Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ondoka, Zunguka Katika Nchi”

“Ondoka, Zunguka Katika Nchi”

“Ondoka, Zunguka Katika Nchi”

“Ondoka, zunguka katika nchi kwa marefu na mapana yake.” —Mwanzo 13:17.

1. Mungu alimpa Abrahamu agizo gani lenye kupendeza?

JE, WEWE hufurahia kutembelea sehemu za mashambani miisho-juma, labda ukisafiri kwa gari? Wengine hupendelea kusafiri kwa baiskeli ili kupata mazoezi na kufurahia mandhari vizuri zaidi. Nao wengine hupenda kutembea kwa miguu ili kulifahamu eneo na kulifurahia bila haraka. Kwa kawaida safari hizo huwa za wakati mfupi. Lakini hebu wazia jinsi Abrahamu alivyohisi baada ya Mungu kumwambia: “Ondoka, zunguka katika nchi kwa marefu na mapana yake, kwa kuwa hiyo nitakupa wewe”!—Mwanzo 13:17.

2. Abrahamu alienda wapi baada ya kuondoka Misri?

2 Fikiria muktadha wa maneno hayo. Abrahamu alikaa Misri akiwa pamoja na mke wake na watu wengine. Mwanzo sura ya 13 inatuambia kwamba waliondoka Misri na kupeleka mifugo yao huko “Negebu.” Kisha Abrahamu “akaenda kambi kwa kambi kutoka Negebu mpaka Betheli.” Tatizo lilipotokea kati ya wachungaji wake na wale wa mpwa wake Loti, na ikaonekana kwamba wote wawili wangepaswa kutafuta viwanja tofauti vya malisho, kwa ukarimu Abrahamu alimwacha Loti achague kwanza. Loti alichagua ‘Wilaya ya Yordani,’ bonde lenye rutuba “kama bustani ya Yehova,” na baadaye akaanza kuishi Sodoma. Mungu alimwambia Abrahamu: “Tafadhali, inua macho yako utazame kutoka mahali ulipo, upande wa kaskazini na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi.” Yaelekea kutoka eneo lililoinuka karibu na Betheli, Abrahamu angeweza kuona sehemu nyingine za nchi hiyo. Hata hivyo, Abrahamu hangeitazama tu nchi hiyo. Mungu alimwambia ‘aondoke na kuzunguka katika nchi’ ili kufahamu maeneo yake na jinsi ilivyokuwa.

3. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kupiga picha akilini kuhusu safari za Abrahamu?

3 Hata Abrahamu awe aliizunguka nchi hiyo kwa kadiri gani kabla ya kufika Hebroni, ni wazi kwamba aliifahamu Nchi ya Ahadi vizuri zaidi kuliko wengi wetu. Fikiria sehemu zinazotajwa katika masimulizi haya—Negebu, Betheli, Wilaya ya Yordani, Sodoma, na Hebroni. Je, unaona ni vigumu kupiga picha akilini kuhusu mahali maeneo hayo yalipokuwa? Wengi huona ni vigumu kufanya hivyo kwa sababu ni wachache sana kati ya watu wa Yehova ambao wanaweza kutembelea mengi ya maeneo wanayosoma katika Biblia, yaani, kusafiri kwa mapana na marefu katika nchi hiyo. Hata hivyo, tuna sababu ya kutaka sana kujua maeneo yanayotajwa katika Biblia. Kwa nini?

4, 5. (a) Methali 18:15 inahusianaje na ujuzi na uelewaji wa nchi zinazotajwa katika Biblia? (b) Sefania sura ya 2 inaonyesha nini?

