Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Hukubali Msaada wa Yehova?

Je, Wewe Hukubali Msaada wa Yehova?

Je, Wewe Hukubali Msaada wa Yehova?

“Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”—WAEBRANIA 13:6.

1, 2. Kwa nini ni muhimu kukubali msaada na mwongozo wa Yehova maishani mwetu?

HEBU wazia unapanda mlima fulani. Hata hivyo, huko peke yako, kwa kuwa mtu fulani amejitolea kuambatana nawe ili akuongoze, naye ni kiongozi bora sana. Yeye ana ujuzi na nguvu nyingi kuliko wewe, lakini yeye anatembea kando yako bila kulalamika. Anaona kwamba unajikwaa mara kwa mara. Kwa kuwa anajali usalama wako, anakunyoshea mkono ili kukusaidia kupita mahali hatari. Je, utakataa msaada wake? Hapana! Usalama wako uko hatarini.

2 Tukiwa Wakristo, tuna njia ngumu ya kufuata. Je, ni lazima tutembee peke yetu katika barabara hiyo yenye nafasi ndogo? (Mathayo 7:14) La, Biblia inaonyesha kwamba tuna Kiongozi bora zaidi, Yehova Mungu, ambaye huwaruhusu wanadamu watembee pamoja naye. (Mwanzo 5:24; 6:9) Je, Yehova huwasaidia watumishi wake wanapotembea? Anasema: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’” (Isaya 41:13) Kama kiongozi aliyetajwa katika mfano wetu, kwa fadhili Yehova huwasaidia na huwa rafiki ya wale wanaojitahidi kutembea pamoja naye. Kwa kweli, hakuna hata mmoja wetu angetaka kukataa msaada wake!

3. Tutachunguza maswali gani katika mazungumzo haya?

3 Katika makala iliyotangulia, tulizungumzia njia nne ambazo Yehova alitumia kuwasaidia watu wake katika nyakati za kale. Je, yeye huwasaidia watu wake katika njia hizohizo leo? Na tunawezaje kuhakikisha kwamba tunakubali msaada wowote kati ya misaada hiyo? Acheni tuchunguze maswali hayo. Kwa kuyachunguza, tunaweza kuwa na uhakika zaidi kwamba Yehova ni Msaidizi wetu.—Waebrania 13:6.

Msaada Kutoka kwa Malaika

4. Kwa nini watumishi wa Mungu leo wanaweza kuwa na uhakika kwamba malaika wanawasaidia?

4 Je, malaika huwasaidia watumishi wa Yehova leo? Ndiyo. Ni kweli kwamba leo malaika hawaonekani waziwazi ili kuwakomboa waabudu wa kweli kutokana na hatari. Hata katika nyakati za Biblia, walifanya hivyo mara chache sana. Kama ilivyo leo, mambo mengi waliyofanya hayakuonekana na wanadamu. Hata hivyo, watumishi wa Mungu walitiwa moyo sana walipojua kwamba malaika walikuwa tayari kuwasaidia. (2 Wafalme 6:14-17) Tuna sababu nzuri ya kuhisi vivyo hivyo.

5. Biblia inaonyeshaje kwamba malaika wanahusika katika kazi ya kuhubiri leo?

5 Malaika wa Yehova wanapendezwa hasa na kazi fulani ya pekee inayotuhusu. Ni kazi gani hiyo? Tunaweza kupata jibu katika andiko la Ufunuo 14:6: “Nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” Hii “habari njema ya milele” inahusianishwa na “habari njema ya ufalme” ambayo kama Yesu alivyotabiri “itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote” kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Mathayo 24:14) Bila shaka, malaika hawahubiri moja kwa moja. Yesu aliwapa wanadamu kazi hiyo muhimu. (Mathayo 28:19, 20) Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba tunapofanya kazi hiyo, tuna msaada wa malaika watakatifu, ambao ni viumbe wa roho wenye hekima na nguvu?

6, 7. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba malaika wanatusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuwe na uhakika wa kupokea msaada wa malaika wa Yehova?

