Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Agizo la Yehova” Haliwezi Kushindwa

“Agizo la Yehova” Haliwezi Kushindwa

“Agizo la Yehova” Haliwezi Kushindwa

“Acheni nirejezee agizo la Yehova; yeye ameniambia: ‘Wewe ni mwanangu . . . Niombe, ili nikupe mataifa yawe urithi wako.’”—ZABURI 2:7, 8.

1. Kuna tofauti gani kati ya kusudi la Mungu na lile la mataifa?

YEHOVA MUNGU ana kusudi kwa wanadamu na dunia. Mataifa yana kusudi pia. Lakini makusudi hayo yanatofautiana kabisa. Tunapaswa kutarajia iwe hivyo, kwa kuwa Mungu anasema: “Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” Kusudi la Mungu litatimia hakika kwa kuwa anaendelea kusema: “Kama vile mvua inayonyesha hushuka, na theluji, kutoka mbinguni nayo hairudi mahali pale, mpaka kwa kweli iwe imeinywesha dunia na kuifanya izae na kuchipuka, na mbegu kweli iwe imepewa mpandaji na mkate kupewa anayekula, ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:9-11.

2, 3. Ni nini kinachoonyeshwa wazi katika zaburi ya pili, na ni maswali gani yanayotokea?

2 Zaburi ya pili inaonyesha wazi kwamba kusudi la Mungu kuhusu Mfalme wake wa Kimasihi litatimizwa. Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliyeitunga zaburi hiyo, aliongozwa na roho ya Mungu kutabiri kwamba kungekuwa na wakati muhimu ambapo mataifa yangekuwa na fujo. Watawala wao wangempinga Yehova Mungu na Mtiwa-Mafuta wake. Hata hivyo, mtunga-zaburi pia aliimba: “Acheni nirejezee agizo la Yehova; yeye ameniambia: ‘Wewe ni mwanangu . . . Niombe, ili nikupe mataifa yawe urithi wako.’”—Zaburi 2:7, 8.

3 “Agizo la Yehova” humaanisha nini kwa mataifa? Linawaathirije wanadamu kwa ujumla? Kwa kweli, matukio hayo yanamaanisha nini kwa wasomaji wa zaburi ya pili wanaomwogopa Mungu?

Mataifa Yana Fujo

4. Unawezaje kueleza kwa ufupi mambo makuu katika Zaburi 2:1, 2?

4 Akirejelea matendo ya mataifa na watawala wao, mtunga-zaburi aanza tungo yake kwa kuimba: “Kwa nini mataifa yamekuwa na fujo na vikundi vya mataifa vimeendelea kusema jambo la upuuzi? Wafalme wa dunia wanachukua msimamo wao nao maofisa wakuu wamejikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.”—Zaburi 2:1, 2. *

5, 6. Ni ‘jambo gani la upuuzi’ ambalo “vikundi vya mataifa vimeendelea kusema”?

5 Ni ‘jambo gani la upuuzi’ ambalo vikundi vya mataifa ‘vimeendelea kusema’? Badala ya kumkubali Mtiwa-Mafuta wa Mungu, yaani, Masihi au Kristo, mataifa ‘yameendelea kusema,’ au kutafakari juu ya kuendeleza mamlaka yao. Maneno hayo ya zaburi ya pili pia yalitimizwa katika karne ya kwanza W.K., wakati wenye mamlaka Waroma na Wayahudi waliposhirikiana kumuua Mfalme-Mteuliwa wa Mungu, Yesu Kristo. Hata hivyo, utimizo ulio mkuu ulianza 1914 wakati Yesu alipowekwa kuwa Mfalme wa kimbingu. Tangu wakati huo, hakuna serikali yoyote duniani ambayo imemtambua Mfalme wa Mungu aliyetawazwa.

6 Ni nini maana ya swali hili la mtunga-zaburi: ‘Kwa nini vikundi vya mataifa vimekuwa vikisema jambo la upuuzi’? Kusudi la vikundi hivyo ndilo la upuuzi; ni la ubatili na halitafanikiwa. Haviwezi kuleta amani na upatano duniani. Na bado, vinafikia kiwango cha kuupinga utawala wa Mungu. Kwa kweli, vimechukua msimamo wa pamoja wenye uhasama, navyo vimejikusanya pamoja kumpinga Aliye Juu Zaidi na Mtiwa-Mafuta wake. Huo ni upumbavu ulioje!