4 Neno la Mungu linasema: “Moyo wa mtu mwenye uelewaji hujipatia ujuzi, nalo sikio la wenye hekima hutafuta kupata ujuzi.” (Methali 18:15) Kuna mambo mengi ambayo mtu anaweza kujifunza, lakini ujuzi sahihi kumhusu Yehova Mungu na shughuli zake ndio muhimu zaidi. Bila shaka, yale tunayosoma katika Biblia ni muhimu ili kupata ujuzi huo. (2 Timotheo 3:16) Hata hivyo, ona kwamba uelewaji unahusika. Uelewaji ni uwezo wa kufahamu jambo, kutambua au kujua jinsi sehemu zake mbalimbali zinavyohusiana na jambo lote zima. Ndivyo ilivyo kuhusiana na maeneo yanayotajwa katika Biblia. Kwa mfano, wengi wetu wanajua Misri iko wapi, lakini tunaelewa kwa kadiri gani masimulizi yanayosema kwamba Abrahamu aliondoka Misri “kwenda Negebu,” baadaye akaenda Betheli, kisha Hebroni? Je, unaelewa maeneo hayo yanahusianaje?

5 Au labda katika ratiba ya usomaji wa Biblia ulisoma Sefania sura ya 2. Katika sura hiyo ulisoma majina ya majiji, watu, na nchi mbalimbali. Sura hiyo moja inataja maeneo haya yote: Gaza, Ashkeloni, Ashdodi, Ekroni, Sodoma, na Ninawi na pia Kanaani, Moabu, Amoni, na Ashuru. Je, ulifanikiwa kupiga picha akilini kuhusu maeneo hayo ambako watu halisi waliishi, watu waliohusika katika kutimizwa kwa unabii wa Mungu?

6. Kwa nini Wakristo fulani wametambua umuhimu wa ramani? (Ona sanduku.)

6 Wanafunzi wengi wa Neno la Mungu wamenufaika sana kwa kutumia ramani za nchi zinazotajwa katika Biblia. Wao huzitumia si kwa sababu tu wanapendezwa na ramani, bali kwa sababu wanatambua kwamba kwa kutumia ramani, wanaweza kuongeza ujuzi wao wa Neno la Mungu. Pia ramani zinaweza kuwasaidia kuongeza uelewaji wao, wanapoona jinsi habari ambazo tayari wanajua zinavyohusiana na habari nyingine. Tunapochunguza mifano fulani, yaelekea pia utamthamini Yehova zaidi na kupata ufahamu zaidi kuhusu masimulizi yaliyo katika Neno lake.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 14.

Kuelewa Umbali Huzidisha Uelewaji

7, 8. (a) Samsoni alifanya jambo gani lenye kustaajabisha huko Gaza? (b) Ni habari gani inayoweza kufanya tendo la ujasiri la Samsoni liwe na maana zaidi? (c) Ujuzi na uelewaji wa masimulizi hayo kuhusu Samsoni unatusaidiaje?

7 Kwenye Waamuzi 16:2, unaweza kusoma kuhusu Mwamuzi Samsoni alipokuwa Gaza. Leo eneo la Gaza hutajwa mara nyingi katika vyombo vya habari, kwa hiyo huenda ikawa unajua kwa kadiri fulani mahali Samsoni alipokuwa, katika eneo la Wafilisti karibu na Pwani ya Mediterania. [gl 11] Sasa ona andiko la Waamuzi 16:3: ‘Samsoni aliendelea kulala mpaka katikati ya usiku, kisha akaamka katikati ya usiku, akakamata milango ya lango la jiji na miimo yake miwili, akaing’oa pamoja na pingo, akaiweka juu ya mabega yake, akaichukua mpaka kwenye kilele cha mlima ulio mbele ya Hebroni.’

