Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Bwana, Tufundishe Jinsi ya Kusali”

“Bwana, Tufundishe Jinsi ya Kusali”

“Bwana, Tufundishe Jinsi ya Kusali”

“Mmoja wa wanafunzi wake akamwambia: ‘Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.’”—LUKA 11:1.

1. Kwa nini mmoja wa wanafunzi wa Yesu alimwomba awafunze jinsi ya kusali?

PINDI moja mwaka wa 32 W.K., mwanafunzi fulani wa Yesu alimwona akisali. Hangeweza kusikia yale Yesu aliyokuwa akimwambia Baba yake, kwa kuwa yaelekea ilikuwa sala ya kimya-kimya. Hata hivyo, Yesu alipomaliza, mwanafunzi huyo alimwambia hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Ni nini kilichomchochea atoe ombi hilo? Sala ilikuwa jambo la kawaida katika maisha na ibada ya Wayahudi. Maandiko ya Kiebrania yana sala nyingi katika kitabu cha Zaburi na kwingineko. Hivyo, mwanafunzi huyo hakuwa akiomba afunzwe jambo ambalo hakujua au ambalo hakuwa amewahi kulifanya. Bila shaka, alijua sala za kidesturi za viongozi wa dini ya Kiyahudi. Lakini sasa alikuwa amemwona Yesu akisali, na yaelekea aliona tofauti kubwa kati ya sala za marabi za kujionyesha kuwa waadilifu na jinsi Yesu alivyosali.—Mathayo 6:5-8.

2. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu hakumaanisha kuwa tunapaswa kurudia sala ya kielelezo neno kwa neno? (b) Kwa nini tunapendezwa kujua jinsi ya kusali?

2 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, miezi 18 hivi awali, Yesu aliwapa wanafunzi wake sala ya kielelezo ambayo ingetumika kama msingi wa sala zao. (Mathayo 6:9-13) Inawezekana kwamba mwanafunzi huyo hakuwepo wakati huo, hivyo kwa fadhili Yesu akarudia sehemu muhimu za sala hiyo ya kielelezo. Ni wazi kwamba Yesu hakuirudia neno kwa neno, hiyo ikionyesha kwamba hakuwa anawapa sala ya kidini ya kurudia-rudia bila kufikiri. (Luka 11:1-4) Kama mwanafunzi huyo asiyetajwa jina, sisi pia tungependa kufundishwa jinsi ya kusali ili sala zetu zitusaidie kumkaribia Yehova zaidi. Kwa hiyo, na tuchunguze sehemu zote za sala hiyo ya kielelezo kama ilivyoandikwa na mtume Mathayo. Sala hiyo ina maombi saba, matatu yanahusu makusudi ya Mungu na manne yanahusu mahitaji yetu ya kimwili na ya kiroho. Katika makala hii tutazungumzia maombi matatu ya kwanza.

Baba Mwenye Upendo

3, 4. Inamaanisha nini kumwita Yehova “Baba yetu”?

3 Yesu alianza mazungumzo yake kwa kuonyesha kwamba sala zetu zinapaswa kudhihirisha uhusiano wa karibu na wenye heshima pamoja na Yehova. Akizungumza hasa kwa manufaa ya wanafunzi wake waliokuwa wamekusanyika karibu naye kwenye mlima, Yesu aliwaambia wasali kwa Yehova kwa kumwita “Baba yetu uliye mbinguni.” (Mathayo 6:9) Kulingana na msomi mmoja, hata kama Yesu alizungumza Kiebrania au Kiaramu kilichotumiwa na wengi, neno alilotumia kumaanisha “Baba” linafanana na jina ambalo mtoto humwita baba yake kwa upendo. Kumwita Yehova “Baba yetu” huonyesha kwamba tuna uhusiano mchangamfu na wenye kutumainika.

4 Kwa kusema “Baba yetu,” pia tunakiri kwamba sisi ni sehemu ya familia kubwa ya wanaume na wanawake wanaomtambua Yehova kuwa Mpaji-Uhai. (Isaya 64:8; Matendo 17:24, 28) Wakristo waliozaliwa kwa roho hufanywa kuwa “wana wa Mungu,” nao wanaweza ‘kupaaza sauti: “Abba, Baba!”’ (Waroma 8:14, 15) Mamilioni wamekuwa waandamani wao washikamanifu, nao wamejiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu wao kwa ubatizo wa maji. Hao “kondoo wengine” wote wanaweza pia kumfikia Yehova katika jina la Yesu na kumwita “Baba yetu.” (Yohana 10:16; 14:6) Tunaweza kusali kwa ukawaida kwa Baba yetu wa mbinguni ili kumsifu, kumshukuru kwa wema wake wote, na kumtwika mahangaiko yetu, tukiwa na hakika kwamba anatujali.—Wafilipi 4:6, 7; 1 Petro 5:6, 7.