Mfalme wa Yehova Mwenye Ushindi

7. Wafuasi wa mapema wa Yesu walitumiaje Zaburi 2:1, 2 katika sala?

7 Wafuasi wa Yesu walitumia maneno ya Zaburi 2:1, 2 kumhusu. Walipoteswa kwa ajili ya imani yao, walisali hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu [Yehova], wewe Ndiye uliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo, na ambaye kupitia roho takatifu ulisema kwa kinywa cha babu yetu Daudi, mtumishi wako, ‘Kwa nini mataifa yakawa yenye fujo na vikundi vya watu vikatafakari juu ya mambo matupu? Wafalme wa dunia walichukua msimamo wao nao watawala wakajikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.’ Ijapokuwa hivyo, Herode [Antipasi] na pia Pontio Pilato pamoja na watu wa mataifa na pamoja na vikundi vya watu wa Israeli kwa kweli walikusanyika pamoja katika jiji hili dhidi ya mtumishi wako mtakatifu Yesu, ambaye ulimtia mafuta.” (Matendo 4:24-27; Luka 23:1-12) * Ndiyo, katika karne ya kwanza kulikuwa na njama dhidi ya Yesu, mtumishi wa Mungu aliyetiwa mafuta. Hata hivyo, zaburi hiyo ingetimizwa tena karne nyingi baadaye.

8. Zaburi 2:3 inahusuje mataifa ya siku hizi?

8 Waisraeli wa kale walipokuwa na mfalme wa kibinadamu, kama Daudi, mataifa na watawala wapagani walikusanyika pamoja dhidi ya Mungu na mtiwa-mafuta wake aliyetawazwa. Lakini namna gani wakati wetu? Mataifa ya siku hizi hayataki kutimiza matakwa ya Yehova na Masihi. Hivyo, yanaonyeshwa yakisema: “Na tuzikate pingu zao na kuzitupa kamba zao mbali nasi!” (Zaburi 2:3) Watawala na mataifa wangepinga vizuizi vyovyote vinavyowekwa na Mungu na Mtiwa-Mafuta wake. Bila shaka, jitihada zozote za kukata pingu hizo na kutupa kamba hizo hazitafanikiwa.

Yehova Anawadharau

9, 10. Kwa nini Yehova anayadharau mataifa?

9 Yehova hahangaishwi na jitihada zozote za watawala wa mataifa za kuanzisha tawala zao. Zaburi ya pili inaendelea kusema: “Yule anayeketi mbinguni atacheka; Yehova mwenyewe atawadharau.” (Zaburi 2:4) Mungu anaendelea tu kutimiza kusudi lake kana kwamba watawala hao si kitu. Anawacheka kwa ushupavu wao na kuwadharau. Acha wajigambe kuhusu yale wanayokusudia kufanya. Yehova atawafanyia dhihaka. Anawacheka kwa sababu ya upinzani wao ambao hautafanikiwa.

10 Kwingineko katika zaburi zake, Daudi anarejelea watu na mataifa maadui na kuimba: “Ee Yehova Mungu wa majeshi, ndiye Mungu wa Israeli. Uamke uyaelekezee mataifa yote fikira zako. Usiwape kibali wasaliti wowote wenye kuumiza. Wao wanaendelea kurudi wakati wa jioni; wanaendelea kubweka kama mbwa na kulizunguka jiji pande zote. Tazama! wanaropoka kwa kinywa chao; panga ziko midomoni mwao, kwa maana ni nani anayesikiliza? Lakini wewe mwenyewe, Ee Yehova, utawacheka; utayadharau mataifa yote.” (Zaburi 59:5-8) Yehova anacheka majivuno na mvurugo wa mataifa katika mwenendo wao wa upumbavu dhidi yake.

