Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara

“Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara

“Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara

“Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani?”—MATHAYO 24:45.

1, 2. Kwa nini ni muhimu tupate chakula cha kiroho kwa ukawaida leo?

JUMANNE alasiri, Nisani 11, 33 W.K., wanafunzi wa Yesu waliuliza swali lenye maana kubwa sana kwetu leo. Walimwuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Yesu aliwajibu kwa kutoa unabii muhimu sana. Alitaja kipindi chenye msukosuko cha vita, njaa, matetemeko ya nchi, na magonjwa. Kipindi hicho kingekuwa tu “mwanzo wa maumivu ya taabu.” Hali zingezidi kuwa mbaya. Hayo ni matazamio yenye kuogopesha kama nini!—Mathayo 24:3, 7, 8, 15-22; Luka 21:10, 11.

2 Tangu mwaka wa 1914 sehemu kubwa ya unabii huo wa Yesu imetimizwa. Wanadamu wamepatwa na “maumivu ya taabu” kwa kiwango kikubwa. Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawahitaji kuogopa. Yesu aliahidi kwamba angewategemeza kwa chakula cha kiroho chenye kujenga. Kwa kuwa sasa Yesu yuko mbinguni, amefanya mipango gani ili tupate chakula cha kiroho hapa duniani?

3. Yesu amefanya mipango gani ili tupate ‘chakula kwa wakati unaofaa’?

3 Yesu mwenyewe alionyesha jibu la swali hilo. Alipokuwa akitoa unabii wake mkuu, aliuliza: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa?” Kisha akasema: “Mtumwa huyo atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika atamkuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:45-47) Naam, kungekuwa na “mtumwa” ambaye angepewa mgawo wa kuandaa chakula cha kiroho, “mtumwa” ambaye angekuwa mwaminifu na mwenye busara. Je, mtumwa huyo alikuwa mtu mmoja tu, watu mmoja-mmoja wenye kufuatana, au kitu kingine tofauti? Kwa kuwa mtumwa mwaminifu huandaa chakula cha kiroho kinachohitajiwa sana, ingefaa tujue jibu la swali hilo.

Je, “Mtumwa” Huyo Ni Mtu Mmoja au Ni Kikundi cha Watu?

4. Tunajuaje kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hawezi kuwa mtu mmoja?

4 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hawezi kuwa mtu mmoja. Kwa nini? Kwa sababu mtumwa huyo alianza kuandaa chakula cha kiroho katika karne ya kwanza, na kulingana na Yesu, angekuwa akifanya hivyo wakati Bwana wake angewasili 1914. Hiyo ingemaanisha kwamba mtu mmoja angetumikia kwa uaminifu kwa miaka 1,900 hivi. Hata Methusela hakuishi muda mrefu hivyo!—Mwanzo 5:27.

5. Eleza kwa nini maneno “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hayarejelei Mkristo mmoja-mmoja.

5 Hivyo basi, je, huenda maneno “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” yakarejelea kiujumla kwa kila Mkristo? Ni kweli kwamba Wakristo wote wanapaswa kuwa waaminifu na wenye busara; hata hivyo, ni wazi kwamba Yesu alikuwa akifikiria jambo lingine aliposema juu ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Tunajuaje? Kwa sababu alisema kwamba wakati ambapo ‘bwana angefika’ angemweka mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” Mkristo mmoja-mmoja angewezaje kuwekwa juu ya kila kitu, yaani, juu ya mali “zote” za Bwana? Haiwezekani!

6. Taifa la Israeli lilikusudiwaje kuwa “mtumishi,” au “mtumwa” wa Mungu?

6 Hivyo, kauli pekee inayopatana na akili ni kwamba Yesu alikuwa akirejelea kikundi fulani cha Wakristo kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Je, inawezekana kwamba maneno hayo yanarejelea kikundi cha mtumwa? Ndiyo. Miaka elfu saba kabla ya Kristo, Yehova aliliita taifa zima la Israeli “mashahidi wangu” na “mtumishi wangu ambaye nimemchagua.” (Isaya 43:10) Kuanzia wakati Sheria ya Musa ilipotolewa mwaka wa 1513 K.W.K. hadi Pentekoste 33 W.K., kila Mwisraeli alikuwa mshiriki wa jamii hiyo ya mtumishi. Waisraeli wengi hawakushiriki moja kwa moja kusimamia mambo ya taifa au kuratibu mpango wa ulishaji wa kiroho wa taifa hilo. Yehova alitumia wafalme, waamuzi, makuhani, manabii na Walawi kufanya kazi hizo. Hata hivyo, taifa la Israeli lilipaswa kuwakilisha enzi kuu ya Yehova na kumsifu kati ya mataifa. Kila Mwisraeli alipaswa kuwa shahidi wa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 26:19; Isaya 43:21; Malaki 2:7; Waroma 3:1, 2.

