Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo Anapaswa Kukumbukwaje?

Yesu Kristo Anapaswa Kukumbukwaje?

Yesu Kristo Anapaswa Kukumbukwaje?

Yesu Kristo “kwa hakika alikuwa mmoja wa watu mashuhuri zaidi waliopata kuishi.”—“The World Book Encyclopedia.”

KWA kawaida, watu mashuhuri hukumbukwa kwa mambo waliyofanya. Basi kwa nini watu wengi hukumbuka kuzaliwa kwa Yesu badala ya yale aliyotenda? Katika dini zote zinazojiita za Kikristo, watu wengi wanaweza kueleza matukio yanayohusiana na kuzaliwa kwake. Ni wangapi wanaokumbuka na kujitahidi kutumia mafundisho yake bora kabisa ya Mahubiri ya Mlimani?

Ni kweli kwamba kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa muhimu sana, lakini wanafunzi wake wa kwanza walitilia maanani yale ambayo alifanya na kufundisha. Bila shaka, Mungu hakukusudia kamwe kuzaliwa kwa Kristo kufanye maisha yake akiwa mtu mzima yapoteze umaana. Hata hivyo, Krismasi na hekaya zake za Mandhari ya Kuzaliwa kwa Yesu zimefanya Kristo apoteze umaana.

Swali lingine lenye kusumbua linajitokeza kuhusiana na jinsi Krismasi inavyosherehekewa. Ikiwa Yesu angerudi duniani leo, angefikiri nini kuhusu jinsi ambavyo Krismasi imefanywa kuwa biashara ya waziwazi? Miaka elfu mbili iliyopita, Yesu alitembelea hekalu huko Yerusalemu. Alikasirishwa sana kuona wabadili-fedha na wachuuzi wakitumia vibaya sherehe za dini ya Kiyahudi ili kujifaidi. Alisema hivi: “Ondoeni vitu hivi kutoka hapa! Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!” (Yohana 2:13-16) Kwa wazi, Yesu hakukubali kuchanganya biashara na dini.

Wakatoliki wengi wa Hispania walio wanyoofu wanahangaika kuona jinsi Krismasi inavyozidi kuwa sherehe ya kibiashara. Hata hivyo, huenda mwelekeo huo wa kibiashara usiepukike kwa sababu ya asili ya desturi nyingi za Krismasi. Mwandishi wa habari Juan Arias anasema hivi: “Kati ya Wakristo, wale ambao, wanachambua jinsi ambavyo Krismasi imekuwa ya ‘kipagani’ na sherehe ya kujifurahisha, kula, na kunywa badala ya kuwa sherehe ya kidini, kwa ujumla hawajui kwamba asili ya Mandhari ya Kuzaliwa kwa Yesu tayari ilikuwa na mambo mengi ya kipagani ya Roma yaliyofanywa wakati wa sherehe [ya jua].”—El País, Desemba 24, 2001.

Katika miaka ya hivi karibuni, ensaiklopedia nyingi na waandishi wengi wa habari wa Hispania wameeleza kuhusu vyanzo vya kipagani vya desturi za sherehe za Krismasi, na vilevile jinsi zilivyo za kibiashara. Kichapo Enciclopedia de la Religión Católica kinasema hivi waziwazi kuhusu tarehe ya mwadhimisho wa Krismasi: “Yaelekea sababu iliyofanya Kanisa Katoliki liamue kuchagua tarehe hiyo kuwa ya Krismasi ni mwelekeo wake wa kubadili sherehe za kipagani ziwe za Kikristo. . . . Tunajua kwamba wakati huo huko Roma, wapagani walitenga Desemba 25 iwe mwadhimisho wa natalis invicti, kuzaliwa kwa ‘jua lisiloweza kushindwa.’”