11. Ni nini kitakachotokea mataifa yatakapojaribu kupinga kusudi la Mungu?

11 Maneno ya Zaburi ya 2 huimarisha imani yetu kwamba Mungu anaweza kutatua tatizo lolote. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote yeye hutimiza mapenzi yake naye hawaachi kamwe watumishi wake washikamanifu. (Zaburi 94:14) Hivyo basi, ni nini kitakachotokea mataifa yatakapojaribu kupinga kusudi la Yehova? Kulingana na Zaburi hiyo, Mungu “atasema nao katika hasira yake,” kana kwamba kwa mngurumo mkubwa wa radi. Isitoshe, “katika ghadhabu yake,” kama katika mpigo mkubwa wa radi, “atawafadhaisha.”—Zaburi 2:5.

Mfalme wa Mungu Awekwa

12. Zaburi 2:6 inahusu kutawazwa gani?

12 Bila shaka, yale ambayo Yehova anaendelea kusema kupitia mtunga-zaburi yanayafadhaisha mataifa. Mungu anasema: “Mimi, naam, mimi nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” (Zaburi 2:6) Mlima Sayuni ulikuwa sehemu iliyoinuka huko Yerusalemu, ambako Daudi aliwekwa kuwa mfalme juu ya Israeli yote. Lakini Mfalme wa Kimasihi hataketi kwenye kiti cha ufalme katika jiji hilo au sehemu nyingine ya dunia. Kwa kweli, tayari Yehova amemweka Yesu Kristo kuwa Mfalme wake wa Kimasihi aliyechaguliwa kwenye Mlima Sayuni wa mbinguni.Ufunuo 14:1.

13. Yehova alifanya agano gani na mwanaye?

13 Sasa Mfalme wa Kimasihi anazungumza. Anasema: “Acheni nirejezee agizo la Yehova [ambaye amefanya agano na mwanaye kwa ajili ya Ufalme]; yeye [Yehova Mungu] ameniambia: ‘Wewe ni mwanangu; Mimi, leo, nimekuwa baba yako.’” (Zaburi 2:7) Kristo alirejezea agano la Ufalme alipowaambia mitume wake hivi: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.”—Luka 22:28, 29.

14. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yesu ana haki ya kuwa mfalme?

14 Kama ilivyotabiriwa katika Zaburi 2:7, Yehova alimtambulisha Yesu kuwa Mwanaye wakati wa ubatizo wake na alipomfufua na kumpa uhai wa roho. (Marko 1:9-11; Waroma 1:4; Waebrania 1:5; 5:5) Naam, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu ndiye Mfalme wa Ufalme wa mbinguni. (Yohana 3:16) Akiwa mzao wa Mfalme Daudi, yeye ana haki ya kuwa mfalme. (2 Samweli 7:4-17; Mathayo 1:6, 16) Kulingana na zaburi hii, Mungu anamwambia Mwanaye hivi: “Niombe, ili nikupe mataifa yawe urithi wako na miisho ya dunia iwe miliki yako mwenyewe.”—Zaburi 2:8.

15. Kwa nini Yesu anaomba apewe mataifa yawe urithi wake?

15 Mfalme huyo, yaani, Mwana wa Mungu mwenyewe, ana cheo cha pili kwa ukuu baada ya Yehova. Yesu ndiye mtu ambaye amekuwa mwaminifu, mshikamanifu, na mwenye kutegemeka kwa Yehova. Isitoshe, kwa kuwa Yesu ni Mzaliwa wa Kwanza wa Mungu, yeye ana haki ya urithi. Kwa kweli, Yesu Kristo “ndiye mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Wakolosai 1:15) Anachohitaji kufanya tu ni kuomba naye Mungu ‘anampa mataifa yawe urithi wake na miisho ya dunia iwe miliki yake mwenyewe.’ Yesu anatoa ombi hilo akiwa yule ambaye ‘anapendezwa na vitu vinavyohusiana na wana wa binadamu,’ na pia kwa sababu ya tamaa yake kubwa ya kufanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni kuelekea dunia na wanadamu.—Methali 8:30, 31.

Agizo la Yehova Dhidi ya Mataifa

16, 17. Kulingana na Zaburi 2:9, mataifa yatapatwa na nini?