“Mtumishi” Afukuzwa

7. Kwa nini taifa la kale la Israeli halikustahili kuwa “mtumishi” wa Mungu?

7 Kwa kuwa taifa la Israeli lilikuwa “mtumishi” wa Mungu karne nyingi zilizopita, je, taifa hilo ndilo pia lililokuwa mtumwa ambaye Yesu alizungumzia? La, kwa kuwa inasikitisha kwamba Israeli la kale liliacha kuwa taifa lenye uaminifu au lenye busara. Paulo anaeleza kwa ufupi hali hiyo anaponukuu maneno haya ya Yehova kwa taifa hilo: “Jina la Mungu linafanyiwa makufuru katikati ya mataifa kwa sababu yenu.” (Waroma 2:24) Naam, Israeli lilifikia kilele cha historia yake ndefu ya uasi kwa kumkataa Yesu, naye Yehova akalikataa.—Mathayo 21:42, 43.

8. “Mtumishi” aliwekwa rasmi lini kuchukua mahali pa Israeli, na chini ya hali gani?

8 Ingawa “mtumishi” huyo, yaani, Israeli, alikosa uaminifu, hiyo haikumaanisha kwamba waabudu waaminifu hawangepata tena chakula cha kiroho. Kwenye Pentekoste 33 W.K., siku 50 baada ya ufufuo wa Yesu, wanafunzi wake 120 hivi walimwagiwa roho takatifu wakiwa katika chumba cha juu huko Yerusalemu. Wakati huo taifa jipya lilizaliwa. Kwa kufaa, kuzaliwa huko kulitangazwa wakati washiriki wa taifa hilo walipoanza kuwatangazia kwa ujasiri wakaaji wa Yerusalemu “mambo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:11) Hivyo, taifa hilo jipya, taifa la kiroho, likawa “mtumishi” ambaye angetangaza utukufu wa Yehova kwa mataifa na kuandaa chakula kwa wakati unaofaa. (1 Petro 2:9) Kwa kufaa, taifa hilo lilikuja kuitwa “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16.

9. (a) Ni nani ambao hufanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Ni nani ‘watumishi wa nyumbani’?

9 Kila mshiriki wa “Israeli wa Mungu” ni Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa kwa roho takatifu na ana tumaini la kwenda mbinguni. Kwa hiyo, maneno “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hurejelea washiriki wote wa taifa hilo la kiroho lililotiwa mafuta ambao wameishi duniani kipindi chochote kile tangu mwaka wa 33 W.K. hadi leo, kama vile tu Mwisraeli yeyote aliyeishi kipindi chochote tangu mwaka wa 1513 K.W.K. hadi Pentekoste 33 W.K., alivyokuwa mshiriki wa jamii ya mtumishi kabla ya Ukristo. Hata hivyo, ni nani walio ‘watumishi wa nyumbani,’ ambao hupokea chakula cha kiroho chenye kujenga kutoka kwa mtumwa huyo? Katika karne ya kwanza W.K., kila Mkristo alikuwa na tumaini la kwenda mbinguni. Kwa hiyo, watumishi wa nyumbani walikuwa pia Wakristo watiwa-mafuta wakiwa mtu mmoja-mmoja bali si wakiwa kikundi. Wote, kutia ndani wale waliokuwa na madaraka kutanikoni, walihitaji chakula cha kiroho kutoka kwa mtumwa huyo.—1 Wakorintho 12:12, 19-27; Waebrania 5:11-13; 2 Petro 3:15, 16.

“Kila Mmoja Kazi Yake”

10, 11. Tunajuaje kwamba washiriki wote wa jamii ya mtumwa hawana mgawo uleule?

10 Ingawa “Israeli wa Mungu” ni jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambayo imepewa mgawo fulani, kila mshiriki pia ana madaraka ya kibinafsi. Yesu alifafanua jambo hilo waziwazi katika Marko 13:34. Alisema: “Ni kama mtu anayesafiri kwenda ng’ambo, ambaye aliacha nyumba yake na kuwapa mamlaka watumwa wake, kila mmoja kazi yake, na kumwamuru mtunza-mlango aendelee kukesha.” Kwa hiyo, kila mshiriki wa jamii ya mtumwa amepewa mgawo wa kuzidisha mali za Kristo duniani. Kila mshiriki wa jamii ya mtumwa hutimiza mgawo huo kulingana na hali na uwezo wake.—Mathayo 25:14, 15.

11 Isitoshe, mtume Petro aliwaambia hivi Wakristo watiwa-mafuta wa siku zake: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.” (1 Petro 4:10) Hivyo, watiwa-mafuta wana daraka la kuhudumiana kwa kutumia zawadi walizopewa na Mungu. Isitoshe, maneno ya Petro yanaonyesha kwamba Wakristo wote hawangekuwa na uwezo, madaraka, au mapendeleo yaleyale. Hata hivyo, kila mshiriki wa jamii ya mtumwa anaweza kusaidia kwa njia fulani ukuzi wa taifa hilo la kiroho. Jinsi gani?

