Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwenye 2 Wakorintho 6:14, Paulo anarejelea nani anapotumia maneno “wasio waamini”?

Kwenye 2 Wakorintho 6:14 tunasoma “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” Tukitazama muktadha, ni wazi kwamba Paulo anazungumza kuhusu watu ambao si washiriki wa kutaniko la Kikristo. Maoni hayo yanaungwa mkono na mistari ya Biblia inayoonyesha jinsi Paulo anavyotumia maneno “asiye mwamini” au “wasio waamini.”

Kwa mfano, Paulo anawakemea vikali Wakristo kwa kwenda mahakamani “mbele ya wasio waamini.” (1 Wakorintho 6:6) Katika mstari huo, watu wasioamini ni mahakimu wanaofanya kazi katika mahakama za Korintho. Katika barua yake ya pili, Paulo anasema kwamba Shetani “amepofusha akili za wasioamini.” Macho ya watu hao wasioamini yamefunikwa kwa “utaji” yasione habari njema. Watu hao wasioamini hawajaonyesha kwamba wanataka kumtumikia Yehova, kwa kuwa Paulo alikuwa ameeleza hivi mapema: “Kunapokuwa na tendo la kugeuka kumwelekea Yehova, utaji huondolewa mbali.”—2 Wakorintho 3:16; 4:4.

Baadhi ya watu wasioamini wanahusika katika uvunjaji wa sheria au kuabudu sanamu. (2 Wakorintho 6:15, 16) Hata hivyo, si wote wanaowapinga watumishi wa Yehova. Baadhi yao wanapendezwa na ukweli. Wengi wana wenzi wa ndoa walio Wakristo nao wanakubali kukaa nao. (1 Wakorintho 7:12-14; 10:27; 14:22-25; 1 Petro 3:1, 2) Lakini Paulo anatumia tena na tena neno “asiyeamini” kurejelea watu ambao, kama ilivyoonyeshwa hapo juu, si sehemu ya kutaniko la Kikristo, ambalo limefanyizwa na watu ‘wanaomwamini Bwana.’—Matendo 2:41; 5:14; 8:12, 13.

Kanuni inayopatikana kwenye 2 Wakorintho 6:14 ni mwongozo wenye thamani kwa Wakristo katika hali zote za maisha, na mara nyingi imetajwa kuwa shauri la hekima kwa Wakristo wanaotafuta mwenzi wa ndoa. (Mathayo 19:4-6) Kwa hekima, Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa hatafuti mwenzi wa ndoa kati ya watu wasioamini, kwa kuwa maadili, miradi, na imani ya wasioamini ni tofauti kabisa na ya Wakristo wa kweli.

Hata hivyo, namna gani watu wanaojifunza Biblia na kushirikiana na kutaniko la Kikristo? Namna gani wale ambao ni wahubiri wasiobatizwa? Je, wao ni wasioamini? La. Watu ambao wamekubali ukweli wa habari njema na ambao wanafanya maendeleo hatua kwa hatua kuelekea ubatizo hawapaswi kuitwa wasioamini. (Waroma 10:10; 2 Wakorintho 4:13) Kabla ya kubatizwa, Kornelio aliitwa “mtu mwenye kuheshimu na kumwogopa Mungu.”—Matendo 10:2.

Hivyo basi, je, lingekuwa jambo la hekima kwa Mkristo aliyejiweka wakfu kuanzisha uchumba na kufunga ndoa na mtu ambaye amekubaliwa kuwa mhubiri asiyebatizwa, kwa kuwa, kusema kweli, shauri la Paulo katika 2 Wakorintho 6:14 haliwezi kutumiwa kumhusu mtu huyo? La, hilo si jambo la hekima. Kwa nini? Kwa sababu ya shauri la moja kwa moja ambalo Paulo alitoa kuhusiana na wajane Wakristo. Paulo aliandika: “Yeye yuko huru kuolewa na yeyote anayemtaka, katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Kupatana na shauri hilo, Wakristo waliojiweka wakfu wanahimizwa watafute wenzi wa ndoa kati ya wale tu walio “katika Bwana.”