6 Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba malaika wanatusaidia katika kazi yetu. Kwa mfano, mara nyingi tunasikia kwamba Mashahidi wa Yehova walipokuwa wakihubiri walikutana na mtu fulani aliyekuwa ametoka tu kusali kwa Mungu amsaidie kupata kweli. Mambo hayo hutukia mara nyingi sana hivi kwamba hayawezi kupuuzwa kuwa mambo ya kawaida tu. Kwa sababu ya msaada huo wa malaika, watu wengi zaidi wanajifunza kufanya yale ambayo ‘malaika anayeruka katikati ya mbingu’ alitangaza: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.”— Ufunuo 14:7.

7 Je, unatamani kupata msaada wa malaika wa Yehova wenye nguvu? Basi fanya yote uwezayo katika huduma yako. (1 Wakorintho 15:58) Tunapojitoa wenyewe kwa hiari kufanya kazi hii ya pekee kutoka kwa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika wa kupokea msaada wa malaika wake.

Msaada Kutoka kwa Mkuu wa Malaika

8. Yesu ana cheo gani cha juu huko mbinguni, na kwa nini jambo hilo linatutia moyo?

8 Yehova pia hutupatia msaada mwingine wa kimalaika. Andiko la Ufunuo 10:1 linamtaja ‘malaika mwenye nguvu’ ambaye “uso wake ulikuwa kama jua.” Ni wazi kwamba malaika huyo aliyeonwa katika maono anawakilisha Yesu Kristo aliyetukuzwa akiwa katika mamlaka ya kimbingu. (Ufunuo 1:13, 16) Je, kweli Yesu ni malaika? Ndiyo, katika maana fulani, kwa kuwa yeye ni malaika mkuu. (1 Wathesalonike 4:16) Yesu ndiye mwenye nguvu zaidi kati ya wana wote wa roho wa Yehova. Yehova amempa mamlaka juu ya jeshi Lake lote la kimalaika. Kwa kuwa yeye ni malaika mkuu, yeye ni chanzo cha msaada wenye nguvu nyingi kwelikweli. Katika njia zipi?

9, 10. (a) Yesu anakuwaje “msaidizi” wetu tunapotenda dhambi? (b) Tunaweza kupata msaada gani katika kielelezo cha Yesu?

9 Mtume Yohana aliyezeeka aliandika hivi: “Yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu.” (1 Yohana 2:1) Kwa nini Yohana alidokeza kwamba Yesu ni “msaidizi” wetu hasa wakati ‘tunapotenda dhambi’? Sisi hutenda dhambi kila siku, nayo dhambi huongoza kwenye kifo. (Mhubiri 7:20; Waroma 6:23) Hata hivyo, Yesu alitoa uhai wake kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu. Naye yuko kando ya Baba yetu mwenye rehema ili kutuombea. Sote tunahitaji msaada huo. Tunawezaje kuukubali? Tunahitaji kutubu dhambi zetu na kuomba msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. Pia tunahitaji kuepuka kurudia dhambi zetu.

10 Mbali na kufa kwa ajili yetu, Yesu alituwekea kielelezo kikamilifu. (1 Petro 2:21) Kielelezo chake hutuongoza na kutusaidia tuishi kwa njia ambayo tunaweza kuepuka dhambi nzito na hivyo kumpendeza Yehova Mungu. Tunafurahi sana kuwa na msaada huo. Yesu aliahidi kuwapa wafuasi wake msaada mwingine.

Msaada wa Roho Takatifu

11, 12. Roho ya Yehova ni nini, nayo ina nguvu kiasi gani, na kwa nini tunaihitaji leo?

11 Yesu aliahidi hivi: “Nitamwomba Baba naye atawapa ninyi msaidizi mwingine awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli, ambayo ulimwengu hauwezi kuipokea.” (Yohana 14:16, 17) “Roho ya ile kweli” au roho takatifu, si mtu bali ni nguvu, yaani nguvu ya utendaji ya Yehova. Nguvu hiyo haina mipaka. Ni nguvu ambayo Yehova alitumia kuumba ulimwengu, kufanya miujiza yenye kustaajabisha, na kufunua mapenzi yake kupitia maono. Kwa kuwa leo Yehova hatumii roho yake katika njia hizo hususa, je, hilo lamaanisha kwamba hatuhitaji nguvu hiyo?

