Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kumbukumbu la Torati

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kumbukumbu la Torati

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kumbukumbu la Torati

NI MWAKA wa 1473 K.W.K. Miaka 40 imepita tangu Yehova awakomboe wana wa Israeli kutoka utumwani Misri. Baada ya kutanga-tanga nyikani kwa miaka hiyo yote, Waisraeli bado ni taifa lisilo na nchi. Hata hivyo, mwishowe wako karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi. Ni nini kitakachowapata wanapoimiliki nchi hiyo? Watapata matatizo gani, nao wanapaswa kuyatatuaje?

Kabla ya Waisraeli kuvuka Mto Yordani na kuingia Kanaani, Musa anawatayarisha kwa ajili ya kazi kubwa iliyo mbele yao. Jinsi gani? Kwa kutoa mfululizo wa hotuba ambazo zinawatia moyo, kuwahimiza, na kuwaonya. Anawakumbusha Waisraeli kwamba wanapaswa kujitoa kikamili kwa Yehova Mungu, na kwamba hawapaswi kuiga mataifa yanayowazunguka. Hotuba hizo ndizo zinazofanyiza sehemu kubwa ya kitabu cha Kumbukumbu la Torati. Leo sisi tunahitaji mashauri yanayotolewa katika hotuba hizo, kwa kuwa sisi pia tunaishi katika ulimwengu ambapo si rahisi kujitoa kikamili kwa Yehova.—Waebrania 4:12.

Musa aliandika kitabu chote cha Kumbukumbu la Torati isipokuwa sura ya mwisho, nacho kinazungumzia kipindi cha miezi zaidi ya miwili hivi. * (Kumbukumbu la Torati 1:3; Yoshua 4:19) Acheni tuone jinsi mambo yaliyoandikwa humo yanavyoweza kutusaidia kumpenda Yehova Mungu kwa moyo wetu wote na kumtumikia kwa uaminifu.

“USISAHAU MAMBO AMBAYO MACHO YAKO YAMEONA”

(Kumbukumbu la Torati 1:1–4:49)

Katika hotuba ya kwanza, Musa anasimulia baadhi ya mambo yaliyotokea nyikani—hasa yale ambayo yatawasaidia Waisraeli wanapojitayarisha kuimiliki Nchi ya Ahadi. Lazima masimulizi kuhusu kuwekwa kwa waamuzi yawe yaliwakumbusha kwamba Yehova huwapanga watu wake katika njia inayohakikisha kwamba wanatunzwa kwa upendo. Musa pia anasimulia kwamba ile ripoti mbaya ya wapelelezi kumi ilifanya vizazi vilivyofuata visiingie katika nchi waliyoahidiwa. Wazia jinsi wasikilizaji wa Musa walivyoguswa moyo na mfano huo wa kuonya huku nchi waliyoahidiwa ikiwa mbele ya macho yao.

Bila shaka, kukumbuka ushindi mbalimbali ambao Yehova aliwapa Waisraeli kabla ya kuvuka Yordani kuliwachochea wawe na ujasiri, kwa kuwa walikuwa tayari kuanza kuteka nchi iliyokuwa ng’ambo ya mto. Nchi ambayo walikuwa karibu kuimiliki ilijaa ibada ya sanamu. Ilifaa sana Musa awaonye kuhusu ibada hiyo.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:4-6, 9, 19, 24, 31-35; 3:1-6—Kwa nini Waisraeli waliwaangamiza baadhi ya watu walioishi mashariki ya Yordani na kuwaacha wengine? Yehova aliwaamuru Waisraeli wasipigane na wana wa Esau. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa wazao wa ndugu ya Yakobo. Waisraeli hawakupaswa kuwatendea vibaya au kupigana na Wamoabi na Waamoni, kwa kuwa walikuwa wazao wa Loti, mpwa wa Abrahamu. Hata hivyo, Wafalme Waamori, Sihoni na Ogu, hawakuwa na haki kama hizi kuhusiana na nchi waliyomiliki kwa kuwa hawakutokana na ukoo wa Israeli. Hivyo, Sihoni alipokataa kuwaruhusu Waisraeli kupita katika nchi yake naye Ogu akaja kupigana nao, Yehova aliwaamuru Waisraeli waharibu majiji yao na kuwaua watu wote.