12. Kila mshiriki wa jamii ya mtumwa, awe mwanamume au mwanamke, alisaidiaje ukuzi wa mtumwa huyo?

12 Kwanza, kila mmoja wao alikuwa na daraka la kuwa shahidi wa Yehova na kuhubiri habari njema ya Ufalme. (Isaya 43:10-12; Mathayo 24:14) Punde tu kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wote waaminifu, wanaume kwa wanawake, wawe walimu. Alisema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.

13. Watiwa-mafuta wote walifurahia pendeleo gani?

13 Wanafunzi wapya walipopatikana, walipaswa kufundishwa kwa makini kufuata mambo yote ambayo Kristo aliwaamuru wanafunzi wake. Baada ya muda, wale waliokubali kufundishwa walikuwa na sifa za kustahili kuwafundisha wengine. Chakula cha kiroho chenye kujenga kiliandaliwa kwa ajili ya wale ambao wangekuwa washiriki wa jamii ya mtumwa katika mataifa mengi. Wakristo wote, wanaume kwa wanawake, walishiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. (Matendo 2:17, 18) Kazi hiyo ingeendelea kuanzia wakati mtumwa huyo alipoanza kazi yake hadi mwisho wa mfumo huu wa mambo.

14. Ni nani tu waliokuwa na pendeleo la kufundisha kutanikoni, nao wanawake waaminifu waliotiwa mafuta walihisije kuhusu jambo hilo?

14 Watiwa-mafuta waliokuwa tu wamebatizwa walipata kuwa sehemu ya mtumwa huyo, na bila kujali walikuwa wamefundishwa na nani kwanza, waliendelea kupokea mafundisho kutoka kwa washiriki wa kutaniko wenye sifa za Kimaandiko zilizowastahilisha kutumikia wakiwa wanaume wazee. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:6-9) Hivyo, wanaume hao waliowekwa rasmi walikuwa na pendeleo la kusaidia ukuzi wa taifa hilo kwa njia ya kipekee. Wanawake Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta hawakuudhika kuona kwamba wanaume Wakristo tu ndio waliopewa mgawo wa kufundisha kutanikoni. (1 Wakorintho 14:34, 35) Badala yake, walifurahia manufaa iliyotokana na kazi ya bidii ya washiriki wanaume wa kutaniko, nao walishukuru kwa mapendeleo ambayo wanawake wangepata, kutia ndani kuwatangazia wengine habari za furaha. Leo, dada watiwa-mafuta huonyesha mtazamo huohuo wa unyenyekevu, hata kama wazee waliowekwa rasmi ni watiwa-mafuta au la.

15. Ni ipi iliyokuwa mojawapo ya vyanzo vikuu vya chakula cha kiroho katika karne ya kwanza, na ni nani walioongoza kukiandaa?

15 Chakula muhimu cha kiroho kilichoandaliwa katika karne ya kwanza kilitokana moja kwa moja na barua za mitume na wanafunzi wengine waliokuwa wakiongoza. Barua walizoandika—hasa zile zinazopatikana kati ya vile vitabu 27 vilivyoongozwa na roho ya Mungu, na ambavyo hufanyiza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo—zilisambazwa katika makutaniko na bila shaka wazee walizitumia kufundisha. Kwa njia hiyo, wawakilishi wa mtumwa mwaminifu waligawanya chakula cha kiroho chenye kujenga kwa Wakristo wanyoofu. Jamii ya mtumwa ya karne ya kwanza ilitimiza kwa uaminifu mgawo iliyopewa.

Yule “Mtumwa” Baada ya Miaka 1,900 Hivi

16, 17. Jamii ya mtumwa ilionyeshaje uaminifu katika kutimiza mgawo wake katika miaka iliyotangulia mwaka wa 1914?

16 Namna gani leo? Kuwapo kwa Yesu kulipoanza mwaka wa 1914, je, alipata kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta ambao walikuwa wakigawanya kwa uaminifu chakula kwa wakati unaofaa? Bila shaka. Kikundi hicho kingeweza kutambuliwa waziwazi kwa sababu ya matunda yake mazuri. (Mathayo 7:20) Tangu wakati huo, historia imethibitisha kwamba kikundi hicho ndicho kimekuwa kikigawanya chakula cha kiroho.