8 Bila shaka malango na miimo ya jiji la Gaza ilikuwa mikubwa na mizito, kwa kuwa jiji hilo lilikuwa ngome. Wazia ukijaribu kubeba malango na miimo hiyo! Samsoni aliibeba, lakini aliipeleka wapi, naye alifunga safari ya aina gani? Gaza liko pwani, karibu na usawa wa bahari. [gl 15] Hata hivyo, Hebroni liko upande wa mashariki kwenye mwinuko wa meta 930—eneo lililo juu kwelikweli! Hatujui mahali hususa ambapo “mlima ulio mbele ya Hebroni” ulikuwa, lakini Hebroni liko umbali wa kilometa 60 hivi kutoka Gaza! Kujua umbali uliohusika kunatusaidia kuelewa ukubwa wa tendo la ujasiri la Samsoni, sivyo? Kumbuka kwamba Samsoni aliweza kufanya mambo hayo kwa sababu ‘roho ya Yehova ilianza kutenda kazi juu yake.’ (Waamuzi 14:6, 19; 15:14) Tukiwa Wakristo leo, hatutarajii roho ya Mungu itupe nguvu za kimwili zisizo za kawaida. Hata hivyo, roho hiyohiyo yenye nguvu inaweza kuongeza utambuzi wetu wa mambo ya kiroho yenye kina na kutufanya tuwe na uwezo kulingana na mtu tuliye kwa ndani. (1 Wakorintho 2:10-16; 13:8; Waefeso 3:16; Wakolosai 1:9, 10) Naam, kuelewa masimulizi kuhusu Samsoni, hukazia uhakika kwamba roho ya Mungu inaweza kutusaidia.

9, 10. (a) Ni nini kilichohusika katika ushindi wa Gideoni dhidi ya Wamidiani? (b) Kujua maeneo na umbali unaohusika kunaweza kusaidiaje kufanya masimulizi hayo yawe na maana zaidi?

9 Masimulizi mengine yanayokazia umuhimu wa kujua umbali unaohusika ni yale yanayohusu ushindi wa Gideoni dhidi ya Wamidiani. Wasomaji wengi wa Biblia wanajua kwamba Mwamuzi Gideoni na kikosi chake cha watu 300 alishinda wavamizi 135,000 walioungana, yaani, Wamidiani, Waamaleki, na vikosi vingine vilivyopiga kambi kwenye nchi tambarare ya Yezreeli, karibu na kilima cha More. [gl 18] Wanaume wa Gideoni walipiga baragumu, wakavunja-vunja mitungi ili kufunua mienge yao, na kupaaza sauti: “Upanga wa Yehova na wa Gideoni!” Jambo hilo liliwatatanisha na kuwaogopesha maadui sana hivi kwamba walianza kupigana wenyewe kwa wenyewe. (Waamuzi 6:33; 7:1-22) Je, jambo hilo lilihusisha hayo tu, tendo la haraka la usiku mmoja tu? Endelea kusoma Waamuzi sura ya 7 na 8. Utaona kwamba Gideoni aliendelea kushambulia. Kati ya sehemu nyingi zinazotajwa, nyingine haziwezi kutambulika leo, kwa hiyo huenda zisionyeshwe katika ramani za Biblia. Hata hivyo, sehemu za kutosha zimetambuliwa ili tuweze kufuatia matendo ya Gideoni.

10 Gideoni alifukuza vikosi vilivyobaki kupitia Beth-shita, kisha akaelekea kusini hadi Abel-mehola, karibu na Yordani. (Waamuzi 7:22-25) Masimulizi hayo yanasema: “Gideoni akaja Yordani, akauvuka, yeye pamoja na wale wanaume mia tatu waliokuwa pamoja naye, wakiwa wamechoka lakini wakiwa wanaendelea kufuatilia.” Baada ya kuvuka Yordani, Waisraeli waliwafuatia maadui wao kuelekea kusini hadi Sukothi na Penueli, karibu na Yaboki, kisha wakapanda vilima kuelekea Yogbeha (karibu na mji wa leo wa Amman, Jordan). Waliwafuatia kwa kilometa 80 hivi huku wakipigana nao. Gideoni aliwakamata na kuwaua wafalme wawili wa Midiani; kisha akarudi katika jiji lake la Ofra, karibu na mahali mapigano yalipoanzia. (Waamuzi 8:4-12, 21-27) Bila shaka, tendo la ujasiri la Gideoni lilihusisha mengi zaidi ya kupiga baragumu, kupeperusha mienge, na kupaaza sauti kwa dakika chache. Fikiria jinsi hilo linavyoongezea uzito maelezo haya kuhusu watu wenye imani: ‘Nitakosa wakati nikiendelea kusimulia juu ya Gideoni na wengine ambao kutoka hali ya udhaifu walifanywa kuwa wenye nguvu, wakawa mashujaa katika vita.’ (Waebrania 11:32-34) Wakristo pia wanaweza kuchoka, lakini ni muhimu kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu.—2 Wakorintho 4:1, 16; Wagalatia 6:9.

