza machoni pa Yehova. Je, ni vigumu kufanya hivyo? Ikiwa daktari angekushauri ule matunda na mboga zaidi lakini uepuke maandazi, aiskrimu, na vitu kama hivyo. Je, ingekuwa vigumu kuamua keki iko katika orodha gani? Sasa tazama tena orodha ya matunda ya roho ya Mungu na matendo ya mwili. Muziki uliotajwa uko katika orodha gani? Bila shaka haulingani kamwe na upendo, wema, kujizuia, na sifa nyingine zinazohusianishwa na matunda ya roho ya Mungu. Mtu hahitaji sheria ya moja kwa moja ili kufahamu kwamba muziki huo haupatani na maoni ya Mungu. Kanuni hizohizo zinaweza kutumiwa kuhusu vitabu, sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya kompyuta, vituo vya intaneti, na kadhalika.

Mavazi na Mapambo Yanayokubalika

Biblia pia hutoa kanuni zinazohusu mavazi na mapambo. Hizo humwezesha kila Mkristo avalie na kujipamba kwa njia inayofaa na inayopendeza sikuzote. Kuhusiana na hilo, mtu anayempenda Yehova haoni jambo hilo kuwa nafasi ya kufanya mapendezi yake, bali ya kufanya mambo yatakayomfurahisha Baba yake wa mbinguni. Kama tulivyotangulia kuona, kwa kuwa tu Yehova hakutoa maagizo ya moja kwa moja kuhusu jambo fulani haimaanishi kwamba hajali jinsi watu wake wanavyotenda. Mitindo ya mavazi hutofautiana sehemu mbalimbali, na hata katika sehemu moja hubadilika mara kwa mara. Hata hivyo, Mungu amewapa watu wake kanuni za msingi zinazopaswa kuwaongoza nyakati zote na sehemu zote.

Kwa mfano, andiko la 1 Timotheo 2:9, 10 linasema hivi: “Vivyo hivyo natamani wanawake wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mavazi yaliyo ghali sana, bali kwa njia inayowafaa wanawake wanaodai kumheshimu Mungu, yaani, kupitia matendo mema.” Kwa hiyo, wanawake Wakristo—na wanaume pia—wanapaswa kufikiria maoni ya watu wa sehemu yao kuhusu mavazi na mapambo ya wale “wanaodai kumheshimu Mungu.” Ni muhimu hasa Mkristo afikirie jinsi mavazi na mapambo yake yatakavyowafanya watu wengine wauone ujumbe wake wa Biblia. (2 Wakorintho 6:3) Mkristo anayeweka mfano mzuri hatahangaikia kupita kiasi mapendezi na haki zake mwenyewe, badala yake atahangaikia kutowakengeusha au kuwakwaza wengine.—Mathayo 18:6; Wafilipi 1:10.

Mkristo anapotambua kwamba mtindo fulani wa mavazi na mapambo yake unawaudhi au kuwakwaza wengine, anaweza kumwiga mtume Paulo kwa kuhangaikia hali njema ya kiroho ya wengine badala ya mapendezi yake mwenyewe. Paulo alisema: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Na Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu: “Kristo hakujipendeza mwenyewe.” Paulo anatoa maagizo yaliyo wazi kwa ajili ya Wakristo wote: “Sisi tulio na nguvu tunapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu, na tusiwe tukijipendeza wenyewe. Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake.”—Waroma 15:1-3.

Kuboresha Nguvu Zetu za Ufahamu

Tunaweza kusitawishaje nguvu zetu za ufahamu ili kujua jinsi ya kumpendeza Yehova hata wakati ambapo hajatuagiza moja kwa moja kuhusu jambo fulani? Tukisoma Neno lake kila siku, kujifunza kwa ukawaida, na kutafakari mambo tunayosoma, tutaona nguvu zetu za ufahamu zikisitawi. Nguvu hizo hazisitawi haraka. Kama mtoto anavyokua kimwili, ndivyo mtu hukua kiroho hatua kwa hatua nao ukuzi huo hauonekani mara moja. Kwa hiyo, tunahitaji kuwa na subira, na hatupaswi kukata tamaa tusipoona mabadiliko mara moja. Pia, kupita kwa wakati tu hakutaboresha nguvu zetu za ufahamu. Lazima tuutumie wakati huo kulichunguza Neno la Mungu kwa ukawaida kama tulivyotangulia kuona, na lazima tuishi kupatana na Neno hilo kwa kadiri tunavyoweza.—Waebrania 5:14.

Sheria za Mungu hupima utii wetu, nazo kanuni zake hupima kiwango cha hali yetu ya kiroho na tamaa yetu ya kumpendeza. Tunapozidi kukua kiroho, tutazidi kuhangaikia kumwiga Yehova na Mwana wake. Tutataka kufanya maamuzi yetu kulingana na maoni ya Mungu yaliyo katika Maandiko kuhusu mambo. Tunapomfurahisha Baba yetu wa mbinguni katika mambo yote tunayofanya, shangwe yetu itaongezeka pia.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mitindo ya mavazi hutofautiana sehemu mbalimbali, lakini kanuni za Biblia zinapaswa kutuongoza kufanya maamuzi