Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku ya Kuhitimu —Siku Nzuri

Siku ya Kuhitimu —Siku Nzuri

Siku ya Kuhitimu —Siku Nzuri

“TUMEBARIKIWA kuwa na siku nzuri. Jua limeangaza. Anga ni la buluu. Nyasi ni ya kijani-kibichi. Ndege wanaimba. Tuna siku nzuri mbele yetu, na hatutakatishwa tamaa. Yehova si Mungu wa kukatisha watu tamaa. Yeye ni Mungu wa baraka.”

Kwa maneno hayo, Ndugu Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alianza programu ya kuhitimu kwa darasa la 117 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Ilikuwa Septemba 11, 2004. Programu hiyo nzuri ilitia ndani shauri lenye kujenga ambalo linatoka katika Biblia na vilevile mambo yaliyoonwa na wanafunzi wa Gileadi walipokuwa shuleni na mengine kutoka kwa wamishonari kadhaa wenye uzoefu. Naam, ilikuwa siku nzuri kwa wote 6,974 waliohudhuria programu hiyo kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, na majengo ya Brooklyn na Wallkill, yaliyounganishwa kwa simu.

Maneno ya Kuwatia Moyo Wanafunzi

John Kikot, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani alitaja maneno yenye kutia moyo alipotoa hotuba yenye kichwa “Dumisha Shangwe Ukiwa Mmishonari.” Alisema kwamba wanafunzi wa Gileadi wanajulikana kwa shangwe yao, kama ilivyokuwa kwenye sherehe hiyo ya kuhitimu. Mafundisho kutoka katika Biblia wakati wa shule yaliwapa wanafunzi shangwe, na sasa wangeweza kuwasaidia wengine wawe na shangwe kama hiyo. Jinsi gani? Kwa kujitoa wenyewe katika huduma yao wakiwa wamishonari. Yesu alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Kadiri wanavyomwiga Yehova, Mungu mkarimu na “mwenye furaha” ambaye hufanya wengine wapate kweli, ndivyo wamishonari wapya watakavyoweza kudumisha shangwe yao.—1 Timotheo 1:11.

Msemaji aliyefuata kwenye programu alikuwa David Splane, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, ambaye hotuba yake ilikuwa na kichwa “Utapatanaje na Watu?” Bila shaka, ni vyema na inapendeza kukaa kwa umoja, ingawa huenda hilo likataka tuwe “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Wakorintho 9:22; Zaburi 133:1) Ndugu Splane alitaja kwamba wanafunzi wanaohitimu wangeshughulika na watu wengi katika kazi ya umishonari—watu katika maeneo, wamishonari wenzao, ndugu na dada katika kutaniko lao jipya, na wale walio katika ofisi ya tawi na ambao wanaelekeza kazi ya kuhubiri na kufundisha. Alitoa madokezo mazuri kuhusu jinsi ya kufanya uhusiano na wengine uwe wenye kupendeza kadiri iwezekanavyo: Jifunze lugha ya wenyeji, uwe macho na tayari kujirekebisha kupatana na desturi za wenyeji, heshimu wakati wa faragha wa wamishonari wenzako, na watii wale wanaoongoza.—Waebrania 13:17.

Kisha, mwalimu wa Gileadi Lawrence Bowen aliuliza, “Unafikiri Nini?” Aliwakumbusha wanafunzi kwamba wale ‘waliohukumu kwa sura ya nje’ hawakumkubali Yesu kuwa Masihi. (Yohana 7:24) Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sote tunahitaji kujilinda dhidi ya ‘kufikiri fikira za wanadamu’ badala ya “fikira za Mungu.” (Mathayo 16:22, 23) Hata watu wa kiroho wanapaswa kuendelea kurekebisha fikira zao. Sawa na meli iliyo baharini, kufanya marekebisho sasa kunaweza kufanya tufikie mradi au tuangamie kiroho. Kuendelea kujifunza Biblia kwa kuzingatia hali mpya hutusaidia kufikiri “fikira za Mungu.”

Wallace Liverance, mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi, alimalizia sehemu hiyo ya programu. Hotuba yake iliyotegemea andiko la Isaya 55:11, ilikuwa na kichwa “Mtanunua Nini?” Aliwatia moyo wanafunzi ‘wanunue’ burudisho, shangwe, na chakula kinachotoka katika ujumbe wa Mungu wa kinabii wa wakati wetu. Unabii wa Isaya ulilinganisha neno hilo la Mungu na maji, divai, na maziwa. Linawezaje kununuliwa “bila pesa na bila bei”? Ndugu Liverance alisema kwamba ni kwa kuzingatia unabii wa Biblia na kuacha fikira na njia zisizo za kiroho na kufuatia fikira na njia za Mungu. (Isaya 55:2, 3, 6, 7) Kwa kufanya hivyo, wamishonari wapya wanaweza kuendelea na migawo yao katika nchi za kigeni. Mara nyingi, wanadamu wasio wakamilifu hufikiri kwamba furaha inategemea kujitahidi kuwa na vitu vya kimwili. “Usiamini jambo hilo,” akasihi msemaji. “Usiamini jambo hilo. Hakikisha kwamba unatenga wakati wa kutosha kujifunza Neno la Mungu la kinabii. Linaweza kukuburudisha, kukuimarisha, na kukupa shangwe katika mgawo wako wa umishonari.”