Watu Hufikiri na Kutendaje?

11. Waisraeli walisafiri umbali gani kabla na baada ya kufika Kadeshi?

11 Huenda watu wengine wakatumia ramani za Biblia kutafuta sehemu mbalimbali, lakini je, unafikiri ramani zinaweza kuwasaidia waongeze ufahamu wao? Kwa mfano, fikiria Waisraeli waliosafiri kutoka Mlima Sinai kuelekea Nchi ya Ahadi. Baada ya kutua mara kadhaa wakiwa safarini, mwishowe walifika Kadeshi (au, Kadesh-barnea). [gl 9] Andiko la Kumbukumbu la Torati 1:2 linaonyesha kwamba hiyo ilikuwa safari ya siku 11, umbali wa kilometa 270 hivi. Kutoka hapo Musa alituma wapelelezi 12 katika Nchi ya Ahadi. (Hesabu 10:12, 33; 11:34, 35; 12:16; 13:1-3, 25, 26) Wapelelezi hao walielekea upande wa kaskazini kupitia Negebu, na yaelekea walipita Beer-sheba, kisha Hebroni, hadi mipaka ya kaskazini ya Nchi ya Ahadi. (Hesabu 13:21-24) Iliwabidi Waisraeli watange-tange nyikani kwa miaka 40 kwa sababu walikubali ripoti mbaya ya wale wapelelezi 10. (Hesabu 14:1-34) Hilo linaonyesha nini kuhusu imani na utayari wao wa kumtumaini Yehova?—Kumbukumbu la Torati 1:19-33; Zaburi 78:22, 32-43; Yuda 5.

12. Tunaweza kufikia mkataa gani kuhusu imani ya Waisraeli, na kwa nini tunapaswa kufikiria jambo hilo?

12 Fikiria hilo kuhusiana na mahali walipokuwa. Kama Waisraeli wangeonyesha imani na kufuata shauri la Yoshua na Kalebu, hawangelazimika kusafiri mbali ili kufika Nchi ya Ahadi. Eneo la Kadeshi lilikuwa kilometa 16 hivi kutoka Beer-lahai-roi, walikoishi Isaka na Rebeka. [gl 7] Lilikuwa umbali unaopungua kilometa 95 kufika Beer-sheba, linalotajwa kuwa sehemu ya kusini kabisa ya Nchi ya Ahadi. (Mwanzo 24:62; 25:11; 2 Samweli 3:10) Baada ya kusafiri kutoka Misri hadi Mlima Sinai, kisha kilometa 270 hadi Kadeshi, walikuwa karibu kabisa kuingia katika Nchi ya Ahadi. Sisi pia tuko karibu sana kuingia katika Paradiso ya kidunia iliyoahidiwa. Tunajifunza nini? Mtume Paulo alihusianisha hali ya Waisraeli na shauri hili: “Kwa hiyo acheni sisi tufanye yote tunayoweza ili kuingia katika pumziko hilo, yeyote asije akaanguka katika kielelezo kilekile cha kutotii.”—Waebrania 3:16–4:11.

13, 14. (a) Wagibeoni walichukua hatua muhimu katika hali gani? (b) Ni nini kinachofunua mtazamo wa Wagibeoni, nasi tunapaswa kujifunza nini kutokana nao?

13 Tukio la Biblia linalohusu Wagibeoni linaonyesha mtazamo tofauti wa kumtumaini Mungu atekeleze mapenzi yake. Baada ya Yoshua kuwaongoza Waisraeli kuvuka Mto Yordani na kuingia katika nchi ambayo Mungu aliahidi familia ya Abrahamu, wakati ulikuwa umefika wa kuwafukuza Wakanaani. (Kumbukumbu la Torati 7:1-3) Wagibeoni walitiwa ndani. Waisraeli walishinda Yeriko na Ai na kupiga kambi karibu na Gilgali. Wagibeoni hawakutaka kufa wakiwa Wakanaani waliolaaniwa, kwa hiyo walituma wawakilishi kwa Yoshua huko Gilgali. Ili waweze kufanya mkataba wa amani pamoja na Waebrania, walijifanya eti walitoka nje ya eneo la Kanaani.

14 Wawakilishi hao walisema: “Watumishi wako wametoka nchi ya mbali sana kwa sababu ya jina la Yehova Mungu wako.” (Yoshua 9:3-9) Mavazi na vyakula vyao vilifanya ionekane kama walikuwa wametoka mbali, lakini kwa kweli Gibeoni lilikuwa kilometa 30 hivi kutoka Gilgali. [gl 19] Kwa kusadiki hilo, Yoshua na wakuu walifanya mkataba wa amani pamoja na Wagibeoni na majiji ya karibu yaliyokuwa na uhusiano na Gibeoni. Je, ujanja wa Wagibeoni ulikuwa tu njia ya kujiepusha na kifo? Hapana, ujanja huo ulionyesha tamaa yao ya kupata kibali cha Mungu wa Israeli. Yehova aliwakubali Wagibeoni, nao wakawa “wakusanyaji wa kuni na watekaji wa maji kwa ajili ya kusanyiko na kwa ajili ya madhabahu ya Yehova,” wakileta kuni kwa ajili ya madhabahu ya dhabihu. (Yoshua 9:11-27) Wagibeoni waliendelea kuonyesha utayari wao wa kufanya kazi za hali ya chini katika utumishi wa Yehova. Yaelekea baadhi yao walikuwa kati ya Wanethini waliorudi kutoka Babiloni na kutumika kwenye hekalu lililojengwa upya. (Ezra 2:1, 2, 43-54; 8:20) Tunaweza kuiga mtazamo wao kwa kujitahidi kudumisha amani pamoja na Mungu, na kuwa tayari kufanya hata kazi za hali ya chini katika utumishi wake.

Kujidhabihu

15. Kwa nini tupendezwe na maeneo yanayotajwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo?

15 Masimulizi ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kama yale yanayohusu safari na huduma ya Yesu na mtume Paulo, yanataja maeneo ya nchi zinazotajwa katika Biblia. (Marko 1:38; 7:24, 31; 10:1; Luka 8:1; 13:22; 2 Wakorintho 11:25, 26) Katika masimulizi yanayofuata, jaribu kufikiria safari zinazohusika.

16. Wakristo huko Beroya walionyeshaje kwamba walimthamini Paulo?

16 Katika safari yake ya pili ya umishonari (mstari wa rangi ya zambarau kwenye ramani), Paulo alifika Filipi, ambalo sasa ni sehemu ya Ugiriki. [gl 33] Alihubiri huko, akafungwa gerezani kisha akaachiliwa, na kuelekea Thesalonike. (Matendo 16:6–17:1) Wayahudi walipochochea fujo, ndugu wa Thesalonike walimsihi Paulo aende Beroya, lililokuwa umbali wa kilometa 65 hivi. Huduma ya Paulo ilifanikiwa sana huko Beroya, lakini Wayahudi wakaja na kuwachochea watu. Hivyo, “akina ndugu wakamsindikiza Paulo mara moja mpaka baharini,” na “wale waliokuwa wakimsindikiza Paulo wakamleta mpaka Athene.” (Matendo 17:5-15) Yaelekea baadhi ya wageuzwa-imani wapya walikuwa tayari kutembea umbali wa kilometa 40 hadi Bahari ya Aegea, kisha kulipa nauli na kusafiri kwa meli umbali upatao kilometa 500. Safari hiyo ingeweza kuwa hatari, lakini ndugu hao walikuwa tayari kukabili hatari hizo, hivyo wakaweza kukaa muda mrefu zaidi pamoja na mwakilishi asafiriye wa Mungu.