4:15-20, 23, 24—Je, katazo la kutengeneza sanamu za kuchongwa lilimaanisha kwamba ni kosa kufanya mifano ya vitu kwa ajili ya mapambo? La. Katazo hili lilihusu kufanya sanamu ili kuziabudu, yaani, ‘kuziinamia na kuzitumikia.’ Biblia haikatazi kuchonga sanamu au kuchora picha kwa ajili ya mapambo.—1 Wafalme 7:18, 25.

Mambo Tunayojifunza:

1:2, 19. Wana wa Israeli walitanga-tanga nyikani kwa miaka 38 hivi, hata ingawa mji wa Kadesh-barnea ulikuwa tu “mwendo wa siku kumi na moja kutoka Horebu [eneo lenye milima karibu na Mlima Sinai ambapo zile Amri Kumi zilitolewa] kupitia njia ya Mlima Seiri.” Walipatwa na msiba ulioje kwa kutomtii Yehova Mungu!—Hesabu 14:26-34.

1:16, 17. Leo Mungu anatumia viwango vilevile vya hukumu. Waliopewa jukumu la kutumika katika halmashauri ya hukumu hawapaswi kuruhusu upendeleo au kumwogopa mwanadamu kupotoe maamuzi yao.

4:9. Ili Waisraeli wafanikiwe ilikuwa muhimu ‘kutosahau mambo ambayo macho yao yalikuwa yameona.’ Ulimwengu mpya ulioahidiwa unapokaribia, pia ni muhimu sisi tukazie fikira matendo mazuri ya Yehova kwa kuwa wanafunzi wenye bidii wa Neno lake.

MPENDE YEHOVA, NA KUTII AMRI ZAKE

(Kumbukumbu la Torati 5:1–26:19)

Katika hotuba yake ya pili, Musa anazungumzia kutolewa kwa Sheria kwenye Mlima Sinai, naye anazitaja tena zile Amri Kumi. Mataifa saba yametajwa waziwazi kwamba yataharibiwa kabisa. Wana wa Waisraeli wanakumbushwa jambo fulani muhimu walilojifunza nyikani: “Mwanadamu haishi kwa mkate tu bali mwanadamu huishi kwa kila neno la kinywa cha Yehova.” Katika hali yao mpya, lazima ‘washike amri yote.’—Kumbukumbu la Torati 8:3; 11:8.

Wanapoingia katika nchi waliyoahidiwa, Waisraeli watahitaji sheria kuhusu ibada, hukumu, utawala, vita, na pia kuhusu maisha yao ya faraghani na ya kijamii. Musa anapitia sheria hizo na kukazia kwamba wanahitaji kumpenda Yehova na kutii sheria zake.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

8:3, 4—Ni katika njia gani nguo za Waisraeli hazikuchakaa wala miguu yao kuvimba katika safari yao nyikani? Huo ulikuwa uandalizi wa kimuujiza, sawa na ule uandalizi wa ukawaida wa mana. Waisraeli walitumia mavazi yaleyale na viatu vilevile walivyokuwa navyo kabla ya kuanza kutanga-tanga nyikani. Yaelekea watoto walipokua, nao watu wazima kufa, vitu hivyo vilipitishwa kwa wengine. Kwa kuwa kule kuhesabiwa mara mbili mwanzoni na mwishoni mwa safari ya nyikani kulionyesha kwamba idadi ya Waisraeli haikuongezeka, nguo na viatu walivyokuwa navyo mwanzoni vingetosha.—Hesabu 2:32; 26:51.