Kulipenda Jina la Yehova

5. Ni lipi ombi la kwanza katika sala ya kielelezo, na kwa nini linafaa?

5 Ombi la kwanza katika sala ya kielelezo linatanguliza mara moja mambo yanayopaswa kutangulizwa. Linasema: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Naam, tunapaswa kuhangaikia sana kutakaswa kwa jina la Yehova kwa sababu tunampenda na tunachukia kuona jinsi ambavyo jina lake limeshutumiwa sana. Wakati alipoasi na kuwashawishi wanadamu wa kwanza wasimtii Mungu, Shetani alilichongea jina la Yehova Mungu na njia yake ya kutawala ulimwengu wote ikatiliwa shaka. (Mwanzo 3:1-6) Isitoshe, tangu uasi wa kwanza, jina la Yehova limeshutumiwa kupitia matendo ya aibu na mafundisho ya wale wanaodai kumwakilisha.

6. Tutaepuka kufanya nini ikiwa tunasali jina la Yehova litakaswe?

6 Tunaposali jina la Yehova litakaswe, tunaonyesha msimamo wetu kuhusiana na suala la enzi kuu, yaani, tunaunga mkono kabisa haki ya Yehova ya kutawala ulimwengu wote. Yehova anataka ulimwengu wote ukaliwe na viumbe wenye akili ambao hujitiisha kwa hiari na kwa furaha chini ya utawala wake wa uadilifu kwa sababu wanampenda na wanapenda yote yanayowakilishwa na jina lake. (1 Mambo ya Nyakati 29:10-13; Zaburi 8:1; 148:13) Kulipenda jina la Yehova kutatusaidia tuepuke kufanya jambo lolote linaloweza kufanya jina hilo takatifu lishutumiwe. (Ezekieli 36:20, 21; Waroma 2:21-24) Kwa kuwa amani ya ulimwengu wote na ya wakaaji wake inategemea kutakaswa kwa jina la Yehova na kujitiisha kwa upendo chini ya utawala wake, tunaposali “jina lako na litakaswe” tunaonyesha uhakika wetu kwamba kusudi la Yehova litatimizwa kwa sifa yake.—Ezekieli 38:23.

Ufalme Tunaoomba

7, 8. (a) Yesu alitufunza tusali kuhusu Ufalme gani? (b) Tunajifunza nini kuhusu Ufalme huo katika kitabu cha Danieli na cha Ufunuo?

7 Ombi la pili katika sala ya kielelezo ni: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:10) Ombi hilo linahusiana sana na lile linalotangulia. Ili kutakasa jina lake takatifu Yehova atatumia Ufalme wa Kimasihi, yaani, serikali yake ya kimbingu ambayo Mwana wake, Yesu Kristo, ndiye amewekwa rasmi kuwa Mfalme anayefaa. (Zaburi 2:1-9) Unabii wa Danieli unafananisha Ufalme wa Kimasihi na “jiwe” lililokatwa kutoka ‘mlimani.’ (Danieli 2:34, 35, 44, 45) Mlima unafananisha enzi kuu ya Yehova, kwa hiyo Ufalme unaofananishwa na jiwe ni wonyesho mpya wa utawala wa Yehova juu ya ulimwengu. Katika unabii huo, jiwe nalo ‘linakuwa mlima mkubwa na kuijaza dunia yote,’ kuonyesha kwamba Ufalme wa Kimasihi utawakilisha mamlaka kuu ya Mungu katika kutawala dunia.

8 Kuna wengine 144,000 ambao wanashirikiana na Kristo katika serikali hii ya Ufalme, ambao “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu” ili watawale pamoja naye wakiwa wafalme na makuhani. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4; 20:6) Danieli anawaita “watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi,” ambao pamoja na Kristo aliye Kichwa chao, hupokea “ufalme na utawala na ukuu wa falme zote chini ya mbingu zote . . . Ufalme wao ni ufalme unaodumu mpaka wakati usio na kipimo, na tawala zote zitawatumikia na kuwatii wao.” (Danieli 7:13, 14, 18, 27) Huo ni ufafanuzi mzuri wa serikali ya kimbingu ambayo Kristo aliwafunza wafuasi wake wasali kuihusu.

Kwa Nini Bado Tusali Ufalme Uje?