Vivyo hivyo, kichapo Enciclopedia Hispánica kinasema hivi: “Tarehe 25 Desemba haikuchaguliwa kuwa siku ya kuadhimisha Krismasi kwa sababu ilikuwa tarehe sahihi ya siku aliyozaliwa Yesu, bali ilichaguliwa ili kufanya sherehe zilizoadhimishwa huko Roma wakati wa majira ya baridi ziwe za Kikristo.” Waroma waliadhimishaje kuchomoza kwa jua wakati wa majira ya baridi kali? Walifanya hivyo kwa kula na kunywa, karamu za kupindukia, na kupeana zawadi. Kwa kuwa wakuu wa kanisa hawakutaka kutupilia mbali sherehe hiyo iliyopendwa sana, “waliifanya kuwa ya Kikristo” kwa kuiita kuzaliwa kwa Yesu badala ya kuzaliwa kwa jua.

Mwanzoni, katika karne ya nne na ya tano, mambo yaliyohusiana na ibada ya jua na desturi zake hayakukomeshwa mara moja. “Mtakatifu” Mkatoliki Augustine (354-430 W.K.) alilazimika kuwahimiza waamini wenzake waache kuadhimisha Desemba 25 kwa kuliheshimu jua kama walivyofanya wapagani. Hata leo, bado sherehe zinazohusiana na ibada ya jua zilizofanywa huko Roma zinaonekana kuwa na uvutano mkubwa.

Sherehe Inayofaa kwa Ajili ya Kula, Kunywa, na Kufanya Biashara

Kwa karne nyingi, mambo mengi yamechangia sana katika kufanya Krismasi iwe sherehe ya kimataifa inayopendwa sana ya kula, kunywa, na kufanya biashara. Pia, desturi za sherehe nyingine za majira ya baridi kali, hasa zile zinazosherehekewa kaskazini mwa Ulaya, zilianza hatua kwa hatua kufanana na sherehe zilizoadhimishwa huko Roma. * Na katika karne ya 20, wauza-bidhaa na wataalamu wa mambo ya biashara walitangaza kwa bidii desturi yoyote ambayo ingeweza kuwaletea faida kubwa.

Matokeo yamekuwa nini? Mwadhimisho wa kuzaliwa kwa Kristo umekuwa muhimu zaidi kuliko maana ya kuzaliwa kwake. Katika visa vingi, watu hata hawamtaji Kristo wakati wa Krismasi. “[Krismasi] ni sherehe ya ulimwenguni pote, ya familia, na kila mtu huiadhimisha kama apendavyo,” lasema gazeti la Hispania El País.

Maelezo hayo yanaonyesha mwelekeo wa wengi huko Hispania na nchi nyingine nyingi ulimwenguni pote. Huku miadhimisho ya Krismasi ikizidi kuwa na madoido mengi, ujuzi kumhusu Kristo unapungua. Kwa kweli, sherehe za Krismasi zimefanana sana na zile zilizofanywa nyakati za Roma—karamu za kupindukia, kula na kunywa, na kupeana zawadi.

Mtoto Amezaliwa Kwetu

Ikiwa desturi za Krismasi hazihusiani kabisa na Kristo, basi Wakristo wa kweli wanapaswa kukumbukaje kuzaliwa na maisha ya Kristo? Karne saba kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, Isaya alitabiri hivi kumhusu: “Kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa; na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake.” (Isaya 9:6) Kwa nini Isaya alionyesha kwamba kuzaliwa kwa Yesu na daraka ambalo angetimiza baadaye yangekuwa mambo muhimu? Kwa sababu Yesu angekuwa mtawala mwenye nguvu. Angeitwa Mkuu wa Amani, na amani au utawala wake wa kifalme haungekuwa na mwisho. Isitoshe, utawala wa Yesu ungetegemezwa “kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu.”—Isaya 9:7.