16 Kwa kuwa zaburi ya pili inatimizwa sasa, wakati wa kuwapo kwa Yesu Kristo kusikoonekana, mataifa yatapatwa na nini? Hivi karibuni Mfalme huyo atatekeleza tangazo hili la Mungu: ‘Utayavunja mataifa kwa fimbo ya chuma ya enzi, utayavunja vipande-vipande, kama chombo cha mfinyanzi.’—Zaburi 2:9.

17 Fimbo za enzi za wafalme wa kale ziliwakilisha mamlaka ya kifalme. Baadhi ya fimbo hizo zilitengenezwa kwa chuma, kama ile inayotajwa katika zaburi hii. Hapa fimbo hiyo inatumiwa kwa njia ya mfano kuonyesha jinsi Kristo aliye Mfalme atakavyoyaharibu mataifa kwa urahisi. Chombo cha mfinyanzi cha udongo huvunjika-vunjika kabisa kinapopigwa kwa nguvu kwa kutumia fimbo ya chuma.

18, 19. Ili wapate kibali cha Mungu, wafalme wa dunia wanahitaji kufanya nini?

18 Je, ni lazima watawala wa mataifa wavunjwe-vunjwe hivyo? La, kwa kuwa mtunga-zaburi anawasihi kwa maneno haya: “Sasa, enyi wafalme, onyesheni ufahamu; kubalini kurekebishwa, enyi waamuzi wa dunia.” (Zaburi 2:10) Wafalme wanaombwa watii na waonyeshe ufahamu. Wanapaswa kufikiria jinsi mipango yao ilivyo ya ubatili, inapolinganishwa na yale ambayo Ufalme wa Mungu utafanya ili kuwanufaisha wanadamu.

19 Ili wapate kibali cha Mungu, wafalme wa dunia wanahitaji kubadili mwenendo wao. Wanahimizwa ‘wamtumikie Yehova kwa woga na washangilie kwa kutetemeka.’ (Zaburi 2:11) Matokeo yatakuwaje wakitenda hivyo? Badala ya kuwa katika fujo, wanaweza kufurahia matarajio ambayo Mfalme wa Kimasihi ameweka mbele yao. Inawabidi watawala wa dunia waache kiburi na majivuno wanayoonyesha katika utawala wao. Isitoshe, wanapaswa kubadilika bila kukawia na kuonyesha kwamba wanafahamu ukuu wa enzi ya Yehova usio na kifani na kwamba Mungu na Mfalme wake wa Kimasihi wana nguvu zisizoweza kupingwa.

“Mbusuni Mwana”

20, 21. Inamaanisha nini ‘kumbusu mwana’?

20 Sasa zaburi ya 2 inatoa mwaliko wenye rehema kwa watawala wa mataifa. Badala ya kujikusanya ili kumpinga, wanashauriwa: “Mbusuni mwana, ili Yeye [Yehova Mungu] asikasirike nanyi msiangamizwe kutoka njiani, kwa maana hasira yake huwaka kwa urahisi.” (Zaburi 2:12a) Watawala hao wanapaswa kumtii Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anapotoa agizo. Mungu alipomtawaza Mwanaye, watawala wa dunia walipaswa kuacha “kusema jambo la upuuzi.” Walipaswa kumkubali Mfalme huyo mara moja na kumtii kabisa.

21 Kwa nini ‘wambusu mwana’? Zaburi hiyo ilipotungwa, watu walibusiana kuonyesha urafiki na kuwakaribisha wageni wao nyumbani ambako wangewaonyesha ukarimu. Kubusiana pia kungeweza kuwa tendo la kuonyesha uaminifu. (1 Samweli 10:1) Katika mstari huo wa zaburi ya pili, Mungu anayaamuru mataifa yambusu, au yamkaribishe Mwanaye akiwa Mfalme mtiwa-mafuta.