14:21—Kwa nini Waisraeli wangeweza kumpa mkaaji mgeni au kumuuzia mgeni mnyama mfu ambaye hajatolewa damu na ambaye wao wenyewe hawangeweza kumla? Katika Biblia, maneno “mkaaji mgeni” yangeweza kurejelea mtu asiye Mwisraeli ambaye aligeuza imani, au mkaaji aliyefuata sheria za msingi za nchi lakini asiye mwabudu wa Yehova. Wageni na wakaaji wageni ambao hawakugeuza imani hawakuwa chini ya Sheria na wangeweza kutumia kwa njia mbalimbali wanyama wafu ambao hawajatolewa damu. Waisraeli waliruhusiwa kuwapa au kuwauzia wanyama hao. Kwa upande mwingine, mtu aliyegeuzwa imani alipaswa kufuata Sheria ya agano. Kama inavyoonyeshwa kwenye Mambo ya Walawi 17:10, mtu kama huyo alikatazwa kula damu ya mnyama.

24:6—Kwa nini kutwaa “kuwa rehani jiwe la kusagia la mkononi au jiwe lake la juu la kusagia” kulilinganishwa na kutwaa “nafsi”? Jiwe la kusagia la mkononi au jiwe lake la juu la kusagia liliwakilisha “nafsi” ya mtu au riziki yake. Kutwaa mojawapo ya mawe hayo kungefanya familia nzima ikose mkate wao wa kila siku.

25:9—Ni nini maana ya kumvua kiatu na kumtemea mate usoni mwanamume aliyekataa kufanya ndoa ya ndugu-mkwe? Kulingana na “desturi ya nyakati za zamani katika Israeli kuhusu haki ya kukomboa . . . mwanamume alipaswa kuvua kiatu chake na kumpa mwenzake.” (Ruthu 4:7) Kwa hiyo kuvua kiatu cha mwanamume aliyekataa kufanya ndoa ya ndugu-mkwe kulithibitisha kwamba alikuwa amekataa cheo na haki yake ya kumzalia mrithi ndugu yake aliyekufa. Hilo lilikuwa jambo la aibu. (Kumbukumbu la Torati 25:10) Lilikuwa tendo la kufedhehesha kumtemea mate usoni.—Hesabu 12:14.

Mambo Tunayojifunza:

6:6-9. Kama vile Waisraeli walivyoamriwa waijue Sheria, sisi pia tunapaswa kujua amri za Mungu, kuzikumbuka nyakati zote, na kuzikazia kwa watoto wetu. Tunapaswa ‘kuzifunga kama ishara kwenye mkono wetu’ katika maana ya kwamba matendo yetu—yanayowakilishwa na mikono yetu—yanapaswa kuonyesha kwamba tunamtii Yehova. Na kama “utepe wa kipaji katikati ya macho,” utii wetu unapaswa kuonekana na wote.

6:16. Na tusimjaribu Yehova kamwe kama vile Waisraeli walivyofanya kwa kukosa imani huko Masa, ambako walilalamika kuhusu ukosefu wa maji.—Kutoka 17:1-7.

8:11-18. Kufuatia vitu vya kimwili kunaweza kutufanya tumsahau Yehova.

9:4-6. Tunapaswa kujihadhari dhidi ya kujiona kuwa waadilifu.

13:6. Hatupaswi kumruhusu yeyote atukengeushe tuache kumwabudu Yehova.

14:1. Kujikatakata mwili kunapaswa kuepukwa kabisa kwa kuwa kufanya hivyo huonyesha kwamba mtu haheshimu mwili wake na huenda kukahusianishwa na ibada ya uwongo. (1 Wafalme 18:25-28) Tumaini letu katika ufufuo hufanya isifae kuombolezea wafu kwa njia kama hiyo inayopita kiasi.

20:5-7; 24:5. Tunapaswa kuwafikiria watu walio katika hali za kipekee, hata kama kuna kazi muhimu ya kufanya.

22:23-27. Mwanamke anapotishwa kulalwa kinguvu, kupiga mayowe ni njia moja ya kujikinga yenye matokeo sana.

