Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukusanyika Kwenye “Kitovu cha Ulimwengu”

Kukusanyika Kwenye “Kitovu cha Ulimwengu”

Kukusanyika Kwenye “Kitovu cha Ulimwengu”

Je, umewahi kusikia maneno “Te Pito o Te Henua”? Katika lugha ya Rapa Nui, ambayo ni lugha ya asili ya Kisiwa cha Easter, maneno hayo yanamaanisha “Kitovu cha Ulimwengu.” Ni nini kilichofanya kusanyiko fulani lililofanyiwa huko liwe la pekee sana?

KISIWA hicho kiko mbali, kinavutia, na si cha kawaida. Hayo ni baadhi ya maneno yanayotumiwa kufafanua Kisiwa cha Easter, au Rapa Nui kama wenyeji wanavyokiita. Kwa kweli, kisiwa hicho kiko mbali sana kwenye Bahari ya Pasifiki Kusini. Kiko umbali wa kilometa 3,790 kutoka Santiago, Chile. Kilipata kuwa mkoa wa Chile Septemba 9, 1888.

Kisiwa hicho chenye umbo la pembetatu na ukubwa wa kilometa 166 za mraba, kimefanyizwa kwa volkeno tatu zilizozimika. Naam, kama visiwa vingi vya Pasifiki, kisiwa hicho ni vilele tu vya milima mikubwa iliyofunikwa kwa maji. Kisiwa chote kimetangazwa kuwa nguzo ya ukumbusho ya asili. Bila shaka, kisiwa hicho ni maarufu kwa sanamu za mawe zenye kuvutia zinazoitwa moai. *

Mbali na mandhari zenye kuvutia na maeneo ya kihistoria, Kisiwa cha Easter kina vyakula vingi vitamu. Kina matunda kama vile mananasi, parachichi, mapapai, na aina tisa za ndizi. Nayo bahari ina samaki wa aina mbalimbali na vyakula vingine vya baharini.

Kisiwa cha Easter kina hali ya hewa yenye kupendeza. Wageni hupata hewa safi na mandhari zenye kuvutia kutokana na pinde za mvua, na pia mvua inayonyesha kwa ukawaida. Sasa kisiwa hicho kina wakaaji wapatao 3,800. Wenyeji wa sasa ni wazao wa walowezi wa kwanza, ambao walichanganyikana na watu wa Ulaya, watu wa Chile, na wa mataifa mengine. Mamia ya watalii kutoka Ulaya na Asia hutembelea kisiwa hicho na kufanya utalii uwe sekta muhimu ya uchumi.

Mbegu za Ufalme Zilizopandwa Kwanza

Kichapo 1982 Yearbook of Jehovah’s Witnesses kiliripoti: “Kwa muda fulani tulikuwa na mhubiri mmoja tu katika Kisiwa cha Easter. Mhubiri huyo aliyekuwa mwanamke alisaidiwa kiroho kupitia barua alizoandikiwa na dada mishonari kwenye ofisi ya tawi [ya Chile]. Ingawa sasa mhubiri huyo amerudi Chile, tuna majina ya watu wa kisiwa hicho ambao wameandikisha gazeti la Mnara wa Mlinzi. Mnamo Aprili 1980 tulishangaa sana kupata simu ya kutoka mbali iliyopigwa na mtu mwenye kupendezwa aliyetaka kujua Ukumbusho ulipaswa kuadhimishwa lini. Baadaye mwaka huohuo, mtu mmoja na mke wake wakahamia kisiwa hicho kutoka Valparaiso, nao wamekuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia na watu wenye kupendezwa. Mnamo Aprili 1981, Ukumbusho ulifanywa katika kisiwa hicho kwa mara ya kwanza, na watu 13 wakahudhuria. Tunafurahi sana kwamba ‘habari njema’ zinapenya eneo hilo la mbali!”

