Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako

Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako

Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako

“IKIWA mtu hajui anaelekea bandari ipi, tatizo lake huwa si upande ambao upepo unaelekea.” Maneno hayo ambayo yaelekea yalisemwa na mwanafalsafa Mroma wa karne ya kwanza, yanaonyesha ukweli ulio wazi kwamba ili maisha yawe na mwelekeo ni muhimu kujiwekea miradi.

Biblia ina mifano ya watu ambao walitambua umuhimu wa kujiwekea miradi. Kwa kufanya kazi kwa bidii kwa miaka 50 hivi, Noa ‘alijenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake.’ Naye nabii Musa “alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.” (Waebrania 11:7, 26) Yoshua, aliyechukua nafasi ya Musa, alipokea mradi kutoka kwa Mungu wa kuimiliki nchi ya Kanaani.—Kumbukumbu la Torati 3:21, 22, 28; Yoshua 12:7-24.

Bila shaka, katika karne ya kwanza W.K., miradi ya kiroho ya mtume Paulo ilichochewa sana na maneno ya Yesu kwamba “hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Kwa kutiwa moyo na njozi na ujumbe mbalimbali wa pekee kutoka kwa Bwana Yesu, kutia ndani mgawo wa ‘kupeleka jina la Yesu kwa mataifa,’ Paulo alitimiza sehemu muhimu katika kuanzisha makutaniko mengi ya Kikristo kuanzia Asia Ndogo mpaka Ulaya.—Matendo 9:15; Wakolosai 1:23.

Naam, sikuzote watumishi wa Yehova wamejiwekea miradi mizuri nao wameitimiza kwa utukufu wa Mungu. Leo tunawezaje kujiwekea miradi ya kiroho? Ni miradi gani tunayoweza kujitahidi kuifikia, na ni hatua gani tunazoweza kuchukua ili kuifikia?

Ni Muhimu Kuwa na Nia Nzuri

Tunaweza kujiwekea miradi katika karibu kila jambo tunalofanya maishani, nao ulimwengu huu pia una watu wanaotambua umuhimu wa kujiwekea miradi. Hata hivyo, miradi ya kiroho, ni tofauti na tamaa ya ulimwengu ya kujitakia makuu. Watu wengi katika ulimwengu wanapojiwekea miradi nia yao kuu huwa ni tamaa yenye pupa ya kupata mali, cheo, na uwezo. Bila shaka, haingekuwa vizuri kufuatia mradi ili kupata uwezo na umaarufu. Miradi ambayo humletea Yehova Mungu sifa inahusiana moja kwa moja na ibada yetu kwake na kutegemeza Ufalme. (Mathayo 6:33) Miradi kama hiyo hutokana na upendo wetu kwa Mungu na kwa wanadamu wenzetu nasi huiweka tukiwa na kusudi la ujitoaji-kimungu.—Mathayo 22:37-39; 1 Timotheo 4:7.

Nia yetu inapaswa kuwa nzuri tunapojiwekea na kufuatia miradi ya kiroho, iwe ni kuongeza mapendeleo yetu ya utumishi au kufanya maendeleo ya kibinafsi ya kiroho. Hata hivyo, nyakati nyingine tunashindwa kutimiza miradi tuliyoweka tukiwa na nia nzuri. Tunawezaje kujiwekea miradi na kufanya iwezekane hata zaidi kuitimiza?

Lazima Tuwe na Tamaa Kuu ya Kuifikia

Fikiria jinsi Yehova alivyotimiza kazi ya kuumba ulimwengu. Maneno, “ikawa jioni, ikawa asubuhi,” yanaonyesha kwamba Yehova ndiye aliamua urefu wa vipindi vya uumbaji. (Mwanzo 1:5, 8, 13, 19, 23, 31) Mwanzoni mwa kila kipindi cha uumbaji, alijua waziwazi mradi au kusudi lake kwa siku hiyo ya uumbaji. Naye Mungu akatimiza kusudi lake la kuumba vitu. (Ufunuo 4:11) ‘Nafsi ya Yehova mwenyewe ina tamaa, naye ataifanya,’ akasema mzee wa ukoo Ayubu. (Ayubu 23:13) Yehova alifurahi kama nini kuona “kila kitu alichokuwa amefanya” na kukitangaza kuwa “chema sana”!—Mwanzo 1:31.