12 Sivyo kabisa! Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ tunahitaji roho ya Yehova zaidi kuliko wakati mwingine wowote. (2 Timotheo 3:1) Hiyo hutuimarisha kuvumilia majaribu. Inatusaidia kusitawisha sifa nzuri ambazo hutufanya tumkaribie Yehova na ndugu na dada zetu wa kiroho. (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo basi, tunawezaje kufaidika na msaada huo bora kutoka kwa Yehova?

13, 14. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova huwapa watu wake roho yake takatifu kwa kupenda? (b) Tunaweza kuonyesha kwa tendo gani kwamba kwa kweli hatukubali zawadi ya roho takatifu?

13 Kwanza tunahitaji kusali tupewe roho takatifu. Yesu alisema: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Naam, Yehova ndiye Baba bora zaidi. Ikiwa tunamwomba kwa unyoofu na kwa imani atupe roho yake takatifu, kwa hakika atatupatia zawadi hiyo. Basi swali ni, Je, sisi humwomba roho takatifu? Tuna sababu nzuri ya kuomba roho hiyo kila siku tunaposali.

14 Pili, tunakubali zawadi hiyo kwa kutenda kupatana nayo. Kwa mfano: Tuseme Mkristo anajaribu kuacha zoea la kutazama picha chafu. Amesali apewe roho takatifu ili imsaidie kushinda zoea hilo chafu. Ametafuta mashauri kutoka kwa wazee Wakristo, nao wamemshauri achukue hatua thabiti na hata aepuke kukaribia mambo hayo machafu. (Mathayo 5:29) Namna gani akipuuza mashauri yao na kuendelea kutazama picha chafu anaposhawishiwa? Je, anatenda kupatana na sala yake kwamba roho takatifu imsaidie? Au badala yake, je, anaelekea kukabili hatari ya kuhuzunisha roho ya Mungu na kupoteza zawadi hiyo? (Waefeso 4:30) Kwa kweli, sote tunahitaji kufanya yote tuwezayo ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kupokea msaada huo bora kutoka kwa Yehova.

Msaada Kutoka kwa Neno la Mungu

15. Tunawezaje kuonyesha kwamba hatuioni Biblia kuwa kitabu cha kawaida tu?

15 Biblia imewasaidia watumishi waaminifu wa Yehova kwa karne nyingi. Badala ya kuiona Biblia kuwa kitabu cha kawaida tu, tunahitaji kukumbuka kwamba kitabu hicho ni chanzo chenye nguvu cha msaada. Jitihada inahitajiwa ili kukubali msaada huo. Tunapaswa kuwa na ratiba ya kusoma Biblia kwa ukawaida.

16, 17. (a) Zaburi 1:2, 3 inaelezaje thawabu za kusoma sheria ya Mungu? (b) Zaburi 1:3 inaonyeshaje kwamba tunapaswa kufanya kazi kwa bidii?

16 Zaburi 1:2, 3 inasema hivi kumhusu mtu anayempendeza Mungu: “Mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. Naye hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.” Je, unaona jambo lililo muhimu zaidi katika mistari hiyo? Ni rahisi kusoma maneno hayo na kukata kauli kwamba yanafafanua tu hali nzuri yenye utulivu, yaani, mti wenye kivuli unaokua kando ya mto. Ingeburudisha kama nini kulala kidogo chini ya mti huo wakati wa alasiri! Lakini zaburi hii haitutii moyo tufikirie kupumzika. Inazungumzia kufanya kazi kwa bidii. Jinsi gani?