17 Wakati Yesu alipofika, watumishi wa nyumbani wapatao 5,000 walikuwa wakieneza kweli ya Biblia kwa bidii. Wafanyakazi walikuwa wachache, lakini mtumwa alibuni njia kadhaa za kueneza habari njema. (Mathayo 9:38) Kwa mfano, mipango ilifanywa ili vichwa vya mazungumzo ya Biblia vichapishwe katika magazeti-habari 2,000 hivi. Kwa njia hiyo, ukweli wa Neno la Mungu uliwafikia makumi ya maelfu ya wasomaji kwa wakati mmoja. Isitoshe, programu ya sinema na slaidi za rangi iliyochukua muda wa saa nane, ilitayarishwa. Kwa sababu ya mbinu hiyo ya kuhubiri, watu zaidi ya milioni tisa katika mabara matatu walitangaziwa ujumbe wa Biblia, kuanzia Uumbaji hadi mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Njia nyingine iliyotumiwa ni vichapo. Kwa mfano, mwaka wa 1914 nakala 50,000 za jarida hili zilichapishwa.

18. Yesu alimweka rasmi mtumwa juu ya mali zake zote wakati gani, na kwa nini?

18 Naam, Bwana alipowasili alimpata mtumwa wake mwaminifu akiwalisha kwa bidii watumishi wa nyumbani na pia kuhubiri habari njema. Sasa mtumwa huyo angepewa madaraka makubwa zaidi. Yesu alisema: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:47) Yesu alifanya hivyo mwaka wa 1919, baada ya mtumwa huyo kupitia kipindi cha ukaguzi. Hata hivyo, kwa nini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alipewa madaraka makubwa zaidi? Kwa sababu mali za Bwana zilikuwa zimeongezeka. Yesu alipewa utawala mwaka wa 1914.

19. Eleza jinsi mahitaji ya kiroho ya “umati mkubwa” yametimizwa.

19 Bwana aliyekuwa tu ametawazwa alimweka rasmi mtumwa wake mwaminifu juu ya mali zipi? Juu ya mali Zake zote za kiroho duniani. Kwa mfano, miaka 20 baada ya Kristo kutawazwa mwaka wa 1914, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ulitambulishwa. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Hawa hawakuwa washiriki watiwa-mafuta wa “Israeli wa Mungu,” lakini walikuwa wanaume na wanawake wanyoofu wenye tumaini la kuishi duniani, ambao walimpenda Yehova nao walitaka kumtumikia kama walivyofanya watiwa-mafuta. Kwa kweli, walimwambia hivi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Wakristo hao waliokuwa tu wamebatizwa na pia watumishi wa nyumbani waliotiwa mafuta, walikula chakula kilekile chenye kujenga kiroho, na tangu wakati huo jamii hizo mbili zimekuwa zikila pamoja kwenye meza hiyo ya kiroho. Washiriki wa “umati mkubwa” wamepata baraka iliyoje!

20. “Umati mkubwa” umetimiza daraka gani katika kuzidisha mali za Bwana?

20 Kwa furaha, washiriki wa “umati mkubwa” walijiunga na jamii ya mtumwa iliyotiwa mafuta wakiwa wahubiri wa habari njema. Kadiri walivyohubiri ndivyo mali za duniani za Bwana zilivyoongezeka, na hivyo kumwongezea “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” madaraka. Hesabu ya watu waliotaka kujifunza kweli ilipoongezeka, ilibidi viwanda vya uchapishaji vipanuliwe ili kutosheleza mahitaji ya vichapo vya Biblia. Ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova zilianzishwa katika nchi moja baada ya nyingine. Mishonari walitumwa kwenda “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Katika mwaka wa 1914, kulikuwa na wasifaji wa Mungu waliotiwa mafuta elfu tano hivi, lakini leo idadi hiyo imeongezeka hadi wasifaji zaidi ya milioni sita ambao wengi wao ni wa “umati mkubwa.” Naam, mali za Mfalme zimeongezeka sana tangu atawazwe mwaka wa 1914!

21. Tutazungumzia mifano gani miwili katika funzo letu linalofuata?

21 Yote hayo yanaonyesha kwamba mtumwa amekuwa “mwaminifu na mwenye busara.” Baada tu ya kuzungumza kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yesu alitoa mifano miwili inayokazia sifa hizo: mfano wa mabikira wenye busara na mabikira wapumbavu, na ule wa talanta. (Mathayo 25:1-30) Mifano hiyo inatuvutia sana! Mifano hiyo inamaanisha nini kwetu leo? Tutazungumzia swali hilo katika makala inayofuata.

Unaonaje?

• Ni nani wanaofanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”?

• Ni nani walio ‘watumishi wa nyumbani’?

• Mtumwa mwaminifu aliwekwa rasmi lini juu ya mali zote za Bwana, na kwa nini aliwekwa wakati huo?

• Ni nani ambao wamesaidia kuzidisha mali za Bwana katika miaka ya hivi majuzi, na jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Jamii ya mtumwa ya karne ya kwanza ilitimiza mgawo wake kwa uaminifu