Malaika Gabrieli alirudia maneno ya Isaya wakati alipomtangazia Maria kuzaliwa kwa Yesu ambako kulikuwa kunakaribia. Alitabiri hivi: “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Bila shaka, kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa muhimu kwa sababu kulihusiana na kazi ambayo Kristo angetimiza akiwa Mfalme aliyewekwa rasmi wa Ufalme wa Mungu. Utawala wa Kristo unaweza kuwafaidi watu wote, kutia ndani wewe na wapendwa wako. Kwa kweli, malaika walionyesha kwamba kuzaliwa kwake kungeleta “salama duniani, katika watu wanaomupendeza [Mungu].”—Luka 2:14, Zaire Swahili Bible.

Sote tunatamani kuishi katika ulimwengu wenye amani na haki. Lakini ili kufurahia amani ambayo utawala wa Kristo utaleta, tunahitaji kumpendeza Mungu na kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Yesu alisema kwamba hatua ya kwanza inayoongoza kwenye uhusiano huo ni kujifunza juu ya Mungu na Kristo. “Uzima wa milele ndio huu,” Yesu alisema, “waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Tunapokuwa na ujuzi sahihi kumhusu Yesu, hatutahangaika tena kujua jinsi angependa tumkumbuke. Je, tungemkumbuka kwa kula, kunywa, na kupeana zawadi tarehe ileile ya sherehe ya kale ya kipagani? Yaelekea hangetaka tumkumbuke kwa njia hiyo? Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake yale aliyotaka. “Yule aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye ambaye hunipenda. Naye anayenipenda atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda.”—Yohana 14:21.

Mashahidi wa Yehova wamejifunza sana Maandiko Matakatifu ambayo yamewasaidia kuelewa maana ya amri ya Mungu na ya Yesu. Watafurahi kukusaidia kuelewa amri hizo muhimu ili umkumbuke Yesu kwa njia inayofaa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Mti wa Krismasi na sanamu ya Baba Krismasi ni mifano miwili yenye kutokeza.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Je, Biblia Inakataza Kula na Kunywa na Kupeana Zawadi?

Kupeana Zawadi

Biblia hukubali utoaji wa zawadi, kwa kuwa Yehova mwenyewe anaitwa Mtoaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yakobo 1:17) Yesu alionyesha kwamba wazazi wazuri wangewapa watoto wao zawadi. (Luka 11:11-13) Marafiki na washiriki wa familia ya Ayubu walimpa zawadi alipopata tena afya nzuri. (Ayubu 42:11) Hata hivyo, hakuna yoyote ya zawadi hizo iliyohitaji kutolewa siku za pekee za mwadhimisho. Zawadi hizo zilitolewa kutoka moyoni.—2 Wakorintho 9:7.

Kukutanika kwa Familia

Kukutanika kwa familia kunaweza kuchangia sana kuunganisha washiriki wa familia, hasa ikiwa hawaishi tena katika nyumba moja. Yesu na wanafunzi wake walihudhuria sherehe ya arusi huko Kana ambayo, bila shaka, ilifanya marafiki na watu wengi wa familia wakutane pamoja. (Yohana 2:1-10) Na katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, baba alisherehekea kurudi kwa mwana wake kwa kufanya karamu ya familia, ambayo ilitia ndani muziki na dansi.—Luka 15:21-25.

Kufurahia Chakula Kizuri

Mara nyingi Biblia hutaja kuhusu watumishi wa Mungu wakiwa wanafurahia chakula kizuri pamoja na familia, marafiki, au waabudu wenzao. Malaika watatu walipomtembelea Abrahamu, aliwafanyia karamu ambayo ilitia ndani nyama ya ng’ombe, maziwa, siagi, na keki za mviringo. (Mwanzo 18:6-8) Sulemani alieleza kwamba ‘kula, kunywa, na kushangilia’ ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Mhubiri 3:13; 8:15.

Ni wazi kwamba Mungu anataka tufurahie chakula kizuri pamoja na marafiki na familia zetu, naye anakubali utoaji wa zawadi. Tuna nafasi nyingi za kufanya hivyo wakati wowote ule wa mwaka.