Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Shauri Lenye Manufaa Zaidi

Kupata Shauri Lenye Manufaa Zaidi

Kupata Shauri Lenye Manufaa Zaidi

MAISHA yenye mafanikio hupendeza kwelikweli. Shauri lenye faida na tamaa yetu ya kutenda kulingana nalo ni mambo muhimu ili kuwa na maisha kama hayo katika ulimwengu huu wenye kutatanisha. Hata hivyo, sikuzote wanadamu hawajawa tayari kusikiliza shauri lenye kunufaisha. Wengi wamedai kwamba mwanadamu anapaswa kuishi jinsi anavyotaka. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba Shetani, mpinzani wa kwanza wa enzi kuu ya Mungu, aliwatolea wanadamu wa kwanza uhuru. Andiko la Mwanzo 3:5 linataja dai lake kwa Hawa: “Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda [ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya] macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”

Je, baadaye Adamu na Hawa walifanikiwa kuishi bila kupatwa na matokeo mabaya, wakifuata tu maoni yao? La. Walikatishwa tamaa papo hapo na matokeo ya kufikiri kwamba walijua kutofautisha mema na mabaya. Kwa haki, Mungu aliwakataa, nao wakaanza maisha magumu chini ya hali ya kutokamilika, na matokeo ya mwisho yakawa kifo. (Mwanzo 3:16-19, 23) Sote tunakufa. Biblia inasema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Hata ingawa uchaguzi wa Adamu na Hawa ulikuwa na matokeo mabaya, bado wengi hawasadiki kwamba ni jambo la hekima kutumia shauri kutoka kwa Mfanyi wa binadamu. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba ‘imeongozwa na roho ya Mungu nayo ni yenye faida,’ na inaweza kutusaidia kuwa ‘watu wa Mungu wenye uwezo kamili, tukiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17) Bila shaka, tutakuwa wenye furaha zaidi tukifuata shauri la Biblia. Hilo hutumika zaidi katika maisha ya familia.

Uaminifu Katika Ndoa

Kulingana na Biblia, Mungu alikusudia ndoa iwe yenye kudumu. (Mwanzo 2:22-24; Mathayo 19:6) Isitoshe, Maandiko yanasema kwamba ‘kitanda cha ndoa kinapaswa kuwa bila unajisi,’ kumaanisha kwamba muungano huo haupaswi kuchafuliwa na uhusiano wa kingono nje ya ndoa. (Waebrania 13:4) Hata hivyo, yaelekea unajua kwamba leo ndoa nyingi hazitimizi takwa hilo. Watu fulani wana mazoea ya kuwachezea kimapenzi watu ambao si wenzi wao wa ndoa wanapokuwa kazini. Wengine hudanganya familia zao ili wawe na wakati wa kutumia pamoja na wapenzi wao wa pembeni. Wengine hata huwaacha wenzi wao wa ndoa ili kuishi na mtu mwingine mwenye umri mdogo, wakisema kwamba kwa kufanya hivyo wanahisi kuwa wenye umri mdogo zaidi na wenye furaha zaidi, kama ilivyotukia katika kisa cha Verónica, aliyetajwa katika makala iliyotangulia.

Hata hivyo, kuazimia kujifurahisha bila kujali matokeo hakutatokeza furaha yenye kudumu. Yaliyompata Ronald yanathibitisha jambo hilo. Akiwa na hakika kwamba angeboresha maisha yake, alimwacha mke wake ili kuanzisha familia mpya pamoja na mwanamke aliyekuwa mpenzi wake wa pembeni kwa miaka sita, na ambaye tayari alikuwa amezaa naye watoto wawili. Lakini muda mfupi baada ya kuvunja ndoa yake, mpenzi wake alimwacha! Mwishowe, Ronald alienda kuishi na wazazi wake. Alieleza hali yake kuwa yenye “kuaibisha.” Huo ni mfano mmoja tu. Tabia hiyo inayochochewa na tamaa za ubinafsi imefanya talaka na kuvunjika kwa familia kuongezeke sana, jambo linalosababisha mateso kwa watu wengi—watoto na vilevile watu wazima.

Kwa upande mwingine, kufuata shauri la Biblia huleta furaha ya kweli. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Roberto anayesema: “Shauri la Biblia lilinisaidia, nami sikupoteza mke wangu. Hatupati furaha ya kweli kwa kushawishiwa kuwa na uhusiano na mtu ambaye si mwenzi wetu wa ndoa, hata kama mtu huyo anaonekana kuwa mwenye kuvutia. Elimu ya Biblia imenisaidia kumthamini mwenzi wangu, ambaye nimeishi naye kwa miaka mingi.” Shauri la Biblia “yeyote asimtendee kwa hila mke wa ujana wake” lilimsaidia sana Roberto. (Malaki 2:15) Tunaweza kunufaika na shauri la Mungu katika hali gani nyingine?