Baadaye, Januari 30, 1991, Dario na Winny Fernandez, mume na mke waliokuwa mapainia wa pekee, walitumwa na ofisi ya tawi kwenda kwenye kisiwa hicho. Ndugu Fernandez anakumbuka: “Baada ya kusafiri kwa ndege kwa muda wa saa tano, tulifika kwenye eneo hilo la mbali la dunia, ambalo lina utamaduni wenye mambo mengi yasiyo ya kawaida.” Mikutano na mahubiri yalipangwa papo hapo kwa msaada wa ndugu mwenyeji na dada aliyekuwa amewasili tu pamoja na watoto wake wawili. Ingawa kulikuwa na magumu ya kifamilia, mhemuko wa kidini, na mitindo fulani ya maisha ambayo ni ya kawaida katika utamaduni wa Polynesia, ndugu hao waliona jinsi Yehova alivyobariki jitihada zao. Ndugu na Dada Fernandez si mapainia wa pekee tena, lakini bado wanaishi katika kisiwa hicho ambako wanamlea mwana wao, aliyezaliwa huko. Leo kuna watangazaji wa Ufalme 32 wenye furaha. Kati yao ni wenyeji wa Rapa Nui, na pia walowezi wa kisiwa hicho au ndugu waliohamia kisiwani humo ili watumikie mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa watangazaji wa Ufalme.

Kujitayarisha kwa Ajili ya Kusanyiko la Mzunguko

Kwa sababu ya umbali mkubwa uliopo kati ya kisiwa hicho na bara, kutaniko lilikuwa likipokea kanda za video za programu ya kusanyiko la pekee, kusanyiko la mzunguko na la wilaya mara tatu kwa mwaka. Lakini kufikia mwisho wa mwaka wa 2000, Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Chile ilikuwa ikifikiria kufanya kusanyiko la kwanza kabisa katika kisiwa hicho. Mwishowe, iliamuliwa kusanyiko la mzunguko lifanywe Novemba 2001, na akina ndugu na dada wachache kutoka sehemu mbalimbali za Chile walialikwa kuhudhuria kusanyiko hilo lililokuwa tukio la pekee. Kusanyiko hilo lingefanywa Jumapili na Jumatatu kwa sababu ya ratiba ya usafiri wa ndege.

Wajumbe 33 walioalikwa walifurahia sana kusafiri kwenda kwenye kisiwa hicho ili kushiriki katika kusanyiko la kwanza la mzunguko kufanywa katika eneo hilo la mbali. Baada ya safari ndefu ya ndege katika anga ya Bahari ya Pasifiki, wajumbe hao walifurahi kukaribishwa na ndugu wenyeji waliokuwa wakiwangojea kwenye uwanja wa ndege. Wajumbe hao walikaribishwa kwa kuvikwa mikufu ya maua, ambayo ni zawadi ya kawaida katika kisiwa hicho. Kisha wakapelekwa kuonyeshwa mahali pao pa kulala, na baada ya kutembea ili kujionea kisiwa hicho, wote waliokuwa na sehemu kwenye programu ya kusanyiko wakakutana katika Jumba la Ufalme.

Tangazo Lafanywa na Mtu Asiyetazamiwa

Wajumbe fulani walipokuwa wakisafiri kwa gari kwenda kusanyikoni, walishangaa kumsikia kasisi mwenyeji akieleza redioni kuhusu ziara yao. Alitaja watalii kutoka bara ambao wangewatembelea watu nyumbani kwao kuzungumza kuhusu mwisho wa ulimwengu. Ingawa aliwahimiza waumini wa kanisa lake wasiwasikilize wageni hao, tangazo lake lilisaidia kusambaza habari kwamba kulikuwa na kikundi kikubwa cha Mashahidi wa Yehova kisiwani humo. Jambo hilo liliwatia wenyeji hamu ya kuwaona wageni hao. Katika siku zilizofuata, wajumbe hao waliwaeleza kwa busara ujumbe wenye kutia moyo wa habari njema.

Kusanyiko Laanza

Jumapili asubuhi, ndugu wenyeji walikuwa wakingoja kwenye kiingilio cha Jumba la Ufalme ili kuwakaribisha wajumbe walipowasili siku ya kwanza ya kusanyiko. “Iorana Koe! Iorana Koe!” “Karibuni!” Dada fulani walivalia mavazi ya kitamaduni na kupamba nywele zao maua kwa mtindo halisi wa Polynesia.

Baada ya muziki mtamu unaotangulia programu, watu mia moja waliimba pamoja wimbo, “Iweni Imara, Bila Kuondoleka!” Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa watu wengi hivyo kuimba pamoja kisiwani humo. Ndugu wenyeji walitoa machozi wakati mwenyekiti alipowakaribisha kwa uchangamfu katika lugha yao ya asili ya Rapa Nui. Wakati wa mapumziko ya mchana, Mashahidi watatu wapya walionyesha wakfu wao kwa Mungu kupitia ubatizo wa maji. Programu ya siku ya kwanza ilipomalizika, kila mtu alihisi kuwa karibu zaidi na Yehova na ndugu zake wote ulimwenguni.—1 Petro 5:9.

