Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Yah Ndiye Wokovu Wangu’

‘Yah Ndiye Wokovu Wangu’

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”

‘Yah Ndiye Wokovu Wangu’

WATU wa Yehova walihitaji kufanya uamuzi. Je, wangeendelea kumtii mtawala mwovu wa Misri ya kale? Au wangemtii Yehova Mungu, waondoke utumwani, na kwenda kuishi katika Nchi ya Ahadi?

Kwa sababu Farao wa Misri mwenye kuasi alikataa kuwaachilia watu wa Yehova, Mungu aliipiga nchi kwa yale Mapigo Kumi. Huo ulikuwa wonyesho wa nguvu za Mungu! Miungu ya Wamisri haingeweza kuzuia mapigo hayo.

Farao alipoambiwa aache watu wa Mungu waende, alisema hivi kwa dharau: “Yehova ni nani, hivi kwamba mimi niitii sauti yake na kuwaruhusu Israeli waende zao? Simjui Yehova hata kidogo na tena sitawaruhusu Israeli waende zao.” (Kutoka 5:2) Kwa sababu hiyo, nchi ya Misri ilipatwa na mapigo haya: (1) maji yalibadilika yakawa damu, (2) vyura, (3) chawa, (4) mainzi, (5) tauni juu ya wanyama wa kufugwa, (6) majipu juu ya mwanadamu na mnyama, (7) mvua ya mawe, (8) nzige, (9) giza, na (10) kufa kwa kila mzaliwa wa kwanza wa Misri, kutia ndani mwana wa Farao. Hatimaye, Farao aliwaruhusu Waebrania hao waende. Hata aliwasihi waondoke!—Kutoka 12:31, 32.

Watu milioni tatu hivi, waliotia ndani wanaume, wanawake, watoto Waisraeli na vilevile jamii kubwa iliyochangamana, waliondoka upesi. (Kutoka 12:37, 38) Hata hivyo, muda mfupi baadaye, Farao akiwa na jeshi lake lenye kutisha, aliwafuata. Ilikuwa kana kwamba Waisraeli walikuwa wamenaswa katikati ya Bahari Nyekundu, jangwa hatari, na majeshi ya Farao. Hata hivyo, Musa aliwaambia hivi watu hao: “Msiogope. Simameni imara muuone wokovu wa Yehova.”—Kutoka 14:8-14.

Yehova aligawanya maji ya Bahari Nyekundu kimuujiza ili Waisraeli waponyoke. Lakini Wamisri walipowafuata, Yehova alisababisha maji yarudi. ‘Yehova alitupa magari ya Farao na majeshi yake baharini.’ (Kutoka 14:26-28; 15:4) Kwa sababu ya kutomheshimu Yehova, Farao mwenye kiburi aliangamia.

Yehova alithibitika kuwa “mtu wa vita” katika Bahari Nyekundu. (Kutoka 15:3) “Israeli wakauona pia ule mkono mkuu ambao Yehova aliufanya utende juu ya Wamisri,” linasema simulizi lililoongozwa kwa roho, “nao watu wakaanza kumwogopa Yehova na kuwa na imani katika Yehova.” (Kutoka 14:31; Zaburi 136:10-15) Walimshukuru Mungu kutoka moyoni huku wanaume wakijiunga na Musa kuimba wimbo wa ushindi, naye dada yake, Miriamu, akiwaongoza wanawake katika dansi. *

Yehova Bado Ni Mkombozi

Watumishi wa Yehova wa siku hizi wanaweza kujifunza mambo yenye kuimarisha imani kutokana na ukombozi huo wa Mungu. Jambo moja tunalojifunza ni kwamba Yehova ana nguvu zisizo na kikomo na anaweza kuwasaidia kabisa watu wake. Katika wimbo wao wa ushindi, Musa na Waisraeli waliimba hivi kwa shangwe: “Mkono wako wa kuume, Ee Yehova, unajionyesha kuwa wenye nguvu katika uwezo, mkono wako wa kuume, Ee Yehova, unaweza kumvunja-vunja adui.”—Kutoka 15:6.

Jambo lingine ni kwamba Mweza-Yote anataka sana kuwalinda watu wake. Waisraeli waliimba hivi: “Nguvu zangu na uwezo wangu ni Yah, kwa maana yeye ndiye wokovu wangu. Huyu ndiye Mungu wangu, nami nitamsifu.” Jambo lingine pia ni kwamba hakuna anayeweza kupinga kwa mafanikio mapenzi ya Yehova Mungu. Katika wimbo wao wa ushindi, watu wa Mungu waliokombolewa waliimba hivi: “Ni nani kati ya miungu aliye kama wewe, Ee Yehova? Ni nani aliye kama wewe, unayejionyesha kuwa mwenye nguvu katika utakatifu? Unayestahili kuogopwa kwa nyimbo za sifa, Unayefanya mambo ya ajabu.”—Kutoka 15:2, 11.

Kama Farao wa Misri ya kale, leo watawala wa ulimwengu wanawatesa watu wa Yehova. Huenda watawala wenye kiburi ‘wakasema maneno mabaya kumhusu yule Aliye Juu Zaidi, na kuwasumbua bila kikomo watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi.’ (Danieli 7:25; 11:36) Lakini Yehova anawahakikishia watu wake hivi: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu. Hilo ndilo fungu la urithi la watumishi wa Yehova.”—Isaya 54:17.

Wanaompinga Mungu hawatafanikiwa kama vile tu Farao na majeshi yake hawakufanikiwa. Matendo ya Yehova ya kukomboa, kama vile kuwatoa Waisraeli Misri, yanaonyesha kwamba inafaa kufuata kanuni iliyotajwa na mitume wa Yesu, waliosema hivi: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona Kalenda ya Mashahidi wa Yehova 2006, Januari/Februari.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

JE, ULIJUA?

• Yehova alisababisha upepo mkali uvume usiku kucha ili Waisraeli wavuke Bahari Nyekundu juu ya nchi kavu.—Kutoka 14:21, 22.

• Huenda njia yenye upana wa kilometa 1.5 hivi ingehitajiwa ili mamilioni ya Waisraeli wavuke Bahari Nyekundu kwa muda mfupi sana.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Miungu ya uwongo ya Misri ilishindwa kuzuia yale Mapigo Kumi kutoka kwa Yehova

[Hisani]

All three figurines: Photograph taken by courtesy of the British Museum