9. Kwa nini inafaa tusali Ufalme wa Mungu uje?

9 Katika sala yake ya kielelezo, Kristo alitufunza tusali Ufalme wa Mungu uje. Kutimizwa kwa unabii wa Biblia kwaonyesha kwamba Ufalme wa Kimasihi ulisimamishwa mbinguni mwaka wa 1914. * Kwa hiyo, je, bado inafaa tusali Ufalme huo “uje”? Bila shaka. Kwa kuwa katika unabii wa Danieli, Ufalme wa Kimasihi unaofananishwa na jiwe, utaponda serikali za kisiasa za wanadamu, zinazofananishwa na sanamu kubwa. Jiwe hilo litaiponda-ponda sanamu hiyo iwe kama unga. Unabii wa Danieli unasema: “Ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.

10. Kwa nini tunatamani Ufalme wa Mungu uje?

10 Tunatamani kuona Ufalme wa Mungu ukija na kuharibu mfumo mwovu wa mambo wa Shetani kwa sababu hilo litamaanisha kutakaswa kwa jina takatifu la Yehova na kuondolewa kwa wanadamu wote wanaopinga enzi kuu ya Mungu. Tunasali hivi kwa bidii: “Ufalme wako na uje,” nasi tunajiunga na mtume Yohana kusema: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.” (Ufunuo 22:20) Naam, Yesu na aje kulitakasa jina la Yehova na kutetea enzi Yake kuu, ili maneno haya ya mtunga-zaburi yaweze kutimia: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—Zaburi 83:18.

“Mapenzi Yako na Yatendeke”

11, 12. (a) Sisi huwa tunaomba nini tunaposali mapenzi ya Mungu “yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni”? (b) Kusali mapenzi ya Yehova yatendeke kunamaanisha nini zaidi?

11 Halafu Yesu akawafunza wanafunzi wake wasali hivi: “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ulimwengu wote ulitokea kwa sababu ya mapenzi ya Yehova. Viumbe wa mbinguni wenye nguvu hupaaza sauti: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Yehova ana kusudi kuelekea “vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:8-10) Tunaposali mapenzi ya Mungu yatendeke, sisi kwa kweli huwa tunamwomba Yehova atimize kusudi lake. Isitoshe, tunaonyesha kwamba tunatamani kuona mapenzi ya Mungu yakitendeka katika ulimwengu wote.

12 Kupitia sala hiyo tunaonyesha pia kwamba tuko tayari kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova. Yesu alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Kama Yesu, sisi ambao ni Wakristo waliojiweka wakfu tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu. Upendo wetu kwa Yehova na kwa Mwana wake hutuchochea tuishi “si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.” (1 Petro 4:1, 2; 2 Wakorintho 5:14, 15) Sisi hujitahidi kuepuka kufanya mambo tunayojua ni kinyume cha mapenzi ya Yehova. (1 Wathesalonike 4:3-5) Kwa kununua wakati wa kusoma na kujifunza Biblia, ‘tunaendelea kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova,’ ambayo yanatia ndani kuhubiri “hii habari njema ya ufalme.”—Waefeso 5:15-17; Mathayo 24:14.

Mapenzi ya Yehova Mbinguni

13. Mapenzi ya Mungu yalikuwa yakitendeka jinsi gani muda mrefu kabla ya uasi wa Shetani?

13 Mapenzi ya Yehova yalikuwa yakitimizwa mbinguni muda mrefu kabla mmoja wa wana wake wa kiroho kuasi na kuwa Shetani. Kitabu cha Methali humfananisha Mwana wa kwanza wa Mungu na hekima. Kinaonyesha kwamba kwa muda usio na kipimo, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu ‘alikuwa akifurahi mbele zake wakati wote,’ akifurahi kufanya mapenzi ya Baba yake. Mwishowe, akawa “stadi wa kazi” wa Yehova katika kuumba vitu vyote “mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana.” (Methali 8:22-31; Wakolosai 1:15-17) Yehova alimtumia Yesu kuwa Neno, au Msemaji wake.—Yohana 1:1-3.

14. Tunaweza kujifunza nini katika Zaburi 103 kuhusu jinsi malaika wanavyotimiza mapenzi ya Yehova mbinguni?

14 Mtunga-zaburi anaonyesha kwamba enzi kuu ya Yehova iko juu ya uumbaji wote na kwamba malaika husikiliza maagizo na amri zake. Tunasoma: “Yehova amekifanya imara kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake mwenyewe umetawala juu ya kila kitu. Mbarikini Yehova, enyi malaika zake, mlio na uwezo katika nguvu, mnaolitenda neno lake, kwa kuisikiliza sauti ya neno lake. Mbarikini Yehova, enyi majeshi yake yote, enyi wahudumu wake, mnaofanya mapenzi yake. Mbarikini Yehova, enyi kazi zake zote, katika mahali pote pa utawala [au, “enzi kuu”] wake.”—Zaburi 103:19-22.