Mahubiri ya Asubuhi

Kwa sababu ya hali za kipekee kisiwani humo, programu ya siku ya pili ya kusanyiko la mzunguko ilianza baada ya chakula cha mchana. Kwa hiyo, wajumbe wakatumia kipindi cha asubuhi kuhubiri. Wangejionea mambo gani?

Mwanamke mmoja mzee mwenye wana na mabinti wanane aliwaambia Mashahidi kwamba hangeweza kuzungumza nao kwa sababu alikuwa Mkatoliki. Baada ya kumwambia kwamba walitaka kuzungumza naye kuhusu matatizo yanayokabili kila mtu, kama vile matumizi ya dawa za kulevya na matatizo ya kifamilia, alikubali kuwasikiliza.

Mwanamke mmoja mzee mwenyeji aliwakaribisha kwa ubaridi mume na mke Mashahidi. Aliwaambia waende wakazungumze na watu kwenye bara ambao ni wakatili sana. Mashahidi hao walimwambia kwamba ujumbe wa “habari njema ya ufalme” unatolewa kwa wote na kwamba kusudi lao la kuja katika kisiwa hicho lilikuwa kuhudhuria kusanyiko ambalo lingewasaidia wote wampende Mungu zaidi. (Mathayo 24:14) Walimwuliza kama angefurahia maisha marefu katika hali za kiparadiso, zinazofanana na za kisiwa hicho lakini bila magonjwa na kifo. Baada ya Mashahidi hao kujadiliana naye kuhusu miaka ambayo mashimo ya volkeno yamekuwako, alitafakari kuhusu ufupi wa maisha kisha akauliza: “Kwa nini tunaishi kwa muda mfupi tu?”Alishangaa aliposoma Zaburi 90:10.

Ndipo Mashahidi hao wakasikia kelele kutoka katika nyumba jirani. Ingawa hawakuelewa kelele hizo, mwanamke huyo aliwaambia kwamba majirani walikuwa wakitoa matusi na kusema wazi kwamba hawakutaka kutembelewa na Mashahidi. Hata hivyo, mwanamke huyo alikuwa nua, au binti mkubwa katika familia hiyo. Tangu baba yake afe, alikuwa na daraka la kuamulia familia hiyo mambo yenye manufaa kwao. Aliwatetea Mashahidi hao mbele ya jamaa zake katika lugha yake ya asili na kukubali kwa upole vichapo alivyopewa. Baadaye juma hilo, alipokuwa akipita barabara fulani, aliwaona Mashahidi na kumwambia ndugu yake asimamishe gari. Ingawa ilikuwa wazi kwamba ndugu yake alikasirika, mwanamke huyo aliwaaga ndugu hao na kuwatakia mema katika huduma yao.

Ingawa hapo mwanzoni ilionekana kwamba wenyeji fulani wa kisiwa hicho walikataa ujumbe uliohubiriwa na Mashahidi wa bara, ilikuwa wazi kwa wageni hao kwamba wakaaji wa Rapa Nui ni wenye fadhili na wenye urafiki. Wengi wao walifurahia kusikiliza habari njema. Kwa kweli, Mashahidi 6 kati ya 20 ambao wamebatizwa katika kisiwa hicho ni wenyeji. Mmoja wao alijifunza kweli ya Biblia kwa kusikiliza akiwa katika chumba kingine wakati mke wake alipokuwa akifunzwa Biblia. Sasa yeye na mke wake ni Mashahidi waliobatizwa, naye ni mtumishi wa huduma kutanikoni.

Programu ya Kiroho Yaendelea

Baada ya chakula cha mchana, siku ya pili ya programu ilianza. Kwa mara nyingine tena, watu kadhaa wenye kupendezwa walijiunga na ndugu na dada wenyeji 32 na wajumbe 33. Watu wapatao 100 walisikiliza programu hiyo kutia ndani hotuba ya watu wote, “Jinsi Upendo na Imani Huushinda Ulimwengu.” Naam, wale waliohudhuria walijionea upendo halisi ulio kati ya watu wa Yehova, hata kati ya wale wa tamaduni mbalimbali.—Yohana 13:35.