17 Ona kwamba mti unaotajwa hapa si mti wa kivuli ambao umekua wenyewe tu kando ya mto. Ni mti unaozaa matunda, “uliopandwa” mahali fulani palipochaguliwa, yaani, “kando ya vijito vya maji.” Mti mmoja ungewezaje kukua karibu na vijito vingi vya maji? Katika shamba la miti ya matunda, huenda mwenye shamba akachimba mitaro ya kuleta maji kwenye mizizi ya miti hiyo yenye thamani. Ah! sasa jambo hilo liko wazi kabisa. Ikiwa katika maana ya kiroho tunasitawi kama mti huo, ni kwa kuwa mtu fulani amefanya kazi nyingi ili kutusaidia. Tunashirikiana na tengenezo ambalo linatuletea maji safi ya kweli, lakini lazima tutimize sehemu yetu. Tunahitaji kufyonza maji hayo yenye thamani kwa kutafakari na kufanya utafiti unaohitajiwa ili kweli za Neno la Mungu zipenye katika akili na moyo wetu. Kwa kufanya hivyo, sisi pia tutazaa matunda mazuri.

18. Tunahitaji kufanya nini ili kupata majibu ya Biblia kwa maswali yetu?

18 Biblia haiwezi kutufaidi ikiwa hatuisomi. Hiyo si hirizi, kwani hatuwezi tu kufumba na kufumbua macho na kutazamia Biblia ijifungue na kujibu swali letu. Tunapokabili maamuzi, tunahitaji kuchimba kana kwamba tunachimba hazina iliyofichwa ili kupata “kumjua Mungu.” (Methali 2:1-5) Mara nyingi, tunahitaji kufanya utafiti kwa bidii na kwa makini ili tupate shauri la Biblia linalozungumzia mahitaji yetu hususa. Tuna vichapo vingi vya Biblia vinavyoweza kutusaidia katika utafiti wetu. Tunapotumia vichapo hivyo kuchimba kwa bidii hekima ya Neno la Mungu ambayo ni kama mawe ya thamani, tunafaidika kikweli na msaada wa Yehova.

Msaada Kupitia Waamini Wenzetu

19. (a) Kwa nini huenda makala fulani katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zikaonwa kuwa msaada ulioandaliwa kupitia waamini wenzetu? (b) Umesaidiwaje na makala fulani katika mojawapo ya magazeti yetu?

19 Sikuzote watumishi wa Yehova duniani wamekuwa wakisaidiana. Je, Yehova amebadilika? Hata kidogo. Bila shaka, sote tunaweza kukumbuka pindi ambazo tulipokea msaada tuliohitaji kutoka kwa waamini wenzetu kwa wakati unaofaa. Kwa mfano, je, unaweza kukumbuka makala fulani katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! ambayo ilikufariji ulipohitaji faraja au ilikusaidia kutatua tatizo fulani au kukabiliana na jaribu la imani yako? Yehova alikupa msaada huo kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye amepewa kazi ya kuandaa ‘chakula kwa wakati unaofaa.’—Mathayo 24:45-47.

20. Wazee Wakristo huwa “zawadi katika wanadamu” katika njia zipi?

20 Hata hivyo, mara nyingi sisi hupokea msaada wa moja kwa moja kutoka kwa waamini wenzetu. Mzee Mkristo anatoa hotuba inayotuchochea, au anafanya ziara ya uchungaji inayotusaidia kukabiliana na hali ngumu, au anatupa shauri lenye fadhili linalotusaidia kutambua na kushinda udhaifu fulani. Mkristo mmoja mwenye shukrani aliandika hivi kuhusu msaada aliopewa na mzee fulani: “Tukiwa katika huduma ya shambani alinitia moyo nieleze yaliyokuwa moyoni mwangu. Usiku uliotangulia, nilisali kwa Yehova, nikimwomba anipe mtu wa kuongea naye. Siku iliyofuata, ndugu huyo aliongea nami kwa huruma. Alinisaidia nione jinsi ambavyo Yehova amekuwa akinisaidia kwa miaka mingi. Ninamshukuru Yehova kwa kumtuma mzee huyo kwangu.” Katika njia hizo zote, wazee Wakristo huonyesha kwamba wao ni “zawadi katika wanadamu” zinazoandaliwa na Yehova kupitia Yesu Kristo ili kutusaidia tuendelee kutembea katika barabara ya uzima.—Waefeso 4:8.