“LAZIMA UCHAGUE UZIMA”

(Kumbukumbu la Torati 27:1–34:12)

Katika hotuba yake ya tatu, Musa anasema kwamba baada ya kuvuka Yordani, Waisraeli wanapaswa kuiandika Sheria kwenye mawe makubwa na pia kutangaza laana kwa wasiotii na baraka kwa wanaotii. Hotuba ya nne inaanza kwa kufanya upya agano kati ya Yehova na Waisraeli. Musa anawaonya watu tena juu ya kutotii na kuwahimiza ‘wachague uzima.’—Kumbukumbu la Torati 30:19.

Mbali na hotuba hizo nne, Musa anazungumzia badiliko la uongozi, anawafunza Waisraeli wimbo mzuri unaomsifu Yehova, na kuwaonya kuhusu ole watakazopata kwa kukosa uaminifu. Baada ya kuyabariki makabila, Musa anakufa na kuzikwa akiwa na umri wa miaka 120. Kunakuwa na maombolezo ya siku 30, ambayo ni karibu nusu ya wakati ambao mambo yanayotajwa katika Kumbukumbu la Torati yalitukia.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

32:13, 14—Kwa kuwa Waisraeli walikatazwa kula mafuta yoyote, kula “mafuta ya kondoo-dume” kunamaanisha nini? Usemi huo unatumiwa hapa kwa njia ya mfano na unaonyesha wanyama bora zaidi kundini. Usemi huo unatumiwa kwa njia hiyo kwa sababu mstari huohuo unataja “mafuta ya figo ya ngano” na “damu ya zabibu.”

33:1-29—Kwa nini Simeoni hakutajwa moja kwa moja wakati Musa alipowabariki wana wa Israeli? Hiyo ni kwa sababu Simeoni na Lawi walitenda kwa “ukali,” na hasira yao ilikuwa “katili.” (Mwanzo 34:13-31; 49:5-7) Urithi wao haukuwa sawa kabisa na urithi wa makabila mengine. Lawi alipata majiji 48, nayo sehemu ya Simeoni ilikuwa ndani ya eneo la Yuda. (Yoshua 19:9; 21:41, 42) Hivyo, Musa hakumbariki Simeoni moja kwa moja. Hata hivyo, Simeoni alibarikiwa pamoja na Waisraeli wengine kwa ujumla.

Mambo Tunayojifunza:

31:12. Watoto wanapaswa kuketi pamoja na watu wazima kwenye mikutano ya kutaniko na kujitahidi kusikiliza na kujifunza.

32:4. Utendaji wote wa Yehova ni mkamilifu kwa sababu yeye huonyesha sifa zake za haki, hekima, upendo, na nguvu kwa njia yenye usawaziko kabisa.

Kina Thamani Kubwa Sana Kwetu

Kitabu cha Kumbukumbu la Torati humwonyesha Yehova kuwa “Yehova mmoja.” (Kumbukumbu la Torati 6:4) Ni kitabu kuhusu watu waliokuwa na uhusiano wa kipekee na Mungu. Pia huonya kuhusu ibada ya sanamu na kukazia kwamba tunahitaji kujitoa kikamili kwa Mungu.

Kwa kweli, kitabu cha Kumbukumbu la Torati kina thamani kubwa sana kwetu! Ingawa hatuko chini ya Sheria, tunaweza kujifunza mambo mengi katika kitabu hicho yatakayotusaidia ‘kumpenda Yehova Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi yote, na nguvu zetu zote.’—Kumbukumbu la Torati 6:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Huenda sura ya mwisho inayozungumzia kifo cha Musa iliongezwa na Yoshua au Kuhani Mkuu Eleazari.

[Ramani katika ukurasa wa 24]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

SEIRI

Kadesh-barnea

Ml. Sinai (Horebu)

Bahari Nyekundu

[Hisani]

Based on maps copyrighted by Pictorial Archive (Near Eastern History) Est. and Survey of Israel

[Picha katika ukurasa wa 24]

Hotuba za Musa zimefanyiza sehemu iliyo kubwa zaidi ya kitabu cha Kumbukumbu la Torati

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tunajifunza nini kutokana na uandalizi wa Yehova wa mana?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kutwaa jiwe la kusagia la mkononi au jiwe lake la juu la kusagia kulilinganishwa na kutwaa “nafsi”