Wakati wa kusanyiko hilo la mzunguko, waangalizi wa mzunguko na wa wilaya walifanya mkutano wa pekee pamoja na mapainia. Mkutano huo ulihudhuriwa na mapainia watatu wa kawaida wenyeji, na wajumbe ambao walikuwa mapainia wa kawaida au wa pekee. Wote walitiwa moyo sana.

Siku iliyofuata, baadhi ya ndugu wenyeji wanaofanya kazi ya kutembeza wageni, waliwatembeza wajumbe hao katika kisiwa hicho. Walitembelea machimbo ya mawe ambako moai zilichongwa, volkeno ambako mashindano ya kale yalifanyiwa, na pia wakatembelea ufuo wa Anakena wenye mchanga mzuri wa rangi ya dhahabu, ambako walowezi wa kwanza kisiwani humo walishuka kutoka melini. *

Tulikutana na akina ndugu mara ya mwisho kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko. Baada ya mkutano huo, Mashahidi wenyeji waliwashangaza wageni wao kwa chakula cha kienyeji. Baadaye, walicheza dansi ya kitamaduni wakiwa wamevalia mavazi yao ya kitamaduni. Wajumbe hao na pia ndugu na dada wa Rapa Nui, walikuwa na hakika kwamba haikuwa kazi bure kufanya mipango kuwe na kusanyiko hilo.

Wajumbe wote walihisi wakiwa na ukaribu sana na ndugu na dada hao wa mbali, ambao walikaa nao kwa juma moja lenye kufurahisha. Haikuwa rahisi kuondoka kisiwani humo. Sikuzote watakumbuka marafiki wapya na pia kitia-moyo cha kiroho walichopata. Wakiwa kwenye uwanja wa ndege, ndugu wenyeji waliwavika wajumbe mikufu waliyotengeneza kwa makombe.

Wajumbe walipokuwa wakiondoka, waliahidi: “Iorana! Iau he hoki mai e Rapa Nui ee,” maneno yanayomaanisha: “Kwaheri! Nitarudi kwako, Rapa Nui.” Naam, wana hamu ya kurudi kuwatembelea marafiki wao wapya na familia ya kiroho inayoishi katika Kisiwa kisicho cha kawaida cha Easter, kilicho mbali, chenye kuvutia, na chenye wakaaji wenye urafiki!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona gazeti la Amkeni!, Juni 22, 2000, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 27 Kwenye mashimo ya volkeno ya Rano Raraku, kuna michoro mingi kwenye mawe. Hapa ndipo mashindano kati ya wale waliotaka kutawala kisiwa hicho yalipoanzia. Mashindano hayo yalihusisha kuteremka mteremko mkali, kuogolea hadi kwenye mojawapo ya visiwa vidogo, kuchukua yai la ndege wa kisiwani humo, kuogelea na kurudi kwenye kisiwa kikuu, kisha kupanda na yai hilo bila kilivunja.

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

Kuhubiri Katika Kisiwa cha Easter

Miaka miwili hivi kabla ya kusanyiko hilo lisilosahaulika, mwangalizi mmoja wa mzunguko na mke wake walitembelea kisiwa hicho na kujionea mambo mengi yenye kupendeza. Kwa mfano, wazia jinsi walivyoshangaa wakati dada mmoja aliyewapeleka mahali pa kulala alipowakumbusha kwamba walijifunza Biblia pamoja naye akiwa tineja huko kusini mwa Chile, miaka 16 hivi iliyopita. Baadaye, mbegu hiyo ilizaa matunda huko Rapa Nui.

Pia walijionea jambo hili lenye kuchekesha: Mwenye duka la bidhaa za kumbukumbu alikubali Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya pamoja na kitabu cha kujifunzia Biblia, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, ambavyo vinachapishwa na Mashahidi wa Yehova. Walipomrudia aliwaambia kwamba hangeweza kusoma Biblia hiyo. Walikuwa wamemwachia Biblia ya Kifaransa wala si ya Kihispania! Tatizo hilo lilitatuliwa haraka, na kwa msaada wa Mashahidi wenyeji, na bila shaka kwa kutumia Biblia katika lugha yake mwenyewe, akatambua kwamba haikuwa vigumu kuielewa Biblia.

[Ramani katika ukurasa wa 22]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

KISIWA CHA EASTER

CHILE

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wawili kati ya wale waliobatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mteremko wa volkeno ya Rano Raraku; picha iliyo ndani: Tunda la mwituni liitwalo “guayaba” hukua katika kisiwa hicho