21, 22. (a) Kunakuwa na matokeo gani washiriki wa kutaniko wanapofuata shauri la Wafilipi 2:4? (b) Kwa nini hata matendo madogo ya fadhili ni muhimu?

21 Mbali na wazee, kila Mkristo mwaminifu anataka kufuata amri iliyoongozwa na roho ya Mungu ya kuendelea ‘kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yake mwenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Wale walio katika kutaniko la Kikristo wanapofuata shauri hilo, kunakuwa na matendo mazuri ya fadhili. Kwa mfano, familia moja ilipatwa na misiba kadhaa kwa ghafula. Baba alikuwa amempeleka binti yake mchanga dukani. Walipokuwa wakirudi nyumbani, walipatwa na aksidenti ya gari. Binti huyo alikufa; naye baba akajeruhiwa vibaya sana. Alipotoka hospitali, alikuwa amelemaa sana hivi kwamba hangeweza kujifanyia chochote. Mke wake alikuwa amefadhaika sana kihisia-moyo hivi kwamba hangeweza kumtunza akiwa peke yake. Hivyo, wenzi fulani wa ndoa katika kutaniko waliwachukua na kuwapeleka nyumbani kwao na kuwatunza kwa majuma kadhaa.

22 Bila shaka, matendo yote ya fadhili hayahusu tu misiba kama hiyo na kujidhabihu. Msaada fulani tunaopokea ni mdogo zaidi. Lakini hata kama tendo la fadhili ni dogo sana, tunalithamini, sivyo? Je, unaweza kufikiria pindi ambazo ulipata msaada uliohitaji kupitia neno au tendo fulani la fadhili kutoka kwa ndugu au dada? Mara nyingi Yehova hututunza katika njia kama hizo.—Methali 17:17; 18:24.

23. Yehova huonaje jitihada zetu za kusaidiana?

23 Je, ungependa Yehova akutumie kuwasaidia wengine? Unaweza kuwa na pendeleo hilo. Kwa kweli, Yehova anathamini jitihada unayofanya kusaidia. Neno lake linasema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Methali 19:17) Tunapata shangwe nyingi tunapojitolea kuwasaidia ndugu na dada zetu. (Matendo 20:35) Wale wanaojitenga kimakusudi na wengine hawapati shangwe inayotokana na kusaidia au kitia-moyo kinachotokana na kupokea msaada. (Methali 18:1) Kwa hiyo, na tukutanike kwa uaminifu na kwa ukawaida katika mikutano ya Kikristo ili tutiane moyo.—Waebrania 10:24, 25.

24. Kwa nini hatupaswi kuhisi kwamba tunakosa chochote kwa sababu hatujashuhudia miujiza yenye kustaajabisha ambayo Yehova alifanya zamani?

24 Inapendeza kama nini kutafakari njia ambazo Yehova hutumia kutusaidia. Ingawa hatuishi wakati ambao Yehova anafanya miujiza yenye kustaajabisha ili kutimiza makusudi yake, hatupaswi kuhisi kuwa tunakosa chochote. Jambo muhimu ni kwamba Yehova anatupatia msaada wowote tunaohitaji ili tuendelee kuwa waaminifu. Na tukivumilia pamoja katika imani, tutashuhudia matendo matukufu na yenye kustaajabisha ya Yehova katika historia yote! Basi na tuazimie kukubali na kutumia kabisa msaada wenye upendo kutoka kwa Yehova ili tuonyeshe kwamba tunakubaliana na maneno haya ya andiko letu la mwaka wa 2005: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

Unafikiri Nini?

Yehova anaandaaje msaada tunaohitaji leo—

• kupitia malaika?

• kupitia roho yake takatifu?

• kwa Neno lake lililoongozwa na roho?

• kupitia waamini wenzetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Inatia moyo kujua kwamba malaika wanategemeza kazi ya kuhubiri

[Picha katika ukurasa wa 21]

Huenda Yehova akatumia mmoja wa waamini wenzetu kutupatia faraja tunayohitaji