Ili tutimize miradi yetu, sisi pia tunapaswa kuwa na tamaa kuu ya kuifikia. Ni nini kitakachotusaidia kukuza tamaa hiyo kuu? Hata wakati dunia ilipokuwa bila umbo, na ukiwa, Yehova angeweza kuona kimbele jinsi ambavyo ingekuwa baadaye—johari maridadi katika anga ambayo ingemletea heshima na utukufu. Vivyo hivyo, tamaa yetu ya kutimiza yale ambayo tumeazimia kufanya inaweza kukuzwa kwa kutafakari matokeo na manufaa ya kutimizwa kwa mradi huo. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na Tony, mwenye umri wa miaka 19. Hakusahau kamwe kile kilichomvutia alipotembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ulaya Magharibi. Tangu wakati huo na kuendelea, Tony alikuwa akifikiria swali hili: ‘Mtu huhisije anapoishi na kutumika mahali kama hapa?’ Tony hakuacha kamwe kufikiria uwezekano wa kutumika Betheli, naye aliendelea kujitahidi kufikia mradi huo. Alifurahi sana wakati miaka kadhaa baadaye ombi lake la kutumika kwenye ofisi ya tawi lilipokubaliwa.

Kushirikiana na wale ambao tayari wamefikia mradi fulani kunaweza pia kutuchochea tuwe na tamaa ya kuufikia. Jayson, mwenye umri wa miaka 30, hakufurahia kuhubiri alipokuwa tineja. Lakini baada ya kumaliza shule ya sekondari, alianza utumishi wa painia kwa bidii, hivyo akawa mhubiri wa wakati wote wa Ufalme. Ni nini kilichomsaidia Jayson kukuza tamaa ya kuwa painia? Anajibu: “Kuzungumza na kuhubiri pamoja na wale ambao wamefanya upainia kulinichochea sana.”

Kuiandika Miradi Yetu Kwaweza Kutusaidia

Yale tunayofikiria yanakuwa wazi tunapochagua maneno ili kuyaeleza. Sulemani aliona kwamba maneno yanayofaa yanaweza kuwa kama michokoo kwa kutoa mwongozo maishani. (Mhubiri 12:11) Maneno hayo yanapoandikwa, yanakazwa akilini na moyoni. Ni kwa sababu hiyo Yehova aliwaamuru wafalme wa Israeli wajiandikie nakala ya Sheria. (Kumbukumbu la Torati 17:18) Kwa hiyo, huenda tukataka kuandika miradi yetu na mbinu za kuifikia, na pia kuandika vizuizi tunavyotarajia kukabiliana navyo na jinsi ya kuvishinda. Pia linaweza kuwa jambo linalofaa kutambua habari tunazopaswa kujua, ustadi ambao tunahitaji kupata, na watu wanaoweza kutusaidia na kututegemeza.

Kujiwekea miradi ya kiroho kulimtuliza Geoffrey ambaye ni painia wa muda mrefu katika eneo la mbali katika nchi fulani ya Asia. Alipatwa na msiba, mke wake alipokufa kwa ghafula. Baada ya kufanya marekebisho ili kufaana na hali zake mpya, Geoffrey aliamua kujitoa kabisa katika utumishi wa painia kwa kujiwekea miradi. Baada ya kuandika mipango yake kwenye karatasi, kwa msaada wa sala alijiwekea mradi wa kuanzisha mafunzo matatu ya Biblia mwishoni mwa mwezi huo. Alikagua utendaji wake kila siku, na kuchunguza maendeleo yake baada ya kila siku kumi. Je, alifikia mradi wake? Ndiyo, kwa kuwa alianzisha mafunzo manne ya Biblia na jambo hilo likamletea furaha kubwa.