Ni nini maana ya usemi “katika Bwana” na usemi unaohusiana na huo, “katika Kristo”? Paulo anazungumza kuhusu watu waliokuwa “katika Kristo” au “katika Bwana” kwenye Waroma 16:8-10 na Wakolosai 4:7. Ukisoma mistari hiyo, utaona kwamba watu hao ni ‘wafanyakazi wenzi,’ ‘waliokubaliwa,’ ‘ndugu wapendwa,’ ‘wahudumu waaminifu,’ na ‘watumwa wenzi.’

Mtu huwa ‘mtumwa katika Bwana’ wakati gani? Hiyo hutokea anapojikana na kufanya kwa hiari yale mtumwa anayopaswa kufanya. Yesu anaeleza: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24) Mtu huanza kumfuata Kristo na kujitiisha kikamili kwa mapenzi ya Mungu anapojiweka wakfu kwa Mungu. Baadaye, yeye hujitoa abatizwe na kuwa mhudumu aliyewekwa rasmi, anayekubalika machoni pa Yehova Mungu. * Hivyo basi, ‘kuoa au kuolewa katika Bwana’ humaanisha kufunga ndoa na mtu ambaye ameonyesha wazi kwamba yeye kwa kweli ni mwamini, “mtumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo” aliyejiweka wakfu.—Yakobo 1:1.

Mtu anayejifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na ambaye anafanya maendeleo ya kiroho anastahili kupongezwa. Hata hivyo, bado hajajiweka wakfu kwa Yehova na kujitoa katika utumishi na kujidhabihu. Bado yeye anaendelea kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. Anahitaji kukamilisha mabadiliko yanayohusika katika kujiweka wakfu na kuwa Mkristo aliyebatizwa kabla ya kufikiria mabadiliko mengine makubwa maishani, kama vile ndoa.

Je, lingekuwa jambo la hekima kwa Mkristo kuanza uchumba na mtu anayeonekana kuwa anafanya maendeleo katika funzo la Biblia—labda akiwa na nia ya kumngojea hadi abatizwe kabla ya kufunga ndoa naye? La. Nia ya mwanafunzi wa Biblia haingekuwa wazi ikiwa angejua kwamba Mkristo fulani aliyejiweka wakfu anataka kufunga ndoa naye na kwamba hatafanya hivyo mpaka abatizwe.

Kwa kawaida, mtu hubaki akiwa mhubiri asiyebatizwa kwa muda mfupi tu, hadi anapofanya maendeleo na kubatizwa. Kwa hiyo, shauri linalotolewa hapo juu la kuoa katika Bwana tu ni nzuri. Hata hivyo, namna gani kuanzisha uchumba na mtu ambaye amefikisha umri wa kufunga ndoa, amelelewa katika familia ya Kikristo, amekuwa mtendaji kutanikoni kwa miaka kadhaa, naye ni mhubiri asiyebatizwa? Ikiwa hali iko hivyo, ni nini kinachomzuia kujiweka wakfu kwa Yehova? Kwa nini anasitasita? Je, ana shaka? Ingawa yeye si mtu asiyeamini, haiwezi kusemwa kwamba yuko “katika Bwana.”

Shauri la Paulo kuhusu ndoa ni kwa manufaa yetu. (Isaya 48:17) Wakati wenzi wote wawili wanaochumbiana wanapojiweka wakfu kwa Yehova, wajibu wao kwa mmoja na mwingine katika ndoa una msingi imara wa kiroho. Wana kanuni na miradi ileile. Hilo huchangia sana kuwa na ndoa yenye furaha. Isitoshe, kwa ‘kuoa au kuolewa katika Bwana,’ mtu huonyesha ushikamanifu kwa Yehova, na hiyo huleta baraka za kudumu, kwa sababu ‘kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu.’—Zaburi 18:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kwa Wakristo watiwa-mafuta ambao Paulo aliandikia kwanza, kuwa “mtumwa wa Bwana” kulihusisha pia kutiwa kwao mafuta kwa roho takatifu wakiwa wana wa Mungu na ndugu za Kristo.

[Picha katika ukurasa wa 31]

‘Kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu’