Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea Katika Njia ya Utimilifu

Tembea Katika Njia ya Utimilifu

Tembea Katika Njia ya Utimilifu

“Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu.”—ZABURI 26:11.

1, 2. (a) Kwa nini utimilifu wa mwanadamu ni sehemu muhimu ya suala linalohusu haki ya Mungu ya kutawala? (b) Viumbe wenye akili wanaweza kuonyeshaje kwamba wanaunga mkono haki ya Yehova ya kutawala?

SHETANI alipoasi katika bustani ya Edeni, alizusha suala linalohusu haki ya Mungu ya kutawala viumbe Wake wote. Baadaye, alibisha kwamba wanadamu humtumikia Mungu kwa sababu ya faida yao wenyewe. (Ayubu 1:9-11; 2:4) Hivyo, utimilifu wa mwanadamu umekuwa sehemu muhimu ya suala la kama Yehova ana haki ya kutawala.

2 Ingawa utawala wa Mungu hautegemei utimilifu wa viumbe wake, wanadamu na wana wa roho wa Mungu wanaweza kuonyesha upande ambao wanaunga mkono katika suala hilo. Jinsi gani? Kwa kuamua kufuata njia ya utimilifu au kutoifuata. Kwa hiyo, utimilifu wa mtu ndio msingi thabiti wa jinsi atakavyohukumiwa.

3. (a) Ayubu na Daudi walitaka Yehova achunguze na kuhukumu nini kuwahusu? (b) Ni maswali gani yanayotokea kuhusu utimilifu?

3 Akiwa na uhakika, Ayubu alisema: “[Yehova] atanipima katika mizani sahihi na Mungu atajua utimilifu wangu.” (Ayubu 31:6) Mfalme Daudi wa Israeli la kale alimwomba Yehova achunguze utimilifu wake aliposali hivi: “Unihukumu, Ee Yehova, kwa maana nimetembea katika utimilifu wangu, nami nimemtumaini Yehova, nisipate kutikisika.” (Zaburi 26:1) Ni muhimu kwetu pia kutembea katika njia ya utimilifu. Lakini utimilifu ni nini, na inamaanisha nini kutembea katika njia ya utimilifu? Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kutembea katika njia ya utimilifu?

‘Nimetembea Katika Utimilifu Wangu’

4. Utimilifu ni nini?

4 Utimilifu humaanisha kuwa mnyoofu, bila lawama, mwadilifu, na bila kosa. Hata hivyo, utimilifu unahusisha mengi zaidi ya kufanya yaliyo sawa. Ni ubora wa maadili au kujitoa kwa Mungu kwa moyo wote. Shetani alitilia shaka nia ya Ayubu alipomwambia Mungu hivi: “Ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kufikia mfupa wake [Ayubu] na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.” (Ayubu 2:5) Zaidi ya kuwa na matendo yanayofaa, utimilifu hutaka tuwe na nia inayofaa.

5. Ni nini kinachoonyesha kwamba si lazima tuwe wakamilifu ili tudumishe utimilifu?

5 Hata hivyo, si lazima tuwe wakamilifu ili tudumishe utimilifu. Mfalme Daudi hakuwa mkamilifu naye alifanya makosa mengi mazito maishani mwake. Lakini Biblia humtaja kuwa mtu aliyetembea “kwa utimilifu wa moyo.” (1 Wafalme 9:4) Kwa nini? Kwa kuwa Daudi alimpenda Yehova. Alikuwa amejitoa kwa moyo kwa Mungu. Alikiri makosa yake kwa hiari, akakubali karipio, na kurekebisha njia zake. Kwa kweli, Daudi alionyesha utimilifu wake kwa kujitoa kwa moyo wote na kumpenda Yehova, Mungu wake.—Kumbukumbu la Torati 6:5, 6.

6, 7. Kutembea katika utimilifu kunahusisha nini?

6 Utimilifu hauhusu tu sehemu fulani ya maisha ya binadamu kama vile ujitoaji wa kidini. Unahusu kila sehemu ya maisha yetu. Daudi ‘alitembea’ katika utimilifu wake. “Kitenzi ‘tembea’ hudokeza ‘njia ya maisha’ au ‘mtindo wa maisha,’” chasema kitabu The New Interpreter’s Bible. Akizungumza kuhusu wale “wasio na kosa katika njia yao,” mtunga-zaburi aliimba hivi: “Wenye furaha ni wale wanaoshika vikumbusho [vya Mungu]; wanaendelea kumtafuta kwa moyo wote. Kwa kweli hawakuzoea kufanya ukosefu wowote wa uadilifu. Wametembea katika njia zake.” (Zaburi 119:1-3) Ili tuwe watimilifu tunahitaji kujitahidi daima kufanya mapenzi ya Mungu na kutembea katika njia yake.

7 Kutembea katika utimilifu hutaka tujitoe kwa ushikamanifu kwa Mungu, hata chini ya hali zisizofaa. Tunadhihirisha utimilifu wetu tunapovumilia majaribu, tunapoendelea kuwa imara licha ya shida, au tunaposhinda vishawishi kutoka kwa ulimwengu usiomwogopa Mungu. ‘Tunaufanya moyo wa Yehova ushangilie’ kwa kuwa anaweza kumjibu yule anayemdhihaki. (Methali 27:11) Hivyo, tuna sababu nzuri ya kuazimia kama alivyofanya Ayubu: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayubu 27:5) Zaburi ya 26 inaonyesha jambo litakalotusaidia kutembea katika utimilifu.

“Usafishe Figo Zangu na Moyo Wangu”

8. Unajifunza nini kutokana na ombi la Daudi kwamba Yehova achunguze figo na moyo wake?

8 Daudi alisali hivi: “Unichunguze, Ee Yehova, na kunijaribu; usafishe figo zangu na moyo wangu.” (Zaburi 26:2) Figo huwa katika sehemu za ndani kabisa mwilini. Kwa njia ya mfano, figo hufananisha mawazo na hisia za ndani kabisa za mtu. Nao moyo wa mfano ni mtu wa ndani, yaani, nia, hisia, na akili yake. Daudi alipomwomba Yehova amchunguze, alikuwa akisali kwamba mawazo na hisia zake za ndani kabisa zichunguzwe.

9. Yehova husafishaje figo na moyo wetu wa mfano?

9 Daudi aliomba kwamba figo na moyo wake zisafishwe. Yehova husafishaje mtu wa ndani? Daudi aliimba: “Nitambariki Yehova, ambaye amenipa shauri. Kwa kweli, nyakati za usiku figo zangu zimenirekebisha.” (Zaburi 16:7) Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba shauri la Mungu liligusa sehemu za ndani kabisa za Daudi na kubaki humo, zikarekebisha mawazo na hisia zake za ndani kabisa. Vivyo hivyo, shauri la Mungu linaweza kurekebisha mawazo na hisia zetu za ndani kabisa ikiwa tutatafakari shauri tunalopokea kutoka kwa Neno la Mungu, wawakilishi wake, na tengenezo lake na kuliruhusu libaki ndani yetu. Kusali kwa Yehova kwa ukawaida ili atusafishe kwa njia hiyo kutatusaidia tutembee katika utimilifu.

‘Fadhili Zako Zenye Upendo Ziko Mbele Yangu’

10. Ni nini kilichomsaidia Daudi kutembea katika kweli ya Mungu?

10 Daudi aliendelea kusema: “Fadhili zako zenye upendo ziko mbele ya macho yangu, nami nimetembea katika kweli yako.” (Zaburi 26:3) Daudi alijua vizuri sana matendo ya fadhili zenye upendo za Mungu, naye aliyatafakari kwa shukrani. Daudi aliimba hivi: “Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu, wala usiyasahau matendo yake yote.” Akikumbuka mojawapo ya “matendo” ya Mungu, Daudi aliendelea kusema: “Yehova anatekeleza matendo ya uadilifu na hukumu kwa wale wote wanaopunjwa. Alimjulisha Musa njia zake, matendo yake kwa wana wa Israeli.” (Zaburi 103:2, 6, 7) Labda Daudi alikuwa akifikiria jinsi Wamisri walivyowapunja Waisraeli katika siku za Musa. Ikiwa ndivyo, bila shaka Daudi aliguswa moyo na kuimarisha azimio lake la kutembea katika kweli ya Mungu kwa kutafakari jinsi Yehova alivyomjulisha Musa njia zake za kukomboa.

11. Ni nini kinachoweza kutusaidia tutembee katika njia ya utimilifu?

11 Kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kutafakari mambo tunayojifunza kutatusaidia pia tutembee katika njia ya utimilifu. Kwa mfano, kukumbuka kwamba Yosefu alikimbia alipotongozwa na mke wa Potifa kutatuchochea tukimbie tunapotongozwa kazini, shuleni, au mahali penginepo. (Mwanzo 39:7-12) Namna gani tunaposhawishiwa kufuatia vitu vya kimwili au umashuhuri na cheo katika ulimwengu? Tuna mfano wa Musa ambaye alikataa utukufu wa Misri. (Waebrania 11:24-26) Bila shaka, kukumbuka uvumilivu wa Ayubu kutatusaidia kuimarisha azimio letu la kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova licha ya magonjwa na misiba. (Yakobo 5:11) Namna gani tunapoteswa? Kukumbuka yaliyompata Danieli alipokuwa ndani ya shimo la simba kutatupa ujasiri.—Danieli 6:16-22.

“Sikuketi na Watu Wasiosema Kweli”

12, 13. Tunapaswa kuepuka mashirika ya aina gani?

12 Akitaja jambo lingine lililoimarisha utimilifu wake, Daudi alisema: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo. Nimelichukia kutaniko la watenda-maovu, wala siketi pamoja na waovu.” (Zaburi 26:4, 5) Daudi hangeketi kamwe na waovu. Alichukia mashirika mabaya.

13 Namna gani sisi? Je, sisi hukataa kushirikiana na watu wasiosema kweli kupitia vipindi vya televisheni, video, sinema, Intaneti, au kwa njia nyingine? Je, sisi hujitenga na wale wanaoficha jinsi walivyo? Huenda watu fulani shuleni au kazini wakajifanya kuwa rafiki zetu wakiwa na makusudio yenye hila. Je, kweli tunataka kuwa na uhusiano wa karibu na watu wasiotembea katika kweli ya Mungu? Ingawa waasi-imani hudai kuwa wanyoofu, huenda wao pia wakaficha nia yao ya kutufanya tuache kumtumikia Yehova. Namna gani ikiwa katika kutaniko la Kikristo kuna wale wanaoishi maisha maradufu? Wao pia huficha jinsi walivyo kikweli. Jayson, ambaye sasa ni mtumishi wa huduma alikuwa na rafiki kama hao alipokuwa kijana. Anasema hivi kuwahusu: “Siku moja, mmoja wao aliniambia: ‘Haidhuru kile tunachofanya sasa kwa kuwa mfumo mpya utakapokuja, tutakuwa tumekufa. Hatutajua tulichokosa.’ Mazungumzo hayo yalifanya nishtuke. Singetaka niwe nimekufa mfumo mpya unapokuja.” Kwa hekima, Jayson aliacha kushirikiana na rafiki hao. Mtume Paulo alionya: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Ni muhimu sana tuepuke mashirika mabaya.

‘Nitatangaza Kazi Zako Zote za Ajabu’

14, 15. Tunawezaje ‘kutembea tukizunguka madhabahu ya Yehova’?

14 Daudi aliendelea kusema: “Nitaiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia, nami nitatembea nikizunguka madhabahu yako, Ee Yehova.” Kwa nini? “Ili kufanya utoaji shukrani usikiwe kwa sauti kubwa, na kutangaza kazi zako zote za ajabu.” (Zaburi 26:6, 7) Daudi alitaka kubaki akiwa safi kiadili ili amwabudu Yehova na kutangaza ujitoaji wake kwake.

15 Kila kitu kinachohusiana na ibada ya kweli kwenye maskani na baadaye kwenye hekalu kilikuwa “mfano wa uhalisi na kivuli cha vitu vya mbinguni.” (Waebrania 8:5; 9:23) Madhabahu yalifananisha nia ya Yehova ya kukubali dhabihu ya Yesu Kristo kwa ajili ya ukombozi wa wanadamu. (Waebrania 10:5-10) Sisi husafisha mikono yetu kwa kutokuwa na hatia na ‘kutembea tukizunguka madhabahu ya Yehova’ kwa kuonyesha imani katika dhabihu hiyo.—Yohana 3:16-18.

16. Tunanufaikaje kwa kuwatangazia wengine kazi za ajabu za Mungu?

16 Tunapofikiria mambo yote ambayo yanawezekana kwa sababu ya fidia, je, mioyo yetu haijawi na shukrani kwa Yehova na Mwana wake mzaliwa-pekee? Tukiwa na shukrani za kutoka moyoni, acheni tuwajulishe wengine kazi za ajabu za Mungu—tangu kuumbwa kwa mwanadamu katika bustani ya Edeni hadi kurudishwa kabisa kwa vitu vyote katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Mwanzo 2:7; Matendo 3:21) Bila shaka, kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi hutulinda kiroho. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Tunapofanya kazi hiyo kwa bidii tunadumisha tumaini letu la wakati ujao likiwa jangavu, tunaimarisha imani yetu katika ahadi za Mungu na upendo wetu kwa Yehova na wanadamu wenzetu.

“Nimependa Makao ya Nyumba Yako”

17, 18. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea mikutano ya Kikristo?

17 Maskani pamoja na madhabahu yake ya kutolea dhabihu, yalikuwa kitovu cha ibada ya Yehova katika Israeli. Akieleza jinsi alivyofurahia kuwa mahali hapo, Daudi alisali: “Yehova, nimependa makao ya nyumba yako na mahali ambapo utukufu wako hukaa.”Zaburi 26:8.

18 Je, sisi hupenda kukusanyika mahali ambapo tunajifunza kumhusu Yehova? Kila Jumba la Ufalme na mikutano inayofanywa humo kwa ukawaida huwa kitovu cha ibada ya kweli katika jumuiya. Isitoshe, kila mwaka tunakuwa na makusanyiko ya wilaya, ya mzunguko, na ya pekee. “Vikumbusho” vya Yehova huzungumziwa katika mikutano hiyo. Tukijifunza ‘kuvipenda sana,’ tutakuwa na hamu ya kuhudhuria mikutano na kuisikiliza kwa makini. (Zaburi 119:167) Inaburudisha kama nini kuwa pamoja na waamini wenzetu ambao wanapendezwa na hali yetu na ambao hutusaidia kuendelea kutembea katika njia ya utimilifu!—Waebrania 10:24, 25.

‘Usiuondoe Uhai Wangu’

19. Daudi hakutaka kuwa na hatia ya dhambi zipi?

19 Kwa kuwa Daudi alijua vizuri matokeo ya kuacha kutembea katika kweli ya Mungu, alisihi hivi: “Usiiondoe nafsi yangu pamoja na watenda-dhambi, wala uhai wangu pamoja na watu wenye hatia ya damu, ambao mikononi mwao wana mwenendo mpotovu, na ambao mkono wao wa kuume umejaa rushwa.” (Zaburi 26:9, 10) Daudi hakutaka kuhesabiwa pamoja na watu wasiomwogopa Mungu na wenye hatia ya mwenendo mpotovu au rushwa.

20, 21. Ni nini kinachoweza kufanya tutembee katika njia ya watu wasiompenda Mungu?

20 Ulimwengu wa leo umejaa mazoea yasiyo ya adili. Televisheni, magazeti, na sinema zinaendeleza mwenendo mpotovu, yaani, “uasherati, uchafu, mwenendo wa aibu.” (Wagalatia 5:19) Wengine wamekuwa watumwa wa ponografia, jambo ambalo mara nyingi huongoza kwenye mwenendo usio wa adili. Vijana hasa huathiriwa na mambo hayo kwa urahisi. Katika nchi fulani, ni desturi kuwa na rafiki wa jinsia tofauti, nao vijana husongwa wafikiri kwamba ni lazima wafanye hivyo. Vijana wengi huwa na uhusiano wa kimahaba, hata ingawa hawajafikia umri wa kufunga ndoa. Ili kutosheleza tamaa ya ngono inayokua ndani yao, punde si punde, wanajihusisha na mwenendo usio wa adili na hata kufanya uasherati.

21 Watu wazima pia huathiriwa na uvutano mbaya. Mazoea yasiyo ya unyoofu katika biashara na mwelekeo wa kufanya maamuzi kwa faida za kibinafsi huonyesha ukosefu wa utimilifu. Kutembea katika njia za ulimwengu kutatutenga tu na Yehova. Acheni ‘tuchukie yaliyo mabaya, na tupende yaliyo mema,’ na kuendelea kutembea katika njia ya utimilifu.—Amosi 5:15.

“Ee Unikomboe na Kunionyesha Kibali”

22-24. (a) Unapata kitia-moyo gani katika maneno ya kumalizia ya Zaburi 26? (b) Tutazungumzia mtego gani katika makala inayofuata?

22 Daudi alimalizia maneno aliyomwambia Mungu kwa kusema hivi: “Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu. Ee unikomboe na kunionyesha kibali. Mguu wangu utasimama mahali tambarare; kati ya makundi yaliyokutanika nitambariki Yehova.” (Zaburi 26:11, 12) Azimio la Daudi la kudumisha utimilifu linahusiana sana na ombi lake la kukombolewa. Hilo linatia moyo kama nini! Licha ya hali yetu ya dhambi, Yehova atatusaidia ikiwa tumeazimia kutembea katika njia ya utimilifu.

23 Na tuonyeshe kwamba tunaheshimu na kuthamini utawala wa Mungu katika sehemu zote za maisha yetu. Kila mmoja wetu na amwombe Yehova achunguze na kusafisha mawazo na hisia zake za ndani kabisa. Tunaweza kutafakari daima kweli yake kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii. Hivyo basi, na tuepuke kabisa mashirika mabaya na kumbariki Yehova kati ya makundi yaliyokusanyika. Na tushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi, na tusiruhusu kamwe ulimwengu uhatarishe uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Mungu. Tunapofanya yote tuwezayo kutembea katika njia ya utimilifu, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatuonyesha kibali.

24 Kwa kuwa utimilifu unahusisha sehemu zote za maisha, tunahitaji kuwa macho kuhusu mtego fulani hatari, yaani, kutumia kileo vibaya. Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini viumbe wenye akili wanaweza kuhukumiwa inavyofaa kwa msingi wa utimilifu wao?

• Utimilifu ni nini, na kutembea katika njia ya utimilifu kunahusisha nini?

• Ni nini kitakachotusaidia kutembea katika njia ya utimilifu?

• Ili kudumisha utimilifu, tunapaswa kuepuka na pia kuwa macho kuhusu mtego gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Je, wewe humwomba Yehova kwa ukawaida achunguze mawazo yako ya ndani kabisa?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Je, sikuzote wewe huweka fadhili zenye upendo za Yehova mbele ya macho yako?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunaufurahisha moyo wa Yehova tunapodumisha utimilifu chini ya majaribu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, wewe hunufaika na maandalizi ya Yehova ya kukusaidia kutembea katika njia ya utimilifu?