Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka kwa Alejandra

Barua Kutoka kwa Alejandra

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

Barua Kutoka kwa Alejandra

KWA muda mrefu kuandika barua kumekuwa njia yenye matokeo sana ya kutoa ushahidi. Ingawa huenda nyakati nyingine tusijue matokeo yatakuwaje, wale wanaoendelea kutumia njia hiyo wamebarikiwa sana. Wao hukumbuka shauri hili la Biblia lenye hekima: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa, hapa au pale, au ikiwa zote mbili zitakuwa njema.”—Mhubiri 11:6.

Alejandra, Shahidi kijana ambaye alikuwa akitumika kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico kwa miaka kumi hivi, alikuwa anatibiwa ugonjwa wa kansa. Hali yake ilizidi kuwa mbaya, naye akawa dhaifu sana asiweze kufanya shughuli zake za kawaida. Hata hivyo, Alejandra aliamua kuandika barua kwa kuwa hakutaka kuacha utumishi. Dada huyo aliandika kuhusu mpango wa kujifunza Biblia bila malipo na kuonyesha namba ya simu ya mama yake. Kisha alimpa mama yake barua hizo ili aziache kwenye nyumba ambazo hazikuwa na watu wakati alipohubiri nyumba kwa nyumba.

Wakati huohuo, Diojany, msichana mdogo kutoka Guatemala, alienda kufanya kazi ya nyumbani huko Cancún, Mexico. Akiwa huko, alikutana na Mashahidi wa Yehova naye alifurahia mazungumzo ya Biblia pamoja nao. Baadaye, waajiri wake, yaani, mume na mke, waliamua kuhamia Mexico City, nao hawakutaka kumwacha Diojany. Diojany alisita kuhama pamoja nao kwa sababu kufanya hivyo kungemtenganisha na Mashahidi.

“Usiwe na wasiwasi,” waajiri wake wakamhakikishia, “kuna Mashahidi kila mahali. Tutawatafuta baada tu ya kufika huko.” Akiwa na tarajio hilo zuri, Diojany alikubali kwenda nao. Walipofika Mexico City, waajiri wake walianza kuwatafuta Mashahidi. Kwa sababu fulani, hawakuweza kuwapata, hata ingawa kulikuwa na Mashahidi zaidi ya 41,000 na makutaniko 730 jijini humo.

Muda si muda, Diojany alianza kuvunjika moyo kwa sababu hakuweza kuwapata Mashahidi ili kuendelea na mazungumzo yake ya Biblia. Siku moja, mke wa mwajiri wake alimjia akisema, “Amini usiamini! Mungu wako alisikia sala zako.” Kisha akampa barua na kusema: “Mashahidi wamekuachia barua hii.” Barua hiyo ilitoka kwa Alejandra.

Diojany aliwasiliana na mama na dada ya Alejandra, aitwaye Blanca, naye akakubali funzo la Biblia. Baada ya majuma kadhaa, Diojany alikutana na Alejandra nao wakafurahi kujuana. Alejandra alimtia moyo aendelee kujifunza Biblia kwa bidii ili aweze kufanya maendeleo ya kiroho.

Miezi michache baadaye, Julai 2003, Alejandra alikufa. Aliwawekea waamini wenzake kielelezo kizuri cha imani na ujasiri. Baada ya mazishi, wengi waliguswa moyo sana walipokutana na Diojany na kumsikia akisema: “Alejandra na familia yake wameniwekea kielelezo kizuri sana. Nimeazimia kumtumikia Yehova na kubatizwa hivi karibuni. Ninatamani sana kumwona Alejandra katika Paradiso ijayo!”

Naam, huenda barua ikawa kitu kidogo, lakini inaweza kuwa na matokeo mazuri na ya kudumu!