17. Ni jambo gani tunaloweza kufahamu vizuri zaidi baada ya kuelewa umbali kati ya Mileto na Efeso?

17 Katika safari yake ya tatu (mstari wa rangi ya kijani-kibichi kwenye ramani), Paulo alifika kwenye bandari ya Mileto. Alituma watu wakawaite wanaume wazee wa kutaniko la Efeso lililokuwa umbali wa kilometa 50 hivi. Wazia wazee hao wakiacha shughuli zao na kwenda kukutana na Paulo. Yaelekea walipokuwa wakitembea kuelekea huko, walizungumza kwa furaha kuhusu kukutana naye. Baada ya kukutana na Paulo na kumsikia akisali, “wote wakalia sana, nao wakamwangukia Paulo shingoni na kumbusu kwa wororo.” Kisha “wakaanza kumsindikiza mpaka kwenye mashua” ili aendelee na safari yake hadi Yerusalemu. (Matendo 20:14-38) Wangekuwa na mambo mengi ya kufikiria na kuzungumzia walipokuwa wakirudi Efeso. Je, huvutiwi na uthamini walioonyesha kwa kutembea umbali huo wote ili kukutana na mtumishi asafiriye ambaye angeweza kuwaelimisha na kuwatia moyo? Je, unaona jambo fulani katika masimulizi hayo unaloweza kutumia katika maisha na kufikiri kwako?

Jifunze Kuhusu Nchi ya Ahadi na Mambo Tunayotarajia

18. Tunaweza kuazimia kufanya nini kuhusiana na maeneo yanayotajwa katika Biblia?

18 Mifano iliyotangulia kutajwa inaonyesha umuhimu wa kufahamu nchi ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, ambayo ni muhimu kuhusiana na masimulizi mengi ya Biblia. (Nasi tunaweza kupanua ufahamu wetu kwa kujifunza pia kuhusu maeneo yanayozunguka nchi zinazotajwa katika masimulizi ya Biblia.) Tunapoongeza ujuzi na uelewaji wetu kuhusu Nchi ya Ahadi hasa, tunapaswa kukumbuka jambo moja muhimu ambalo Waisraeli walitakiwa kufanya ili kuingia na kufurahia ile nchi ya “maziwa na asali.” Jambo hilo lilikuwa kumwogopa Yehova na kushika amri zake.—Kumbukumbu la Torati 6:1, 2; 27:3.

19. Tunapaswa kuendelea kufikiria paradiso gani mbili?

19 Vivyo hivyo, leo tunapaswa kutimiza sehemu yetu ya kumwogopa Yehova na kushikamana na njia zake. Kwa kufanya hivyo, tutachangia kuboresha na kurembesha paradiso ya kiroho iliyopo sasa katika kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote. Tutaongeza ujuzi wetu kuhusu sehemu zake mbalimbali na baraka zake. Na tunajua kwamba kutakuwa na baraka nyingi zaidi. Yoshua aliwaongoza Waisraeli kuvuka Yordani na kuingia katika nchi yenye rutuba na yenye kuridhisha. Sasa tuna sababu nzuri ya kutazamia kwa uhakika Paradiso halisi, ile nchi nzuri iliyo mbele yetu.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kuwa na tamaa ya kuongeza ujuzi na uelewaji wetu kuhusu nchi zinazotajwa katika Biblia?

• Ni habari gani kuhusu maeneo yaliyozungumziwa katika makala hii ambayo hasa imekuelimisha?

• Ni jambo gani lililofafanuliwa kabisa kwako ulipojifunza mengi zaidi kuhusu umbali na maeneo yanayohusika katika tukio fulani?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

‘Ona Nchi Nzuri’

Mashahidi wa Yehova walifurahi kupokea broshua ‘Ona Nchi Nzuri’ kwenye makusanyiko ya wilaya ya mwaka wa 2003 na 2004. Kichapo hicho kipya kinachopatikana katika lugha 80 hivi, kina ramani nyingi zenye rangi kamili na chati zinazoonyesha maeneo mbalimbali yanayotajwa katika Biblia, hasa Nchi ya Ahadi katika vipindi tofauti-tofauti.