Kulea Watoto Wetu

Miaka 40 hivi iliyopita watu wengi walipendezwa na lile wazo la kwamba wazazi hawapaswi kuwawekea watoto wao vizuizi vingi wanapowalea. Lilionekana kuwa jambo la akili kuwaachilia watoto wafanye maamuzi yao wenyewe kuhusu jinsi ya kufikiri na jinsi ya kujiendesha. Lengo lilikuwa kuepuka kuzuia ukuzi wao. Katika sehemu fulani, hata walianzisha mifumo ya elimu ambayo haikuwa na mpangilio maalumu, na kati ya mambo mengine, wanafunzi wangeweza kuamua kama wangehudhuria masomo au la, na pia wangeweza kuamua muda ambao wangetumia katika tafrija au kujifunza. Shule moja kama hiyo ilikuwa na sera ya “kuwaruhusu watoto waonyeshe hisia zao zote bila kushutumiwa au kuingiliwa na mtu mzima.” Leo, watu fulani ambao hutoa mashauri kuhusu tabia ya wanadamu bado hudai kwamba aina fulani za nidhamu hazina manufaa, hata katika hali ambapo wazazi wanaona ni lazima kutoa nidhamu yenye upendo.

Matokeo yamekuwaje? Kuna watu wengi ambao wanaamini kwamba njia za kuwalea watoto kwa kuwaendekeza huwafanya wawe na uhuru mwingi sana. Wanahisi kwamba jambo hilo limechangia ongezeko kubwa la uhalifu na matumizi ya dawa za kulevya. Uchunguzi mmoja huko Marekani ulionyesha kwamba asilimia 70 hivi ya watu waliohojiwa walifikiri kwamba watoto na vijana hawapewi mwongozo wa wazazi ambao wanahitaji. Wanapojaribu kueleza sababu inayofanya matineja wafyatue risasi shuleni na kufanya uhalifu mwingine mbaya, wengi huwalaumu “wazazi kwa kuwa waendekevu.” Na hata kama hali haitakuwa mbaya hivyo, wazazi na watoto watapatwa na matokeo mabaya ya kuwalea watoto vibaya.

Biblia inasema nini kuhusu habari hiyo? Biblia inawashauri wazazi watumie mamlaka yao kwa upendo na pia kwa uthabiti. Biblia inasema: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana; fimbo ya nidhamu ndiyo itakayouondolea mbali.” (Methali 22:15) Bila shaka, nidhamu yote inayotolewa na wazazi inapaswa kupatana na hali. Nidhamu inapaswa kutolewa kwa upole, kwa kujizuia, na kwa ufikirio. Inapotolewa hivyo, nidhamu inakuwa ishara ya upendo. Mamlaka ya wazazi inapotumiwa kwa njia ya upendo, wala si kwa ukali, kunakuwa na uwezekano mkubwa wa kufanikiwa.

Kumekuwa na matokeo mazuri ya kufuata shauri hilo. Arturo, mwanamume mwenye umri wa miaka 30 anayeishi Mexico na ambaye alioa hivi karibuni, anasema: “Baba aliniambia mimi pamoja na ndugu zangu waziwazi kwamba yeye na mama ndio wenye mamlaka katika familia. Hawakusita kututia nidhamu. Hata hivyo, sikuzote walitafuta nafasi ya kuzungumza nasi. Sasa nikiwa mtu mzima, ninathamini maisha yangu matulivu, na ninajua kwamba maisha yangu yamekuwa hivyo hasa kwa sababu ya mwongozo mzuri niliopata.”

Tumia Shauri Lenye Manufaa Zaidi

Neno la Mungu, Biblia, lina shauri lenye manufaa zaidi kwa wanadamu. Mwongozo wake hauhusu tu familia. Husaidia kutuandaa katika njia nyingi kwa sababu hutufundisha jinsi ya kutenda katika ulimwengu ambapo wengi hawataki kukubali kwamba ili wanufaike, wanapaswa kuongozwa na Chanzo bora cha hekima.

Yehova Mungu, Muumba wa wanadamu alitoa uhakikisho huu kupitia mtunga-zaburi Daudi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zaburi 32:8) Je, unaweza kuwazia Muumba akitutazama ili kutulinda tusipatwe na hatari? Hata hivyo, sote tunapaswa kujiuliza swali hili: ‘Je, nitakubali kwa unyenyekevu mwongozo wa Yehova wenye ulinzi?’ Neno lake hutuambia hivi kwa upendo: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

Kumjua Yehova hutaka jitihada na kujitoa, nao wanadamu wanaweza kumjua kupitia Biblia. Njia ya maisha ambayo Yehova anapendekeza ‘ina ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.’ Kwa kweli, hiyo ni njia ya kupata faida kubwa tunapozingatia manufaa nyingi tunazopata kwa kufanya hivyo.—1 Timotheo 4:8; 6:6.

Ikiwa unavutiwa na ufahamu wa Biblia na baraka zinazotokana na kuishi kupatana na ufahamu huo, fanya kusoma na kutafakari Neno la Mungu kuwe jambo kuu maishani mwako. Kufanya hivyo, kutakusaidia ufanikiwe kukabili magumu ya sasa na yoyote ya wakati ujao. Isitoshe, utajifunza kuhusu tumaini la kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, ambapo wote watafunzwa na Yehova nao watakuwa na amani nyingi.—Isaya 54:13.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Shauri la Biblia linaweza kuimarisha ndoa

[Picha katika ukurasa wa 6]

Shauri la Biblia ndio msingi wa mwongozo bora, hata hivyo halituzuii kujifurahisha

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wale wanaofuata shauri la Biblia wanaweza kufurahia maisha yenye usawaziko