Mambo Yaliyoonwa na Mahojiano Yenye Kupendeza ya Wanafunzi

Wanafunzi walishiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri. Ndugu Mark Noumair, mwalimu mwingine wa Gileadi alishughulikia sehemu ya mambo yaliyoonwa ambayo yaliigizwa na wanafunzi kadhaa na ambayo yalikazia habari yenye kichwa ‘Kutoionea Aibu Habari Njema.’ (Waroma 1:16) Wasikilizaji walifurahi kusikia jinsi wahudumu hao wenye uzoefu walivyotoa ushahidi nyumba kwa nyumba, barabarani, na madukani. Wanafunzi waliojua lugha za kigeni walichukua hatua ya kwanza katika eneo la kutaniko lao kuwahubiria watu wanaozungumza lugha hizo. Wengine walitumia vizuri vichapo vinavyozungumzia Biblia ambavyo huchapishwa na Mashahidi wa Yehova. Walivitumia kwenye ziara za kurudia na katika kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani. ‘Hawakuona aibu’ kuhubiri habari njema.

Ndugu William Nonkes, ambaye anafanya kazi katika Idara ya Utumishi, aliwahoji wamishonari wenye uzoefu kutoka Burkina Faso, Latvia, na Urusi. Walitoa shauri zuri lililotegemea kichwa “Yehova Huwathawabisha kwa Upendo Walio Waaminifu.” Mmojawapo wa ndugu waliohojiwa aliwatia moyo wanafunzi wakumbuke jeshi la Gideoni la askari-jeshi 300. Kila askari-jeshi alikuwa na mgawo fulani ambao ulifanikisha kampeni ya Gideoni. (Waamuzi 7:19-21) Vivyo hivyo, wamishonari ambao hubaki katika migawo yao huthawabishwa.

Kisha Ndugu Samuel Roberson alishughulikia sehemu ya mahojiano iliyokazia kichwa, ‘Iweni Mambo Yote kwa Watu wa Namna Zote.’ Aliwahoji washiriki wanne wa Halmashauri ya Tawi kutoka Senegal, Guam, Liberia, na Madagaska. Jumla ya wamishonari 170 wanatumika katika nchi hizo. Wanafunzi waliokuwa wakihitimu walijifunza jinsi Halmashauri za Tawi husaidia wamishonari wapya wazoee migawo yao. Mara nyingi hiyo humaanisha wajifunze desturi ambazo huenda zikaonwa kuwa za kiajabu na watu wa Nchi za Magharibi. Kwa mfano, katika nchi fulani ni jambo la kawaida kuona wanaume wawili ambao ni marafiki, kutia ndani wale walio katika kutaniko la Kikristo wakishikana mikono wanapotembea pamoja. Katika sehemu nyingine chini ya ofisi ya tawi ya Guam, kuna vyakula visivyo vya kawaida. Lakini wengine wamezoea vyakula hivyo, nao wamishonari wapya wanaweza kuvizoea pia.

Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alichanganua habari yenye kichwa “Endeleeni Kuwa Washikamanifu kwa ‘Ufalme wa Bwana Wetu.’” Aliwakumbusha wasikilizaji hivi: “Yehova aliumba vitu akiwa na kusudi fulani. Alikuwa na kusudi fulani kwa uumbaji wake. Kusudi lake kuelekea dunia hii halijabadilika. Linaelekea kutimizwa pasipo kuzuiwa na chochote. Hakuna kitu kinachoweza kulibadili.” (Mwanzo 1:28) Ndugu Pierce aliwatia moyo wote wajitiishe kwa ushikamanifu kwa enzi kuu ya Mungu licha ya matatizo ambayo yametokea kwa sababu ya dhambi ya mwanadamu wa kwanza, Adamu. “Tunaishi katika saa ya hukumu. Tuna wakati mfupi wa kuwafikia watu wenye mioyo minyoofu na kuwasaidia waijue kweli. Tumieni wakati huo vizuri ili kuwapelekea wengine habari njema za Ufalme,” akahimiza Ndugu Pierce. Wale wanaounga mkono Ufalme wa Mungu kwa ushikamanifu wanaweza kuwa na uhakika kwamba atawategemeza.—Zaburi 18:25.

Katika sehemu ya kumalizia, mwenyekiti alisoma salamu na heri njema kutoka ofisi mbalimbali za tawi ulimwenguni. Kisha akawapa diploma wanafunzi waliohitimu, naye mwanafunzi mmoja akasoma barua kutoka kwa wanafunzi wenzake iliyoeleza shukrani zao za kutoka moyoni kwa ajili ya mazoezi waliyopata. Programu hiyo nzuri ilimalizikia hapo nayo itakumbukwa kwa muda mrefu na wote waliohudhuria.

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 11

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 22

Idadi ya wanafunzi: 48

Wastani wa umri: 34.8

Wastani wa miaka katika kweli: 18.3

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.4

[Picha katika ukurasa wa 24]

Darasa la 117 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Thompson, Norvell, G.; Powell, T.; Kozza, M.; McIntyre, T. (2) Reilly, A.; Clayton, C.; Allan, J.; Blanco, A.; Muñoz, L.; Rustad, N. (3) Guerrero, Z.; Garcia, K.; McKerlie, D.; Ishikawa, T.; Blanco, G. (4) McIntyre, S.; Cruz, E.; Guerrero, J.; Ritchie, O.; Avellaneda, L.; Garcia, R. (5) Powell, G.; Fiskå, H.; Muñoz, V.; Baumann, D.; Shaw, S.; Brown, K.; Brown, L. (6) Shaw, C.; Reilly, A.; Peloquin, C.; Münch, N.; McKerlie, D.; Ishikawa, K. (7) Münch, M.; Peloquin, J.; Kozza, T.; Avellaneda, M.; Allan, K.; Ritchie, E.; Norvell, T. (8) Cruz, J.; Baumann, H.; Clayton, Z.; Fiskå, E.; Thompson, M.; Rustad, J.