15. Mapenzi ya Mungu yalitendekaje mbinguni Yesu alipopokea mamlaka ya Ufalme?

15 Baada ya Shetani kuasi, bado angeweza kuingia mbinguni, kama inavyoonyeshwa katika kitabu cha Ayubu. (Ayubu 1:6-12; 2:1-7) Hata hivyo, kitabu cha Ufunuo kilitabiri kwamba wakati ungefika ambapo Shetani na roho wake waovu wangefukuzwa mbinguni. Yaonekana wakati huo ulifika muda mfupi baada ya Yesu Kristo kupokea mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914. Tangu wakati huo, waasi hao hawana mahali tena mbinguni. Wamezuiwa katika ujirani wa dunia. (Ufunuo 12:7-12) Sasa hakuna yeyote mbinguni anayepinga enzi kuu ya Yehova, bali wote wameungana kumsifu “Mwana-Kondoo,” Kristo Yesu, na kumsifu Yehova kwa utii. (Ufunuo 4:9-11) Kwa kweli, mapenzi ya Yehova yanatimizwa mbinguni.

Mapenzi ya Mungu Kuhusu Dunia

16. Sala ya kielelezo inapingaje fundisho la makanisa yanayojiita ya Kikristo kuhusu tumaini la wanadamu?

16 Makanisa yanayojiita ya Kikristo hayataji dunia katika makusudi ya Mungu, yakidai kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni. Lakini Yesu alitufunza tusali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Je, tunaweza kusema kwamba mapenzi ya Yehova yanatimizwa kikamili leo katika dunia hii yenye jeuri, ukosefu wa haki, magonjwa, na kifo? Sivyo! Kwa hiyo, tunapaswa kusali kwa bidii mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kupatana na ahadi hii iliyoandikwa na mtume Petro: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya [serikali ya Ufalme wa Kimasihi wa Kristo] na dunia mpya [jamii ya wanadamu waadilifu], na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

17. Ni nini kusudi la Yehova kuelekea dunia?

17 Yehova aliiumba dunia akiwa na kusudi. Alimwongoza nabii Isaya kwa roho yake aandike: “Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’” (Isaya 45:18) Mungu aliwaweka wenzi wa kwanza wa kibinadamu katika bustani ya kiparadiso na kuwaagiza hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:27, 28; 2:15) Ni wazi kwamba kusudi la Muumba ni kwamba dunia ikaliwe na jamii ya wanadamu wakamilifu na waadilifu, ambao hujitiisha kwa furaha chini ya enzi kuu ya Yehova na kuishi milele katika Paradiso iliyoahidiwa na Kristo.—Zaburi 37:11, 29; Luka 23:43.

18, 19. (a) Ni nini kinachopaswa kufanywa kabla ya mapenzi ya Mungu kutimizwa kikamili duniani? (b) Ni mambo gani mengine kuhusu sala ya kielelezo ya Yesu yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?

18 Mapenzi ya Yehova kuhusu dunia hayawezi kamwe kutimizwa kikamili huku dunia ikiwa na wanaume na wanawake wanaokaidi enzi kuu yake. Akitumia majeshi yenye nguvu ya viumbe wa roho chini ya uongozi wa Kristo, Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ Mfumo wote mwovu wa Shetani pamoja na dini za uwongo, siasa fisadi, biashara yenye pupa na isiyo ya unyoofu, na majeshi yenye kuleta uharibifu, yataharibiwa kabisa. (Ufunuo 11:18; 18:21; 19:1, 2, 11-18) Enzi kuu ya Yehova itatetewa na jina lake kutakaswa. Tunaomba mambo hayo yote tunaposema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

19 Hata hivyo, katika sala yake ya kielelezo, Yesu alionyesha kwamba tunaweza pia kusali kuhusu mambo ya kibinafsi. Mambo hayo ambayo yametajwa katika mafundisho yake kuhusu sala yatazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ona sura ya 6 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Kwa Kupitia

• Kwa nini inafaa tumwite Yehova “Baba yetu”?

• Kwa nini ni muhimu sana tusali jina la Yehova litakaswe?

• Kwa nini tunasali Ufalme wa Mungu uje?

• Inamaanisha nini kusali mapenzi ya Mungu yatendeke hapa duniani kama mbinguni?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sala za Yesu zilikuwa tofauti sana na sala za Mafarisayo za kujionyesha kuwa waadilifu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo husali Ufalme wa Mungu uje, jina lake litakaswe, na mapenzi yake yatendeke