22. Watawala wa mataifa wanapaswa kutii onyo gani?

22 Wale wanaokataa kutambua mamlaka ya Mfalme aliyechaguliwa na Mungu wanamtukana Yehova. Hawaitambui enzi kuu ya Yehova Mungu, na pia mamlaka yake, na uwezo wake wa kuwachagulia wanadamu Mfalme aliye bora zaidi. Watawala wa mataifa wanatambua kwamba hasira ya Mungu itawapata kwa ghafula, wanapojaribu kutekeleza mipango yao. “Hasira yake huwaka kwa urahisi” au kwa haraka, nayo haiwezi kuzuiliwa na yeyote. Watawala wa mataifa wanapaswa kukubali onyo hilo kwa shukrani na kulitii. Kufanya hivyo kunamaanisha uhai.

23. Watu mmoja-mmoja bado wana wakati wa kufanya nini?

23 Zaburi hii yenye kutokeza inamalizika hivi: “Wenye furaha ni wale wote wanaomkimbilia [Yehova].” (Zaburi 2:12b) Bado kuna wakati kwa watu mmoja-mmoja kupata usalama. Hata viongozi mmoja-mmoja, ambao wamekuwa wakiunga mkono mipango ya mataifa, wanaweza kufanya hivyo pia. Wanaweza kumkimbilia Yehova ambaye huandaa kimbilio chini ya utawala wake wa Ufalme. Lakini lazima wachukue hatua kabla Ufalme wa Kimasihi haujavunja-vunja mataifa yanayoupinga.

24. Tunawezaje kuishi maisha yenye furaha zaidi hata katika ulimwengu huu wenye taabu?

24 Tukijifunza Biblia kwa bidii na kufuata shauri lake maishani, tunaweza kuishi maisha yenye furaha zaidi hata sasa katika ulimwengu huu wenye taabu. Kufuata shauri la Biblia hufanya familia ziwe na uhusiano wenye furaha zaidi na kutokuwa na mahangaiko na wasiwasi unaokumba ulimwengu huu. Kufuata mwongozo wa Biblia hutupa uhakika kwamba tunampendeza Muumba. Hakuna mwingine ila Bwana Mwenye Enzi Kuu ambaye anaweza kutoa uhakikisho wa “uzima wa sasa na ule utakaokuja” baada ya kuwaondoa duniani wale wanaopinga yaliyo haki kwa kuukataa utawala wa Ufalme.—1 Timotheo 4:8.

25. Kwa kuwa “agizo la Yehova” haliwezi kushindwa, tunaweza kutarajia nini kitukie wakati wetu?

25 “Agizo la Yehova” haliwezi kushindwa. Akiwa Muumba wetu, Mungu anajua kilicho bora kwa wanadamu, naye atatimiza kusudi lake la kuwabariki wanadamu watiifu kwa kuwapa amani, uradhi, na usalama wa kudumu chini ya Ufalme wa Mwanaye mpendwa. Nabii Danieli aliandika hivi kuhusu wakati wetu: “Na katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Kwa kweli basi, huu ndio wakati muhimu zaidi wa ‘kumbusu Mwana’ na kumtumikia Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mwanzoni, Mfalme Daudi ndiye aliyekuwa “mtiwa-mafuta,” nao “wafalme wa dunia” walikuwa watawala Wafilisti waliojikusanya pamoja dhidi yake.

^ fu. 7 Maandishi mengine katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia yanaonyesha kwamba Yesu ndiye Mtiwa-Mafuta wa Mungu anayetajwa katika zaburi ya pili. Jambo hilo linakuwa wazi tunapolinganisha Zaburi 2:7 na Matendo 13:32, 33 na Waebrania 1:5; 5:5. Ona pia Zaburi 2:9 na Ufunuo 2:27.

Ungejibuje?

• Vikundi vya mataifa ‘vimeendelea kusema jambo gani la upuuzi’?

• Kwa nini Yehova anayadharau mataifa?

• Ni nini agizo la Mungu dhidi ya mataifa?

• Inamaanisha nini ‘kumbusu mwana’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Daudi aliimba kuhusu Mfalme wa Kimasihi mwenye ushindi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Watawala na watu wa Israeli walipanga njama dhidi ya Yesu Kristo

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kristo amewekwa kuwa Mfalme kwenye Mlima Sayuni wa mbinguni