Makala inayoambatana na makala hii inarejelea ramani hususa kwa kuonyesha namba ya ukurasa katika herufi nzito, kama vile [gl 15]. Ikiwa una broshua hiyo mpya, tumia wakati fulani kujifahamisha mambo mbalimbali yanayoweza kukusaidia kupanua ujuzi na uelewaji wako wa Neno la Mungu.

(1) Ramani nyingi zina ufunguo au sanduku lenye orodha ya maelezo kuhusu alama muhimu zilizo katika ramani [gl 18]. (2) Ramani nyingi zina skeli inayoonyesha maili na kilometa ambazo zitakuwezesha kuelewa ukubwa au umbali unaohusika [gl 26]. (3) Kwa kawaida, kuna alama ya mshale inayoelekezwa kaskazini ili kukusaidia ujue upande unaohusika [gl 19]. (4) Mara nyingi, ramani zimetiwa rangi ili kuonyesha miinuko kwa ujumla [gl 12]. (5) Huenda ramani ikawa na herufi/namba pembeni ili uweze kuwazia mistari fulani unayoweza kutumia kupata majiji au majina [gl 23]. (6) Katika faharisi yenye kurasa mbili ya majina ya maeneo mbalimbali [gl 34-35], unaweza kuona namba ya ukurasa katika herufi nzito, mara nyingi ikifuatwa na herufi na namba za kukusaidia kupata eneo unalotafuta kama vile E2. Baada ya kutumia vitu hivyo mara chache, huenda ukashangaa kuona kwamba vinasaidia sana kuongeza ujuzi na uelewaji wako wa Biblia.

[Chati/Ramani katika ukurasa wa 16, 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

CHATI YA MAENEO YA ASILI

A. Pwani ya Bahari Kuu

B. Nchi Tambarare Magharibi ya Yordani

1. Nchi Tambarare ya Asheri

2. Ukanda wa Pwani wa Dori

3. Viwanja vya Malisho vya Sharoni

4. Nchi Tambarare ya Ufilisti

5. Bonde la Kati la Mashariki-Magharibi

a. Nchi Tambarare ya Megido

b. Nchi Tambarare ya Chini ya Yezreeli

C. Milima Iliyo Magharibi ya Yordani

1. Vilima vya Galilaya

2. Vilima vya Karmeli

3. Vilima vya Samaria

4. Shefela (vilima vya chini)

5. Nchi Yenye Vilima ya Yuda

6. Nyika ya Yuda

7. Negebu

8. Nyika ya Parani

D. Araba (Bonde la Ufa)

1. Bonde la Hula

2. Eneo la Bahari ya Galilaya

3. Bonde la Yordani

4. Bahari ya Chumvi

5. Araba (kusini ya Bahari ya Chumvi)

E. Milima/Nyanda za Juu Mashariki ya Yordani

1. Bashani

2. Gileadi

3. Amoni na Moabu

4. Uwanda wa Mlima wa Edomu

F. Milima ya Lebanoni

[Ramani]

Ml. Hermoni

More

Abel-mehola

Sukothi

Yogbeha

Betheli

Gilgali

Gibeoni

Yerusalemu

Hebroni

Gaza

Beer-sheba

Sodoma?

Kadeshi

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

KANAANI

Megido

GILEADI

Dothani

Shekemu

Betheli (Luzi)

Yerusalemu (Salemu)

Ai

Bethlehemu (Efrathi)

Mamre

Hebroni (Makpela)

Gerari

Beer-sheba

Sodoma?

NEGEBU

Rehobothi?

[Milima]

Moria

[Bahari na Ziwa]

Bahari ya Chumvi

[Mito]

Yordani

[Picha katika ukurasa wa 15]

Abrahamu alisafiri kuivuka nchi hiyo

[Ramani katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Troa

SAMOTHRAKE

Filipi

Neapoli

Amfipoli

Thesalonike

Beroya

Athene

Korintho

Efeso

Mileto

RODE