Jiwekee Miradi Midogo-Midogo Ili Kufikia Miradi ya Muda Mrefu

Huenda ikaonekana vigumu sana kufikia miradi fulani. Kuhusu Tony aliyetangulia kutajwa, kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova kulionekana kama ndoto. Ilikuwa hivyo kwa sababu alikuwa akijiendesha vibaya, naye alikuwa hata hajajiweka wakfu kwa Mungu. Lakini Tony aliamua kuambatanisha maisha yake na njia za Yehova, naye akajiwekea mradi wa kustahili kubatizwa. Baada ya kubatizwa, alijiwekea mradi wa kuwa painia-msaidizi na wa kawaida, na akaandika kwenye kalenda tarehe za kuanza upainia. Baada ya kufanya upainia kwa wakati fulani, hakuona kutumika kwenye ofisi ya tawi kuwa mradi usioweza kufikika.

Ni vizuri sisi pia kujiwekea miradi midogo-midogo ili kufikia miradi yetu ya muda mrefu. Miradi hiyo inaweza kutusaidia kujitahidi kufikia mradi wetu wa muda mrefu. Kuchunguza kwa ukawaida maendeleo yetu kuhusu jinsi tunavyotimiza miradi hiyo midogo-midogo kutatusaidia kukaza akili yetu kwenye mradi huo. Kusali kwa ukawaida kwa Yehova kuhusu mipango yetu kutatusaidia pia kuendelea kuifuatia. “Salini bila kuacha,” akahimiza mtume Paulo.—1 Wathesalonike 5:17.

Azimio na Bidii Zinahitajiwa

Licha ya kufikiria mipango yetu kwa makini na tamaa kubwa ya kuitimiza, bado kuna miradi tusiyoweza kuifikia. Yaelekea mwanafunzi Yohana Marko alikata tamaa sana wakati mtume Paulo alipokataa kwenda pamoja naye katika safari yake ya pili ya umishonari. (Matendo 15:37-40) Marko alijifunza jambo fulani kutokana na kukata tamaa huko naye akarekebisha mradi wake wa kuongeza utumishi wake. Ni wazi kwamba alijifunza jambo fulani. Baadaye, Marko alisifiwa na Paulo, naye alishirikiana kwa ukaribu na mtume Petro huko Babiloni. (2 Timotheo 4:11; 1 Petro 5:13) Labda pendeleo lake kuu zaidi lilikuwa kuandika masimulizi yaliyoongozwa na roho ya Mungu kuhusu maisha na huduma ya Yesu.

Katika kufuatia miradi ya kiroho, huenda sisi pia tukakabili vizuizi. Badala ya kukata tamaa, tunapaswa kuichunguza upya miradi yetu, na inapowezekana kubadili mipango. Vizuizi vinapotokea, tunahitaji kujitahidi kufanya maendeleo tukiwa na azimio na bidii. Mfalme Sulemani mwenye hekima anatuhakikishia hivi: “Mkabidhi Yehova mwenyewe kazi zako nayo mipango yako itafanywa imara.”—Methali 16:3.

Hata hivyo, nyakati nyingine hali zinafanya isiwezekane kufikia miradi fulani. Kwa mfano, huenda afya mbaya au madaraka ya kifamilia yakatuzuia kufikia miradi fulani. Na tusisahau kamwe kwamba thawabu yetu muhimu zaidi ni uzima wa milele, iwe mbinguni au katika Paradiso duniani. (Luka 23:43; Wafilipi 3:13, 14) Tunaipataje? “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 2:17) Ingawa huenda hali yetu ikatuzuia kufikia mradi fulani hususa, bado tunaweza ‘kumwogopa Mungu wa kweli na kushika amri zake.’ (Mhubiri 12:13) Miradi ya kiroho hutusaidia tuendelee kukaza akili katika kufanya mapenzi ya Mungu. Hivyo basi, na tuitumie kumtukuza Muumba wetu.

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

Miradi ya Kiroho Tunayoweza Kufikiria

○ Kusoma Biblia kila siku

○ Kusoma kila nakala ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

○ Kuboresha sala zetu

○ Kuonyesha matunda ya roho

○ Kujitahidi kuongeza utumishi

○ Kuwa wenye matokeo zaidi katika kuhubiri na kufundisha

○ Kukuza ustadi wa kuhubiri kwa njia ya simu, kwa njia isiyo rasmi, na katika maeneo ya biashara